Kutangaza Habari Njema—Tukiwa Familia
1 Familia iliyo wakfu inayoshiriki kikamili katika utumishi mtakatifu—pamoja na baba, mama, na watoto wanaotumikia Mungu kwa nafsi yote—ni sifa kwa jina kuu la Yehova. Tuna furaha kwamba familia nyingi za jinsi hiyo zapatikana katika makundi ya watu wa Yehova duniani pote.
2 Bila shaka, baba ndiye mwenye daraka la kwanza la kutunza mahitaji ya kiroho ya familia yake. (1 Kor. 11:3) Kwa ushirikiano wa mke na watoto wake, familia yake yaweza kuwa na uvutano mkubwa juu ya wengine. (Mt. 5:16) Ni yapi baadhi ya maeneo ambayo ushirikiano huo waweza kudhihirishwa?
WAZAZI ONGOZENI
3 Katika visa vingi, baba aweza kuwa ni mzee au mtumishi wa huduma. Hiyo yamaanisha kwamba kuongezea masilahi yake kwa familia yake, baadhi ya wakati na uangalifu wake lazima upewe mambo ya kundi. Daraka la baba ni kuhakikisha kwamba wakati uliopo unagawanywa ili kwamba familia yake isipuuzwe. Huenda hilo lisiwe rahisi sikuzote kwa sababu ya matakwa yaliyopo kwa wakati wake mchache. Lakini kwa sababu familia yake ndiyo daraka lake la kwanza, yeye apaswa kuratibu kwa ukawaida baadhi ya wakati wake wenye thamani kuwa pamoja na familia yake katika funzo, katika utumishi wa shambani, kwenye mikutano, na katika tafrija inayofaa. Mambo na madaraka mengine huenda yakabadili ratiba ya baba pindi kwa pindi, lakini jinsi inavyothawabisha wakati awezapo kutumia wakati kila mwezi katika utumishi wa shambani pamoja na washiriki wa familia yake!
4 Ushirikiano kutoka kwa mke ni wa muhimu. Yeye aweza kukamilisha mume wake katika njia ya maana sana kwa kusaidia kuzoeza watoto katika huduma. Bidii na ujitoaji wake ulio kielelezo vitatimiza mengi katika kuvutia watoto wakue katika uthamini wao wa huduma.—2 Tim. 3:14, 15.
5 Kuna vielelezo vingi vizuri vya hali ambazo katika hizo mzazi mmoja alichukua mzigo wa daraka la kiroho na kuzoeza kwa kufanikiwa watoto katika huduma. Kwa sababu ya kielelezo bora cha mama au baba yao, vijana wengi wamechukua msimamo imara kwa ajili ya ukweli, hata kuchukua huduma ya wakati wote.
DARAKA LA WATOTO
6 Vipi daraka la watoto? Hata Mwana mkamilifu wa Mungu, Yesu, alipokuwa angali mtoto mchanga alipaswa kuwa chini ya mwelekezo na maagizo ya wazazi wake. (Luka 2:51) Kwa hiyo, wakati baba na mama wanapopanga familia itumie wakati pamoja katika huduma, ni wajibu wa watoto kuonyesha ujitoaji kimungu wao kwa kushirikiana na wazazi wao.—Efe. 6:1-3.
7 Kuabudu pamoja wakiwa familia—kujifunza, kushiriki katika huduma ya shambani, na kuhudhuria mikutano—hutia nguvu kifungo cha upendo na umoja katika kifungo cha familia. Wazazi na watoto hushiriki daraka katika jambo hilo.