MASWALI KWA AJILI YA WALE WANAOTAKA KUBATIZWA
Mazungumzo ya Kumalizia Pamoja na Wale Wanaotaka Kubatizwa
Kwa kawaida, ubatizo hufanywa kwenye makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Mwishoni mwa hotuba ya ubatizo, msemaji atawaomba wale wanaotaka kubatizwa wasimame na kujibu maswali mawili yafuatayo kwa sauti inayosikika waziwazi:
1. Je, umetubu dhambi zako, ukajiweka wakfu kwa Yehova, na kukubali njia yake ya wokovu kupitia Yesu Kristo?
2. Je, unaelewa kwamba ubatizo wako unakutambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayeshirikiana na tengenezo la Yehova?
Kujibu maswali hayo ni “tangazo la hadharani” la kwamba wale wanaotaka kubatizwa wana imani katika fidia na kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova kwa moyo wote. (Rom. 10:9, 10) Wale wanaotaka kubatizwa wanapaswa kusali na kufikiria kwa uzito maswali hayo mapema ili waweze kujibu kupatana na usadikisho wao.
Je, umejiweka wakfu kwa Yehova kupitia sala, ukimwahidi kwamba utamwabudu yeye peke yake na kwamba jambo kuu zaidi maishani mwako litakuwa kufanya mapenzi yake?
Je, unaamini kabisa kwamba unastahili kubatizwa kwenye kusanyiko lijalo?
Ni mavazi gani yanayofaa wakati wa ubatizo? (1 Tim. 2:9, 10; Yoh. 15:19; Flp. 1:10)
Tunapaswa kuvalia kwa “kiasi na utimamu wa akili” ili kuonyesha kwamba ‘tunamtumikia Mungu.’ Hivyo, wale wanaobatizwa hawapaswi kuvaa mavazi ya kuogelea yanayoonyesha sehemu za mwili au mavazi yenye maandishi au matangazo ya biashara. Wanapaswa kuvalia kwa njia nadhifu, safi, inayofaa, na inayoonyesha heshima kwa ajili ya pindi hiyo.
Mtu anapaswa kujiendeshaje anapobatizwa? (Luka 3:21, 22)
Wakristo leo wanapaswa kuiga jinsi Yesu alivyofanya alipobatizwa. Alitambua kwamba ubatizo ni hatua nzito, naye alionyesha hivyo kwa mtazamo na matendo yake. Kwa hiyo, eneo la ubatizo si mahali pa kufanyia utani, kucheza, kuogelea, au kufanya mambo mengine ambayo yanaweza kupunguza uzito wa pindi hiyo; wala Mkristo mpya hapaswi kusisimuka kana kwamba amepata ushindi mkubwa. Ijapokuwa ubatizo ni pindi ya shangwe, shangwe hiyo inapaswa kuonyeshwa kwa heshima.
Kuhudhuria mikutano na kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko kutakusaidiaje kutimiza wakfu wako kwa Yehova?
Baada ya kubatizwa, kwa nini ni muhimu kudumisha ratiba nzuri ya kujifunza kibinafsi na kushiriki kwa ukawaida katika huduma?
MAAGIZO KWA WAZEE WA KUTANIKO
Mhubiri ambaye hajabatizwa anaposema kwamba anataka kubatizwa, anapaswa kutiwa moyo apitie kwa makini “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” yaliyo kwenye ukurasa wa 185-207 wa kitabu hiki. Anapaswa kuelekezwa kwenye sehemu yenye kichwa, “Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa,” kuanzia ukurasa wa 182, inayoeleza jinsi anavyoweza kujitayarisha kwa ajili ya mazungumzo hayo pamoja na wazee. Yule anayetaka kubatizwa anaweza kutumia maandishi aliyoandika mahali pengine na anaweza pia kufungua kitabu hiki wakati wa mazungumzo hayo. Hata hivyo, hakuna haja ya mtu mwingine kupitia maswali hayo pamoja naye kabla ya kukutana na wazee.
Yeyote anayetaka kubatizwa anapaswa kumjulisha mratibu wa baraza la wazee. Baada ya mtu anayetaka kubatizwa kupitia “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” mratibu wa baraza la wazee atamuuliza ikiwa amejiweka wakfu kwa Yehova kupitia sala ili kufanya mapenzi Yake. Ikiwa mtu huyo amejiweka wakfu, mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili wazungumzie pamoja naye “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa.” Kila sehemu itashughulikiwa na mzee mmoja. Si lazima kusubiri mpaka tarehe ya kusanyiko itangazwe ndipo mazungumzo hayo yafanywe.
Kwa kawaida, sehemu hizo mbili zinaweza kuzungumziwa katika vikao viwili vya saa moja hivi kila kimoja, ingawa si vibaya kutumia muda zaidi ikiwa inahitajika. Kila sehemu inapaswa kuanza na kumalizika kwa sala. Yule anayetaka kubatizwa wala wazee hawapaswi kuwa na haraka wanapopitia maswali hayo. Wazee waliopewa mgawo huo wanapaswa kuhakikisha kwamba mazungumzo hayo yanapewa kipaumbele katika ratiba zao.
Kwa kawaida, ingefaa kupitia maswali pamoja na kila mtu anayetaka kubatizwa akiwa peke yake, wala si wakiwa kikundi. Anayetaka kubatizwa akitoa maelezo katika kila swali, wazee wataelewa vizuri kina cha ufahamu wake, na kuhakikisha kabisa ikiwa anastahili kubatizwa. Pia, huenda yule anayeomba kubatizwa akawa huru zaidi kutoa maelezo akiwa peke yake. Mume na mke wanaweza kupitia maswali hayo pamoja.
Ikiwa yule anayetaka kubatizwa ni dada, mazungumzo hayo yanapaswa kufanywa mahali ambapo mzee na dada huyo hawatakuwa peke yao. Ikiwa ni muhimu kwenda na mtu mwingine, itafaa awe mzee au mtumishi wa huduma, ikitegemea sehemu wanayopitia kama inavyoonyeshwa katika fungu linalofuata.
Katika makutaniko ambayo hakuna wazee wa kutosha, watumishi wa huduma wanaostahili wenye utambuzi na uwezo wa kufanya uamuzi mzuri wanaweza kutumiwa kupitia maswali ya ubatizo katika “Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo.” Ni wazee tu wanaopaswa kushughulikia “Sehemu ya 2: Maisha ya Kikristo.” Ikiwa kutaniko halina ndugu wa kutosha wanaostahili, mnaweza kuwasiliana na mwangalizi wa mzunguko ili aamue ikiwa wazee wa kutaniko la karibu wanaweza kusaidia.
Ikiwa anayetaka kubatizwa ni mtoto, mzazi au wazazi wake ambao ni Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwepo wakati wa mazungumzo ya maswali ya ubatizo. Ikiwa mzazi au wazazi hawataweza kuhudhuria, wazee wawili (au mzee na mtumishi wa huduma, ikitegemea sehemu wanayozungumzia) wanapaswa kuwepo katika kila sehemu ya mazungumzo hayo.
Wazee watahakikisha kwamba mtu anayetaka kubatizwa anaelewa vya kutosha mafundisho ya msingi ya Biblia. Pia, watajitahidi kuthibitisha ikiwa mtu anayetaka kubatizwa anaithamini sana kweli na anaheshimu ifaavyo tengenezo la Yehova. Ikiwa mtu huyo haelewi mafundisho ya msingi ya Biblia, wazee watapanga asaidiwe kibinafsi ili astahili kubatizwa wakati mwingine. Huenda wengine wakahitaji kupewa wakati zaidi ili wathamini zaidi utumishi wa shambani au waonyeshe ujitiisho chini ya mipango ya kitengenezo. Wazee watatumia hekima kuamua jinsi watakavyotumia muda huo wa saa moja hivi katika kila sehemu ili wajue vizuri ikiwa mtu huyo yuko tayari kwa ajili ya ubatizo. Ingawa muda zaidi unaweza kutumiwa katika maswali fulani na maswali mengine yakachukua muda mfupi, maswali yote yanapaswa kuzungumziwa.
Wazee waliopewa mgawo wa kupitia maswali na anayetaka kubatizwa watakutana baada ya kikao cha pili na kuamua ikiwa mtu huyo anapaswa kubatizwa au la. Wazee wanapaswa kuzingatia malezi, uwezo, na hali nyingine za kila mmoja anayetaka kubatizwa. Tunapendezwa hasa na wale ambao wameanza kusitawisha upendo kumwelekea Yehova na wanaoelewa kweli za msingi za Biblia. Mkiwasaidia kwa upendo, wale wanaobatizwa watakuwa wametayarishwa vya kutosha ili watimize mgawo wao muhimu wakiwa wahudumu wa habari njema.
Baadaye, mzee mmoja au wote wawili waliopewa mgawo wa kuzungumza naye wanapaswa kukutana na mtu huyo na kumjulisha ikiwa anastahili kubatizwa au la. Ikiwa anastahili kubatizwa, wazee watapitia pamoja naye habari yenye kichwa “Mazungumzo ya Kumalizia Pamoja na Wale Wanaotaka Kubatizwa,” iliyo kwenye ukurasa wa 206-207. Ikiwa hajamaliza kujifunza kitabu Furahia Maisha Milele!, wazee wamtie moyo kumalizia baada ya ubatizo. Watamwambia yule anayetaka kubatizwa kwamba tarehe yake ya ubatizo itaandikwa kwenye Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri iliyo na jina lake. Watamkumbusha kwamba wazee hukusanya taarifa hizo za kibinafsi kutoka kwa mhubiri ili tengenezo liweze kushughulikia utendaji wa kidini wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote na ili mhubiri ashiriki katika shughuli za kiroho na kupokea msaada wa kiroho. Zaidi ya hilo, wazee wanaweza kuwakumbusha wahubiri wapya kwamba taarifa zozote za kibinafsi hushughulikiwa kulingana na Sera ya Mashahidi wa Yehova ya Kulinda Taarifa Ulimwenguni Pote inayopatikana kwenye tovuti ya jw.org. Mazungumzo hayo yasizidi dakika kumi.
Mwaka mmoja baada ya mhubiri kubatizwa, wazee wawili wanapaswa kukutana naye ili kumtia moyo na kumpa mapendekezo yatakayomsaidia. Mzee mmoja anapaswa kuwa mwangalizi wa kikundi cha utumishi cha mhubiri huyo. Ikiwa mhubiri huyo ni mtoto, wazazi au mzazi wake Mkristo anapaswa kuwepo. Kikao hicho kinapaswa kuwa chenye uchangamfu na kujenga. Wazee watazungumzia maendeleo yake ya kiroho na kumpa madokezo ya jinsi anavyoweza kuendelea kuwa na ratiba nzuri ya funzo la kibinafsi na usomaji wa Biblia kila siku, ibada ya familia ya kila juma, kuhudhuria na kushiriki mikutano kwa uaminifu, na kushiriki utumishi wa shambani kila juma. (Efe. 5:15, 16) Ikiwa hajamaliza kujifunza kitabu Furahia Maisha Milele! wazee wanapaswa kufanya mipango ili mhubiri fulani amsaidie kumalizia. Wazee wanapaswa kumpongeza kwa upendo. Kwa kawaida, shauri au pendekezo moja au mawili yanatosha.