GEHENA
(Gehena) [Tafsiri ya Kigri. ya neno la Kiebr. Geh Hin·nomʹ, “Bonde la Hinomu”].
Jina hilo linapatikana mara 12 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na ingawa watafsiri wengi wametumia maneno “moto wa mateso,” idadi kubwa ya tafsiri za kisasa zinafasiri neno hilo moja kwa moja kutoka katika neno la Kigiriki geʹen·na.—Mt 5:22, UV, BHN, ZSB, NBT, na Biblia ya Kiafrika.
Baadaye, Bonde la Hinomu lililo refu na jembamba lilikuja kujulikana kwa jina hilo la Kigiriki, nalo linapatikana KUS. na KUS. MAGH. mwa Yerusalemu la kale na ndilo jiji la Wadi er-Rababi (Ge Ben Hinnom) la kisasa. (Yos 15:8; 18:16; Yer 19:2, 6; ona HINOMU, BONDE LA.) Wafalme wa Yuda, Ahazi na Manase, waliendeleza ibada ya sanamu katika eneo hilo, na ibada hiyo ilihusisha kumtolea Baali dhabihu za kuteketezwa za wanadamu. (2Nya 28:1, 3; 33:1, 6; Yer 7:31, 32; 32:35) Baadaye, ili kuzuia matendo kama hayo yasiendelee kufanywa tena mahali hapo, Mfalme mwaminifu Yosia alipaharibu mahali pa ibada ya sanamu hasa sehemu iliyoitwa Tofethi.—2Fa 23:10.
Si Ishara ya Mateso wa Milele. Yesu Kristo alihusianisha moto na Gehena (Mt 5:22; 18:9; Mk 9:47, 48), na mbali na Mathayo, Marko na Luka, mwandikaji mwingine wa Biblia aliyetumia neno hilo ni mwanafunzi Yakobo. (Yak 3:6) Baadhi ya wachambuzi wa Biblia wanajaribu kuunganisha kutajwa kwa Gehena pamoja na kuteketezwa kwa dhabihu za wanadamu kulikofanywa kabla ya utawala wa Yosia, na kwa msingi huo, wanadai kwamba neno Gehena lilitumiwa na Yesu kama ishara ya mateso ya milele. Hata hivyo, kwa kuwa Yehova anachukizwa na zoea hilo, na anasema lilikuwa ‘jambo ambalo hakuamuru na ambalo hata halijawahi kamwe kuingia moyoni mwake’ (Yer 7:31; 32:35), haipatani na akili kufikiri kwamba Mwana wa Mungu, alipokuwa akizungumzia hukumu ya Mungu, angetumia ibada hiyo ya sanamu kuwa msingi unaowakilisha maana ya Gehena. Mungu alitangaza kupitia unabii kwamba Bonde la Hinomu lingekuwa mahali ambapo maiti za watu wengi zingetupwa na si mahali pa kuwatesea watu wakiwa hai. (Yer 7:32, 33; 19:2, 6, 7, 10, 11) Kwa hiyo, katika andiko la Yeremia 31:40 maneno ‘bonde la mizoga na la majivu’ yanamaanisha Bonde la Hinomu, na lango lililojulikana kama “Lango la Marundo ya Majivu” lilikuwa ukingoni mwa upande wa mashariki wa bonde hilo katika makutano yake na bonde la Kidroni.—Ne 3:13, 14.
Basi, kwa ujumla, matumizi ya neno Gehena katika Biblia yanapatana na mapokeo ya kirabi na vyanzo vinginevyo. Mapokeo hayo ni kwamba Bonde la Hinomu lilitumiwa kama mahali pa kutupa takataka za jiji la Yerusalemu. (Kwenye Mt 5:30 The New Testament in Modern English hurejelea geʹen·na kuwa “rundo la takataka.”) Kuhusiana na “Gehinnom,” msomi Myahudi David Kimhi (1160?-1235?), anatoa habari hizi za kihistoria anapozungumza kuhusu Zaburi 27:13: “Ni mahali ambapo pamepakana na Yerusalemu, tena ni mahali pa kuchukiza sana, na watu hutupa humo vitu vichafu na mizoga. Vilevile, humo mlikuwa na moto ulioendelea kuwaka ili kuchoma vitu vichafu na mifupa ya mizoga. Kwa hiyo, hukumu ya waovu huitwa Gehinnom kwa njia ya mfano.”
Ufananisho wa Uharibifu wa Milele. Ni wazi kwamba Yesu alitumia neno Gehena kama ufananisho wa uharibifu wa milele unaotokana na hukumu kali ya Mungu, bila tumaini lolote la ufufuo. (Mt 10:28; Lu 12:4, 5) Kikundi kiovu cha waandishi na Mafarisayo kilihesabiwa kuwa ‘kinastahili Gehena.’ (Mt 23:13-15, 33) Ili kuepuka uharibifu huo, wanafunzi wa Yesu walipaswa kuondoa kitu chochote kinachoweza kusababisha kukwazika kwa njia ya kiroho, huku ‘kukata mkono au mguu’ na ‘kung’oa jicho’ kukiwakilisha kwa njia ya mfano kuviua viungo hivyo kuhusiana na dhambi.—Mt 18:9; Mk 9:43-47; Kol 3:5; linganisha Mt 5:27-30.
Inaonekana Yesu alirejelea Isaya 66:24 alipokuwa akielezea Gehena kuwa “mahali ambapo funza hawafi na moto hauzimwi.” (Mk 9:47, 48) Bila shaka, wazo linalopatikana hapa si la mateso, bali ni la uharibifu wa milele, kama maneno yaliyo kwenye kitabu cha Isaya ambayo hayarejelei watu walio hai, bali ‘maiti za watu waliomwasi’ Mungu. Kama ushahidi uliopo unavyoonyesha, ikiwa Bonde la Hinomu lilikuwa mahali ambapo vitu vichafu na mizoga ilitupwa, basi moto ambao huenda ulioongezwa nguvu kwa kiberiti (linganisha Isa 30:33), ungekuwa njia pekee inayofaa ya kumaliza takataka hizo. Mahali ambapo moto huo haukufika, minyoo au funza wangezaliana na kula kitu chochote ambacho hakikuteketezwa na moto. Kwa msingi huo, maneno ya Yesu yangemaanisha kwamba matokeo ya hukumu ya Mungu yenye kuangamiza hayangesitishwa mpaka uharibifu wa milele ulipofikiwa.
Matumizi ya Njia ya Mfano. Namna ambavyo mwanafunzi Yakobo ametumia neno Gehena inaonyesha kwamba ulimi usiothibitiwa ni ulimwengu usio na uadilifu, na hivyo maisha yote ya mtu yanaweza kuathiriwa na maneno yanayowaka moto na kuutia unajisi mwili wa mzungumzaji. Ulimi wa mtu kama huyo ‘umejaa sumu yenye kuua’ na hivyo kuonyesha wazi hali mbaya ya moyo, na unaweza kumfanya mtu huyo ahukumiwe na Mungu kuwa anastahili Gehena ya mfano.—Yak 3:6, 8; linganisha Mt 12:37; Zb 5:9; 140:3; Ro 3:13.
Matumizi ya Biblia ya Gehena ya mfano yanalingana na yale ya “ziwa la moto” kwenye kitabu cha Ufunuo.—Ufu 20:14, 15; ona ZIWA LA MOTO.