Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • it kur. 119-121
  • Shangwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Shangwe
  • Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Tumikia Yehova kwa Shangwe ya Moyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Shangwe​—Sifa Inayotoka kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Mtumikie Yehova kwa Moyo Wenye Kujaa Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kutumikia Yehova Kwa Shangwe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Ufahamu wa Kina wa Maandiko
it kur. 119-121

SHANGWE

Hisia anayopata mtu anapopata au kutazamia jambo jema; hali ya kuwa na furaha; uchangamfu. Maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotumiwa katika Biblia kumaanisha shangwe, kushangilia, uchangamfu, na kufurahi, yanaonyesha hali au viwango mbalimbali vya shangwe. Vitenzi vya maneno hayo vinaonyesha hisia za ndani na jinsi zinavyoweza kuonyeshwa kwa nje, na vinamaanisha “kuwa na shangwe; kuchangamka; kupaza sauti kwa shangwe; kuruka kwa shangwe.”

Yehova Mungu na Yesu Kristo. Yehova anaitwa “Mungu mwenye furaha.” (1Ti 1:11) Anaumba na kufanya kazi kwa shangwe kwa ajili yake mwenyewe na viumbe wake. Kazi zake zote humletea shangwe. (Zb 104:31) Anataka pia viumbe wake wafurahie kazi zake na kazi wanazofanya. (Mhu 5:19) Kwa kuwa yeye ndiye Chanzo cha vitu vyote vyema (Yak 1:17), viumbe wake wote wenye akili, wanadamu na malaika, wanaweza kupata shangwe kubwa zaidi kwa kumjua. (Yer 9:23, 24) Mfalme Daudi alisema hivi: “Mawazo yangu na yampendeze. Nitashangilia kwa sababu ya Yehova.” (Zb 104:34) Aliimba hivi pia: “Mwadilifu atashangilia kwa sababu ya Yehova na kumkimbilia; wote walio wanyoofu moyoni watashangilia.” (Zb 64:10) Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo washangilie sikuzote kwa sababu wanamjua Yehova na wanajua jinsi anavyoshughulika nao, aliwaandikia hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana [“Yehova,” kulingana na tafsiri kadhaa]. Nitasema tena, Shangilieni!”​—Flp 4:4.

Yesu Kristo, aliyekuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova, anamjua vizuri sana (Mt 11:27), hivyo anaweza kuwaeleza wafuasi wake Kumhusu. (Yoh 1:18) Kwa hiyo, Yesu ana shangwe naye anaitwa “yule Mtawala Mkuu wa pekee na mwenye furaha.” (1Ti 6:14, 15) Kwa sababu anampenda Baba yake, yuko tayari sikuzote kufanya mambo yanayompendeza Yehova. (Yoh 8:29) Kwa hiyo, alipopewa mgawo wa kuja duniani, kuteseka, na kufa ili aliondolee lawama jina la Baba yake, “kwa sababu ya shangwe iliyowekwa mbele yake, alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu.” (Ebr 12:2) Pia, aliwapenda sana wanadamu na alipata shangwe kwa sababu yao. Kabla ya kuja duniani, Maandiko yanamfananisha na hekima anaposema hivi: “Wakati huo nilikuwa kando yake [Yehova] nikiwa mfanyakazi stadi. Mimi ndiye aliyenipenda sana siku baada ya siku; nilishangilia mbele zake wakati wote; nilishangilia dunia yake inayokaliwa, nami niliwapenda sana wanadamu.”​—Met 8:30, 31.

Yesu alitamani wafuasi wake wawe na shangwe hiyohiyo, aliwaambia hivi: “Nimewaambia mambo haya, ili shangwe yangu iwe ndani yenu na shangwe yenu ijae.” Malaika walifurahia wakati dunia ilipoumbwa. (Yoh 15:11; 17:13; Ayu 38:4-7) Wanatazama pia maisha ya watu wa Mungu, wakifurahia wanapokuwa waaminifu na kushangilia hasa mtu fulani anapoacha mwenendo wake wa dhambi na kurudi katika ibada safi na kumtumikia Mungu.​—Lu 15:7, 10.

Kinachomfanya Mungu awe na shangwe. Moyo wa Yehova hushangilia watumishi wake wanapokuwa waaminifu na washikamanifu kwake. Shetani Ibilisi amekuwa akitilia shaka haki ya Mungu ya kuwa mwenye enzi kuu na utimilifu wa wote wanaomtumikia Mungu. (Ayu 1:9-11; 2:4, 5; Ufu 12:10) Maneno haya yanaelekezwa kwao: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili niweze kumjibu yule anayenidhihaki.” (Met 27:11) Watu wa Yehova duniani wanaweza kumfanya Mungu ashangilie kwa kuendelea kuwa waaminifu na washikamanifu kwake.​—Isa 65:19; Sef 3:17.

Sifa ya Tunda la Roho. Kwa kuwa Yehova ndiye Chanzo cha shangwe na angependa watu wake wawe na sifa hiyo, shangwe ni sifa ya tunda la roho yake takatifu. Shangwe inatajwa baada tu ya upendo katika orodha iliyo kwenye Wagalatia 5:22, 23. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo wa Thesalonike: “Mlituiga sisi na Bwana pia, kwa kuwa mlilikubali neno kwa shangwe ya roho takatifu ingawa mlikuwa na dhiki nyingi.” (1Th 1:6) Hivyo, Paulo aliwashauri Wakristo wa Roma kwamba Ufalme wa Mungu “unamaanisha uadilifu na amani na shangwe pamoja na roho takatifu.”​—Ro 14:17.

Shangwe ya kweli ni sifa ya moyoni inayoweza kuboresha afya ya mtu. Mwandishi mwenye hekima wa Methali alisema hivi: “Moyo wenye shangwe hufanya uso uchangamke,” na “moyo wenye shangwe ni dawa nzuri, [au, “humsaidia mtu kupona”].”​—Met 15:13; 17:22, maelezo ya chini.

Shangwe Katika Utumishi wa Mungu. Mambo ambayo Yehova anataka watumishi wake watimize si mzigo mzito. (1Yo 5:3) Anataka wafurahie kumtumikia. Watu wake Waisraeli walipaswa kufurahia sherehe za majira alizowapangia, nao walipaswa kufurahia utendaji mwingine maishani mwao na katika ibada ya Mungu. (Law 23:40; Kum 12:7, 12, 18) Walipaswa kuzungumza kwa shangwe kumhusu Mungu. (Zb 20:5; 51:14; 59:16) Ikiwa hawangemtumikia kwa shangwe moyoni wangekuwa na tatizo mioyoni mwao na kuonyesha kwamba hawathamini upendo wake mshikamanifu na wema wake. Kwa hiyo, aliwaonya kuhusu jambo ambalo lingetokea ikiwa wangekosa kutii na kukosa shangwe katika utumishi wao: “Laana hizi zote hakika zitawajia . . . kwa sababu hamkuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu kwa kushika amri zake na sheria zake . . . Nazo zitaendelea kuwaandama ninyi na wazao wenu . . . kwa sababu hamkumtumikia Yehova Mungu wenu kwa furaha na shangwe moyoni mlipokuwa na wingi wa kila kitu.”​—Kum 28:45-47.

Mkristo anapaswa pia kufurahia kumtumikia Mungu. La sivyo, anakosa uthamini moyoni mwake. (Zb 100:2) Mtumishi mmoja mwaminifu wa Mungu alisema hivi: “Shangwe ya Yehova ndiyo ngome yenu.” (Ne 8:10) Malaika wa Mungu alisema kwamba habari njema inayotangazwa na Wakristo ni “habari njema ya shangwe kubwa ambayo watu wote watakuwa nayo.” (Lu 2:10) Kuitwa kwa jina la Yehova na kujua kweli inayopatikana katika Biblia ni mambo yanayopaswa kuwaletea shangwe. Nabii Yeremia alisema hivi: “Neno lako likawa furaha na shangwe ya moyo wangu, kwa maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Yehova Mungu wa majeshi.”​—Yer 15:16.

Zaidi ya hayo, maamuzi ya Yehova ya haki na uadilifu yanayoliongoza kutaniko la Kikristo na maisha ya Wakristo huwaletea shangwe, hasa wakati huu ambapo ulimwengu umetupilia mbali haki na uadilifu. (Zb 48:11) Pia, tumaini zuri sana la wakati ujao linatupatia sababu kubwa ya kuwa na shangwe. (“Shangilieni katika tumaini”; Ro 12:12; Met 10:28.) Wokovu wao unawaletea shangwe. (Zb 13:5) Isitoshe, mtumishi wa Mungu hupata shangwe anapowasaidia wengine kumjua Yehova na kuanza kumtumikia. (Flp 4:1; 1Th 2:19) Kukutana pamoja na kufanya kazi pamoja na watu wa Mungu ni kati ya mambo yanayoleta shangwe kubwa zaidi.—Zb 106:4, 5; 122:1.

Mateso huleta shangwe. Mkristo anayelinda moyo wake anapaswa kukabiliana na mateso kwa shangwe, licha ya kwamba mateso yenyewe hayaleti shangwe, kwa sababu anapovumilia kwa utimilifu anakuwa mshindi. Mungu atamsaidia mtu mwaminifu. (Kol 1:11) Zaidi ya hayo, ni uthibitisho kwamba ana kibali cha Mungu. Yesu alisema kwamba Mkristo anaposhutumiwa na kuteswa anapaswa “kushangilia sana.”​—Mt 5:11, 12; Yak 1:2-4; 1Pe 4:13, 14.

Mambo Mengine Kutoka kwa Mungu Yanayoleta Shangwe. Yehova ametayarisha mambo mengine mengi ambayo wanadamu wanaweza kufurahia kila siku. Baadhi ya mambo hayo ni ndoa, (Kum 24:5; Met 5:18), kuwa baba au mama ya mtoto mwadilifu na mwenye hekima (Met 23:24, 25), chakula (Mhu 10:19; Mdo 14:17), divai (Zb 104:14, 15; Mhu 10:19), na vitu vingine vingi alivyoumba (Yak 1:17; 1Ti 6:17).

Shangwe Isiyo ya Kweli au Isiyodumu. Yesu alisema kwamba baadhi ya watu wangesikia kweli na kuipokea kwa shangwe lakini hawangepata maana yake. Watu hao hawasitawishi neno lililopandwa mioyoni mwao, na kwa sababu hiyo, baada ya muda wanapoteza shangwe yao na kukwazika wanapopata dhiki au mateso kwa sababu ya hilo neno. (Mt 13:20, 21) Shangwe inayotegemea vitu vya kimwili si shangwe ya kweli na haidumu. Pia, mtu anayeshangilia msiba wa mwingine, hata ikiwa mtu huyo anamchukia, lazima awajibike kwa Yehova kwa sababu ya dhambi yake. (Ayu 31:25-30; Met 17:5; 24:17, 18) Ni upumbavu kwa kijana kufikiri kwamba atafurahia maisha kwa kufuata “tamaa za ujana.” (2Ti 2:22; Mhu 11:9, 10) Vilevile, kupenda raha kutamsababishia mtu matatizo. (Met 21:17; Mhu 7:4) Hata Mkristo anayefurahia kujilinganisha na wengine anafanya kosa. Badala yake, anapaswa kuchunguza matendo yake mwenyewe na kuwa na sababu ya kushangilia kuhusiana na yeye mwenyewe.​—Gal 6:4.

Shangwe ya Milele. Yehova aliahidi kuwarudisha watu wake Waisraeli kutoka uhamishoni Babiloni. Aliwarudisha Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K., nao walishangilia sana msingi wa hekalu ulipojengwa. (Isa 35:10; 51:11; 65:17-19; Ezr 3:10-13) Lakini unabii wa Isaya (65:17) kuhusu “mbingu mpya na dunia mpya” utatimizwa kwa njia kubwa zaidi wakati ambapo wanadamu wote watapata shangwe milele chini ya “Yerusalemu Jipya.”​—Ufu 21:1-3.

Katika hali za sasa, wanadamu hawawezi kufurahia shangwe kamili inayodumu kwa sababu ya uovu, magonjwa, na kifo. Lakini kulingana na maneno haya ya Biblia, “Mfalme mwenye hekima huwapepeta waovu,” Yesu Kristo akiwa Mfalme atawaangamiza maadui wote wa Mungu na wa uadilifu. (Met 20:26; 1Ko 15:25, 26) Kwa hiyo, mambo yote yanayowazuia wanadamu wasipate shangwe kamili yataondolewa, kwa kuwa hata “kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” (Ufu 21:4) Huzuni kwa sababu ya kufiwa haitakuwapo tena kamwe, itaondolewa wafu watakapofufuliwa. Jambo hilo linawafariji Wakristo hata leo, na kwa sababu hiyo ‘hawahuzuniki kama wanavyofanya watu wasio na tumaini.’​—1Th 4:13, 14; Yoh 5:28, 29.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki