Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w97 3/15 kur. 17-22
  • Acha Ufahamu Ukulinde Salama

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Acha Ufahamu Ukulinde Salama
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uhitaji wa Pekee wa Kupata Ufahamu
  • Namna Gani Kuweka Fedha Katika Biashara ili Kupata Faida?
  • Wakati Ambapo Biashara za Kujasiria Hazifaulu
  • Namna Gani Kukiwa na Upunjaji?
  • Ufahamu na Kufanywa kwa Maamuzi
  • Elekeza Moyo Wako Kwenye Ufahamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Je, Waweza Kusitawisha Ufahamu Zaidi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Kudumisha Umoja wa Kikristo Katika Mahusiano ya Kibiashara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • “Bwana Huwapa Watu Hekima”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
w97 3/15 kur. 17-22

Acha Ufahamu Ukulinde Salama

“Busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi [“utakulinda salama,” “NW”].”—MITHALI 2:11.

1. Ufahamu waweza kutulinda salama dhidi ya nini?

YEHOVA ataka udhihirishe ufahamu. Kwa nini? Kwa sababu ajua kwamba sifa hiyo itakulinda salama dhidi ya hatari mbalimbali. Mithali 2:10-19 yaanza kwa kusema: “Hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yatakupendeza nafsi yako; busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi.” Utakulinda salama dhidi ya nini? Dhidi ya mambo kama ile “njia ya uovu,” wale wanaoacha mapito manyoofu, na watu wenye vipengee katika mwendo wao wa kawaida.

2. Ufahamu ni nini, na Wakristo watamani upi hasa?

2 Yamkini utakumbuka kwamba ufahamu ni uwezo wa akili ambao kwao hiyo akili yaweza kutofautisha kati ya jambo moja na jingine. Mtu mwenye ufahamu huona tofauti kati ya mawazo au mambo mbalimbali na aweza kuamua mambo vizuri. Tukiwa Wakristo, twatamani kuwa na ufahamu wa kiroho hasa unaotegemea ujuzi sahihi wa Neno la Mungu. Tunapojifunza Maandiko, ni kana kwamba twachimbua matufali ya kujengea ufahamu wa kiroho. Yale tunayojifunza yaweza kutusaidia kufanya maamuzi yanayompendeza Yehova.

3. Twaweza kujipatiaje ufahamu wa kiroho?

3 Mungu alipomwuliza Mfalme Solomoni wa Israeli ni baraka gani aliyotaka, yule mtawala mchanga alisema: “Nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua [“kufahamu kati ya,” NW] mema na mabaya.” Solomoni aliomba apewe ufahamu, naye Yehova akampa sifa hiyo kwa kadiri isiyo ya kawaida. (1 Wafalme 3:9; 4:30) Ili kujipatia ufahamu, twahitaji kusali, na ni lazima tujifunze Neno la Mungu kwa msaada wa vichapo vyenye kuelimisha vinavyoandaliwa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Hilo litatusaidia kukuza ufahamu wa kiroho kwa kadiri ya kwamba tutakuwa “watu wazima katika nguvu za kuelewa,” wawezao “kupambanua [au, kufahamu kati ya] mema na mabaya.”—1 Wakorintho 14:20; Waebrania 5:14.

Uhitaji wa Pekee wa Kupata Ufahamu

4. Kuwa mwenye jicho “sahili” kwamaanisha nini, nalo laweza kutunufaishaje?

4 Tukiwa na ufahamu ufaao, twaweza kutenda kwa kupatana na maneno haya ya Yesu Kristo: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu], na vitu vingine vyote hivi [vya kimwili] mtaongezewa.” (Mathayo 6:33) Yesu alisema hivi pia: “Taa ya mwili ni jicho lako. Wakati jicho lako ni sahili, mwili wako wote ni mwangavu pia.” (Luka 11:34) Jicho ni taa ya kitamathali. Jicho lililo “sahili,” ni lenye unyoofu, lenye kuelekezwa upande mmoja tu. Tukiwa na jicho kama hilo, twaweza kuonyesha ufahamu na kutembea bila kujikwaa kiroho.

5. Kwa habari ya shughuli za kibiashara, twapaswa kukumbuka nini juu ya kusudi la kutaniko la Kikristo?

5 Badala ya kuweka jicho lao sahili, watu fulani wamevuruga maisha zao na maisha za wengine kwa shughuli za kibiashara zenye kushawishi. Lakini twapaswa kukumbuka kwamba kutaniko la Kikristo ni “nguzo na tegemezo la ile kweli.” (1 Timotheo 3:15) Sawa na nguzo za jengo, kutaniko hutegemeza kweli ya Mungu, halitegemezi shughuli za kibiashara za mtu yeyote yule. Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova hayakuanzishwa ili yawe mahali mbalimbali pa kuendelezea masilahi, bidhaa, au huduma za kibiashara. Twapaswa kuepuka kufuatia mambo ya biashara ya kibinafsi katika Jumba la Ufalme. Ufahamu watusaidia kuona kwamba Majumba ya Ufalme, Mafunzo ya Kitabu ya Kutaniko, makusanyiko, na mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova ni mahali mbalimbali pa ushirika wa Kikristo na pa mazungumzo ya kiroho. Ikiwa tungetumia mahusiano ya kiroho ili kuendeleza namna yoyote ya ubiashara, je, hilo lisingeonyesha angalau ukosefu fulani wa uthamini kuelekea mambo ya kiroho? Mahusiano ya kikutaniko hayapasi kutumiwa kamwe ili kupata faida ya kifedha.

6. Kwa nini bidhaa na huduma za kibiashara hazipasi kuuzwa au kuendelezwa kwenye mikutano ya kutaniko?

6 Watu fulani wametumia mahusiano ya kitheokrasi ili kuuza dawa au vipodozi, bidhaa za vitamini, huduma za uwasiliano wa simu, vifaa vya ujenzi, mipango ya kusafiri, programu na vifaa vya kompyuta, na kadhalika. Hata hivyo, mikutano ya kutaniko si mahali pa kuuzia au pa kuendelezea bidhaa au huduma za kibiashara. Twaweza kufahamu kanuni ya msingi tukikumbuka kwamba Yesu “aliondosha nje ya hekalu wale wote wenye kondoo na ng’ombe, naye akamwaga sarafu za wabadili-fedha na kupindua meza zao. Naye akawaambia wale wenye kuuza njiwa: ‘Ondoleeni mbali vitu hivi kutoka hapa! Komeni kufanya nyumba ya Baba yangu kuwa nyumba ya bidhaa za biashara!’”—Yohana 2:15, 16.

Namna Gani Kuweka Fedha Katika Biashara ili Kupata Faida?

7. Kwa nini ufahamu na hadhara zahitajiwa kuhusiana na habari ya mipango ya kuweka fedha katika biashara ili kupata faida?

7 Ufahamu na hadhari zinahitajiwa wakati mtu anapofikiria kuweka fedha katika biashara ya kujasiria ili kupata faida. Tuseme mtu ataka kukopa fedha na atoa ahadi za namna hii: “Nakuhakikishia kwamba utapata faida.” “Huwezi kukosa faida. Hili ni jambo hakika.” Jihadhari mtu atoapo mahakikishio kama hayo. Ama haoni mambo kihalisi ama yeye si mwenye kufuatia haki, kwa kuwa ni nadra kwamba kuweka fedha katika biashara kunakuwa jambo hakika. Kwa kweli, watu fulani wasio wanyoofu, wenye kusema kwa kurairai wamepunja washiriki wa kutaniko. Hilo latukumbusha wale “watu wasiomwogopa Mungu” waliopenyeza katika kutaniko la karne ya kwanza, ‘wakageuza fadhili isiyostahiliwa ya Mungu kuwa sababu ya kujitetea kwa ajili ya mwenendo mlegevu.’ Walikuwa kama miamba yenye ncha kali iliyofichwa chini ya maji ambayo ingeweza kurarua na kuua waogeleaji. (Yuda 4, 12) Ni kweli, makusudio ya wapunjaji ni tofauti, lakini wao pia huwinda washiriki wa kutaniko.

8. Ni jambo gani limetendeka kwa kuhusiana na biashara za kujasiria zionekanazo kuwa zenye kuleta faida?

8 Hata Wakristo wenye nia njema wameshiriki pamoja na Wakristo wengine habari juu ya biashara za kujasiria zionekanazo kuwa zenye kuleta faida, lakini wamepata kugundua tu kwamba wao pamoja na wale wanaofuata kielelezo chao wamepoteza fedha walizoweka katika biashara hizo. Tokeo ni kwamba, Wakristo kadhaa wamepoteza mapendeleo kutanikoni. Biashara za kujasiria za kutajirika-haraka zinapothibitika kuwa miradi ya upunjaji, mtu pekee apataye faida ni yule mpunjaji, ambaye mara nyingi hutoweka upesi. Ufahamu waweza kumsaidiaje mtu kuepuka hali kama hizo?

9. Kwa nini ufahamu wahitajiwa ili kuchanganua madai juu ya mipango ya kuweka fedha katika biashara ili kupata faida?

9 Ufahamu humaanisha kuweza kuelewa kile kilichofichika. Uwezo huo wahitajiwa ili kuchanganua madai juu ya mipango ya kuweka fedha katika biashara ili kupata faida. Wakristo huwa na itibari kati yao, na huenda baadhi yao wakasababu kwamba ndugu na dada zao wa kiroho wasingejihusisha katika biashara za kujasiria ambazo zingehatarisha mali za waamini wenzao. Lakini uhakika wa kwamba mfanyabiashara ni Mkristo hautoi uhakikisho kwamba yeye atafaulu kupita wengine katika mambo ya biashara au kwamba shughuli yake ya biashara itafanikiwa.

10. Kwa nini Wakristo fulani hujaribu kupata mikopo ya biashara kutoka kwa waamini wenzao, na tokeo la mipango hiyo ya kuweka fedha katika biashara ili kupata faida lingeweza kuwa nini?

10 Wakristo fulani hujaribu kupata mikopo ya biashara kutoka kwa waamini wenzao kwa sababu mashirika makubwa ya kutoa mikopo yasingetolea mikopo biashara zao zenye kujasiria. Wengi wamepumbazwa kuamini kwamba kwa kuweka tu fedha zao katika biashara, wangeweza kuwa na mafanikio ya haraka, bila kufanya kazi nyingi au labda bila kufanya kazi yoyote kabisa. Watu fulani wanavutiwa kuweka fedha katika biashara kwa sababu ya msisimko unaohusianishwa na kufanya hivyo, lakini wanapata tu kupoteza akiba zao za fedha zilizokusanywa kwa muda mrefu! Mkristo mmoja aliweka kiasi kikubwa cha fedha katika biashara, akitarajia kupata faida ya kiwango cha asilimia 25 baada ya majuma mawili tu. Alipoteza fedha hizo zote wakati kampuni hiyo ilipotangazwa kuwa imefilisika! Katika biashara nyingine ya kujasiria, msitawishaji wa mashamba na majengo alikopa fedha nyingi kutoka kwa wengine kutanikoni. Aliahidi kuwapa wakopeshaji hao faida kubwa kupita kiasi lakini alifilisika, akapoteza fedha alizokopa.

Wakati Ambapo Biashara za Kujasiria Hazifaulu

11. Paulo alitoa shauri gani kwa habari ya pupa na upendo wa fedha?

11 Kutokufaulu kwa biashara kumeongoza kwenye hali ya kukata tamaa na hata kwenye kupoteza hali ya kiroho kwa upande wa Wakristo fulani waliojihusisha katika biashara za kujasiria zisizo thabiti. Tokeo la kutoruhusu ufahamu uwalinde salama limekuwa maumivu ya moyoni na uchungu. Pupa imenasa watu wengi. ‘Pupa hata isitajwe miongoni mwenu, kama vile ifaavyo watu watakatifu,’ akaandika Paulo. (Waefeso 5:3) Na alionya hivi: “Wale waazimiao kuwa matajiri huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo. Kwa maana kupenda fedha ni mzizi wa mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikilia kupenda huku wengine wameongozwa wapotee njia kutoka kwenye imani na wamejichoma wenyewe kotekote kwa maumivu mengi.”—1 Timotheo 6:9, 10.

12. Wakristo wakifanya biashara kati yao, wao wapaswa kukumbuka nini hasa?

12 Ikiwa Mkristo angekuza upendo wa fedha, yeye angejisababishia madhara mengi ya kiroho. Mafarisayo walikuwa wapenda-fedha, na hicho ni kitabia cha watu wengi katika siku hizi za mwisho. (Luka 16:14; 2 Timotheo 3:1, 2) Kinyume cha hilo, njia ya maisha ya Mkristo yapaswa kuwa “bila upendo wa fedha.” (Waebrania 13:5) Bila shaka, Wakristo waweza kufanya biashara kati yao au kuanzisha biashara pamoja. Hata hivyo, wakifanya hivyo mazungumzo na mapatano yapasa kutenganishwa na mambo ya kikutaniko. Na mkumbuke: Hata miongoni mwa ndugu za kiroho, andikeni mapatano ya kibiashara sikuzote. Yenye kusaidia kwa habari hii ni makala “Andikeni!,” iliyochapishwa katika Amkeni! la Agosti 8, 1984, kurasa 14 hadi 16.

13. Ungetumiaje Mithali 22:7 kwa habari ya biashara za kujasiria?

13 Mithali 22:7 yatuambia: “Akopaye ni mtumwa wake akopeshaye.” Mara nyingi ni jambo lisilo la hekima kwetu kujiweka wenyewe au kuweka ndugu yetu katika hali hiyo ya kuwa mtumwa. Yeyote atuombapo tumkopeshe fedha kwa ajili ya biashara ya kujasiria, ingefaa kufikiria uwezo wake wa kurudisha fedha hizo. Je, yeye ajulikana kuwa mwenye kutegemeka na kutumainiwa? Bila shaka, twapaswa kutambua kwamba kutoa mkopo huo kungeweza kumaanisha kupoteza fedha kwa sababu biashara nyingi za kujasiria hazifaulu. Kuwa na mkataba kwenyewe hakuhakikishi mafanikio ya biashara hiyo ya kujasiria. Na kwa hakika si jambo la busara kwa yeyote kujasiria kukopesha fedha nyingi kwa shughuli fulani ya kibiashara kuliko kiasi cha hasara awezacho kustahimili.

14. Kwa nini twahitaji kuonyesha ufahamu ikiwa tumemkopesha fedha Mkristo mwenzetu ambaye biashara yake haifaulu?

14 Twahitaji kuonyesha ufahamu ikiwa tumemkopesha Mkristo fedha kwa sababu za kibiashara na hizo fedha zilipotezwa, ingawa mazoea ya kutokufuatia haki hayakuhusika. Ikiwa kutokufaulu kwa biashara hakukuwa kosa la mwamini mwenzetu aliyekopa hizo fedha, je, twaweza kusema kwamba tulikosewa? La, kwa sababu tulimpa mkopo huo kwa hiari, labda tumekuwa tukikusanya riba kutoka kwazo, na hakuna jambo la kutokufuatia haki ambalo limetendeka. Kwa kuwa kutokufuatia haki hakukuhusika, hatuna msingi wowote wa kuchukua hatua ya kisheria dhidi ya mkopaji. Kwa hakika, kungekuwa na manufaa gani kumshtaki kisheria Mkristo mwenzetu mwenye kufuatia haki aliyelazimika kufuata hatua ya kisheria ya kuwa na hali ya kufilisika kwa sababu biashara yake ya kujasiria yenye nia njema haikufaulu?—1 Wakorintho 6:1.

15. Ni mambo yapi yanayotaka kufikiriwa ikiwa hali ya kufilisika yatangazwa?

15 Nyakati nyingine wale wasiofaulu kibiashara hutafuta kitulizo kwa kutangaza wana hali ya kufilisika. Kwa kuwa Wakristo hawapuuzi madeni, hata baada ya kuondolewa madeni fulani kisheria, baadhi yao wamehisi wajibu wa kujaribu kulipa madeni yaliyofutwa ikiwa wakopeshaji wangekubali malipo. Lakini, namna gani ikiwa mkopaji alipoteza fedha za ndugu yake kisha akaishi kwa namna ya kufurahia anasa? Au namna gani ikiwa mkopaji alijipatia fedha za kutosha za kurudisha zile alizokopa lakini akapuuza huo wajibu wa kiadili ambao huenda akawa nao kuelekea ndugu yake kifedha? Basi kungekuwa na shaka juu ya sifa za ustahili za mkopaji za kutumikia katika cheo chenye madaraka kutanikoni.—1 Timotheo 3:3, 8; Ona Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1994, kurasa 30-31.

Namna Gani Kukiwa na Upunjaji?

16. Ni hatua zipi zaweza kuchukuliwa ikiwa twaonekana kuwa wahasiriwa wa upunjaji wa kibiashara?

16 Ufahamu watusaidia kung’amua kwamba faida hazitokani na kila mpango wa kuweka fedha katika biashara ili kupata faida. Lakini namna gani ikiwa upunjaji unahusika? Upunjaji ni “kule kutumia kimakusudi udanganyifu, hila, au upotoshaji wa kweli kwa kusudi la kushawishi mtu mwingine kutoa kitu fulani chenye thamani kilicho chake au kuacha haki fulani ya kisheria.” Yesu Kristo aliorodhesha hatua ziwezazo kuchukuliwa mtu anapoona amepunjwa na mwabudu mwenzake. Kulingana na Mathayo 18:15-17, Yesu alisema hivi: “Ndugu yako akifanya dhambi, nenda ufunue wazi kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako. Lakini ikiwa yeye hasikilizi, chukua pamoja nawe mmoja au wawili zaidi, ili kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila jambo lipate kuthibitishwa. Ikiwa yeye hawasikilizi wao, liambie kutaniko. Ikiwa hasikilizi hata kutaniko, mwache awe kwako kama vile mtu wa mataifa na kama mkusanya-kodi.” Kielezi ambacho Yesu alitoa baada ya hapo chaonyesha kwamba alikuwa akifikiria dhambi kama zile zinazohusu mambo ya kifedha, kutia ndani upunjaji.—Mathayo 18:23-35.

17, 18. Mtu anayedai kuwa Mkristo akitupunja, ufahamu waweza kutulindaje salama?

17 Bila shaka, kusingekuwa na msingi wa Kimaandiko wa kuchukua hatua zilizoorodheshwa kwenye Mathayo 18:15-17 ikiwa hakukuwa na uthibitisho wowote au hata dokezo la upunjaji. Hata hivyo, namna gani ikiwa mtu anayedai kuwa Mkristo alitupunja kwa kweli? Ufahamu waweza kutulinda salama dhidi ya kuchukua hatua iwezayo kuharibu sifa njema ya kutaniko. Paulo alishauri Wakristo wenzake wajiruhusu wakosewe na hata wapunjwe badala ya kumpeleka ndugu mahakamani.—1 Wakorintho 6:7.

18 Ndugu na dada zetu wa kweli si ‘wenye kujaa kila namna ya upunjaji na ulaghai,’ sawa na yule mchawi Bar-Yesu. (Matendo 13:6-12) Kwa hiyo acheni tutumie ufahamu wakati fedha zinapopotea katika biashara za kujasiria zinazohusisha waamini wenzetu. Ikiwa twafikiria kuchukua hatua ya kisheria, twapaswa kufikiria matokeo yawezayo kutupata sisi binafsi, kumpata yule mtu au watu wengine, kulipata kutaniko, na kuwapata walio nje ya kutaniko. Kufuatilia malipo ya ridhaa kungeweza kutumia wakati wetu mwingi, nishati, na mali nyingine. Tokeo la kufanya hivyo huenda likawa kuwatajirisha tu mawakili na wataalamu wengine. Kwa kuhuzunisha, Wakristo fulani wamedhabihu mapendeleo ya kitheokrasi kwa sababu ya kujihusisha kupita kiasi katika mambo hayo. Kukengeushwa-fikira kwetu kwa namna hiyo ni lazima kuwe kwamfurahisha Shetani, lakini twataka kuufanya moyo wa Yehova ushangilie. (Mithali 27:11) Kwa upande mwingine, kukubali kupatwa na hasara kwaweza kutuzuia tusiwe na maumivu ya moyoni na kwaweza kutuokolea sisi na wazee wakati mwingi. Kutatusaidia tuhifadhi amani ya kutaniko na kutatuwezesha kufuliza kuutafuta Ufalme kwanza.

Ufahamu na Kufanywa kwa Maamuzi

19. Ufahamu wa kiroho na sala zaweza kutufanyia nini tunapofanya maamuzi yenye kuleta mkazo?

19 Kufanya maamuzi kuhusu mambo ya kifedha au ya kibiashara kwaweza kuwa jambo lenye kuleta mkazo. Lakini ufahamu wa kiroho waweza kutusaidia kupima mambo yote na kufanya maamuzi yenye hekima. Isitoshe, kumtegemea Yehova kwa sala kwaweza kutuletea “amani ya Mungu.” (Wafilipi 4:6, 7) Hiyo ni utulivu na ustarehe unaotokana na uhusiano wa kibinafsi wenye ukaribu pamoja na Yehova. Kwa hakika, amani ya jinsi hiyo yaweza kutusaidia tudumishe usawaziko wetu tunapokabiliwa na maamuzi magumu.

20. Twapaswa kuazimia kufanya nini kwa habari ya mambo ya biashara na kutaniko?

20 Acheni tuazimie kutoruhusu mabishano juu ya biashara yavuruge amani yetu au ile ya kutaniko. Twahitaji kukumbuka kwamba kutaniko la Kikristo lafanya kazi ili kutusaidia kiroho, si kutumika likiwa kitovu cha ufuatiaji wa kibiashara. Mambo ya biashara yapasa sikuzote kutenganishwa na utendaji mbalimbali wa kutaniko. Twahitaji kutumia ufahamu na hadhari tuanzapo biashara za kujasiria. Na acheni sikuzote tudumishe maoni yenye usawaziko kuhusu mambo hayo, tukitafuta masilahi ya Ufalme kwanza. Iwapo biashara ya kujasiria inayohusisha waabudu wenzetu haifaulu, na tujitahidi kuwafaidi wote wanaohusika.

21. Twaweza kutumiaje ufahamu na kutenda kwa kupatana na Wafilipi 1:9-11?

21 Badala ya kuhangaikia kupita kiasi mambo ya kifedha na mambo mengine yasiyo ya maana sana, sisi sote na tuelekeze mioyo yetu kwenye ufahamu, tusali ili tupate mwongozo wa Mungu, na tufulize kutanguliza masilahi ya Ufalme. Kwa kupatana na sala ya Paulo ‘upendo wetu na upate kuzidi pamoja na ujuzi sahihi na ufahamu kamili kwamba tupate kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi na tusiwakwaze wengine’ au sisi wenyewe. Sasa kwa kuwa Kristo Mfalme yu kwenye kiti chake cha ufalme cha kimbingu, acheni tuonyeshe ufahamu wa kiroho katika kila sehemu ya maisha. ‘Na tujazwe matunda ya uadilifu kupitia Yesu Kristo, kwa utukufu na sifa ya Mungu wetu,’ Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu.—Wafilipi 1:9-11.

Ungeitikiaje?

◻ Ufahamu ni nini?

◻ Kwa nini kuna uhitaji wa pekee wa kuonyesha ufahamu kwa habari ya shughuli za biashara miongoni mwa Wakristo?

◻ Ufahamu waweza kutusaidiaje ikiwa twahisi kwamba mwamini mwenzetu ametupunja?

◻ Ufahamu wapaswa kuwa na fungu jipi katika kufanywa kwa maamuzi?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Ufahamu utatusaidia kutumia shauri la Yesu la kufuliza kuutafuta Ufalme kwanza

[Picha katika ukurasa wa 20]

Andikeni mapatano ya kibiashara sikuzote

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki