HATI
Makubaliano ya maandishi yaliyotiwa sahihi na nyakati nyingine yalitiwa muhuri, yakiwa na masharti ya kisheria ili kutimiza lengo lililokusudiwa; nyaraka iliyotumiwa kununua ardhi na nyumba. Matumizi pekee katika Biblia ya neno la Kiebrania seʹpher katika maana hiyo, yalihusiana na shamba lililonunuliwa na Yeremia kutoka kwa Hanameli, mwana wa ndugu ya baba yake.—Yer 32:6-15.
Maelezo ya jinsi hati hiyo ilivyotengenezwa yanavutia. Uzito wa pesa zilizotolewa, “shekeli saba na vipande kumi vya fedha,” ulipimwa mbele ya mashahidi. (Yer 32:9) Ikiwa maneno ‘saba na kumi’ yataonwa kuwa mfumo halali wa kisheria unaomaanisha shekeli 17 za fedha (karibu dola 37 za Marekani), ingekuwa bei inayofaa ukizingatia muda na hali ya eneo hilo lilipokuwa likiuzwa. Ulikuwa wakati wa vita na njaa (miezi michache baadaye, Yerusalemu lilitekwa na Nebukadneza).
Pesa zilipotolewa, hati mbili zilizofanana ziliandikwa, “kulingana na amri na masharti ya kisheria.” Hati moja ilijulikana kama “hati ya ununuzi, iliyotiwa muhuri,” na nyingine iliitwa hati “ambayo haikuwa na muhuri.” (Yer 32:11) Ni hati ya kwanza tu iliyotiwa muhuri na mashahidi, na makubaliano yote yalifanyika mbele ya “Wayahudi wote waliokuwa wameketi katika Ua wa Walinzi.” (Yer 32:12) Kisha hati zote ziliwekwa katika chombo cha udongo ili zihifadhiwe.—Yer 32:14.
Desturi ya kutengeneza nakala mbili za hati na kuweka muhuri katika nakala moja ilifaa sana. Kutotia muhuri nakala moja kuliwawezesha wale waliotaka kununua kuichunguza. Ikiwa ingeharibika, au uhalali wake kutiliwa shaka, au ikiwa kuna wasiwasi kwamba huenda ilibadilishwa, basi nakala yenye muhuri iliweza kutolewa na kupewa mahakimu wa jiji ambao, baada ya kuuchunguza muhuri, wangefungua na kulinganisha nakala hizo mbili.