Je, Waweza Kusitawisha Ufahamu Zaidi?
UFAHAMU ni “nguvu au uwezo wa akili ambao unatumiwa kutofautisha kitu kimoja kutoka kwa kingine.” Unaweza pia kuwa “ustadi wa uamuzi” au “nguvu za kutambua tofauti za mambo au mawazo.” Ndivyo isemavyo Webster’s Universal Dictionary. Kwa wazi, ufahamu ni sifa ya kutamanika. Thamani yao inaonekana katika maneno haya ya Sulemani: ‘Hekima iingiapo moyoni mwako, na maarifa kukupendeza nafsi yako. Ufahamu utakuhifadhi. Ili kukuokoa na njia ya uovu.’—Mithali 2:10-12.
Ndiyo, ufahamu utatusaidia kukinza “njia ya uovu,” iliyopo kwa wingi leo. Nao huleta faida nyingine nyingi. Kwa kielelezo, mara nyingi wazazi husikia watoto wao wakisema, ‘Ninyi hamwelewi!’ Kwa kuchunguza kidogo, wazazi wenye ufahamu hujua jinsi ya kutambua hisia na masuala yanayosumbua watoto wao. (Mithali 20:5) Mume mwenye ufahamu atamsikiliza mkeye na kupata ufahamu wenye kina wa kufikiri kwake na hisia zake badala ya kufanya maamuzi ya haraka. Mke atafanya vivyo hivyo kwa mumeye. Hivyo, ‘nyumba itajengwa kwa hekima, na kwa ufahamu itathibitika.’—Mithali 24:3.
Ufahamu husaidia mtu kushughulikia hali kwa mafanikio. Mithali 17:27 husema: “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa; na mwenye roho ya utulivu [“ufahamu,” NW] ana busara.” Mtu mwenye ufahamu si mkali, akijiingiza katika hali yoyote bila kufikiri. Yeye hufikiri kwa uangalifu matokeo yawezayo kutokea kabla ya kujiingiza kwa maneno. (Luka 14:28, 29) Pia yeye hufurahia uhusiano wenye amani na wengine kwa sababu “mdomo wenye busara” humwongoza kuchagua maneno yake kwa uangalifu. (Mithali 10:19; 12:8, NW) Lakini la maana zaidi, mtu mwenye ufahamu kwa unyenyekevu hutambua mapungukio yake mwenyewe naye humtegemea Mungu badala ya wanadamu kwa mwongozo. Hilo ni lenye kupendeza Yehova nalo ni sababu nyingine ya kusitawisha ufahamu.—Mithali 2:1-9; Yakobo 4:6.
Kukosa Ufahamu kwa Israeli
Hatari ya kushindwa kudhihirisha ufahamu inaonekana kwenye tukio moja katika historia ya mapema ya Israeli. Akikumbuka wakati huo, mtunga-zaburi aliyepuliziwa alisema hivi: “Baba zetu katika Misri hawakufikiri matendo yako ya ajabu; hawakukumbuka wingi wa fadhili zako; wakaasi penye bahari, bahari ya Shamu.”—Zaburi 106:7.
Musa alipoongoza Israeli kutoka Misri, tayari Yehova alikuwa ameonyesha uwezo wake na azimio lake kutoa watu wake utumwani kwa kutaabisha sana mamlaka hiyo ya ulimwengu yenye uwezo mwingi kwa mapigo kumi. Baada ya Farao kuacha Waisraeli waende, Musa aliwaongoza kwenye fuo za Bahari Nyekundu. Hata hivyo, majeshi ya Misri yalifuatia nyuma yao. Ilionekana kana kwamba Waisraeli walikuwa wameingia mtegoni na kwamba uhuru wao mpya waliokuwa wamepata ulikuwa wa muda mfupi sana. Hivyo rekodi ya Biblia husema hivi: “Wakaogopa sana; wana wa Israeli wakamlilia BWANA.” Nao wakamgeukia Musa, wakisema: “Mbona umetutendea haya, kututoa katika nchi ya Misri? . . . Maana ni afadhali kuwatumikia Wamisri kuliko kufa jangwani.”—Kutoka 14:10-12.
Hofu yao huenda ikaeleweka hadi tukumbukapo kwamba tayari walikuwa wameona maonyesho kumi yenye kutokeza ya nguvu za Yehova. Walijua kwa kujionea wenyewe yale Musa angewakumbusha miaka 40 baadaye: “BWANA akatutoa kutoka Misri kwa mkono wa nguvu, na kwa mkono ulionyoshwa, na kwa utisho mwingi, na kwa ishara, na kwa maajabu.” (Kumbukumbu la Torati 26:8) Hivyo basi, kama vile mtunga-zaburi alivyoandika, Waisraeli walipogeuka dhidi ya mwongozo wa Musa, “hawakufikiri.” Hata hivyo, Yehova, kama alivyoahidi, aliyashinda kabisa majeshi ya Misri.—Kutoka 14:19-31.
Imani yetu vilevile ingesitasita ikiwa tungekabili majaribu tukiwa na shaka. Ufahamu utatusaidia sikuzote kuona mambo jinsi yalivyo hasa, tukikumbuka jinsi Yehova alivyo mkuu zaidi kuliko yeyote ambaye huenda akatupinga. Ufahamu utatusaidia pia kukumbuka yale Yehova tayari ametufanyia. Utatusaidia tusisahau kamwe uhakika wa kwamba yeye Ndiye “huwahifadhi wote wampendao.”—Zaburi 145:18-20.
Kupata Ufahamu wa Kiroho
Ufahamu hauji vivi hivi kadiri mtu anavyokua kwa umri. Ni lazima usitawishwe. Mfalme Sulemani mwenye hekima, aliyepata umashuhuri kwa ajili ya ufahamu wake, alisema hivi: “Heri mtu yule aonaye hekima, na mtu yule apataye ufahamu. Maana biashara yake ni bora kuliko biashara ya fedha, na faida yake ni nyingi kuliko dhahabu safi.” (Mithali 3:13, 14) Sulemani alipata ufahamu wake wapi? Kutoka kwa Yehova. Yehova alipomuuliza Sulemani alitaka baraka ipi, Sulemani alijibu hivi: “Nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua [“kufahamu,” NW] mema na mabaya.” (1 Wafalme 3:9) Ndiyo, Sulemani alimtegemea Yehova kuwa msaidiaji wake. Aliomba ufahamu, na Yehova akampa ufahamu kupita kawaida. Tokeo likawa nini? “Hekima ya Sulemani ikapita hekima ya wana wote wa mashariki, na hekima zote za Misri.”—1 Wafalme 4:30.
Ono la Sulemani latuonyesha mahali pa kwenda kutafuta ufahamu. Kama Sulemani, tunapaswa kumtegemea Yehova. Jinsi gani? Yehova ameandaa Neno lake, Biblia, ambalo hutupa ufahamu wenye kina wa mawazo yake. Tusomapo Biblia, tunachimba chanzo chenye ujuzi wenye thamani ambao utatuandalia misingi ya ufahamu wa kiroho. Twapaswa kuzitafakari habari tukusanyazo kutoka kwa usomaji wetu wa Biblia. Kisha, zinaweza kutumiwa kufanya maamuzi yanayofaa. Baada ya muda, nguvu zetu za utambuzi zinakuzwa kwa kadiri ambayo tunakuwa “watu wazima katika nguvu za kuelewa,” tukiweza “kutofautisha [au, kufahamu kati ya] lililo sawa na lililo kosa pia.”—1 Wakorintho 14:20, (NW); Waebrania 5:14, (NW); linganisha 1 Wakorintho 2:10, (NW).
Kwa kupendeza, bado twaweza kunufaika kutokana na ufahamu ambao Yehova alimpa Sulemani. Jinsi gani? Sulemani akawa na ustadi mwingi wa kusimulia hekima kwa njia ya mithali, ambazo zilikuwa hekima fupifupi zilizopuliziwa kimungu. Nyingi za semi hizo zimehifadhiwa katika kitabu cha Biblia cha Mithali. Kujifunza kitabu hicho hutusaidia kunufaika kutokana na ufahamu wa Sulemani na pia kukuza ufahamu.
Ili kutusaidia katika funzo letu la Biblia, twaweza kutumia fasihi za kujifunza Biblia, kama vile magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kwa zaidi ya miaka 116, Mnara wa Mlinzi limekuwa likitangaza Ufalme wa Yehova kwa watu wenye mioyo minyoofu. Gazeti la Amkeni! na yale yaliyolitangulia limekuwa likitoa maelezo juu ya hali za ulimwengu tangu 1919. Magazeti hayo mawili huchunguza kweli za Biblia na kuandaa mnurisho wa kiroho hatua kwa hatua ambao hutusaidia kufahamu makosa, yawe yanafundishwa na Jumuiya ya Wakristo au yawe yanapatikana katika njia yetu ya kufikiri.—Mithali 4:18.
Msaada mwingine wa kusitawisha ufahamu ni ushirika unaofaa. Moja ya mithali za Mfalme Sulemani yasema hivi: “Enenda pamoja na wenye hekima, nawe utakuwa na hekima; bali rafiki wa wapumbavu ataumia.” (Mithali 13:20) Ni jambo la kusikitisha kwamba Rehoboamu mwana wa Mfalme Sulemani hakukumbuka mithali hiyo katika kipindi fulani cha maana maishani mwake. Baada ya kifo cha baba yake, makabila ya Israeli yalimwendea kudai kwamba awapunguzie mzigo wao. Kwanza, Rehoboamu aliomba mashauri kwa wanaume wazee, na hawa walionyesha ufahamu walipomtia moyo asikilize raia wake. Kisha akawaendea wanaume vijana. Hawa walionyesha ukosefu wa ujuzi na ukosefu wa ufahamu, wakimtia moyo Rehoboamu ajibu Waisraeli kwa matisho. Rehoboamu alisikiliza wanaume vijana. Tokeo likawa nini? Israeli ikaasi, na Rehoboamu akapoteza sehemu kubwa ya ufalme wake.—1 Wafalme 12:1-17.
Njia kubwa ya kusitawisha ufahamu ni kutafuta msaada wa roho takatifu. Kwa kutafakari jinsi Yehova alivyoshughulika na Waisraeli baada ya kuachiliwa kwao kutoka utumwani Misri, mwandikaji wa Biblia Nehemia alisema hivi: “Ukawapa na roho yako mwema ili kuwaelimisha.” (Nehemia 9:20) Roho ya Yehova pia yaweza kutuelimisha. Ukisali ili roho ya Yehova ikupe ufahamu, sali ukiwa na uhakika kwa sababu Yehova ‘huwapa wote kwa ukarimu, wala hakemei.’—Yakobo 1:5; Mathayo 7:7-11; 21:22.
Ufahamu na Ufahamu Wenye Kina
Mtume Paulo alionyesha ufahamu alipohubiri kweli kwa watu wa mataifa. Kwa kielelezo, wakati fulani, akiwa Athene, alikuwa ‘akipita huko na huko na kuona’ sanamu zao za ibada. Paulo alikuwa amezungukwa na sanamu mbalimbali, na roho yake ikawa yenye kuudhika ndani yake. Sasa alikuwa na uamuzi wa kufanya. Je, afuate mwendo ulio salama na kunyamaza? Au je, azungumze waziwazi kuhusu sanamu nyingi mbalimbali alizoona kuwa zenye kuchukiza sana, hata ingawa kufanya hivyo kungekuwa hatari sana?
Paulo alitenda kwa ufahamu. Alikuwa ameona madhabahu yenye mwandiko huu: “KWA MUNGU ASIYEJULIKANA.” Kwa busara, Paulo alijulisha ujitoaji wao kwa sanamu mbalimbali kisha akatumia madhabahu hiyo kuwa njia ya kuanzisha habari ya “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo.” Ndiyo, Yehova ndiye aliyekuwa Mungu wasiyemjua! Kwa njia hiyo Paulo alitambua wepesi wa hisia zao kwa jambo hilo naye aliweza kutoa ushahidi wa ajabu. Tokeo likawa nini? Idadi fulani ya watu wakakubali kweli, kutia ndani “Dionisio, Mwareopago, na mwanamke mmoja jina lake Damari, na watu wengine pamoja na hao.” (Matendo 17:16-34) Paulo alikuwa kielelezo kizuri kama nini cha ufahamu!
Bila shaka, ufahamu hauji kwa urahisi au wenyewe tu. Lakini kwa saburi, sala, bidii-nyendelevu, ushirika wenye hekima, funzo la Biblia na kutafakari juu yayo, na kwa kutegemea roho takatifu ya Yehova, wewe pia waweza kuusitawisha.