HATIA YA DAMU
Nyakati nyingine neno “damu” katika Kiebrania (dam; wingi, da·mimʹ) hurejelea hatia inayotokana na kumwaga damu isiyo na hatia na hivyo hutafsiriwa kuwa “hatia ya damu.”—Kut 22:2.
“Mikono inayomwaga damu isiyo na hatia” ni kati ya vitu vinavyomchukiza sana Yehova tangu damu ya Abeli mwadilifu ilipomlilia kwa sauti kutoka ardhini. (Met 6:16, 17; Mwa 4:10; Zb 5:6) Pia, kwa muda mrefu wanadamu wametambua utakatifu wa damu; Noa na familia yake walipotoka kwenye safina walijulishwa matokeo mabaya ambayo yangewapata wale ambao wangekuwa na hatia ya damu.—Mwa 9:6; 37:21, 22; 42:22.
Baada ya muda fulani sheria ziliandikwa, zilifafanua makosa yaliyoleta adhabu ya kifo, na hivyo, kila mtu angeepuka mambo ambayo yangemfanya awe na hatia ya damu. Sheria nyingine zilitungwa ili kuwazuia watu wasimwage damu isiyo na hatia. Ukuta ulijengwa kuzunguka ukingo wa paa tambarare la nyumba ili watu wasianguke kutoka kwenye paa. (Kum 22:8) Mtu alipaswa kumfunga ng’ombe dume wake ili asiwapige watu pembe. (Kut 21:29) Ikiwa mwizi angepatikana akivunja nyumba usiku na kuuawa, aliyemuua hangekuwa na hatia ya damu; lakini ikiwa angeuawa mchana, hali ingekuwa tofauti. (Kut 22:2, 3) Majiji ya makimbilio yalitengwa ili kumlinda mtu aliyeua bila kukusudia asiuawe na mlipiza kisasi cha damu. (Hes 35:25; Kum 19:9, 10; Yos 20:2, 3; ona MTU ANAYELIPIZA KISASI CHA DAMU.) Ikiwa Ezekieli hangetimiza mgawo wake akiwa mlinzi wa Israeli, damu ya wakaaji hao ingekuwa juu yake. (Eze 3:18, 20; 33:6, 8) Tukiwa na hilo akilini tunaweza kuelewa mtume Paulo alimaanisha nini aliposema kwamba yeye ni safi kutokana na hatia ya damu.—Mdo 18:6; 20:26.
Biblia inataja watu ambao hawakuwa na hatia ya damu na wale waliokuwa na hatia ya damu, na wote hao ni mifano inayotuonya. Mfano mmoja ni Sauli, ambaye wakati mmoja alijizuia kumuua Daudi na akaepuka hatia ya damu; lakini baadaye Sauli alitenda kwa upumbavu kwa kuwaua Wagibeoni na akailetea familia yake yote hatia ya damu. (1Sa 19:5, 6; 2Sa 21:1) Kuna wengine pia ambao walikuwa na hatia ya damu kwa sababu mbalimbali. (Amu 9:24; 2Sa 1:16; 4:6-12) Kwa upande mwingine, Daudi aliepuka hatia ya damu alipotii onyo la Yehova kupitia Abigaili. (1Sa 25:24-26, 31, 33) Jiji la Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. kwa sababu lilijaa hatia ya damu. (Eze 22:2-4; 23:37, 45) Viongozi wa dini ya uwongo katika siku za Yesu sawa na viongozi katika siku za Yeremia walikuwa na hatia ya damu kwa sababu pindo za nguo zao zilikuwa nyekundu kwa damu ya watumishi waaminifu wa Yehova. (Yer 2:34; Mt 23:35, 36; 27:24, 25; Lu 11:50, 51) Yule “kahaba” mkubwa Babiloni Mkubwa ana hatia kubwa ya damu hivi kwamba anasemwa kuwa amelewa damu ya watu wa Yehova.—Ufu 17:5, 6; 18:24.
Kwa kweli watu hao wenye hatia ya damu hawastahili kuishi hata nusu ya maisha yao, kama Daudi alivyosema. (Zb 55:23) Kama Daudi alivyofanya, sote tunapaswa kusali kwamba Yehova atuokoe kutoka katika hatia ya damu na kutoka kwa watu wenye hatia ya damu. (Zb 51:14; 59:2; 139:19) Kama unabii wa Ufunuo ulivyotabiri, hivi karibuni sauti kubwa ya sifa itapaa kwa Yehova kwa sababu sehemu ya mwisho ya Babiloni Mkubwa itaharibiwa na damu ya watu wasio na hatia italipiziwa kisasi milele.—Ufu 19:1, 2.
Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanataja njia tatu hususa ambazo Mkristo anaweza kuwa na hatia ya damu mbele za Mungu: (1) kwa kumwaga damu, kuua—hilo linaweza kutia ndani wote wanaounga mkono moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja matendo ya shirika lenye hatia ya damu (kama vile Babiloni Mkubwa [Ufu 17:6; 18:2, 4] au mashirika mengine ambayo yamemwaga damu nyingi isiyo na hatia [Ufu 16:5, 6; linganisha Isa 26:20, 21]); (2) kwa kula au kunywa damu kwa njia yoyote ile (Mdo 15:20); na (3) kwa kukataa kuhubiri habari njema ya Ufalme, na hivyo kuwazuia wengine kupata habari hiyo inayookoa uhai.—Mdo 18:6; 20:26, 27; linganisha Eze 33:6-8.