Kudumisha Umoja wa Kikristo Katika Mahusiano ya Kibiashara
“Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja.”—ZABURI 133:1.
1. Kwa sababu gani umoja wa Kikristo ni wenye kutamanika sana?
KWELI kweli ni jambo ‘jema na la kupendeza ndugu Wakristo wakae pamoja kwa umoja,’ hasa leo wakati ambao kuna ukosefu mwingi sana wa umoja ulimwenguni. Mahali palipo na wingi wa umoja wa kweli, umoja huo unakuwa jambo lenye sura ya kupendeza, ukitokeza kifungo cha karibu sana cha upendo wa kidugu kati ya watu, na kufanya iwe furaha mtu kushirikiana na mwenzake. Kwa upande ule mwingine, ukosefu wa umoja una sura mbaya na unatokeza hali ya kutofurahia watu? chuki, na kuvunja urafiki kati ya washirika.
2. Maoni yetu ya ujumla juu ya kanuni za Biblia yanapasa yaongezeje umoja wetu wa kidugu hata katika mambo ya kibiashara?
2 Wakati Wakristo wanapojihusisha katika mambo ya kibiashara pamoja na watumishi wengine wa Yehova, maoni yao wote kwa ujumla juu ya kanuni za Biblia yanapasa yaongeze umoja wao wa kidugu. Mwangalizi mmoja katika kundi moja la Mashahidi wa Yehova alieleza jambo hilo kwa njia hii: “Wakati ulimwengu unapozidi kuwa usiotumainika, inaburudisha kufanya kazi pamoja na Wakristo wenzetu wenye kufuata kanuni. Inakuwa si lazima sisi ‘tujihadhari’ kila dakika. Washiriki wa kibiashara walio safi na wanyofu wanazidi kuwa adimu katika mfumo huu. Inapendeza kama nini kufanya kazi pamoja na watu wanyofu wasiovuta tumbako au wasiotumia msemo mchafu, watu wenye kujiweza, ambao jambo kuu linalowasukuma si pupa ya kupata vitu vya kimwili.”
3. (a) Ni mahusiano gani ya kibiashara yanayotia ndani waamini wenzetu? (b) Ni kanuni gani ambazo ni lazima ziongoze shughuli za kibiashara?
3 Ni sehemu gani za mahusiano ya kibiashara ambayo huenda yakatia ndani waamini wenzetu? Moja ni ambapo Wakristo wawili au zaidi wanaamua kuingia katika shughuli fulani ya kibiashara wakiifanya kishirika. Nyingine ni ambapo mmoja ni mwajiri-kazi na yule mwingine ni mwajiriwa-kazi. Na bado nyingine ni ambapo Mkristo anatolea mwamini mwingine bidhaa fulani au utumishi. Katika yo yote ya shughuli hizo za kibiashara, kanuni za unyofu na ukamilifu zilizoandikwa katika Neno la Yehova lenye uongozi wa roho yake ni lazima ziongoze vitendo vyao. Kwa njia hiyo umoja wa kidugu na furaha ya kufanya kazi pamoja vinaongezewa.—1 Wakorintho 10:31.
4. Ni hatari gani iliyopo kwa Wakristo walio katika biashara?
4 Lakini, hatari ipo ya kwamba huenda wengine wakakosa kuendeleza maoni ya Kikristo yaliyoinuka. Huenda wakaanza kufikiria mno mapendezi yao wenyewe. (Wafilipi 2:4) Huenda pesa zikawa za maana kuliko umoja wa Kikristo. Lakini uchoyo katika biashara unaweza kuharibu mahusiano ya kidugu na uhusiano wa mtu pamoja na Yehova. Tusingetaka kamwe jambo hilo litukie!—Yohana 13:34, 35; Waebrania 13:5; 1 Timotheo 3:2, 3; 1 Yohana 3:16; 4:20, 21.
Umaana wa Mapatano Rasmi
5. Jambo lililopata Abrahamu katika kununua shamba linaonyeshaje ubora wa kuwa na mapatano rasmi?
5 Ili kusaidia kuzuia hali za kutoelewana katika shughuli za kibiashara, fikiria jinsi Abrahamu alivyonunua kipande cha shamba. Yeye “akampimia Efroni ile fedha aliyotaja masikioni mwa bani Hethi, shekeli za fedha mia nne ya namna inayotumika na wenye biashara. Basi shamba la Efroni lililokuwa katika Makpela . . . viliyakinishwa kuwa mali yake [Abrahamu], mbele ya bani Hethi, mbele ya watu wote waingiao katika mlango wa mji wake.” Hayo hayakuwa mapatano ya faraghani yenye kufanywa kwa uungwana wa wanaume ati. Yalikuwa mapatano rasmi, yaliyoyakinishwa (yaliyothibitishwa) mbele ya mashahidi. Hakukuwa na kutokuelewana juu ya kilichokuwa kimenunuliwa na bei barabara iliyotolewa.—Mwanzo 23:2-4, 14-18.
6. Wakristo wanaweza kufanyaje shughuli za kibiashara za maana ziwe rasmi?
6 Vivyo hivyo, ni jambo la hekima Wakristo wafanye shughuli za maana ziwe rasmi. Ikiwa shughuli yenyewe inahusu kuuza bidhaa fulani, wanaohusika wanaweza kuandika kilichouzwa, bei yacho,njia itakayotumiwa kulipa wakati na jinsi gani bidhaa hiyo itakavyopelekwa, na masharti mengine yaliyokubaliwa. Ikiwa linalohusika ni utumishi fulani unaopasa kufanywa, wanaohusika wanaweza kuandika ni kazi gani itakayofanywa, ni wakati gani inapopasa kumalizwa, bei kwa kuifanya, na mambo mengine. Hati hiyo inayoandikwa inapasa iwe na tarehe na kutiwa sahihi, na nakala inapasa iwekwe na pande zote mbili zinazohusika. Mapatano hayo yaliyoandikwa ni ya maana sana hasa katika biashara ya kishirika. Inasaidia watu wa pande zote mbili waelewe uhusiano wao waziwazi na kuwasaidia waishi kupatana na shauri hili la Yesu: “Maneno yenu yawe Ndiyo, ndiyo; Siyo, siyo.”’(Mathayo 5:37) Katika mambo yanayohusu hali zilizo ngumu zaidi kushughulikiwa, inaweza kufaa zaidi kutafuta msaada wa wastadi wa kibiashara katika kutayarisha mapatano yanayoandikwa.
7. (a) Ni jambo gani jingine ambalo ni lazima lifikiriwe kuhusu mapatano ya kuandikwa? (b) Wakristo wanapaswa waendeshe mambo ya kibiashara wakiwa na roho gani?
7 Wanapopanga rasmi mapatano yaliyoandikwa, wanaohusika hawapaswi kufikiria malengo yao tu bali pia mambo yanayoweza kutokea, kama vile jinsi ya kukomesha mpango huu ikiwa uhitaji wa lazima umetokea. (Mithali 21:5, NW) Shughuli zote za kibiashara zina kiasi fulani cha hatari, na hakuna hati inayoweza kutia ndani kila hali inayoweza kutokea. Ikiwa hali zinabadilika, huenda ikawa lazima mapatano yale yafanyiwe marekebisho au yafanywe upya. Baada ya muda, huenda hata ikaonekana wazi kwamba mmoja amejitia katika wajibu wa kibiashara bila hekima na huenda ikawa lazima ajiondoe humo kwa njia yenye kuheshimika. Lakini, hiyo isiwe njia iliyotungwa tu ili kuepuka daraka la kulipa madeni aliyoyapata kwa sababu ya yeye mwenyewe kuponda mali au kuwa na usimamizi mbaya. Jambo hilo linahitaji kuzungumzwa ili kuona kama mapatano yale yanaweza kuvunjwa na ni malipano gani ya pesa yanayohitaji kufanywa, kama kuna yo yote. Ingawa hivyo, kwa uhakika mtu mwenye kufanya mambo kulingana na dhamiri atatenda yote anayoweza ili aheshimu wajibu mbalimbali ulioandikwa katika mkataba, hata ikiwa ni lazima apunguze mtindo wake wa maisha kwa muda fulani. (2 Wathesalonike 3:12) Ikiwa Mkristo anataka kutembea bila kosa na kuzoea uadilifu, atajaribu kutimiza wajibu wake mbalimbali katika mapatano hata ingawa kufanya hivyo hakutakuwa kumemfaidi sana, lakini atafanya hivyo ili aendelee kuwa na kibali cha Yehova. “Ingawa ameapa kwa hasara yake, hayabadili maneno yake.” (Zaburi 15:1-4) Katika hatua zote hizo, watumishi wa Yehova wanahitaji kuacha ‘mambo yao yote yatendeke katika upendo.’—1 Wakorintho 16:14.
8. Kwa sababu gani ni vizuri ‘kuhesabu gharama’ kabla ya kuingia katika uhusiano wa kibiashara?
8 Kwa sababu hiyo, kabla ya kuingia katika uhusiano wa kibiashara ni vizuri kuhesabu gharama. (Luka 14:28-30) Huenda wengine wakajitumbukiza katika biashara wakiwa na matazamio mazuri lakini waje kutatizwa sana na magumu ambayo hawakuwa wameona. Kwa mfano, wengine wamehisi kwamba faida zilizochumwa na waajiri wao wa kazi zingaliweza kuwa zao kama wao wangalikuwa na biashara yao wenyewe inayofanana na hiyo. Lakini walikosa kutambua kwamba usimamizi wa biashara si jambo rahisi katika ulimwengu huu wa mashindano ya kikatili. Kila mwaka makumi ya maelfu ya biashara zanafilisika katika sehemu zote za ulimwengu. Hivyo, baada ya Wakristo wengi kupatwa na hali za kuwakatisha tamaa vikali katika shughuli za kibiashara, wao wamepata kitulizo kwa kuwa tena waajiriwa-kazi wakiwa na mshahara usiobadilika-badilika.
Kuheshimu Mahusiano ya Kibiashara
9. Ni njia zipi ambazo katika hizo Wakristo wanaweza kuonyeshana heshima kazini?
9 “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” Linasema andiko la Warumi 12:10 (NW). Wakristo waajiriwa-kazi wanaofanya hivyo hawangejaribu kumtumia kwa faida yao wenyewe mwajiri-kazi wao ati kwa sababu yeye ni Shahidi mwenzao, huku wakifuata mwelekeo wa ulimwengu kwamba kwa kuwa mwajiri-kazi ana uwezo, inampasa avumilie hali za kupungukiwa za waajiriwa-kazi wake. Badala ya kufanya hivyo, wangemwonyesha heshima mwajiri-kazi wao kwa mwelekeo wao na kazi ya bidii. (1 Timotheo 6:2) Halafu tena, Wakristo ambao ni waajiri-kazi wangeheshimu Mashahidi wenzao ambao ni waajiriwa-kazi kwa jinsi wanavyosema nao na kushughulika nao. Mwajiri-kazi hapaswi kamwe kuhisi kwamba yeye yuko juu ya mwamini mwenzake anayemfanyia kazi bali anapaswa kukumbuka kwamba wote wawili ni watumwa wa Yehova, walio sawa machoni Pake. (Waefeso 6:9) Pia, wote wawili, mwajiri-kazi na mwajiriwa-kazi wanapaswa sikuzote wazingatie shauri hili kwenye Wagalatia 6:10: “Na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.”
10. Unyenyekevu unasaidiaje katika kuonyeshana heshima?
10 Si vigumu kuonyesha heshima mahali ambapo pana wingi wa unyenyekevu. Kwa mfano, mzee mnyenyekevu katika kundi la Kikristo hataona ni jambo gumu katika biashara kujitiisha mwenywe chini ya mwelekezo wa Mkristo mwenzake asiye na mapendeleo yale yale katika kundi. Halafu tena, mwajiri-kazi aliye mnyenyekevu hataona ni jambo gumu kujitiisha mwenyewe kwa mwajiriwa-kazi wake, aliye mzee, katika shughuli za kundi. Pia, unyenyenkevu utaendelea kuzuia wote wawili wasiwe wakilaumiana kupita kiasi au kutazamia mwingine kuwa na ukamilifu, kwa kuwa “wote wamefanya dhambi na hupungukiwa na utukufu wa Mungu.—Warumi 3:23; 12:3, NW.
11. Wakristo wanaweza kuonyeshaje kiasi katika mambo ya kibiashara?
11 Biblia inaamuru hivi pia: “Acheni kiasi chenu kijulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5, NW) Halingekuwa jambo la kiasi Mkristo aliye katika biashara kutazamia mapendeleo ya pekee au apewe kazi bora au sikuzote auziwe vitu kwa bei zilizo chini zaidi kwa sababu tu yeye anashughulika na mwamini wenzake. Wala haimpasi Mkristo atazamie kwamba ana haki ya kupata wakati fulani wa kutokufanya kazi au mapendeleo mengine, kama vile kutumia mashine au magari ati, kwa sababu mwajiri-kazi wake ni mwamini mwenzake. Huenda hali za kupendelewa, kupewa kazi kubwa kuliko wengine, kuuziwa vitu kwa bei za chini, au kupewa wakati wa kutokufanya kazi zikaja lakini hazipasi kudaiwa. Matazamio yasiyo ya kiasi yanaweza kusababisha udhia kati ya Wakristo, yaharibu uhusiano wao.—Mithali 18:19.
12. Ni uangalifu gani unaohitaji kufanywa katika mahali pa kazi?
12 Ingawa Wakristo wanataka kujulisha watu wasioamini habari njema za Ufalme wa Mungu, mahali pa kazi wanapaswa wajizoeze uangalifu ili kutoa ushuhuda wa Ufalme kwa njia hiyo kufanywe katika wakati unaofaa. (Mhubiri 3:1, 7) Kukifanywa saa za kazi, na iwe hivyo kwa kibali cha mwajiri-kazi. Ama sivyo mwajiri-kazi huenda asifurahishwe na jambo hilo, na hilo lingeweza kuleta suto juu ya Yehova na watu wake. (1 Timotheo 6:1) Kuna nyakati nyingine, kama vile wakati wa chakula cha mchana au vipindi vya pumziko kazini, ambapo ushuhuda huo unaweza kutolewa. Pia, mahali ambako kuna Mashahidi kadha katika kazi hiyo, wao hawangetaka watumie wakati wakisemezana juu ya mambo ya kitheokrasi ambao wamepaswa wautumie wakifanya kazi.
Kulinda Makusudio ya Kufanya Biashara
13. Paulo na wenye nyumba waliomkaribisha katika Korintho waliionaje kazi yao ya kimwili?
13 Mtume Paulo alipokuwa katika Korintho, aliingia katika uhusiano wa kibiashara pamoja na Wakristo waliomkaribisha nyumbani kwao, yaani, Akila na Prisila. (Matendo 18:1-3) Wao walifanya kazi ili wapate mahitaji ya maisha, lakini kufanya hivyo kulikuwa jambo la pili kwa lengo lao lililo kubwa—kuendeleza ibada ya Yehova. Hakika hawangeweza kushtakiwa juu ya ‘kudhani ya kuwa utawa ni njia ya kupata faida ya kimwili.’ (1 Timotheo 6:5) Wote watatu walibarikiwa sana na Yehova na wanatajwa kwa njia nzuri katika Biblia.—Warumi 16:3-5.
14. (a) Kwa sababu gani ni vizuri kuchunguza makusudio kabla ya kuingia katika shughuli ya kibiashara? (b) Mashahidi watatu walitatuaje tatizo lao?
14 Kwa kuchunguza makusudio yetu kwa uangalifu kabla ya kuingia katika shughuli ya kibiashara, Mkristo anaweza kuepuka magumu mengi. Kwa mfano, huenda Mkristo mmoja akataka apate wakati mwingi zaidi ili kuendeleza faida za Ufalme, hali mwenzake huenda akataka kufanyia maendeleo mtindo wake wa maisha. Huenda mmoja akataka kwamba faida zikipatikana zirudishwe tena benki ili kuikuza biashara, lakini yule mwingine yuko tayari kulipa kodi nyingi zaidi lakini wasirudishe faida zao benkini ili kuepuka kujihusisha na mambo mengi zaidi. Katika nchi moja, watatu wa Mashahidi wa Yehova waliokuwa pia na uhusiano wa kimwili wakawa na biashara kishirika. Lakini baada ya muda fulani maoni yao yalitofautiana juu ya kadiri ambayo kila mmoja wao alitaka kujihusisha mwenyewe katika biashara. Walitatua tatizo lao kwa uamuzi wa pamoja wa kutenganisha shughuli zao za kibiashara na kugawana wateja wao. Kwa njia hiyo walihifadhi uhusiano wao wa kiroho na pia wa kijamaa. Wao walikuwa wametii shauri la Biblia la ‘kufuata mambo ya amani na mambo yafaavyo kwa kujengana.’—Warumi 14:19.
15. Kwa sababu gani ni lazima hasa tujihadhari na makusudio yetu kuhusu pesa?
15 Mtu anapaswa atumie uangalifu wa pekee katika kulinda kusudio lake kuhusu pesa. Biblia inatuhakikishia kwamba “mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele; lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa [hatabaki akiwa bila hatia, NW].” (Mithali 28:20) Kwa ‘kufanya haraka awe tajiri,’ Mkristo anaweza kupofuka asione jambo fulani lililo la thamani kubwa zaidi—udugu wake wa Kikristo. Jambo hilo linaweza kusababisha ukosefu wa umoja katika kundi, kwa kuwa huenda wengine wasifurahie jinsi anavyotanguliza pesa kuliko faida za Ufalme. Hivyo Biblia inaonya hivi: “Wale wenye kuazimia wawe matajiri wanaanguka katika kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kujaa madhara, zinazotumbukiza wanadamu katika uharibifu na maangamizi. Kwa maana kupenda pesa ni mzizi wa mambo ya namna zote yenye kudhuru, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo watu fulani wamepotezwa kutoka kwenye imani na wamejichoma-choma wenyewe mwili wote kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10, NW.
16. Ni lazima mambo yote ya kibiashara yaongozweje?
16 Njia moja ambayo “kupenda pesa” kunaweza kupoteza Mkristo ni kwa kumshawishi aanze kufuata mazoea ya kibiashara yasiyo ya kiadili au yenye ukosefu mkubwa wa unyofu. Wakati Wakristo wenzake wanapokuwa wamehusika katika biashara na mtu kama huyo, ukosefu wa umoja unaweza kutokea. Na mazoea hayo yanatia mtu katika hali ya kuharibu uhusiano wake na Yehova. Ili uhusiano wa kibiashara uendelee kwa ulaini, ni jambo la maana kuzingatia kwamba kupunja katika biashara “ni chukizo kwa [Yehova].” (Mithali 11:1; 20:23) Bali, Wakristo wanataka waweze kusema, kama alivyofanya mtume Paulo: “Sisi tunatumaini tuna dhamiri nyofu, kwa kuwa tunataka kujiendesha wenyewe kwa unyofu katika mambo yote.”—Waebrania 13:18, NW.
Kutatua Matatizo Mazito ya Kibiashara
17. Matatizo mengine madogo-madogo ya kibiashara yanaweza kutatuliwaje?
17 Katika uhusiano wo wote wa kibiashara kati ya akina ndugu, matatizo yanaweza kutokea. Mengine ya matatizo madogo-madogo yanaweza kutatuliwa kwa kutumia tu kanuni iliyo kwenye 1 Petro 4:8 (NW), inayosema hivi:‘“Zaidi ya mambo yote, mwe na upendo mwingi sana kwa mmoja na mwenzake, kwa sababu upendo unafunika wingi wa dhambi.” Ikiwa matatizo hayawezi kutatuliwa kwa njia hiyo, hayapasi yaruhusiwe kutunga usaha na kuwa mabaya zaidi. Kuyaruhusu kungeweza kufanya kuheshimiana kupotee na kuleta mfarakano. Mara nyingi utatuzi unategemea kupashana habari kwa fadhili na kwa kuelezana mambo waziwazi kabla hali haijawa mbaya zaidi. Neno la Mungu linatushauri tumalize magombano upesi.—Mathayo 5:23-25; Waefeso 4:26, 27.
18. Mkristo anaweza kufanya nini ikiwa anaamini amekosewa kwa uzito katika biashara na Mkristo mwenzake?
18 Hata hivyo, wakati Mkristo anapoamini kwamba amekosewa kwa uzito na mwamini mwenzake katika biashara, zile hatua zilizopangwa kwenye Mathayo 18:15-17 zinapasa zifuatwe kwa uangalifu. Hatua ya kwanza au mbili hivi zinapasa kumaliza jambo lile. Ikiwa sivyo, ile hatua ya tatu ingekuwa ya wazee waliowekwa rasmi wachunguze jambo hilo. Ikitukia hivyo, wazee wangewavunja moyo akina ndugu kwa mkazo mwingi wasihusike katika kushtakiana mahakamani. Kushtaki mwamini mwenzako mahakamani kungemaanisha, kama vile Paulo alivyosema, “Ushinde kabisa kwenu ninyi.” Yeye aliongeza hivi: “Kwa nini badala ya kufanya hivyo msijiache mkosewe? Kwa nini badala ya kufanya hivyo msijiache mpunjwe?” (1 Wakorintho 6:1-8, NW) Ni afadhali kupatwa na hasara ya kifedha badala ya kuleta suto juu ya jina la Yehova na kundi na kuvuruga umoja wetu kwa kupeleka mwamini mwenzetu mahakamani. Bila shaka, huenda ikahitajiwa kabisa kwamba kundi lichukue hatua ya namna fulani ikiwa ukosefu wa unyofu unahusika, hata ingawa hatua ya mahakama haikuchukuliwa.
19. Ni mifano gani bora kabisa ya Biblia ambayo wazee wanaweza kuelekezea wanapotoa mashauri juu ya matatizo ya kibiashara?
19 Wakati wazee wanaposhauri wale walio na magumu ya kibiashara, wangeweza kuwaelekeza kwenye mfano usio wa ubinafsi uliowekwa na Abrahamu wakati uhusiano wake na Loti ulipokaribia kuharibika. Ingawa Abrahamu ndiye aliyekuwa na umri mkubwa zaidi, yeye alimfadhili Lutu kwa kumpa uchaguzi wa kwanza wa nchi badala ya kujasiria kutia pengo katika uhusiano wao. (Mwanzo 13:5-11) Wazee wangeweza pia kuelekeza kwenye mfano mwema wa Zakayo. Yeye alikuwa na nia ya kuwapa maskini nusu ya mali zake kisha kwa nusu ile nyingine arudishe mara nne vita alivyokuwa amenyang’anya watu kwa shtaka la uwongo.—Luka 19:1-10; ona pia 1 Wakorintho 10:24.
20, 21. Ni jambo gani ambalo ni lazima lizingatiwe akilini kwanza kabisa juu ya utendaji wa kimwili?
20 Ni Jambo Zuri kama nini wakati Wakristo wanapomaliza kwa matokeo mazuri matatizo ya kibiashara kwa kufuata shauri la Biblia kwa uangalifu! Kwa njia hiyo wao wanabaki wakiwa na umoja hata wakati shughuli za kibiashara zisipofanikiwa. Hayo ndiyo yatakayokuwa matokeo yenye kufurahisha tunapozingatia akilini kwanza kabisa nyakati zote kwamba kwa Wakristo, utendaji wa kimwili unachukua nafasi ya pili kwa faida za Ufalme na umoja wa kidugu. Ni jambo zuri sana pia wakati shughuli za kibiashara zinapoweza kupangwa ili kuruhusu wakati mwingi zaidi kwa mambo yaliyo ya maana zaidi yanayohusiana na utendaji wa Ufalme.—Mathayo 6:33; linganisha Wafilipi 1:9, 10.
21 Hivyo, jambo lililo la maana kweli kweli katika maisha zetu ni uhusiano wetu kwa Yehova na kwa udugu wetu wa Kikristo. (Mathayo 22:36-39) Hatungetaka kamwe uhusiano huo uharibiwe na mavutano ya kilimwengu au mambo ya kibiashara, kwa sababu hakuna jambo lo lote kamwe kamwe linaloweza kulinganishwa na uhusiano wetu na Yehova au linaloweza kufanana na uzuri wa udugu wetu wenye umoja!
Maulizo ya Kurudia
◻ Kutii Neno la Mungu kunaongezaje uhusiano wa kibiashara?
◻ Kwa sababu gani ni jambo la hekima kufanya shughuli za maana ziwe rasmi?
◻ Wakristo wanaweza kuonyeshanaje heshima kazini?
◻ Kwa sababu gani tuchunguze makusudio yetu katika biashara?
◻ Ni mielekeo gani inayopasa kuonyeshwa katika kumaliza matatizo ya kibiashara?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Abrahamu alithibitisha ununuzi wa nchi kwa mapatano rasmi pamoja na Efroni
[Picha katika ukurasa wa 18]
Kufanya kazi ili kupata riziki kulikuwa jambo lenye umaana wa pili kwa Paulo, Akila, na Prisila