Sanduku La Swali
◼ Kabla ya mhubiri kukubaliwa kubatizwa, anapaswa kuwa amehudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki katika huduma ya shambani kwa kadiri gani?
Uamuzi muhimu zaidi ambao mtu anaweza kufanya ni kubatizwa. Kwa hiyo, kabla ya mtu kukubaliwa kubatizwa, anapaswa kuwa anaelewa vya kutosha mambo ambayo Mungu anataka atimize. Kwa kuongezea, anapaswa kuwa tayari ameonyesha azimio lake la kuishi kupatana na matakwa ya Mungu.
Wakristo wameamriwa wasipuuze kukusanyika pamoja, kwa hiyo mhubiri ambaye hajabatizwa anapaswa kuwa tayari anahudhuria mikutano ya kutaniko kwa bidii. (Ebr. 10:24, 25) Pia, awe na kawaida ya kutoa maelezo kwenye mikutano. Kuna uwezekano kwamba atakuwa amejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ingawa hilo si takwa.
Isitoshe, kwa kuwa Wakristo wamepewa utume wa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi, mhubiri ambaye hajabatizwa anapaswa kuwa anashiriki kwa ukawaida katika huduma kabla ya kubatizwa. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Anapaswa kuwa amehubiri kwa miezi mingapi kabla hajabatizwa? Inafaa muda wa kutosha upite ili athibitishe kwamba yeye ni mhubiri mwenye bidii aliyeazimia kushiriki kwa ukawaida katika huduma mwezi baada ya mwezi. (Zab. 78:37) Hata hivyo, si lazima muda mrefu sana upite kuanzia wakati anapoanza kuhubiri hadi kufikia wakati anapostahili kubatizwa, huenda kipindi cha miezi michache tu kikatosha. Anapaswa kuwa anahubiri kiwango gani cha wakati kila mwezi? Hakuna sheria kuhusiana na hilo. Wazee wanapaswa kuzingatia hali za pekee za kila mhubiri na wanapaswa kuwa na usawaziko na wenye kiasi.—Luka 21:1-4.
Wazee (au watumishi wa huduma katika makutaniko yenye wazee wachache sana) wanaokutana na mhubiri anayetaka kubatizwa wanapaswa kukumbuka kwamba kila mtu ni tofauti, na wanapaswa kutumia utambuzi kuamua ikiwa anastahili kubatizwa au la. Watatarajia kwamba mhubiri huyo anatamani kwelikweli kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kwamba anathamini pendeleo la kushirikiana na tengenezo la Yehova na kushiriki katika huduma. Wazee wanaelewa kwamba hajakomaa kiroho na hana ustadi kama ule wa wahubiri wenye uzoefu ambao wamebatizwa. Wazee wakihisi kwamba mhubiri huyo hastahili kubatizwa, wanapaswa kumjulisha kwa fadhili sababu za Kimaandiko za uamuzi waliofikia na kumsaidia apate msaada wa kiroho.