Nyongeza
Ujumbe kwa Wazazi Wakristo:
Ukiwa mzazi, ungependa kuwasaidia watoto wako wapendwa wampende Yehova na kujiweka wakfu kwake. Unaweza kufanya nini ili uwasaidie wajitayarishe kwa ajili ya ubatizo? Utajuaje kwamba wako tayari kwa ajili ya hatua hiyo muhimu?
Yesu aliwaagiza wanafunzi wake hivi: ‘Fanyeni wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na kuwabatiza.’ (Mt. 28:19) Kulingana na agizo hilo, takwa la msingi ili mtu astahili kubatizwa ni kuwa mwanafunzi, yaani, anapaswa kuelewa, kuamini, na kujitahidi kuishi kupatana na mafundisho ya Yesu. Hata watoto wanaweza kutimiza jambo hilo.
Wawekee watoto wako kielelezo chema, na ukazie sheria za Yehova mioyoni mwao. (Kum. 6:6-9) Unaweza kutumia habari zilizo katika kitabu Furahia Maisha Milele! ili kuwafundisha kweli za msingi na jinsi ya kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Wasaidie watoto wako wajue jinsi ya kueleza mambo wanayoamini kwa maneno yao wenyewe wanapoongea na wengine. (1 Pet. 3:15) Kitia-moyo na ujuzi wanaopokea kutoka kwako pamoja na mambo wanayojifunza kibinafsi, ibada ya familia, mikutano ya kutaniko, na marafiki wazuri, yatawasaidia kufikia ubatizo na kufanya maendeleo zaidi. Wasaidie wajiwekee miradi ya kiroho.
Andiko la Methali 20:11 linasema hivi: “Hata mtoto hujulikana kwa matendo yake, kama tabia yake ni safi na ya unyoofu.” Ni mambo gani yanayoweza kuonyesha kwamba mtoto, iwe ni msichana au mvulana, amekuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo na yuko tayari kubatizwa?
Mtoto anayefanya maendeleo ili astahili kubatizwa anapaswa kuwatii wazazi wake. (Mdo. 5:29; Kol. 3:20) Biblia inasema kwamba Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, ‘aliendelea kuwatii wazazi wake.’ (Luka 2:51) Bila shaka, hutazamii mtoto wako awe mkamilifu. Hata hivyo, mtoto anayetaka kubatizwa atajitahidi kufuata kielelezo cha Yesu na bila shaka atajitiisha kwa wazazi wake.
Pia, ataonyesha kwamba anapenda kujifunza kweli za Biblia. (Luka 2:46) Je, mtoto wako anapenda kuhudhuria na kushiriki mikutano? (Zab. 122:1) Je, ana hamu ya kusoma Biblia kwa ukawaida na kujifunza kibinafsi?—Mt. 4:4.
Mtoto anayefanya maendeleo ili astahili kubatizwa hujitahidi kutanguliza Ufalme. (Mt. 6:33) Anatambua jukumu lake la kuwaambia wengine kuhusu imani yake. Anashiriki namna mbalimbali za huduma naye haogopi kuwaeleza walimu na wanafunzi wenzake kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Anachukua kwa uzito migawo yake katika Mkutano wa Huduma na Maisha.
Pia, atajitahidi kudumisha usafi wa maadili kwa kuepuka mashirika mabaya. (Met. 13:20; 1 Kor. 15:33) Jambo hilo litadhihirika wazi kupitia muziki anaopenda, sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya video, na matumizi yake ya Intaneti.
Watoto wengi wameunga mkono bidii na jitihada za wazazi wao kwa kufanya kweli iwe mali yao, na kustahili kubatizwa wakiwa bado wachanga. Yehova na awabariki mnapowasaidia watoto wenu kufikia hatua hiyo muhimu sana katika uhusiano wao pamoja naye.
Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa:
Kuwa mhubiri wa kutaniko ambaye hajabatizwa ni pendeleo. Unastahili pongezi kwa sababu ya maendeleo ya kiroho uliyofanya. Umemjua Mungu kwa kujifunza Neno lake na kuamini ahadi zake.—Yoh. 17:3; Ebr. 11:6.
Huenda ulishirikiana kwa njia fulani au hukuwa mwamini wa dini nyingine kabla ya kuanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Labda ulifanya mambo fulani yasiyopatana na kanuni za Biblia. Hata hivyo, sasa umeonyesha imani yako kwa kutubu, yaani, umesikitishwa sana na dhambi ulizofanya wakati uliopita na umegeuka, yaani, umekataa mwenendo usiofaa na umeazimia kufanya yaliyo sawa machoni pa Mungu.—Mdo. 3:19.
Au huenda umeyajua maandishi matakatifu “tangu utoto mchanga.” Kwa sababu hiyo, umelindwa dhidi ya mwenendo usio wa Kikristo na dhambi nzito. (2 Tim. 3:15) Umejifunza kupambana na vishawishi kutoka kwa marafiki na vishawishi vingine vya kufanya mambo yanayomchukiza Yehova. Umeonyesha imani kwa kuunga mkono ibada ya kweli na kuwaeleza wengine mambo unayoamini. Umezoezwa huduma ya Kikristo. Sasa umeamua mwenyewe kumtumikia Yehova ukiwa mhubiri ambaye hajabatizwa.
Vyovyote vile, iwe ulijifunza njia za Yehova tangu utotoni au ulimjua Yehova baadaye maishani, huenda sasa unafikiria kupiga hatua nyingine mbili katika maendeleo yako ya kiroho, yaani, kujiweka wakfu na kubatizwa. Unajiweka wakfu kwa Yehova kwa kusali na kumjulisha kwamba umeamua mwenyewe kumtumikia yeye peke yake milele. (Mt. 16:24) Kisha, unaonyesha kwamba umejiweka wakfu kwa kubatizwa katika maji. (Mt. 28:19, 20) Unapojiweka wakfu na kubatizwa, unakuwa mhudumu aliyewekwa rasmi wa Yehova Mungu. Hilo ni pendeleo kubwa!
Hata hivyo, kama ulivyojifunza katika Biblia, huenda ukakabili changamoto mbalimbali. Kumbuka kwamba muda mfupi baada ya kubatizwa, ‘Yesu aliongozwa na roho kuingia nyikani ili kujaribiwa na Ibilisi.’ (Mt. 4:1) Baada ya kubatizwa na kuwa mwanafunzi wa Kristo, huenda ukapatwa na majaribu ya namna mbalimbali. (Yoh. 15:20) Unaweza kupingwa na watu wa familia. (Mt. 10:36) Huenda ukadhihakiwa na wanashule wenzako, wafanyakazi wenzako, au rafiki zako wa zamani. Sikuzote kumbuka maneno ya Yesu katika Marko 10:29, 30: “Kwa kweli ninawaambia, hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso—na katika mfumo wa mambo unaokuja, uzima wa milele.” Hivyo, endelea kujitahidi kukaa karibu na Yehova na kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu.
Ukitaka kubatizwa, mjulishe mratibu wa baraza la wazee. Wazee watatumia maswali yaliyo kwenye kurasa zinazofuata habari hii wanapozungumza nawe ili kuona ikiwa unastahili kubatizwa. Unaweza kuanza kupitia maswali haya katika funzo lako la kibinafsi la kawaida.
Unapojitayarisha kwa ajili ya mazungumzo hayo, tenga wakati wa kusoma na kutafakari Maandiko yaliyotajwa au kunukuliwa. Unaweza kuandika maelezo yako katika kitabu hiki au mahali pengine. Unaweza kutumia maelezo hayo pamoja na kitabu hiki utakapokuwa ukizungumza na wazee. Ukishindwa kuelewa swali lolote, usisite kumwomba yule anayekufundisha Biblia au mzee yeyote akusaidie.
Utakapokuwa ukizungumza na wazee, usihisi kwamba unahitaji kujibu maswali haya kwa kutoa maelezo marefu yenye mambo mengi. Jibu rahisi, la moja kwa moja na kwa maneno yako mwenyewe litafaa. Kwa maswali yaliyo mengi, ingefaa kurejelea andiko moja au mawili yanayoonyesha msingi wa Kimaandiko wa jibu lako.
Ikiwa bado hujapata ujuzi wa kutosha wa mafundisho ya msingi ya Biblia, wazee watapanga upate msaada ili uweze kuyafahamu Maandiko vizuri na kuyaeleza kwa maneno yako mwenyewe ili ustahili kubatizwa wakati mwingine.
[Taarifa kwa wazee wa kutaniko: Maagizo kuhusu mazungumzo pamoja na wale wanaotaka kubatizwa yanapatikana kwenye ukurasa wa 208-212.]