Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • it uku. 496
  • Kutaniko

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutaniko
  • Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Kutaniko na Limsifu Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kutaniko na Lijengwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kundi la Kikristo na Utendaji Wake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Mipango na Usimamizi Katika Kutaniko
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
Pata Habari Zaidi
Ufahamu wa Kina wa Maandiko
it uku. 496

KUTANIKO

Kikundi cha watu waliokusanyika pamoja kwa sababu ya kusudi au shughuli fulani. Neno la Kiebrania ambalo kwa kawaida hutafsiriwa kuwa “kutaniko” katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni qa·halʹ, ambalo linatokana na mzizi unaomaanisha “kuita pamoja; kukusanya.” (Hes 20:8; Kum 4:10) Mara nyingi hutumiwa kuhusiana na kikundi kilichopangwa, linapatikana katika maneno “kutaniko lote la Israeli” (Yos 8:35), “kutaniko lote la Waisraeli” (1Fal 8:14), “kutaniko la Mungu wa kweli” (Neh 13:1), na “kutaniko la Yehova” (Hes 20:4; Kum 23:2, 3; 1Nya 28:8; Mik 2:5). Neno Qa·halʹ linahusiana na vikundi mbalimbali vya wanadamu waliokusanyika kwa ajili ya shughuli za kidini (Kum 9:10; 18:16; 1Fal 8:65; Za 22:25; 107:32), mambo ya umma (1Fal 12:3), na kwa ajili ya vita (1Sa 17:47; Eze 16:40). Katika kitabu cha Mhubiri, Sulemani anatambulishwa kuwa “mkutanishaji” (Kiebr., qo·heʹleth). (Mhu 1:1, 12) Akiwa mfalme, aliwakutanisha au kuwakusanya watu ili wamwabudu Yehova, pindi moja ya pekee ni alipowakusanya raia zake kwenye hekalu jipya lililojengwa huko Yerusalemu.​—1Fal 8:1-5; 2Nya 5:2-6.

Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo neno linalotafsiriwa “kutaniko” ni ek·kle·siʹa, ambalo ndilo chanzo cha neno la Kiingereza “ecclesia.” Neno Ek·kle·siʹa linatokana na maneno mawili ya Kigiriki, ek, linalomaanisha “pamoja,” na ka·leʹo, linalomaanisha “ita.” Hivyo, linahusiana na kikundi cha watu kilichoitwa pamoja, iwe ni rasmi au isivyo rasmi. Ni neno lilelile linalotumiwa kuhusu kutaniko la Waisraeli kwenye Matendo 7:38 na vilevile linatumiwa kuhusiana na “kusanyiko” lililochochewa na fundi wa fedha Demetrio dhidi ya Paulo na waandamani wake huko Efeso. (Mdo 19:23, 24, 29, 32, 41) Hata hivyo, mara nyingi neno hilo hutumiwa kuhusiana na kutaniko la Kikristo. Linatumiwa kuhusiana na kutaniko la Kikristo kwa ujumla (1Kor 12:28); kutaniko katika jiji fulani kama vile Yerusalemu (Mdo 8:1), Antiokia (Mdo 13:1), au Korintho (2Kor 1:1); au kikundi hususa kilichokutanika katika nyumba ya mtu fulani (Ro 16:5; Fil 2). Vilevile, makutaniko hususa ya Kikristo au “makutaniko ya Mungu” yanatajwa pia. (Mdo 15:41; 1Kor 11:16) Baadhi ya tafsiri za Biblia hutumia neno “kanisa” katika maandiko yanayohusu kutaniko la Kikristo, kama vile kwenye 1 Wakorintho 16:19. (UV; BHN) Kwa kuwa watu wengi hufikiri kwamba kanisa ni jengo linalotumiwa kwa ajili ya ibada badala ya kutaniko linaloabudu, neno “kanisa” linaweza kupotosha maana.

Kwa kawaida neno la Kigiriki ek·kle·siʹa hutumiwa katika Septuajinti kutafsiri neno la Kiebrania qa·halʹ, kwa mfano kwenye Zaburi 22:22 (21:23, LXX).

Kutaniko la Israeli. Tangu siku za Musa na kuendelea, taifa la Israeli liliitwa kutaniko. Yehova alifanya mpango ili kutaniko hilo lisiongozwe kidemokrasia na watu, bali kitheokrasi, yaani na Mungu mwenyewe. Ili kutimiza hilo, taifa la Israeli lilifanya agano la Sheria. (Kut 19:3-9; 24:6-8) Kwa kuwa Musa ndiye aliyekuwa mpatanishi wa agano hilo, ingeweza kusemwa kwamba: “Musa alitupatia amri, sheria, kuwa miliki ya kutaniko la Yakobo.” (Kum 33:4) Yehova alikuwa Mwamuzi, Mpaji-sheria, na Mfalme wao. (Isa 33:22) Kwa hiyo, taifa hilo lilikuwa kutaniko la Mungu na hivyo liliitwa “kutaniko la Yehova.”​—Hes 16:3; 1Nya 28:8.

Wakati mwingine, neno la Kiebrania qa·halʹ (kutaniko) linatumiwa pamoja na neno la Kiebrania ʽe·dhahʹ (kusanyiko). (Law 4:13; Hes 20:8, 10) ʽE·dhahʹ linatokana na mzizi unaomaanisha “weka rasmi,” hivyo linamaanisha kikundi kilichokusanyika kwa makubaliano, na mara nyingi linatumiwa kuhusiana na taifa la Israeli, kama vile maneno ‘kusanyiko la Israeli.’ (Kut 12:3) Katika taifa la Israeli wale waliokuwa na asili ya Kiebrania walifanyiza kutaniko (qa·halʹ; Hes 15:15), lakini inaonekana kusanyiko (ʽe·dhahʹ) lilitia ndani Waisraeli na wakaaji wageni walioshirikiana nao. (Kut 12:19) Basi washiriki wa kutaniko, katika maana pana walitia ndani wakaaji wageni waliotahiriwa.​—Hes 15:14-16.

Hata hivyo, kuna watu ambao hawakuruhusiwa kuwa sehemu ya “kutaniko la Yehova.” Mwanamume aliyehasiwa au “kukatwa uume” hangeruhusiwa kuingia katika kutaniko; wana haramu, wanaume Waamoni, na wanaume Wamoabu hawakuruhusiwa, “hata kufikia kizazi cha kumi.” Lakini “kizazi cha tatu” cha wana waliozaliwa na Waedomu na Wamisri kingeweza “kuja katika kutaniko la Yehova.” (Kum 23:1-8) Kutengwa hadi “kufikia kizazi cha kumi” kwa wana haramu kuliunga mkono sheria ya Yehova dhidi ya uzinzi. (Kut 20:14) Ingawa watu wasio na viungo vya uzazi wangetengwa na “kutaniko la Yehova,” watu hao walifarijiwa na maneno ya Isaya, kwenye Isaya 56:1-7. Bila shaka, watu waliotengwa na “kutaniko la Yehova” katika Israeli la kale wangeweza kupata maandalizi na baraka ambazo Yehova aliwapa watu wa mataifa kwa ujumla.​—Mwa 22:15-18.

Watu waliokuwa katika kutaniko la Israeli walionyeshwa rehema walipofanya dhambi bila kukusudia. Lakini walipata adhabu ya kifo kwa kufanya dhambi kimakusudi. (Hes 15:27-31) Kwa mfano, mtu angetengwa, na hata kuuawa, kwa kukataa kujitakasa ikiwa hakuwa safi kisherehe, kwa kula wanyama wa dhabihu za ushirika akiwa katika hali hiyo ya kutokuwa safi, kwa kula dhabihu zenye mafuta au damu, au kwa kula vitu vitakatifu akiwa si safi. (Hes 19:20; Law 7:21-27; 17:10, 14; 22:3) Vilevile, watu waliuawa kwa kufanya kazi siku ya Sabato (Kut 31:14), kwa kutoa watoto wao dhabihu kwa Moleki, kwa kutafuta habari kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho na wabashiri wa matukio, kwa kufanya ngono za aina fulani, na kwa kukataa “kujitesa” Siku ya Kufunika Dhambi.​—Law 20:1-6, 17, 18; 23:27-30; tazama pia Kut 30:31-33; Law 17:3, 4, 8, 9; 18:29; 19:5-8.

Ingawa watu walifanyiza kutaniko la Israeli, taifa hilo lilikuwa na makabila, ukoo, na nyumba. Kisa cha Akani kinaonyesha utaratibu huo, kwa maana Waisraeli waliitwa, kwanza kabila kwa kabila, kisha ukoo kwa ukoo, kisha nyumba kwa nyumba, na mwishowe mwanamume kwa mwanamume, hadi Akani akapatikana kuwa mwenye kosa.​—Yos 7:10-19.

Katika Israeli, mara nyingi watu waliwakilishwa na wanaume wenye mamlaka. (Ezr 10:14) Kwa hiyo, baada ya hema la ibada kutengenezwa, ‘wakuu wa makabila’ walileta matoleo. (Hes 7:1-11) Vilevile, katika siku za Nehemia “mapatano thabiti” yalitiwa muhuri na makuhani, Walawi, na “viongozi wa watu.” (Neh 9:38–10:27) Waisraeli walipokuwa nyikani, kulikuwa na “wakuu wa kusanyiko, wanaume maarufu waliowekwa rasmi,” na 250 kati yao walijiunga na Kora, Dathani, Abiramu, na Oni kwa kukusanyika dhidi ya Musa na Haruni. (Hes 16:1-3) Musa alifuata mwongozo wa Mungu kwa kuchagua wanaume 70 kati ya wazee wa Israeli waliokuwa maofisa ambao wangemsaidia kubeba “mzigo wa watu” ambao hangeweza kuubeba peke yake. (Hes 11:16, 17, 24, 25) Kitabu cha Mambo ya Walawi 4:15 kinataja “wazee wa kusanyiko,” na inaonekana kwamba wanaume wazee, viongozi, waamuzi, na wakuu ndio waliokuwa na jukumu la kuwawakilisha watu.​—Hes 1:4, 16; Yos 23:2; 24:1.

Walipokuwa nyikani, tarumbeta mbili za fedha zilitumiwa kuwakusanya watu na kuvunja kambi. Kusanyiko hilo lilikutana na Musa kwenye mwingilio wa hema la ibada baada ya kusikia mlio wa tarumbeta zote mbili. Mlio wa tarumbeta moja ulimaanisha kwamba, ‘wakuu peke yao, yaani, viongozi wa maelfu katika Israeli’ ndio waliopaswa kukusanyika hapo. (Hes 10:1-4) Nyakati nyingine, wafalme waliwakusanya watu (1Fal 8:5; 2Nya 20:4, 5), Hezekia aliwatuma wajumbe kuwaita watu waje Yerusalemu ili kusherehekea Pasaka kuu katika kipindi cha utawala wake.​—2Nya 30:1, 2, 10-13.

Baadaye, kikundi kilichotoa maamuzi ambacho kiliitwa Sanhedrini kilikuwa na mamlaka kubwa. Kikundi hicho kilikuwa na washiriki 71​—kuhani mkuu na wanaume wengine maarufu 70 wa taifa hilo​—“kikundi cha wazee.”​—Mt 26:59; Lu 22:66.

Wayahudi walipokuwa uhamishoni huko Babiloni, au muda mfupi baadaye, masinagogi yalianza kutumiwa kama majengo ambamo Wayahudi walikusanyika. Baada ya muda kupita, masinagogi yalijengwa katika maeneo mbalimbali; kwa mfano, Yesu alifundisha katika sinagogi huko Nazareti. (Lu 4:16-21) Masinagogi yalikuwa shule ambako Maandiko yalisomwa na kufundishwa, na pia yalikuwa mahali pa kutoa sala na kumsifu Mungu.​—Mdo 15:21; ona SINAGOGI.

Kutaniko la Israeli lilikuwa na pendeleo la pekee. Musa aliwakumbusha hivi: “Ninyi ni watu watakatifu kwa Yehova Mungu wenu, na Yehova Mungu wenu amewachagua ninyi muwe watu wake, mali yake ya pekee, kutoka kati ya mataifa yote yaliyo duniani.” (Kum 7:6) Lakini kutaniko la Wayahudi liliacha kuwa kutaniko la Mungu, likatupiliwa mbali kwa sababu ya kumkataa Mwana wa Mungu.​—Mdo 4:24-28; 13:23-29; Mt 21:43; 23:37, 38; Lu 19:41-44.

Kutaniko la Kikristo la Mungu. Kabla taifa la Wayahudi halijakataliwa na kuacha kuwa kutaniko la Mungu, Yesu Kristo alijitambulisha kuwa “mwamba” ambao juu yake angejenga kile alichokiita “kutaniko langu.” (Mt 16:18) Yesu alikuwa akizungumza na Petro, na baadaye mtume huyo alimtambulisha Yesu kuwa “jiwe” la mfano ambalo lilikataliwa na watu lakini “lililochaguliwa na lenye thamani kwa Mungu” na kwamba Yesu alikuwa “jiwe kuu la pembeni” ambalo mtu angeweka imani juu yake bila kukatishwa tamaa. (1Pe 2:4-6; Zab 118:22; Isa 28:16) Vilevile, Paulo alimtambulisha Yesu Kristo kuwa msingi ambao kutaniko la Kikristo lilijengwa juu yake. (Efe 2:19-22; 1Kor 3:11) Kwa kuwa kutaniko hilo ni mali ya Yehova, kwa kufaa linaitwa “kutaniko la Mungu.”​—Mdo 20:28; Gal 1:13.

Yesu ndiye kichwa cha kutaniko (Kigr., ek·kle·siʹa) hilo la Kikristo, lililojengwa juu ya Kristo. Kwa hiyo, ilisemwa: “[Mungu] alivitiisha pia vitu vyote chini ya miguu yake na kumfanya kuwa kichwa juu ya vitu vyote kuhusiana na kutaniko, ambalo ni mwili wake, ujazo wake anayejaza vitu vyote katika vyote.”​—Efe 1:22, 23; pia ona Kol 1:18.

Kutaniko la Kikristo la Mungu lilichukua mahali pa kutaniko la Israeli siku ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., roho takatifu ilipomiminwa juu ya wafuasi wa Yesu huko Yerusalemu. Wale ambao wangekuwa washiriki wa kwanza wa kutaniko hilo walichaguliwa muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa, mwanzoni mwa huduma yake duniani. (Mdo 2:1-4; Yoh 1:35-43) Yesu alichagua mitume 12 kati ya wafuasi wake wa mwanzoni (Lu 6:12-16), na baadaye akamchagua Sauli wa Tarso, aliyekuja kuwa “mtume kwa mataifa.” (Mdo 9:1-19; Ro 11:13) Mitume12 waaminifu wa Mwanakondoo Yesu Kristo, kutia ndani Mathia ambaye alichukua mahali pa Yuda, wanafanyiza msingi wa pili wa kutaniko la Kikristo.​—Mdo 1:23-26; Ufu 21:1, 2, 14.

Kutaniko hili linaitwa “kutaniko la wazaliwa wa kwanza ambao wameandikishwa mbinguni,” idadi yake kamili ni watu 144,000, chini ya ukichwa wa Kristo. (Ebr 12:23; Ufu 7:4) Watu hao waliochaguliwa “[wamenunuliwa] kutoka kati ya wanadamu” ili kutimiza kazi ya pekee hapa duniani na baadaye kuwa pamoja na Kristo mbinguni wakiwa bibi harusi wake. Kama vile kulivyokuwa na matakwa kwa washiriki wa kutaniko la Mungu la Waebrania, vivyo hivyo kuna matakwa kwa washiriki wa “kutaniko la Mungu” la Kikristo. Kutaniko hilo linafanyizwa na mabikira wa kiroho ambao wanaendelea kumfuata Mwanakondoo, Yesu Kristo, popote anapoenda, “na hamna udanganyifu uliopatikana katika vinywa vyao; wao hawana dosari.”​—Ufu 14:1-5.

Washiriki wa kutaniko la Kikristo la Mungu wanachaguliwa na Yehova. (Ro 8:30; 2Th 2:13) Washiriki wa kwanza waliitwa kutoka kwa kutaniko la Wayahudi lililokataliwa, ambalo lilimkataa Mwana wa Mungu kuwa Masihi. Hata hivyo, kuanzia na Kornelio mwaka wa 36 W.K., washiriki wa kutaniko la Kikristo waliitwa pia kutoka kwa watu wa mataifa kwa ujumla, hivi kwamba Paulo alisema: “Hakuna Myahudi wala Mgiriki, hakuna mtumwa wala mtu huru, hakuna mwanamume wala mwanamke, kwa maana ninyi nyote ni kitu kimoja katika muungano na Kristo Yesu.” (Gal 3:28; Mdo 10:34, 35; Ro 10:12; Efe 2:11-16) Agano la Sheria ambalo lilipatanishwa na Musa na ambalo liliongoza kutaniko la Israeli lilitimizwa na Kristo na kisha Yehova Mungu akaliondolea mbali. (Mt 5:17; 2Kor 3:14; Kol 2:13, 14) Washiriki wa kutaniko la Kikristo wanafaidika na agano jipya lililopatanishwa na Musa Mkuu, Yesu Kristo. (Mt 26:28; Ebr 12:22-24; Mdo 3:19-23) Vilevile, ingawa makuhani na wafalme Waisraeli walichaguliwa kwa kutiwa mafuta (Kut 30:22-30; 2Fal 9:6), wale wanaochaguliwa na Mungu kuwa washiriki wa kutaniko la Kikristo wanatiwa mafuta kwa roho takatifu (2Kor 1:21, 22; 1Yoh 2:20) na wanafanywa kuwa wana wa Yehova Mungu.​—Efe 1:5.

Kimsingi kutaniko la Waebrania lilifanyizwa na Waisraeli wa asili. Wale wanaofanyiza kutaniko la Kikristo la Mungu la watiwa mafuta ni Waisraeli wa kiroho, wanaofanyiza makabila ya kiroho ya Israeli. (Ufu 7:4-8) Kwa kuwa idadi kubwa ya Waisraeli wa asili walimkataa Yesu Kristo, “si wote wanaotokana na Israeli ni ‘Israeli’ kihalisi,” yaani, Israeli wa kiroho. (Ro 9:6-9) Kuhusu kutaniko la Kikristo la Mungu linalofanyizwa na Wayahudi wa kiroho, Paulo alisema: “Yeye si Myahudi aliye hivyo kwa nje, wala kutahiriwa si kitu kilicho nje, juu ya mwili. Bali yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani, na kutahiriwa kwake ni kule kwa moyo kupitia roho.”​—Ro 2:28, 29.

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanapotaja “kutaniko” kwa kawaida hurejelea washiriki wake 144,000, wafuasi watiwa mafuta wa Kristo bila kutia ndani Yesu mwenyewe. (Efe 5:32; Ebr 12:23, 24) Hata hivyo, ufafanuzi ulioongozwa na roho wa maneno ya Daudi kwenye Zaburi 22:22 kumhusu Yesu Kristo kwenye Waebrania 2:12 unaonyesha kwamba neno “kutaniko” linaweza kutia ndani kichwa cha kutaniko, Yesu Kristo. Mwandikaji wa kitabu cha Waebrania alimnukuu Daudi aliposema: “Kwa maana yule anayetakasa na wale wanaotakaswa pia wote hutokana na mmoja, na kwa sababu hiyo yeye [Yesu Kristo] haoni aibu kuwaita ndugu, kama anavyosema: ‘Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kutaniko nitakusifu kwa wimbo.’” (Ebr 2:11, 12) Kama Daudi, ambaye alikuwa mshiriki wa kutaniko la Israeli ambamo alimsifu Yehova, katika andiko hilo, Yesu Kristo anaweza kuonwa kuwa mshiriki wa kutaniko la kiroho, na washiriki wengine wanaitwa “ndugu” zake. (Linganisha Mt 25:39, 40.) Daudi alikuwa mshiriki wa kutaniko la Israeli la Yehova Mungu, na pia Yesu Kristo alikuwa mshiriki wa kutaniko hilo alipokuwa duniani, na aliwahubiria washiriki wake. Washiriki wachache wa kutaniko hilo walikuja kuwa sehemu ya kutaniko la Yesu.

Jinsi Ambavyo Kutaniko la Kikristo Limepangwa. Ingawa makutaniko ya Mungu yalianzishwa sehemu mbalimbali, hayakujitegemea. Badala yake, makutaniko hayo yote yalitambua mamlaka ya baraza linaloongoza la Kikristo huko Yerusalemu. Baraza hilo linaloongoza lilifanyizwa na mitume na wanaume wazee katika kutaniko la Yerusalemu, na hakukuwa na vikundi vingine vilivyojaribu kuliongoza kutaniko. Suala la kutahiriwa lilipelekwa kwa baraza linaloongoza la Kikristo la karne ya kwanza W.K. ili liamuliwe. Baraza linaloongoza lilipofanya uamuzi, kwa mwongozo wa roho takatifu, uamuzi huo ulikubaliwa na kufuatwa na makutaniko yote ya Kikristo, nayo yalitii uamuzi huo kwa hiari.​—Mdo 15:22-31.

Baraza linaloongoza huko Yerusalemu liliwatuma wawakilishi wanaosafiri. Kwa hiyo, Paulo na wengine walipeleka uamuzi uliotajwa, na maandiko yanasema: “Walipokuwa wakipita katika majiji, walikuwa wakiwapa maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wazee waliokuwa Yerusalemu ili wayashike.” Kuhusu matokeo yaliyopatikana, maandiko yanasema: “Ndipo kwa kweli makutaniko yakaendelea kuimarishwa katika imani na kuongezeka idadi siku baada ya siku.” (Mdo 16:4, 5) Awali, mitume huko Yerusalemu “waliposikia kwamba Samaria imelikubali neno la Mungu, [waliwatuma] Petro na Yohana kwao; nao wakashuka kwenda huko, wakasali kwa ajili yao ili wapate roho takatifu.”​—Mdo 8:14, 15.

Kila kutaniko lilifuata kwa ukaribu mwongozo wa baraza linaloongoza la Kikristo, ambalo lilisimamia kuwekwa rasmi kwa wanaume wazee. (Tito 1:1, 5) Kwa hiyo, baraza linaloongoza liliagiza chini ya mwongozo wa roho takatifu kwamba waangalizi na pia wasaidizi, watumishi wa huduma wawekwe rasmi katika kila kutaniko. Wanaume waliopewa majukumu hayo walipaswa kusitawisha sifa fulani. (1Ti 3:1-13; Tito 1:5-9) Wawakilishi wanaosafiri wa baraza linaloongoza, kama vile Paulo, walimwiga Kristo na kuweka mfano mzuri wa kuigwa. (1Kor 11:1; Flp 4:9) Kwa kweli, wachungaji wote wa kiroho walipaswa “kuwa vielelezo kwa kundi” (1Pe 5:2, 3), walipaswa kuwahangaikia na kuwapenda washiriki wa kutaniko (1Th 2:5-12), na walipaswa kuwasaidia wale walio dhaifu kiroho.​—Gal 6:1; Yak 5:13-16; ona MWANAMUME MZEE; MWANGALIZI; MHUDUMU.

Hivyo, kama vile Yehova alivyolipanga kutaniko la Israeli lisimamiwe na wanaume wazee, vichwa, waamuzi, na wakuu (Yos 23:2), vivyo hivyo, Alihakikisha kwamba kutaniko la Kikristo linasimamiwa na wanaume wazee waliowekwa rasmi ili kutimiza majukumu. (Mdo 14:23) Na kama vile kulivyokuwa na wanaume wenye majukumu waliowakilisha kutaniko zima la Israeli, kwa mfano kwenye masuala ya kisheria (Kum 16:18), Mungu alifanya mpango ili kila kutaniko la Kikristo liwakilishwe katika mambo kama hayo na wanaume waliochaguliwa na roho takatifu ili kutimiza majukumu hayo. (Mdo 20:28; 1Kor 5:1-5) Hata hivyo, ikiwa matatizo yangetokea kati ya washiriki wa kutaniko la Kikristo la Mungu, maneno ya Yesu kwenye Mathayo 18:15-17 yangekuwa msingi wa kutatua matatizo kama hayo (maneno hayo yalisemwa kabla ya kutaniko la Wayahudi la Mungu kukataliwa na Yehova, na hivyo mwanzoni maneno hayo yaliwahusu.)

Yehova Mungu amewapanga washiriki wa “mwili” wa kiroho wa Kristo “kama alivyopenda.” Paulo alisema: “Mungu amewaweka watu mbalimbali katika kutaniko: kwanza, mitume; pili, manabii; tatu, walimu; kisha matendo yenye nguvu; kisha zawadi za uponyaji; huduma za kusaidia; uwezo wa kuelekeza; na lugha mbalimbali.” Ingawa wote hawakutimiza majukumu yaleyale, wote walihitajika katika kutaniko la Kikristo. (1Kor 12:12-31) Paulo alifafanua kwamba mitume, manabii, waeneza injili, wachungaji, na walimu waliwekwa katika makutaniko ya Kikristo “ili kuwarekebisha watakatifu, kwa ajili ya kutimiza huduma, na kuujenga mwili wa Kristo, mpaka sote tuwe na umoja katika imani na tuwe na ujuzi sahihi kumhusu Mwana wa Mungu, na kuwa mtu aliyekomaa kabisa, na kufikia kiwango cha kimo kamili cha Kristo.”​—Efe 4:11-16.

Kutaniko la Israeli lilipewa sheria za Mungu na kufundishwa kwamba “mwanadamu haishi kwa mkate tu bali huishi kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Kum 8:1-3) Vilevile, Yesu Kristo alitambua kwamba mwanadamu hawezi kuishi kwa mkate tu “bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.” (Mt 4:1-4) Hivyo, maandalizi ya kutosha yamefanywa katika kutaniko la Kikristo kwa ajili ya chakula cha kiroho kinachohitajiwa, na Kristo mwenyewe alimtaja “mtumwa” ambaye angetumiwa kuwapa chakula hicho “watumishi wa nyumbani,” yaani, Wakristo. Yesu alipokuwa akitabiri kuhusu kuwapo kwake na “umalizio wa mfumo wa mambo,” alionyesha kwamba, atakapowasili, “bwana” angemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” “asimamie mali zake zote.”​—Mt 24:3, 45-47.

Katika kutaniko la Israeli, kukutanika ili kumwabudu Yehova na kuchunguza sheria kulikuwa jambo muhimu sana. (Kum 31:12; Neh 8:1-8) Vivyo hivyo, kukutana ili kumwabudu Yehova na kujifunza Maandiko ni sehemu muhimu ya kutaniko la Kikristo la Mungu, na mwandikaji wa kitabu cha Waebrania aliwahimiza Wakristo hao wasiache kukutanika pamoja. (Ebr 10:24, 25) Baadaye katika historia ya Wayahudi, shughuli katika sinagogi zilitia ndani kusoma na kufundisha Maandiko, kutoa sala, na kumsifu Mungu. Mazoea hayo yaliendelezwa katika mikutano ya Wakristo, ingawa hayakuhusisha desturi ambazo baadaye zilifanywa katika masinagogi. Katika sinagogi hakukuwa na kikundi cha viongozi, Maandiko yalisomwa na kufafanuliwa na mwanamume yeyote Myahudi aliyemwogopa Mungu. Vivyo hivyo, kutaniko la mapema la Wakristo halikuwa na makasisi. Katika makutaniko hayo au kwenye masinagogi wanawake hawakuruhusiwa kufundisha wala kuwa na mamlaka juu ya wanaume.​—1Ti 2:11, 12.

Utaratibu uliodumishwa katika mikutano ya kutaniko la Kikristo la Mungu ulipatana na wazo la kwamba Yehova, ambaye alianzisha mpango wa kutaniko kati ya wafuasi wa Kristo, “si Mungu wa machafuko bali ni wa amani.” Wote waliohudhuria mikutano hiyo walifaidika sana kiroho kutokana na utaratibu huo.​—1Kor 14:26-35, 40; ona KUSANYIKO.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki