Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • it uku. 211
  • Kufunika Dhambi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kufunika Dhambi
  • Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Kwa Nini Tunathamini Msamaha wa Yehova?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Siku ya Upatanisho (Atonement Day)
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Dhambi
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Je, Unathamini Yale Ambayo Yehova Amefanya Ili Kukukomboa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Ufahamu wa Kina wa Maandiko
it uku. 211

KUFUNIKA DHAMBI

Maneno haya ya Kiswahili “kufunika dhambi” yanatokana na neno “funika” na linapotumiwa katika Biblia linamaanisha kufunika dhambi. Katika Maandiko ya Kiebrania maneno yanayohusiana na kufunika dhambi yanatokea mara nyingi, hasa katika vitabu vya Mambo ya Walawi na Hesabu. Ka·pharʹ ni neno la Kiebrania kwa ajili ya kufanya kufunika dhambi, na huenda kiasili lilimaanisha “funika,” ingawa neno “futa” limependekezwa pia.

Uhitaji wa Mwanadamu wa Kufunika Dhambi. Kwa sababu ya dhambi aliyorithi, mwanadamu anahitaji kitu cha kufunika dhambi (1Fa 8:46; Zb 51:5; Mhu 7:20; Ro 3:23), na wajibu huo upo juu ya mwanadamu mwenyewe, si wa Mungu. (Kum 32:4, 5) Adamu, aliyepoteza uzima wa milele na ukamilifu wa wanadamu alileta dhambi na kifo (Ro 5:12), na hivyo wazao wa Adamu wakaja kuwa chini ya laana ya kifo. Ikiwa wanadamu wangerudishiwa nafasi ya kufurahia uhai mkamilifu, basi, upatanisho unaolingana ungehitajiwa kwa kile ambacho Adamu alipoteza kulingana na kanuni ya kisheria ambayo baadaye Yehova aliiweka kwenye Sheria ya Musa, yaani, uhai unapaswa kulipiwa kwa uhai.​—Kum 19:21.

Kulingana na jinsi maneno “kufunika dhambi” yanavyotumiwa kwenye Biblia, kimsingi yanatokeza wazo la “kufunika” au “kubadilishana,” na kile kinachotolewa kwa ajili ya kubadilishana, au kama “kifuniko” cha, kitu kingine kinapaswa kulingana kabisa. Kwa hiyo, kitu chochote kinachotolewa ili kulipia kile kilichopotea au kuharibiwa kinapaswa kuwa na “upatano” na kile kilichopotea, kikikifunika vilivyo na kulingana kabisa. Hakupaswi kuwa na ziada au upungufu wowote. Hakuna mwanadamu asiyekamilika ambaye angeweza kutoa kifuniko cha aina hiyo ili kumrudishia uhai mkamilifu mwanadamu mmoja au wote. (Zb 49:7, 8) Ili kufunika dhambi kabisa kwa sababu ya kile ambacho Adamu alichopoteza, toleo la dhambi lililokuwa na thamani ileile ya uhai mkamilifu wa kibinadamu lilipaswa kutolewa.

Yehova Mungu alianzisha mpango wa kufunika dhambi kati ya Waisraeli ambao ulifananisha uandalizi mkubwa zaidi wa kufunika dhambi. Si mwanadamu, bali ni Yehova anayeweza kuamua na kufunua njia ya kufunika ile dhambi tuliyorithi na kutoa kitulizo kutokana na matokeo ya laana ya kifo.

Dhabihu za Kufunika Dhambi. Kama Mungu alivyoagiza, Waisraeli walipaswa kutoa dhabihu kama matoleo ya dhambi ili kufunika dhambi. (Kut 29:36; Law 4:20) Dhabihu yenye kutokeza zaidi ilitolewa Siku ya Kufunika Dhambi, ambapo kuhani mkuu wa Israeli alitoa dhabihu za wanyama na kufanya upatanisho kwa ajili yake mwenyewe, kwa ajili ya Walawi wengine, na kwa ajili ya makabila yasiyokuwa ya kikuhani ya Israeli. (Law 16) Wanyama waliotolewa kama dhabihu walipaswa kutokuwa na kasoro yoyote, kuashiria umuhimu wa ukamilifu kwa upande wa ufananisho waliotoa. Pia, ukweli wa kwamba kufunika dhambi kunagharimu sana unaonyeshwa pale uhai wa kiumbe unapotolewa, damu yake ikimwagwa ili kufunika dhambi. (Law 17:11) Bila shaka, dhabihu za dhambi zilizotolewa na Waisraeli na baadhi ya mambo yaliyotendeka kwenye Siku ya Kufunika Dhambi ya kila mwaka yalikazia akilini mwao jinsi walivyokuwa watenda dhambi na uhitaji wao mkubwa wa kufunika dhambi kabisa. Hata hivyo, dhabihu za wanyama hazingeweza kufunika kabisa dhambi za mwanadamu, ambaye alipewa mamlaka ya kuwatawala.​—Mwa 1:28; Zb 8:4-8; Ebr 10:1-4; ona SIKU YA KUFUNIKA DHAMBI; DHABIHU//MATOLEO.

Utimizo kwa Yesu Kristo. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanahusianisha moja kwa moja kufunikwa kwa dhambi na Yesu Kristo. Kwa kuwa Yesu ndiye yule ambaye dhabihu mbalimbali za wanyama zilielekeza kwake, alitimiza ufananisho na vivuli vya Sheria ya Musa. Akiwa mwanadamu mkamilifu asiye na dhambi, Yesu alikuwa dhabihu ya dhambi kwa ajili ya wazao wote wa Adamu ambao wanakombolewa kutoka kwenye dhambi waliyorithi pamoja na kifo. (2Ko 5:21) Kristo “alitoa dhabihu moja kwa ajili ya dhambi daima” (Ebr 10:12), na bila shaka yeye ni “Mwanakondoo wa Mungu ambaye huondoa dhambi ya ulimwengu.” (Yoh 1:29, 36; 1Ko 5:7; Ufu 5:12; 13:8; linganisha Isa 53:7.) Msamaha unategemea kumwagwa kwa damu (Ebr 9:22), na Wakristo ambao wanatembea katika nuru wanahakikishiwa kwamba “damu ya Yesu Mwana [wa Mungu] hutusafisha kutoka katika dhambi yote.”​—1Yo 1:7; Ebr 9:13, 14; Ufu 1:5.

Uhai mkamilifu wa kibinadamu wa Yesu uliotolewa kama dhabihu ni ufananisho wa dhabihu za dhambi. Ni kitu chenye thamani ambacho kinakamilisha kununuliwa kwa wanadamu, kuwakomboa kutokana na dhambi waliyorithi pamoja na kifo. (Tit 2:13, 14; Ebr 2:9) Yesu mwenyewe alithibitisha hivi: “Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa uhai wake uwe fidia badala ya wengi.” (Mk 10:45; ona FIDIA.) Dhabihu yake ilifunika kile ambacho kihalisi kilipotezwa na Adamu mwenye dhambi, na kwa kuwa Yesu alikuwa mkamilifu basi alilingana kabisa na Adamu kabla hajatenda dhambi.​—1Ti 2:5, 6; Efe 1:7.

Upatanisho wawezekana. Dhambi ilisababisha utengano kati ya Mungu na mwanadamu, kwa kuwa Yehova hapendezwi na dhambi. Ufa huo kati ya mwanadamu na Muumba wake ungeweza kuzibwa kupitia tu kutimizwa kwa uhitaji wa “kifuniko” cha kweli, au kufunikwa kwa dhambi hiyo. (Isa 59:2; Hab 1:13; Efe 2:3) Lakini, Yehova Mungu amefanya upatanisho kati yake na wanadamu wenye dhambi uwezekane kupitia mwanamume mkamilifu Yesu Kristo. Kwa hiyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Tunashangilia katika Mungu kupitia Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kupitia kwake sasa tumepokea upatanisho.” (Ro 5:11; ona UPATANISHO.) Ili tupate kibali cha Yehova, ni lazima tukubali uandalizi wake wa upatanisho kupitia Yesu Kristo. Ni kupitia uandalizi huo tu ndipo tunapoweza kufikia ile hali ambayo Adamu alikuwa nayo kabla hajatenda dhambi. Upendo wa Mungu unaonekana kwa kufanya mpango kwa ajili ya upatanisho kama huo.​—Ro 5:6-10.

Haki yatimizwa kupitia upatanisho. Bado, haki ilihitaji kutimizwa. Ingawa mwanadamu aliumbwa akiwa mkamilifu, alipoteza ukamilifu kupitia dhambi na hivyo basi Adamu na wazao wake wakawa chini ya laana ya Mungu. Sifa ya haki na uaminifu kwa viwango vya uadilifu zilifanya iwe lazima kwa Mungu kutekeleza hukumu iliyotokana na sheria yake dhidi ya Adamu aliyekosa kutii. Hata hivyo, upendo ulimchochea Mungu kuanzisha mpango mwingine ambao kupitia huo haki ingepatikana, na bila kupuuza sehemu nyingine za sifa ya haki, wazao waliotubu wa mwanadamu mwenye dhambi, Adamu, wangeweza kusamehewa na kurudisha amani pamoja na Mungu. (Kol 1:19-23) Kwa hiyo, Yehova “akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.” (1Yo 4:10; Ebr 2:17) Upatanisho ni kitu kinachotuliza au kufaa. Dhabihu ya Yesu ya upatanisho inaondoa sababu ya Mungu ya kuwalaani viumbe wa kibinadamu na inafanya iwezekane kwa mwanadamu kupata kibali na rehema za Mungu. Upatanisho huo unaondoa adhabu ya dhambi na matokeo ambayo ni laana ya kifo kwa Waisraeli wa kiroho na wengine wote wanaonufaika nayo.​—1Yo 2:1, 2; Ro 6:23.

Wazo la mmoja kuwa badala ya wengine linaonekana mara nyingi kwenye mistari ya Biblia inayohusiana na kufunika dhambi. Kwa mfano, Paulo alisema kwamba “Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu kulingana na Maandiko” (1Ko 15:3), na kwamba “Kristo alitununua, akatuweka huru kutoka katika laana ya Sheria akawa laana badala yetu, kwa sababu imeandikwa: ‘Amelaaniwa kila mtu aliyetundikwa kwenye mti.’” (Gal 3:13; Kum 21:23) Petro alieleza hivi: “Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tufe kuhusiana na dhambi na tuishi kuhusiana na uadilifu. Na ‘kwa vidonda vyake mliponywa.’” (1Pe 2:24; Isa 53:5) Petro aliandika hivi pia: “Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kwa ajili ya dhambi, mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu, ili awaongoze ninyi kwa Mungu.”​—1Pe 3:18.

Uandalizi wa upendo watokeza uwajibikaji kupitia imani. Yehova na Kristo wameonyesha upendo kuhusiana na uandalizi wa kufunika daima dhambi ilizorithiwa na wanadamu. (Yoh 3:16; Ro 8:32; 1Yo 3:16) Hata hivyo, ni lazima mtu atubu kikweli na kuonyesha imani ili mtu anufaike na uandalizi huo. Yehova hakupendezwa na dhabihu za taifa la Yuda wakati walipozitoa wakiwa na mtazamo usiofaa. (Isa 1:10-17) Mungu alimtuma Kristo awe “dhabihu ya upatanisho kupitia imani katika damu yake.” (Ro 3:21-26) Wale ambao kwa imani wanaukubali uandalizi wa Mungu kwa ajili ya kufunika dhambi kupitia Yesu Kristo wanaweza kupata ukombozi; wale ambao wanaukataa hawawezi kupata ukombozi. (Mdo 4:12) Na kwa yeyote “[anayeendelea] kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi wa kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi, bali kuna tarajio hakika linaloogopesha.”​—Ebr 10:26-31.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki