Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova hujitahidi kuwa wafuatiaji wa haki na hutumainiana, kwa nini wanahisi kwamba ni jambo la maana kufanya mkataba ulioandikwa kunapokuwa na shughuli za kibiashara kati yao?
Kufanya kwao hivyo, ni jambo la Kimaandiko, lifaalo, na lenye upendo. Jinsi gani hivyo? Acheni tuzungumzie sehemu hizo za mikataba ya kibiashara.
Biblia huonyesha rekodi iliyoandikwa ya shughuli mbalimbali za Mungu pamoja na watu wake wa agano, Waisraeli. Hizo hutia ndani shughuli za kibiashara zilizohusisha waabudu wa kweli. Mwanzo sura ya 23 ina simulizi moja tuwezalo kufikiria kwa uangalifu. Sara wake mpendwa alipokufa, Abrahamu alitaka kupata mahali pa kuzikia. Alianza kushughulika na Wakanaani walioishi karibu na Hebroni. Mstari wa 7-9 huonyesha kwamba yeye alitoa bei dhahiri kwa kipande cha shamba alichotaka. Mstari wa 10 huthibitisha kwamba toleo hili lilifanywa hadharani, watu wengine wakisikia kwenye lango la jiji. Mstari wa 13 waonyesha kwamba mwenye shamba alijitolea kumpa Abrahamu shamba, lakini aliitikia kwamba angechukua hilo shamba tu ikiwa lingeuzwa. Na mstari wa 17, 18, na 20 hueleza kwamba hivyo ndivyo ilivyofanywa, ikihakikishwa “mbele ya wazawa wa Hethi, mbele ya watu wote waingiao katika mlango wa mji wake.”
Hata hivyo, je, ingekuwa tofauti wakati watu wote wawili wanaokuwa na shughuli kama hiyo ya kibiashara ni waabudu wa kweli? Sura ya 32 ya Yeremia huandaa jibu. Kuanzia mstari wa 6 na kuendelea, twaona kwamba Yeremia alipaswa anunue shamba kutoka kwa binamu yake. Mstari wa 9 waonyesha kwamba bei ya kadiri ilikubaliwa. Sasa soma mstari wa 10-12: “Nami [Yeremia] nikaitia sahihi ile hati, na kuipiga muhuri, nikawaita mashahidi, nikampimia ile fedha katika mizani. Nikaitwaa ile hati ya kununua, ile iliyopigwa muhuri kama ilivyo sheria na ada, na ile nayo iliyokuwa wazi; na ile hati ya kununua nikampa Baruku, mwana wa Neria, mwana wa Maaseya, mbele ya uso wa Hanameli, mwana wa mjomba wangu, na mbele ya mashahidi wale walioitia sahihi hati ya kununua, mbele ya Wayahudi wote walioketi katika uwanda wa walinzi.”
Ndiyo, ijapokuwa Yeremia alikuwa akishughulika na mwabudu mwenzake, hata mtu wake wa ukoo, alitimiza utaratibu wa kisheria ufaao. Rekodi mbili zilizoandikwa zilifanywa—moja ikiachwa wazi kwa ajili ya kuirejezea kwa urahisi, ya pili ilitiwa muhuri ili iandae ithibati ya kuunga mkono kukiwepo shaka yoyote kuhusu usahihi wa rekodi iliyokuwa wazi. Yote haya yalishughulikiwa, “mbele yao,” kama mstari wa 13 usemavyo. Kwa hiyo ilikuwa shughuli ya biashara ya kisheria iliyoshuhudiwa hadharani. Basi, kwa wazi, ni kwa kielelezo cha Kimaandiko kwamba waabudu wa kweli hushughulikia mambo katika njia hiyo iliyothibitishwa na kuandikwa katika hati.
Ni jambo lifaalo pia. Twajua jinsi ulivyo wa kweli ule msemo kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11, NW) Hiyo yatia ndani Wakristo waliojitoa na walio waaminifu. Yakobo 4:13, 14 husema hivi: “Haya basi, ninyi msemao: ‘Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida,’ walakini hamjui yatakayokuwako kesho.” Kwa sababu hiyo, huenda tukaanza mradi fulani, kama vile kufanya ununuzi, kufanya kazi au utumishi tuliokubaliana, au kumtengenezea mtu fulani kitu. Lakini kesho—au mwezi ujao au mwaka ujao—utatokeza nini? Vipi ikiwa sisi au yule mtu mwingine angepata aksidenti? Hilo laweza kuonekana kufanya uwekaji wa ule mwafaka kuwa jambo lisilowezekana. Vipi ikiwa hatuwezi kufanya hiyo kazi au huo utumishi, au yule mtu mwingine aona haiwezekani kufanya malipo au kutimiza sehemu yake ya makubaliano? Ikiwa hakuna makubaliano yaliyoandikwa, matatizo halisi yangeweza kuzuka, yale ambayo yangaliweza kutatuliwa au yangaliweza kuepukwa kwa kuwa na mkataba sahili ulioandikwa.
Zaidi ya hayo, hatupaswi kusahau kwamba hali isiyo hakika ya sehemu nyingi za maisha yaweza hata kumaanisha kwamba mtu mwingine angelazimika kuchukua daraka au kufanya uamuzi wa mambo ya biashara yetu au ya yule mtu mwingine. Yakobo aliongeza hivi katika mstari wa 14: “Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka.” Kwa kweli, twaweza kufa bila kutazamia. Makubaliano yaliyoandikwa, mkataba, ungeweza hasa kuruhusu wengine kuendelea kushughulikia mambo ikiwa jambo lisilotazamiwa latukia katika upande wowote ule.
Katika maana fulani, hili pia laongoza kwenye sehemu ya tatu—mikataba iliyoandikwa ni yenye upendo. Kwa hakika, mhusika mmoja wa upande wowote ule akifa au kupata aksidenti yenye kulemaza, lingalikuwa jambo lenye upendo kwa Mkristo kuandaa rekodi iliyoandikwa ya wajibu wake na matarajio yake ya kifedha. Na badala ya kuonyesha ukosefu wa tumaini, hilo huonyesha upendo kwa yule ndugu ambaye tunashughulika naye kufanya mkataba ulioandikwa ambao utataarifu waziwazi na lile hasa analowajibishwa kufanya au kile anachoweza kupokea. Hatua hii yenye upendo itapunguza kisababishi chochote cha hisia zenye uchungu au chuki ikiwa mmoja wa wahusika wasiokamilika asahau mambo fulani au madaraka fulani. Na ni nani kati yetu aliye mkamilifu, asiyesahau, au asiyeelekea kufahamu kimakosa mambo au nia fulani?—Mathayo 16:5.
Kuna njia nyinginezo ambazo tungeweza kuendelea kutaja ambazo kwazo kufanya makubaliano ya kibiashara yaliyoandikwa huonyesha upendo kwa ndugu yetu, kwa familia yetu, na kwa kutaniko kwa ujumla. Lakini lazima ieleweke wazi kwamba zaidi ya kuwa jambo lenye upendo, rekodi hizo zilizoandikwa kwa habari inayotosha ni jambo lifaalo na la Kimaandiko.