SURA YA 11
Mipango ya Mahali pa Ibada
WAABUDU wa kweli wa Yehova wanaamuriwa wakusanyike pamoja ili wafundishwe na watiane moyo. (Ebr. 10:23-25) Mahali pa kwanza ambapo Waisraeli, watu waliochaguliwa na Mungu, walikusanyika kwa ajili ya ibada paliitwa “hema la ibada, yaani, hema la mkutano.” (Kut. 39:32, 40) Baadaye, Sulemani mwana wa Daudi alijenga nyumba, au hekalu, kwa utukufu wa Mungu. (1 Fal. 9:3) Baada ya hekalu hilo kuharibiwa mwaka wa 607 K.W.K., Wayahudi walipanga kukutana kwenye majengo yaliyoitwa masinagogi ili kumwabudu Mungu. Baada ya muda, hekalu lilijengwa tena, na kwa mara nyingine likawa kituo cha ibada ya kweli. Yesu alifundisha kwenye masinagogi na pia hekaluni. (Luka 4:16; Yoh. 18:20) Yesu alifanya mkutano hata kwenye mlima.—Mt. 5:1–7:29.
2 Baada ya Yesu kuuawa, Wakristo walikusanyika katika sehemu za umma na kwenye nyumba za watu ili kufundisha Maandiko na kushirikiana na waamini wenzao. (Mdo. 19:8, 9; Rom. 16:3, 5; Kol. 4:15; Flm. 2) Nyakati nyingine Wakristo wa karne ya kwanza walilazimika kukutana mahali ambapo hapakuwa na watu ili kuwaepuka watesaji. Kwa kweli, zamani watumishi waaminifu wa Mungu walitamani sana kukusanyika mahali pa ibada ili ‘kufundishwa na Yehova.’—Isa. 54:13.
3 Leo pia, sehemu za umma na nyumba za watu hutumiwa kwa ajili ya mikutano ya Kikristo. Mara nyingi nyumba za watu hutumiwa kwa ajili ya mikutano ya utumishi wa shambani. Wale wanaoruhusu mikutano hiyo ifanywe kwenye nyumba zao huliona hilo kuwa pendeleo kubwa. Wengi wanaona kwamba wamenufaika kiroho kwa kuruhusu nyumba zao zitumiwe.
JUMBA LA UFALME
4 Mashahidi wa Yehova hukutana hasa kwenye Jumba la Ufalme. Kwa kawaida, uwanja hununuliwa kisha Jumba jipya la Ufalme hujengwa, au jengo fulani linanunuliwa na kufanyiwa marekebisho. Inapowezekana, makutaniko kadhaa yanaweza kutumia Jumba moja la Ufalme ili kupunguza gharama na kulitumia kwa ukamili. Katika maeneo mengine, inalazimu kukodi jumba. Jumba jipya la Ufalme likijengwa au kufanyiwa ukarabati mkubwa, inafaa liwekwe wakfu. Hata hivyo, ikiwa Jumba la Ufalme limefanyiwa marekebisho au ukarabati mdogo tu, basi hakuna haja ya kuliweka wakfu.
5 Jumba la Ufalme halipaswi kuwa jengo lenye madoido ili kuwavutia watu. Ingawa huenda muundo wake ukatofautiana ikitegemea eneo, sikuzote majengo hayo hutimiza kusudi linalofaa. (Mdo. 17:24) Ikitegemea hali, jumba linapaswa kuwa zuri na mahali panapofaa kufanyiwa mikutano ya Kikristo.
6 Makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova huchangia gharama za matumizi, uendeshaji, na udumishaji wa Jumba lao la Ufalme. Hakuna sadaka zinazokusanywa; wala Mashahidi hawachangishi pesa kutoka kwa watu. Kuna sanduku la michango kwa ajili ya wahudhuriaji ambao huenda wangependa kuchangia gharama muhimu za matumizi ya jumba hilo. Wanachangia kwa hiari na kutoka moyoni.—2 Kor. 9:7.
7 Washiriki wote wa kutaniko hufurahia kuchangia pesa na kujitolea kulisafisha na kulidumisha Jumba la Ufalme. Kwa kawaida mzee au mtumishi wa huduma hupewa mgawo wa kuratibu kazi hiyo. Mara nyingi usafi hufanywa na vikundi vya utumishi, chini ya uongozi wa mwangalizi wa kikundi au msaidizi wake. Iwe ni ndani au nje, Jumba la Ufalme linapaswa kumwakilisha Yehova na tengenezo lake kwa njia inayofaa.
Washiriki wote wa kutaniko hufurahia kuchangia pesa na kujitolea kulisafisha na kulidumisha Jumba la Ufalme
8 Mahali ambako makutaniko kadhaa yanatumia jumba moja, wazee wa makutaniko yanayohusika huunda Halmashauri ya Uendeshaji wa Jumba la Ufalme, ili kusimamia mambo yote yanayohusiana na jengo na uwanja wa jumba. Mabaraza ya wazee humteua ndugu mmoja kuwa mratibu wa halmashauri ya uendeshaji. Ikifanya kazi chini ya mwelekezo wa mabaraza ya wazee, halmashauri hiyo husimamia usafi wa jumba, na kuhakikisha kwamba linatunzwa vizuri na kuna vifaa vya kutosha. Ili kufanikisha hilo makutaniko yanayohusika yanapaswa kushirikiana.
9 Makutaniko kadhaa yanapotumia Jumba moja la Ufalme, huenda ratiba ya mikutano ikabadilika-badilika. Wazee wanapopanga ratiba hiyo wanapaswa kuchochewa na roho ya ufikirio na upendo. (Flp. 2:2-4; 1 Pet. 3:8) Kutaniko moja halipaswi kufanya uamuzi kwa niaba ya makutaniko mengine. Mwangalizi wa mzunguko anapotembelea mojawapo ya makutaniko hayo, makutaniko mengine katika jumba hilo yatabadili muda wa mikutano yao katika juma hilo.
10 Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko ikiidhinisha, Jumba la Ufalme linaweza kutumiwa kwa ajili ya hotuba ya ndoa na ya maziko. Wazee hao hufikiria ombi lililotolewa kwa uangalifu na kufanya uamuzi kupatana na mwongozo wa ofisi ya tawi.
11 Wale wanaoruhusiwa kutumia Jumba la Ufalme kwa makusudi hayo wanapaswa kujiendesha kwa njia ya Kikristo. Hakuna jambo linalopaswa kufanyika katika Jumba la Ufalme ambalo litaudhi kutaniko au kumletea Yehova suto na kuharibu sifa nzuri ya kutaniko. (Flp. 2:14, 15) Chini ya mwelekezo wa ofisi ya tawi, Jumba la Ufalme linaweza kutumiwa kwa shughuli nyingine za kiroho, kama vile Shule ya Huduma ya Ufalme na Shule ya Utumishi wa Painia.
12 Nyakati zote kutaniko linapaswa kuheshimu mahali pa mikutano. Mavazi, mapambo na tabia zinapaswa kuonyesha heshima inayostahili ibada ya Yehova. (Mhu. 5:1; 1 Tim. 2:9, 10) Tunaonyesha kwamba tunathamini mikutano yetu ya Kikristo tunapotii ushauri huo.
13 Ni muhimu kudumisha utaratibu mikutano inapoendelea. Inapendekezwa kwamba watoto waketi pamoja na wazazi wao. Wazazi wenye watoto wadogo wanatiwa moyo kuketi mahali ambapo hawatawakengeusha sana wasikilizaji ikiwa watahitaji kuwatoa nje watoto wao ili kuwatia nidhamu au kwa sababu nyingine.
14 Ndugu wanaostahili hupewa mgawo wa kuwa wakaribishaji wakati wa mikutano katika Jumba la Ufalme. Wanapaswa kuwa chonjo, wenye urafiki na utambuzi. Majukumu yao yanatia ndani kuwasalimu na kuwakaribisha wapya, kuwaonyesha waliochelewa mahali pa kuketi, kuandika hudhurio la mikutano, na kuhakikisha kwamba mifumo ya kupitisha hewa inafanya kazi vizuri. Inapohitajika, wakaribishaji wanapaswa kuwakumbusha wazazi wawaangalie watoto wao wasikimbie-kimbie ndani ya jumba kabla na baada ya mikutano au kucheza jukwaani. Kwa fadhili na busara, mkaribishaji anaweza kumwomba mzazi mwenye mtoto mtundu amtoe nje, ili wasikilizaji wasikengeushwe. Kazi inayofanywa na wakaribishaji huwawezesha wote kufurahia mikutano. Inafaa wazee na watumishi wa huduma watumiwe kuwa wakaribishaji.
UJENZI WA MAJUMBA YA UFALME
15 Katika karne ya kwanza, Wakristo fulani walikuwa na mali kuliko wengine, ndiyo sababu mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia usawazisho, ziada yenu kwa sasa ijazie uhitaji wao, ili ziada yao pia ijazie upungufu wenu, ili kuwe na usawazisho.” (2 Kor. 8:14) Leo, kuna “usawazisho” kama huo. Michango inayokusanywa katika makutaniko ulimwenguni pote huunganishwa ili kutoa msaada wa kifedha wa kujenga na kukarabati Majumba ya Ufalme. Ukarimu huo wa akina ndugu ulimwenguni pote unathaminiwa sana na tengenezo na makutaniko yanayonufaishwa na michango hiyo.
16 Ikitegemea mpango na ukubwa wa eneo, ofisi ya tawi hupanga makutaniko kadhaa yatumie Majumba fulani ya Ufalme. Pia, ofisi ya tawi huamua wakati na mahali pa kujenga Majumba mapya ya Ufalme na yale yaliyopo kufanyiwa ukarabati. Majanga yanapotokea, mipango inayohitajiwa hufanywa ili kurekebisha Majumba ya Ufalme yaliyoharibika, na nyakati nyingine, kurekebisha nyumba za akina ndugu.
17 Ofisi ya tawi huratibu jinsi wajitoleaji watakavyosaidia kupata uwanja, vibali, kusanifu, kudumisha, na kujenga Jumba la Ufalme. Kwa sababu kuna uhitaji mkubwa wa Majumba ya Ufalme katika nchi nyingi, wajitoleaji wengi wanahitajiwa. Wahubiri wote waliobatizwa wanaostahili na wangependa kusaidia, wanatiwa moyo kujaza fomu na kuwapa wazee walio katika Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lao. Hata wahubiri ambao hawajabatizwa wanaweza kusaidia kujenga au kukarabati Jumba lao la Ufalme.
MAJUMBA YA KUSANYIKO
18 Kwa kawaida, Wakristo wa karne ya kwanza walikutana katika vikundi vidogo. Hata hivyo, nyakati nyingine “umati mkubwa” ulikusanyika. (Mdo. 11:26) Vivyo hivyo, watu wa Yehova leo hufanya mikutano mikubwa kama vile makusanyiko ya mzunguko na makusanyiko ya eneo. Mara nyingi, wao hukodi sehemu za kufanyia makusanyiko hayo, hata hivyo isipowezekana, wanajenga mahali pa ibada panapoitwa Jumba la Kusanyiko.
19 Nyakati nyingine, wao hununua jengo, hulirekebisha, na kulitumia kama Jumba la Kusanyiko. Hata hivyo, mara nyingi uwanja hununuliwa na jumba jipya kujengwa. Ukubwa wa Majumba ya Kusanyiko hutofautiana ikitegemea mahitaji ya eneo. Uamuzi wa kununua au kujenga hufanywa na ofisi ya tawi baada ya kuchanganua kwa uangalifu gharama na jinsi jumba hilo litakavyotumika.
20 Ofisi ya tawi huwaweka rasmi ndugu wasimamie uendeshaji na udumishaji wa Jumba la Kusanyiko. Mipango hufanywa katika mizunguko ili jumba hilo lisafishwe kwa ukawaida, usafi mkubwa ufanywe mara mbili kwa mwaka, na ukarabati ufanyike ili kulidumisha. Ingefaa wahubiri wajitolee kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo, makutaniko yanahimizwa kuunga mkono mipango hiyo kwa moyo wote.—Zab. 110:3; Mal. 1:10.
21 Nyakati nyingine, Jumba la Kusanyiko linaweza pia kutumiwa kwa ajili ya shughuli nyingine za kitheokrasi, kama vile Shule za Biblia na mikutano ya pekee ya waangalizi wa mzunguko. Jumba la Kusanyiko ni mahali pa ibada palipowekwa wakfu sawa na Jumba la Ufalme. Tunapokutana katika Jumba la Kusanyiko, mwenendo, mavazi, na mapambo yetu yanapaswa kuwa ya heshima, kama tu tunapohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme kwa ajili ya ibada.
22 Mwishoni mwa siku hizi za mwisho, watu wengi wapya wanafanya haraka kuwa sehemu ya tengenezo la Mungu. Huo ni uthibitisho wa baraka za Yehova. (Isa. 60:8, 10, 11, 22) Kwa hiyo, tunapenda kuunga mkono mipango ya kupata na kudumisha mahali safi na pazuri pa ibada. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunathamini umuhimu wa mahali pa ibada katika kutusaidia kutiana moyo kadiri tunavyoona siku ya Yehova ikikaribia.