Azimio Letu Imara Juu ya Uhai na Damu
1, 2. Maulizo juu ya damu yanatokea mara kwa mara katika njia gani?
‘HAKIMU Atoa Ruhusa ya Kutia Damu Mishipani’ ndivyo makala (tungo) kuu ya gazeti kutoka Virginia, U. S. A. ilivyotangaza:
“Alhamisi asubuhi hakimu wa wilaya aliiruhusu Portsmouth Naval Hospital kumtia damu mishipani mwanamke ambaye ni mgonjwa mahututi aliyekuwa amekataa siku nne kutiwa damu mishipani kwa kuhatirisha uhai wake, kama ilivyosemekana, . . . ”
2 Ripoti za namna hii zatokea mara kwa mara na kuvuta fikira sana juu ya thamani ya uhai na damu. Kabla ya kuzungumza yaliyotokea katika kisa hiki kinachotajwa hapo juu, na tufikirie maulizo fulani ya msingi: Ni imani gani zenye maana sana zinazoongoza watu kama huyu wakatae kutiwa damu mishipani? Je! Kweli Neno la Mungu linataka jambo hili kutoka kwa Wakristo wote? Ikiwa ndivyo, imani zetu za kidini zingekuwa imara kadiri gani ikiwa daktari (mganga) angesema kwamba tunahitaji kutiwa damu mishipani? Tena, je! kunaweza kuwa na njia nyingine mbali na matumizi ya damu katika matibabu ambazo katika hizo maoni yetu juu ya uhai na damu ni yenye maana na hata yanaweza kuwa na matokeo juu ya wakati wetu ujao?
UZIMA KUTOKANA NA DAMU
3. Kulingana na Ufunuo 7:14, tuna sababu gani ya kuheshimu sana damu?
3 Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha mfano wa kuthamini damu kunakoonyeshwa leo na watu mia elfu nyingi. Baada ya kuona katika njozi wale 144,000 wanaotarajia kuwa warithi wa ufalme wa Kimasihi, mtume Yohana aliona “mkutano mkubwa, . . . watu wa kila taifa,” wanaotarajia kuishi milele katika paradiso ya kidunia itakayorudishwa. Lakini wanadamu wanawezaje kuishi milele, tena bila dhambi na makosa? Kwa kuthamini “mkutano mkubwa” unapasa sauti hivi: “Wokovu una Mungu wetu, . . . na Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo. Wanafahamu kwamba wokovu huu unawezekana kwa sababu tu “wamefua mavazi yao na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Yesu.—Ufu. 7:9, 10, 14.
4, 5. (a) Ni kwa sababu gani maoni yanayofaa juu ya uhai na damu yanahusu zaidi ya kuamini tu? (b) Biblia inaonyeshaje hilo?
4 Kama inavyoonyeshwa katika makala hiyo inayotangulia, kuanzia na kitabu cha kwanza cha Biblia, Mungu alielekeza kwenye dhabihu ambayo ingetolewa kwa kumwagwa kwa damu ya Yesu ili wanadamu wapate uzima wa milele. (Mwa. 3:15; 22:2-10; Isa. 53:10-12) Ingawa dhabihu hiyo ilikuwa ya wakati ujao, Yehova alionyesha waziwazi kwamba waabudu wake wanapaswa kuona uhai na damu kuwa vitu vitakatifu. Tena alitaka kwamba matendo yao yapatane na maoni hayo ya kimungu. Je! mwenendo haukumaanishwa katika yale ambayo Mungu alimwambia Nuhu na jamaa yake alipokuwa akiwaruhusu mara ya kwanza kula nyama? Mungu alisema: “Kila kiendacho kilicho hai kitakuwa chakula chenu, kama nilivyowapa mboga za majani, kadhalika nawapeni hivi vyote. Bali nyama pamoja na uhai, yaani, damu yake, msile.” (Mwa. 9:3, 4) Hivyo ikiwa wangeua mnyama kwa chakula, iliwapasa wachukue hatua kwa makusudi waondoe damu katika mnyama huyo ili damu isiliwe.
5 Hii haikuwa sheria ya vivi hivi ya chakula, maana Mungu aliona ubora sana wa kanuni ya wema na ubaya katika damu: Ile damu ya kiumbe ilifananisha uhai uliotoka kwa Mungu. Tena inafaa kuangaliwa kwamba yeye aliendelea kusema kwamba, ingawa mnyama angeuawa kwa chakula, mwanadamu hangeuawa. Kwa hiyo, ikiwa damu ya mnyama ikifananisha uhai ilionwa kuwa takatifu na haikupaswa kuliwa ili kuendeleza uhai, ni wazi kwamba uhai na damu ya mwanadamu vilipaswa kuonwa kama vitakatifu hata zaidi.—Linganisha Mathayo 6:26.
6, 7. (a) Mwanzo 9:3, 4 inawahusu (inawapasa) nani? (b) Agano la Torati liliungaje mkono takwa katika Mwanzo 9?
6 Kwa kuwa Nuhu ndiye aliyekuwa babu wa wanadamu wote, mwenendo unaopatana na kuona uhai na damu kuwa takatifu ulitakiwa kutoka kwa wanadamu wote. Wanachuo wengi wa Biblia wanakubali ukamatano huu. Kwa mfano:
“Damu ilionwa kuwa chanzo cha uhai, na kwa hiyo ni kitu bora sana . . . Katazo la damu likawa mojawapo la sheria zilizokuwa katika torati ya Musa kuhusu vyakula, lakini baadaye Wayahudi waliliona kuwa linahusu wanadamu wote, kwa sababu lilitiwa ndani ya mipango ya agano hili lililofanywa pamoja na Nuhu.”—A New Catholic Commentary on Holy Scriptures, uku. 187.
7 Kama maelezo ya kitabu hicho yalivyoonyesha, wakati Mungu alipowapa Waisraeli torati baadaye, alikataza pia kula damu. Aliamuru hivi: “Ila ujihadhari kwamba usile damu, kwani ile damu ndiyo uhai; na uhai usile pamoja na nyama. . . . imwage juu ya nchi kama maji.” (Kum. 12:23, 24; Law. 17:10, 13) Wakati huo Mungu hakuifanya sheria yake ya kukataza kula damu iwe lazima kwa wanadamu wote, kama vile asivyofanya sheria yake inayokataza kuabudu sanamu. (Matendo 17:30, 31; 14:16) Kwa hiyo Mataifa wangenunua na kula nyama yenye damu. (Kum. 14:21) Lakini yule anayemwabudu Muumba hangefanya hivyo. Kwa kweli, ikiwa Mwisraeli angekula nyama ambayo haikuwa imeondolewa damu bila kujua, ilimpasa achukue hatua ajitakase na kosa hilo alilolifanya bila kukusudia.—Law. 17:15, 16.
8. Je! ni damu ya wanyama au ni ya wanadamu iliyokatazwa (2 Sam. 23:14-27)
8 Ikiwa damu ya wanyama, inayosimamia uhai, haingeliwa ili kuendeleza uhai, ingekuwa hivyo hata zaidi kuhusu damu ya wanadamu. Tunaweza kuona hili kwa urahisi kutokana na yale yaliyotokea wakati Yesu aliposema kwa njia ya mfano juu ya kula mwili wake na kunywa damu yake. Wengine wa wanafunzi wake Wayahudi wasiofahamu kwamba alikuwa akitumia mfano, walichukizwa wakamwacha. (Yohana 6:60-66) Ndiyo, wazo la kula damu, kwamba ni ya wanyama ama ya wanadamu, lilikuwa lenye kuchukiza sana kwa wale wanaojali maoni ya Mungu.
TAKWA LA KIKRISTO
9. Hilo laweza kuonyeshwaje kwamba linawapasa Wakristo vilevile?
9 Walakini, labda umesikia dai la kwamba katazo la Biblia la kula damu haliwapasi Wakristo. Mambo ya hakika ni yapi? Uamuzi ulifikiwa juu ya jambo hili katika mwaka wa 49 W.K., katika mkutano wa mitume na wazee wengine Wakristo katika Yerusalemu. Kwa kuongozwa na roho takatifu ya Mungu baraza hiyo iliamua kwamba haikuwapasa Wakristo waishike torati ya Musa. Lakini namna gani juu ya mambo ambayo yalikuwa yameonyeshwa kuwa mabaya hata kabla ya Waisraeli kupewa Torati? Baraza hiyo iliyaandikia makundi ya Kikristo hivi:
“Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiongeze mzigo zaidi kwenu ninyi, isipokuwa mambo haya ya lazima, kuendelea kushika mwiko wa vitu vinavyotolewa dhabihu kwa sanamu na wa damu na wa vitu vinavyonyongwa [ili kuiacha damu ndani yao] na wa uasherati.”—Matendo 15:19, 20, 28, 29, NW.
10-12. Ni ushuhuda gani unaoonyesha kwamba Matendo 29 haikuwa amri ya kushikwa kwa kitambo tu?
10 Kama Mtaalam Edward Meyer alivyoeleza katika kitabu Origin and Beginning of Christianitya ile “damu” inayotajwa katika Matendo 15:29 ilikuwa “kuliwa kwa damu iliyokatazwa katika sheria (Mwa. 9:4) iliyopewa Nuhu na vilevile wanadamu wote.” Na ijapokuwa viongozi wengi wa kidini wanadai kwamba ile amri iliyo katika Matendo 15:28, 29 ilitolewa kwa muda tu ili Wayahudi wasiudhike, Mtaalam Meyer anaripoti kwamba zaidi ya karne moja na robo baada ya baraza hiyo ya Yerusalemu, ‘lile katazo la kula damu lilikuwa likifuatwa kwa kawaida’ na Wakristo. Ili athibitishe haya, anataja yaliyotukia mwaka wa 177 W.K. wakati adui wa kidini Ulaya walipowashtaki Wakristo uongo kula vitoto vichanga. Mwanamke moja kijana alijibu shtaka hilo la uongo, akisema: “Twawezaje kula vitoto vichanga, hali ni haramu kwetu kula damu ya wanyama?”
11 Maandishi mengi ya karne ya pili na ya tatu yanahakikisha kwamba Wakristo wa wakati huo walifahamu kwamba katazo hili halikuwa jambo la wakati uliopita; liliwapasa. Kwa kweli, kitabu The Works of the Rev. Joseph Bingham kinasema hivi:
“Ilikuwa desturi ya Kanisa Katoliki, mpaka karibu na wakati wa Mtakatifu [Augustino], kujiepusha kula damu, kwa kutii kanuni iliyotolewa na Mitume kwa waongofu wa Mataifa: kwa hiyo viongozi wote wa kidini walikuwa na wajibu wa kujiepusha na [damu] kwa sheria za kale za Kanisa ama sivyo waondolewe katika vyeo [vyao].”
Kwa sababu gani, basi, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo hayafuati “kanuni” hii? Maelezo ya Martin Luther yanatoa jibu. Ingawa yeye mwenyewe alikuwa na maelekeo ya kupinga baraza zote, Luther alisema hivi juu ya Matendo 15:
“Basi tukitaka tuwe na kanisa linalofuata baraza hii (maana yafaa, kwa kuwa ndiyo baraza ya kwanza na iliyo kuu nayo ilifanywa na mitume wenyewe), yatupasa tufundishe na kusisitiza kwamba tangu sasa, mkuu, bwana, . . . wala mkulima wasile mabata bukini, kulungu, paa, wala nyama ya nguruwe iliyopikwa katika damu, . . . [na] ni lazima kujiepusha hasa na utumbo mwekundu na utumbo wenye damu, . . . Basi, anzeni, mtu ye yote anayetaka au anayeweza kuipatanisha Jumuiya ya Wakristo na baraza hii; nitafurahi kumfuata.”
Yeye aliona kwamba, kwa kuwa kutii uamuzi ulio katika Matendo 15:28, 29 lilikuwa jambo gumu na watu wote waliudharau, lingekuwa jambo lisilowezekana kutaka wafuasi wote wa kanisa waufuate. Kwa hiyo, yeye mwenyewe vilevile hangefanya hivyo.
12 Huenda ikawa kwamba Martin Luther pamoja na wengine wengi katika siku zake hawakutaka kutii sheria ya Mungu, na labda wengi leo katika Jumuiya ya Wakristo hawataki kufanya hivyo. Lakini si Mashahidi Wakristo wa Yehova!
MATUMIZI YA DAMU KATIKA MATIBABU
13, 14. (a) Ungewezaje kusaidia mtu aone kwamba katazo la Biblia linatia ndani kutiwa damu ya wanadamu mishipani? (b) Kwa sababu gani kukataa kutiwa damu mishipani kunalingana na mifano iliyoandikwa katika Biblia?
13 Kama tulivyotangulia kuona, kutii sheria ya Mungu juu ya damu katika matibabu ni jambo ambalo mara nyingi linatokeza mashindano. Kutia damu mishipani kunakofanywa katika watu milioni nyingi kila mwaka kunaonwa na watu wengi kama jambo la lazima na la kuokoa uhai katika utabibu wa kisasa. Walakini, mahali pa kuongoza fikira zao na mwenendo wao kufuatana na maoni ya matabibu wa kisasa yanayoenea kote, Wakristo wa kweli wanahitaji kukumbuka kwanza kwamba Mungu anaamuru: ‘Jiepusheni na damu.’
14 Ni kweli kwamba Biblia ilipokuwa ikiandikwa, utabibu wa kutia damu mishipani haukutumiwa. Walakini, yale yanayosemwa na Neno la Mungu yanatia ndani mazoea ya kutia damu mishipani. Daktari anayekataza mgonjwa kutumia dawa fulani kwa sababu inakuwa na matokeo mabaya kwake hangekataza tu kuitumia kwa mdomo bali vilevile kwa kutungwa sindano. Vivyo hivyo, amri ya Mungu ya ‘kujiepusha na damu’ inakataza kuitumia kwa mdomo na vilevile kwa kuipitishia mishipani. Zaidi ya hayo, Biblia inaonyesha wazi kwamba sheria hiyo ya kimungu haikupaswa kuachiliwa hata wakati mtu anapokabiliwa (elekeana) na hatari inayohatirisha uhai wake. (1 Sam. 14:31-35) Wao wamekuwa na uhakika kabisa na uwezo wa Mungu wa kurudisha uhai, na kuamini maneno haya ya Yesu Kristo: “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima, Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi.”—Yohana 11:25; 5:28, 29.
15. Sababu gani kukataa kutiwa damu mishipani ni jambo la akili kulingana na matibabu?
15 Huenda watu wengi wakashangaa kujua kwamba kukataa kutiwa damu na kuomba matibabu mengine mahali pake kuna faida. Sababu ya hili ni kwamba kuna ushuhuda unaoendelea kuongezeka unaoonyesha kwamba kuna hatari nyingi mbalimbali zinazotokana na kutiwa damu mishipani.b Kwa mfano, angalia jibu la barua aliyotumiwa daktari na mwanamke mmoja ambaye, baada ya kupasuliwa moyo, alipatwa na ugonjwa wa maini, unaoua watu elfu nyingi kila mwaka. Dakt. Robert Mendelsohn, anayetoa habari za matibabu kwa magazeti, alisema kwamba yeye hakushangaa, akaongeza:
“Katika hospitali fulani kubwa, idadi kubwa ya wagonjwa Mashahidi wa Yehova wanaokataa kutiwa damu mishipani, wamepasuliwa moyo kwa kutumia namna nyingine za dawa mahali pa damu kukawa na matokeo mazuri. . . . Labda sisi sote tunaohitaji kupasuliwa kunakoonekana kukihitaji damu itumiwe tunapaswa kuwauliza madaktari wetu kama wanafahamiana na ripoti hizi za kisayansi. Huenda hii ikatupunguzia sisi sote magonjwa ya maini yanayotokea baada ya kutiwa damu mishipani pamoja na kutupa faida nyingine zinazofurahiwa sasa na Mashahidi [wa Yehova] peke yao.”—The Idaho Statesman, Feb. 15, 1978, uku. 8C.
16. Mambo yaliyoonwa yanaonyesha nini kwa habari ya kufanya upasuaji pasipo kutumia damu?
16 Kupasuliwa moyo ni mojawapo tu wa upasuaji mwingi ambao madaktari hodari wameona unaweza kufanywa pasipo kutumia damu. Kwa mfano, ebu kumbuka kisa kilichotajwa mwanzoni mwa makala hii, Shahidi mwenye umri wa miaka 52 aliyehitaji kupasuliwa tumbo kwa kuwa na kidonda kilichokuwa kikitoka damu. Damu yake ilipopunguka sana akawa hatarini, hakimu alitoa ruhusa atiwe damu mishipani. Walakini mumewe alimpeleka katika hospitali nyingine iliyokuwa na maongozi ya kuheshimu maoni ya mgonjwa. Matokeo yakawa nini? Baadaye makala za magazeti zilitangaza hivi: “Imani Yapatia Mume na Mke Ushindi Waliokataa Kutiwa Damu Mishipani.” Alipona!
17. Ni mambo gani yanayohusu wema na ubaya ya kutia damu mishipani yanayopaswa kufikiriwa?
17 Vilevile madaktari wengi wenye kufikiri wanakuja kujua juu ya hali ya mema na mabaya inayohusiana na habari hii, wakifikia uamuzi wa kwamba wagonjwa wana haki ya kuamua kukubali ama kukataa namna fulani ya matibabu. Dakt. D. Goldstein aliandika hivi: “Hata daktari akiwa na uhakika namna gani wa kwamba namna fulani ya matibabu anayopendekeza ndiyo peke yake yanayoweza kuokoa uhai, yeye hana haki inayohusiana na wema na ubaya ya kutenda kinyume cha imani ya kidini ya mgonjwa.” Madaktari wengine waliokuwa wametibu watoto Mashahidi waliokuwa na ugonjwa wa donda baya walieleza hivi:
“Uamuzi wetu wa kukubaliana na maombi yao ya kutotumia matibabu ya kutia damu mishipani ulifanywa juu ya mambo mawili ya hakika. Kwanza, kila mmoja wa watoto hawa alikuwa na ugonjwa ambao ungemwua, na hatungeweza kutabiri kwamba kungekua na matokeo yenye kufaulu bila kuwa na mashaka mengi. Pili, tulikubali kwamba wakati kunapokuwa na ugonjwa unaohatirisha uhai, uhitaji wa wazazi kuwa na imani isiyotikisika unasitawishwa.”—Pediatrics, Des. 1977, usu 919.
18. Imani inahusikaje katika kutiwa damu mishipani?
18 Imani waliyo nayo Wakristo wa kweli, na ambayo wameazimia kuishi kulingana nayo, inakamatana na imani katika uwezo wenye kuokoa wa damu ya Kristo. (Rum. 3:25; Ebr. 13:12; 1 Yohana 5:5, 6) Hakuna damu nyingine yo yote itakayopatikana ambayo kwayo wanaweza kupata uzima wa milele. (Ebr. 10:29-31) Kwa hiyo, wakati wao ujao unakamatana na uaminifu wao kwa Yehova Mungu. Hii inatia ndani yale anayosema juu ya damu.
JITAHIDI USIWE NA HATIA YA DAMU
19. Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani juu ya kuwa na hatia ya damu? (Zab. 26:9; 55:23)
19 Inafaa kabisa Wakristo wajitahidi kwa bidii sana waepuke kuvunja sheria ya Mungu juu ya damu, ama katika matibabu au katika njia nyingine yo yote. Kuvunja sheria hiyo kungemfanya mtu aonekane na hatia mbele za Mungu. Mfalme Daudi alionyesha nia ambayo tunahitaji kutunza. Aliomba hivi: “Ee Mungu, Mungu wa wokovu wangu, uniponye na damu.”—Zab. 51:14.
20. Njia fulani ambazo katika hizo mtu anaweza kuwa na hatia ya damu ni zipi?
20 Watu wengi wanafikiri kwamba mtu anakuwa na hatia ya damu wakati tu anapoua kwa makusudi. Bila shaka Mungu ameonyesha katika maandiko kwamba anachukia umwagaji wa damu kama huo. (Zab. 5:6; Mit. 6:16, 17) Lakini Maandiko yanaonyesha kwamba, kwa kuwa uhai ni kitu kitakatifu huenda mtu akawa na hatia ya damu hata ikiwa mtu angeua mwingine pasipo kukusudia. (Kum. 22:8; Hes. 35:15-33; Kut. 21:29) Je! sisi wenyewe tunaonyesha kuheshimu sana uhai na damu katika maisha zetu za kila siku? Kwa mfano, heshima hiyo inapaswa ituongoze tuwe na kiasi na waangalifu tunapoendesha magari, tutii sheria zinazohifadhi usalama na kuweka magari yetu katika hali nzuri ili kuyaendesha kwa usalama. Vivyo hivyo, tunapaswa kuwa waangalifu tuondoe hali zenye hatari zinazoweza kutokeza misiba nyumbani na kazini ambayo inaweza kutokeza kifo kwako wewe mwenyewe au kwa wengine. Je! hayo ndiyo maoni yako?
21. Leo mtu anawezaje kuwa na hatia ya damu katika njia isiyo ya moja kwa moja, na hili linahitaji mtu ajichunguzeje?
21 Sehemu nyingine ya kuepuka kuwa na hatia ya damu inakamatana na matengenezo yanayoonwa na Mungu kuwa na hatia ya damu. Kwa mfano, Mungu anaonyesha waziwazi kwamba Babeli Mkuu, milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, ina hatia ya kumwaga damu ya waabudu wa kweli. (Ufu. 17:6; 18:24; 19:2) Vilevile amekubali matengenezo ya kisiasa na ya kijeshi ambayo yamemwaga damu nyingi sana katika kame nyingi. Tamaa yetu ya unyofu ya kuwa huru na hatia ya damu inatuhitaji tujitenge na tuwe waangalifu tusisaidie matengenezo ambayo Mungu ameyahukumu. Je! sisi tunaonyesha haya yote katika kila sehemu ya maisha zetu?
22, 23. (a) Ni sehemu gani nyingine za kuwa na hatia ya damu tunazopaswa kujali? (Matendo 18:6) (b) Hivyo, basi, azimio letu juu ya uhai na damu linapaswa kuwa nini?
22 Tena tunaweza kuonyesha azimio letu la kuwa huru na hatia ya damu kwa kuwa na juhudi na shauku katika kuhubiri ujumbe wa Ufalme. (Marko 13:10) Juu ya hili fikiria shauri ambalo nabii Ezekieli alipewa na Mungu kabla Yerusalemu haujaanguka katika mwaka 607 K.W.K. Ezekieli aliambiwa na Mungu kwamba, ikiwa yeye kama mlinzi, angeshindwa kutoa onyo, angekuwa na hatia ya damu ya Waisraeli ambao wangeangamia. (Eze. 3:17-21; 33:2-16) Hata hivyo, Lo! namna tunavyoweza kupata uradhi tunapotimiza daraka letu la Kikristo la kueneza kweli juu ya mwisho unaokuja juu ya taratibu hii mbovu na juu ya paradiso itakayofuata! Kufanya hivyo kunamfanya mtu ajione kama alivyojiona mtume Paulo, aliyewaambia wazee Wakristo hivi: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu awaye yote. Kwa maana sikujiepusha na kuwahubiria habari ya kusudi lote la Mungu.” (Matendo 20:26, 27) Lo! pendeleo kubwa namna gani! Tunapojiepusha na hatia ya damu sisi wenyewe, tunaweza kusaidia wengine wapate uzima wa milele wakionyesha imani katika damu ya Kristo.
23 Kwa hiyo, ingawa huenda watu wengi wasijue yale anayosema Mungu na huenda wakaona damu kama kitu tu cha kuendeleza uhai wa kibinadamu kwa muda mfupi tu, sivyo ilivyo kwa Wakristo wa kweli. Juu ya msingi wa Neno la Mungu tunajua maoni ya Yehova juu ya uhai na damu. Na tuazimie kutegemeza maoni hayo na kuishi kulingana nayo.
[Maelezo ya Chini]
a Ursprung und Anfänge des Christentums (1962), kur.186, 187.
b Kwa habari zaidi tazama kijitabu Blood (1977), kur. 41-49.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Epuka kuwa na hatia ya damu kutokana na (1) kula damu, (2) kushirikiana na matengenezo yaliyo na hatia ya damu, au (3) kushinwa kuwaonya watu juu ya siku ya hukumu