Sanduku la Swali
● Kabla ya kukubaliwa kwa ubatizo, ni kwa kadiri gani mhubiri asiyebatizwa apaswa kuwa akishiriki katika huduma ya shambani?
Mtu anayestahili kuwa mhubiri asiyebatizwa tayari amedhihirisha kwa njia mbalimblali tamanio lake lenye nguvu la kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. (Zab. 110:3) Funzo la bidii la Maandiko limetokeza badiliko katika kufikiri, mtazamo, na njia yake ya maisha. Kwa kuchochewa na tamanio la moyoni la kupendeza Yehova na kufanya mapenzi Yake, mwanafunzi huyo wa Biblia mwenye kuchukua mambo kwa uzito hushirikiana kwa ukawaida na watu wa Yehova kwenye mikutano ya kundi, makusanyiko, na mikusanyiko. (Ebr. 10:24, 25) Zaidi ya hudhurio la kawaida kwenye makongamano hayo ya Kikristo, yaelekea pia amekwisha sukumwa kutoka moyoni afanye tangazo rasmi la hadharani la imani yake kwa kutoa maelezo kwenye mikutano, na yawezekana amejiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.—Zab. 40:9, 10; omSW uku. 73.
Mwanafunzi wa Biblia akiisha kukubali ukweli na kuonyesha anathamani kikweli thamani ya ujumbe wa Ufalme, huenda akapata pendeleo la kushiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Hiyo ndiyo kazi ya msingi ya Mashahidi wa Yehova. (Mt. 24:14; 28:19, 20; omSW uku. 111) Katika habari hiyo, mhubiri anayeongoza funzo na wazee wana daraka zito la kuhakikisha kwamba maisha yote ya mwanafunzi huyo yanapatana na kanuni za Kikristo. Lazima yeye awe na tamanio halisi la kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na athamini pendeleo la kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi.—Gal. 6:6; wSW88 11/15 uku. 17; omSW kur. 98-9, 174.
Haihitaji kuwa muda mrefu sana tangu wakati mwanafunzi wa Biblia anastahili kushiriki pamoja nasi katika huduma hadi anapoweza kujitoa mwenyewe kwa ajili ya ubatizo wa maji. Kufikia sasa mwendo wake wa maisha tayari unapatana kikamili na kanuni za Kikristo, lakini yeye hana ujuzi katika huduma ya peupe. Apaswa kupewa wakati wa kutosha adhihirishe kwamba ameazimia kwa imara kuwa na ushiriki wa kawaida na wenye bidii katika huduma ya shambani.—Zab. 40:8; Rum. 10:9, 10, 14, 15.
Kufikia wakati ambao mtu yuko tayari kwa ajili ya ubatizo, yaelekea sana atakuwa anashiriki kwa ukawaida habari njema pamoja na wengine, akitumia zaidi ya saa moja tu au mbili katika utumishi wa shambani kila mwezi. (wSW84 11/1 uku. 8 fu. 2) Bila shaka, mambo ya kibinafsi ya kila anayeomba ubatizo yapasa kupitiwa, ikifikiriwa malezi, umri, vizuizi, na kadhalika. Wazee watataka kuongozwa na mwelekezo unaotolewa kwao kwenye ukurasa 175 wa kitabu Huduma Yetu: “Tunapendezwa na wale ambao mioyo yao inaelekezwa kwa Yehova na ambao wamezifahamu kweli za msingi za Biblia. Kwa msaada wenu wa upendo, wale wanaobatizwa watatiwa moyo na kusaidiwa waingie katika huduma ya Kikristo, wakiwa wametayarishwa vya kutosha watimize mgawo huo wa maana.”—Mt. 16:24; Yn. 4:34; 1 Pet. 2:21.