Mtumikie Yehova kwa Moyo Wenye Kujaa Furaha
“Mtumikieni Yehova kwa kushangilia. Ingieni mbele zake kwa kilio cha furaha.—Zaburi 100:2, NW.
1, 2. Ni maoni gani yenye kutofautiana juu ya maisha yaliyoonyeshwa hapa?
NIMEVURUGA maisha yangu. Sasa imekuwa kuchelewa mno nisiweze kuyabadili . . . Ninapoenda kutembea peke yangu, ninafikiria maisha yangu ya zamani, nami nahuzunikia namna nilivyoyatumia.” Ndivyo alivyosema mwanamke wa makamo aliyekuwa amejipatia sifa ya kuwa mchezaji wa sinema ambaye alionekana kama kwamba alikuwa na sababu nzuri ya kuwa na furaha. Lakini ni wazi kwamba hakusema aliyoyasema akiwa na moyo wenye furaha ya kweli.
2 Kwa kutofautisha, mfikirie mwanamume fulani ambaye amekuwa akishindana sana na hali ya kupooza mwili muda wa miaka 37. Inaweza kuonekana kwamba mtu huyo hana sababu kubwa ya kuwa na furaha. Hata hivyo yeye anasema ni mwenye furaha na kwamba amepata kitu ‘kinachofanya maisha yawe yenye kuthawabisha kikweli na yenye maana.’
3. (a) Ni mambo gani yanayotupata sisi binafsi ambayo huenda yakatufanya tutake kujua kama kuna mwanadamu ye yote anayeweza kuwa na furaha ya kweli? (b) Furaha inaweza kuelezwa kuwa nini?
3 Wengi wetu hawajapata kulazimika kuvumilia kwa muda mrefu ugonjwa wenye kulemea mwili na kuuumiza. Wala hawajapata kuwa wanasarakasi (watumbuizaji) walio mashuhuri ulimwenguni pote. Inaelekea kuwa sisi ni akina yahe tu wanaolazimika kuelekeana na mahangaiko na magumu ya kila siku ya maisha. Mambo yaliyotupata yanathibitisha kwamba “mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu,” na bila shaka tunakubali kwamba “viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja.” (Ayubu 14:1; Warumi 8:22) Basi huenda tukataka kujua kama mtu ye yote duniani anaweza kuwa na furaha ya kweli—ule “msisimuko wa moyoni wa kupendezwa sana unaoletwa na kitu kizuri au chenye kuridhisha.” Wewe unawaza namna gani? Je! furaha inaweza kweli kupatikana?
Je! Wewe Unaweza Kuipata?
4. Ni akina nani walio kati ya mamilioni ya watu wanaopata furaha ya kweli?
4 Mamilioni ya watu wana furaha. Malaika waadilifu wa kimbingu ‘wanatimiza ‘neno la Mungu’ kwa kufurahi. (Zaburi 103:20, NW) Sikuzote wao wamemtumikia Yehova Mungu wakiwa na furaha ya kweli. Naam, wakati dunia ilipokuwa ikipigwa msingi, hao ‘nyota wa asubuhi wajipiga kelele kwa furaha’! (Ayubu 38:4-7) Kwa uhakika malaika yule mwaminifu aliyetangaza kuzaliwa kwa Yesu alikuwa na mgawo wenye kupendeza, kwa maana alikuwa akitangaza “habari njema ya furaha kuu.”—Luka 2:8-14, NW.
5. Kwa habari ya furaha, imekuwaje kwa Mwana pekee wa Mungu?
5 Lakini namna gani yule “Mwana pekee wa Mungu”? (Yohana 3:18) Kabla hajawa mwanadamu Yesu Kristo alikuwa “stadi wa kazi” wa Yehova huko mbinguni. je! huo ulikuwa utumishi wenye furaha? Hakika ulikuwa, kwa maana tunaambiwa: “Nikawa furaha yake [Yehova] kila siku; nikifurahi daima mbele zake.” (Mithali 8:22-31) Yesu alipokuwa duniani akiwa mwanadamu alipata upendezi katika kufanya mapenzi ya Mungu. (Zaburi 40:6-8; Waebrania 10:5-10) Zaidi ya hilo, “kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili [mti wa mateso] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu.” (Waebrania 12:2) Sasa, Yesu Kristo akiwa ndiye “yule Mwenye uweza peke yake aliye na furaha” ambaye karibuni atafikiliza hukumu za kimungu duniani ili watu wazitambue, anamtumikia Yehova kwa moyo wenye furaha.—1 Timotheo 6:13-16, NW; 2 Wathesalonike 1:6-10.
6. Unaweza kupata wapi furaha leo?
6 Basi, je! wewe unaweza kupata furaha leo? Ndiyo, tena yule mwanamume mwenye kusumbuliwa na ugonjwa aliyetajwa mwanzoni anaonyesha njia ya kuipata kwa kusema: “Mimi nimejionea ukweli wa kwamba furaha iliyo kubwa zaidi inapatikana kwa kumtumikia Mungu. Jambo hilo linafanya maisha yathawabishe kikweli na kuwa yenye maana. Kuwa mtu aliyepooza mwili hakukuninyang’anya mapendeleo na baraka za kumtumikia Muumba.” Furaha ya kweli inapatikana kati ya wale waliojitoa kwa moyo mzima wamtumikie Yehova Mungu. Wataikosaje na hali wanazitangaza “habari njema” kutoka kwa “yule Mungu mwenye furaha”—ujumbe wenye kutia moyo wenye habari za uzima usiokoma katikati ya baraka kubwa-kubwa chini ya utawala wa “ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 24:14; 1 Timotheo 1:11, NW; Mathayo 5:3) Kwa hiyo wao wana sababu ya ‘kumtumikia Yehova kwa kushangilia,’ ‘kuingia mbele zake kwa kilio cha furaha.’—Zaburi 100:2, NW.
7, 8. (a) Wajapokuwa na furaha, kwa sababu gani si sikuzote watu waliojitoa kumtumikia Yehova wanapokuwa na mioyo isiyo mizito? (b) Kwa sababu gani magumu ya maisha hayalemei kabisa watu wa Yehova?
7 Maana yake si kwamba mtu aliyejitoa kumtumikia Mungu hatakuwa na moyo mzito hata wakati mmoja. Katika jamii isiyokamilika ya kibinadamu, watu wa Yehova wanapatwa na huzuni ya kadiri fulani nyakati nyingine. (Warumi 5:12) Kwa mfano, wakati Esau alipojitwalia wanawake Wahiti wawe wake zake, “walikuwa chanzo cha uchungu mkali wa roho kwa [wazazi wake wenye kumcha Mungu] Isaka na Rebeka.” (Mwanzo 26:34, 35, NW) Tena, kwa kutumia mateso ya moja kwa moja na “matendo ya ujanja mwingi” yasiyo ya moja kwa moja, Shetani Ibilisi anajaribu kuharibu uhusiano wenye thamani nyingi ambao Mkristo anao pamoja na Yehova. (Waefeso 6:11, The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures) Kwa hiyo, wapenda Mungu wanaweza kutazamia magumu fulani yatokee maishani. Lakini magumu hayo hayawalemei kabisa watu wa Yehova. Wao wanajipatia ‘faraja kutokana na Maandiko’ na kusali wakiwa na uhakika waombe roho ya Mungu na msaada wake katika kulisitawisha tunda la furaha la roho hiyo. (Warumi 15:4, NW; Luka 11:13; Wagalatia 5:22, 23) Yajapokuwapo majaribu katika maisha, Wakristo wanaweza kuwa na ‘furaha ya roho takatifu.’ (1 Wathesalonike 1:6) Hasa baraka zinazotoka kwa Yehova ndizo zinazozidisha furaha hiyo.
8 Baraka ya Yehova inatajirisha kikweli. (Mithali 10:22) Lakini ikiwa wewe ni Mkristo, je! umepata kuhesabu baraka zako? Zinapasa kukufanya ‘ushangilie katika Yehova.’ (Zaburi 32:11) Fikiria chache tu kati ya baraka ambazo zitakupa sababu inayotosha ya kumtumikia Yehova ukiwa na moyo wenye kujaa furaha.
Mapendeleo Yenye Furaha Yasiyo na Kifani
9. Maana yake nini kumjua Yehova, na jambo hilo linahusuje furaha?
9 Kumjua Yehova na kumtumikia ni baraka zisizo na kitu cha kulingana nazo. Mungu alisema hivi kupitia nabii Yeremia: “Ajisifuye na ajisifu kwa sababu hii, ya kwamba ananifahamu mimi, na kunijua, ya kuwa mimi ni [ Yehova], nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi.” (Yeremia 9:24) Ni wazi kwamba kuwa tu na maarifa ya kulijua jina la kimungu hakutoshi. Kumjua Yehova maana yake ni kuzijua sifa zake, njia zake za kufanyia mambo, nia zake na makusudi yake. Maana yake ni kumtii, kuitambua mamlaka yake na kuinyenyekea. (1 Yohana 5:3) Kujifunza Maandiko kwa juhudi na kuyatafakari maneno na matendo ya Mwana wa Mungu, ambaye ana upatani kamili kabisa pamoja na Baba yake, ni mambo yanayofanya iwezekane kuwa na uhusiano wa kibinafsi wa kuwa karibu na Mungu. (Yohana 1:18; 14:9-11) Wale wanaomjua Yehova kwa njia hiyo ni wenye furaha kweli kweli. Kusema kweli, “kwa mtu aliye mwema mbele zake [Yehova] ametoa hekima na maarifa na kushangilia.”—Mhubiri 2:26, NW.
10. Ni njia gani iliyo ya maana zaidi na yenye kuridhisha zaidi ambayo inaweza kufuatwa katika maisha ya kibinadamu?
10 Pendeleo lisilo na ulinganifu la kumtolea “utumishi mtakatifu” yule Mungu wa kweli ni baraka nyingine inayofurahiwa na Mashahidi wa Yehova. Hakuna mwanadamu ambaye anaweza kutumia maisha kwa njia ya maana au yenye kuridhisha zaidi ya hiyo. Kwa uhakika, Zekaria (aliyekuwa baba ya Yohana Mbatizaji) alitaja maoni mazuri katika kumbariki Yehova kwa kuwapa watu Wake “pendeleo la kutoa bila woga utumishi mtakatifu kwake kwa ushikamanifu na uadilifu” wakati wa maisha yao yote.—Luka 1:67-79, NW; linganisha Warumi 12:1; Ufunuo 7:9, 13-15, NW.
11. Ni pendeleo gani lenye kutokeza furaha linaloshirikishwa na kumtolea Mungu “utumishi mtakatifu”!
11 Pendeleo la kulichukua jina la Yehova tukiwa mashahidi wake linashirikishwa na lile la kumtolea Mungu “utumishi mtakatifu.” (Isaya 43:10-12) Hakika jambo hilo linapasa kuendeleza furaha, sawa na vile Yeremia alivyosema: “Maneno yako yalikuwa ni furaha kwangu, na shangwe ya moyo wangu; maana nimeitwa kwa jina lako, Ee [Yehova], Mungu wa majeshi.”—Yeremia 15:16.
12. Ikiwa tumevunjika moyo, ni kufikiria tofauti gani mbalimbali kunakoweza kuinua moyo wetu?
12 Ikiwa wewe unamtumikia Mungu lakini mara kwa mara unavunjika moyo, kufikiria kifupi tofauti fulani-fulani huenda kukainua moyo wako. Kwa mfano, tunapofikiria kwamba malaika wale waovu ‘wamewekwa akiba kwa pingu za milele wakiwa chini ya giza zito sana’ kwa ajili ya hukumu kali ya Mungu, ile hesabu kubwa iliyobaki ya malaika waadilifu walio katika utumishi wa Yehova inakuwa tofauti kwa sababu ni wenye furaha zaidi sana. (Yuda 6, NW) Tena pana tofauti kubwa sana kati ya cheo cha kufurahisha cha Yesu na kile cha Shetani Ibilisi, anayeelekeana na uharibifu wa milele! (Ufunuo 20:10, 14) Halafu, tena, kwa uhakika utunzaji wa Yehova wenye huruma na baraka zake unaturahisishia kuona “tofauti kati ya mtu mwadilifu na mtu mwovu, kati ya mtu anayetumikia Mungu na yeye ambaye hajamtumikia.” (Malaki 3:17,18, NW) Walakini, bado fikiria baraka nyingine zinazotoa sababu nzuri za kumtumikia Yehova kwa moyo wenye kujaa furaha.
Uhuru wa Kweli na Nuru ya Kiroho
13, 14. Katika mambo ya kidini, ni uhuru gani wa kweli na nuru ya kiroho ambayo watumishi wa Yehova wanafurahia?
13 Kwa uhakika kukombolewa katika ‘Babeli Mkuu,’ ile milki ya ulimwengu mzima ya dini ya uongo, ni baraka nyingine inayoendeleza furaha. Wakristo wa kweli wanafurahi kwa sababu ‘hawatashiriki dhambi zake na kupokea mapigo yake.’ (Ufunuo 18:2, 4) Tena, watumishi wa Yehova wanafurahia uhuru wa kutokuwa na woga wa namna mbalimbali unaotiwa katika watu na dini ya uongo, na pia hawasimuliwi ngano za uongo za dini hiyo. “Mtaifahamu kweli,” akasema Yesu, “nayo hiyo kweli itawaweka huru.” (Yohana 8:32) Uhuru huo wa kweli unaonekana kuwa wenye thamani zaidi wakati tunapofikiria utumwa wa wale walio katika giza la kiroho.
14 Kwa mfano, waabudu wa Yehova wako tofauti na wafuasi wengi sana wa dini ya uongo kwa sababu hawainamii wala kuiomba mifano isiyoweza wala kusema, kuona, kusikia, kunusa, kuhisi wala kutembea. (Zaburi 115:4-8) Wala Wakristo walio huru kiroho na walioangaziwa nuru hawaogopi wafu kama wakaaji wengi sana wa dunia. Lile fundisho la uongo la kidini la kusema mwanadamu ana nafsi isiyoweza kufa ndilo linaloikuza hofu nyingi hii ya kwamba mtu aliyekufa anaweza kurudi kunyanyasa-nyanyasa au kupiga-piga walio hai kwa taabu nyingi. Lakini nuru ya kiroho kutoka kwa Mungu imefukuzia mbali woga huo, kwa maana Wakristo wa kweli wanajua kwamba wafu “hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5, 10) Kuna mafaa mengi zaidi kutambua kwamba wapendwa waliokufa walio katika kumbukumbu la Mungu watafufuliwa! (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Kwa uhakika, Mashahidi wa Yehova waliojitoa wamtumikie wanaweza kushangilia kwa sababu Baba wa kimbingu wanayetumikia kwa upatani ametumia roho takatifu yake kuwafunulia “mafumbo ya Mungu.” (1 Wakorintho 2:10) Ndiyo, yeye amewapa watu wake nuru ya kiroho yenye kutokeza furaha na hata akawapa kweli.—Zaburi 43:3.
Furaha ya Kusaidia Wengine
15, 16. (a) Kulitukia nini wakati wanafunzi wa kwanza wa Yesu walipoacha ‘nuru yao ikaangaza’? (b) Ni jambo gani wanalopata Wakristo leo katika kazi ya kufanya wanafunzi?
15 Ni baraka pia kuangaza nuru ya kiroho baada ya kuipokea. Yesu aliambia wafuasi wake hivi: “Ninyi ni nuru ya ulimwengu. . . . Nuru yenu na iangaze mbele ya watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni.” (Mathayo 5:14-16) Kulitukia nini wakati wanafunzi hao wa kwanza walipoendelea kuacha ‘nuru yao iangaze’ kwa maneno na matendo yao? Wengine walipata faida, lakini utendaji huo uliwaletea furaha wafuasi wenyewe pia wa Kristo. (Luka 10:1, 17-20; Matendo 8:4-8) Kwa uhakika, hao wafanya wanafunzi walikuwa wakimtumikia Yehova kwa moyo wenye kujaa furaha.—Mathayo 28:19, 20.
16 Leo Wakristo wanapata furaha kama hiyo katika kazi ya kuutangaza ujumbe wa ufalme. Hasa ndivyo ilivyo kwa watu wanaosaidia wapate maarifa ya kuijua kweli ya Mungu. Mtume Paulo alikuwa na furaha hiyo, kwa maana yeye alisema kwamba Wafilipi aliokuwa amewasaidia walikuwa ‘furaha yake na taji yake.’ (Wafilipi 4:1) Kwa habari ya wale aliokuwa amewasaidia huko Thesalonike, mtume aliandika hivi: “Maana tumaini letu, au furaha yetu, au taji ya kujionea fahari, ni nini? Je! si ninyi, mbele za Bwana wetu Yesu, wakati wa [kuwapo] kwake? Maana ninyi ndinyi utukufu wetu, na furaha yetu.” (1 Wathesalonike 2:19, 20) Ndiyo, Paulo—sawa na Wakristo leo—alipata furaha kutokana na wale aliokuwa amewasaidia kiroho. Je! wewe unajinyosha sana katika jitihada za utumishi wa Yehova na kujipatia furaha ya namna hiyo?
17. Kujapokuwako matokeo machache katika maeneo fulani, kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanapata furaha katika kazi ya kufanya wanafunzi?
17 Wajapopata matokeo machache tu katika maeneo fulani leo, Mashahidi wa Yehova wanapata furaha kwa kujua kwamba wanampendeza Mungu wao na kumpa sifa. Hivyo ndivyo ilivyo hata ikiwa wenye nyumba fulani hawafurahii kuona Mashahidi wakibisha hodi milangoni pao. Watumishi wa Yehova hawavunjwi moyo na hilo, kwa maana wanatambua kwamba kutumikia Mungu ndilo pendeleo zuri zaidi ya mapendeleo yote yanayoweza kufurahiwa na mtu awaye yote duniani.
Hata Mateso Yanaleta Furaha
18. Kwa sababu gani Wakristo wanaweza kuwa na furaha wajapokuwa wakipatwa na mateso?
18 Wakristo wanamtumikia Yehova kwa moyo wenye kujaa furaha ingawa mara nyingi wanapatwa na mateso. Yesu aliwatangaza ni wenye furaha wale wenye kuteswa kwa ajili yake, naye mtume Petro akasema hivi: “Endeleeni kushangilia kwa kuwa ninyi ni washiriki katika taabu za Kristo, ili ninyi mpate kushangilia na kufurikwa na furaha pia wakati wa ufunuo wa utukufu wake. Ikiwa ninyi mnalaumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha.” Kwa sababu gani? “Kwa sababu,” anasema Petro, “roho ya utukufu, naam, ile roho ya Mungu, inatua juu yenu.” (1 Petro 4:13, 14, NW; Mathayo 5:11, 12) Huenda kupatwa na mateso kwa sababu ya kuwa Mkristo kukaonekana si baraka. Lakini ikiwa unavumilia taabu ya namna hiyo una ushuhuda wa kwamba roho na kibali ya Mungu ipo pamoja nawe—na, kwa uhakika, hiyo inaendeleza furaha.
19. Mtu mmoja aliyepatwa na mateso ya Wanazi alitoa maoni gani?
19 Kwa sababu ya kuwa na roho takatifu ya Mungu na nguvu ambazo Yehova anawapa, Wakristo wenye kuteswa wanaweza kudumisha furaha yao wakiwa chini ya hali zenye kupita kadiri. (Wafilipi 4:13) Miaka kadha iliyopita, Shahidi mmoja kijana aliyehukumiwa kifo akiwa katika kambi ya mateso ya Wanazi aliandikia wazazi wake barua akawaambia: “Usiku wa manane umekwisha kuanza. Bado ningali na wakati wa kubadili nia. Ah! ningeweza kweli kuwa na furaha tena katika ulimwengu huu baada ya kumkana Bwana wetu? Hakika nisingeweza! Lakini sasa ninyi mna uhakikisho wa kwamba mimi nauacha ulimwengu huu nikiwa na furaha na amani.” Ndiyo, Wakristo wenye kuteswa wanamtumikia Yehova wakiwa na moyo wenye kujaa furaha.
Sababu Nyingine za Kuwa na Furaha
20. Kunakuwa na matokeo gani juu ya furaha kwa kushirikiana na waamini. wenzetu?
20 Yajapokuwapo mateso yanayovumiliwa na Mashahidi wa Yehova, wao wanapata furaha ya kweli kwa kushirikiana na waamini wenzao. Baraka gani hiyo! Katika ulimwengu uliojawa na udanganyifu, uongo na matendo mabaya, ni vizuri kama nini kuwa na washirika wanyofu wenye kusema kweli na wasiofuata njia kombokombo, watu ambao wamekwisha kuvaa “utu mpya”! (Wakolosai 3:8-11) Halafu, tena, kuna uradhi mwingi sana katika kujua kwamba mwenendo wako mwenyewe unafanya moyo wa Yehova ushangilie.—Mithali 27:11, NW.
21. Ni nini nyingine za njia za kuendelezea faida za ibada ya kweli kwa furaha?
21 Ni baraka pia kuendeleza faida za ibada ya kweli kwa furaha, labda kwa kushiriki katika ujenzi, udumishaji kusaidia kulipia gharama za mahali pa mikutano ya Kikristo. (Kutoka 36:1-7 2 Wafalme 12:4-15) Kwa uhakika, jitihada za namna hiyo zinaletea mtu furaha ya moyoni. Tena ni vigumu sana mtu ye yote kukadiria vizuri kabisa baraka na furaha zinazokuja kwa wingi kwa kukutana kwa ukawaida pamoja na watu wa Yehova, na vilevile kwa kufanya ushirikiano nao katika ile kazi ya kutoa ushuhuda tuliyopewa na Mungu.—Zaburi 122:1; 1 Wakorintho 3:5-9.
22. Uaminifu katika kufanya vitendo vya kumcha Mungu unatokeza nini?
22 Uaminifu katika kufanya vitendo vya kumcha Mungu unatokeza baraka nyingi pia—taraja la kupata wokovu na wakati ujao wenye furaha katika mfumo mpya wa mambo ulioahidiwa na Mungu. (2 Petro 3:11-13) Kuna tofauti kubwa sana kati ya watumishi wa Yehova wenye kujawa na tumaini na watu ‘wasio na tumaini, wasio na Mungu duniani’! (Waefeso 2:11, 12) Kwa uhakika, watu wa Yehova wanaweza kumwambia Mungu maneno haya pamoja na Daudi: “Kwa habari yangu mimi, katika fadhili za upendo wako nimetumaini; acha moyo wangu uwe wenye kujaa furaha katika wokovu wako.” (Zaburi 13:5, NW) Kwa kweli, wakati Wakristo wanapohesabu baraka zao, wanapata sababu nyingi za kumtumikia Yehova kwa moyo wenye kujaa furaha.
Endelea ‘Kumtumikia Yehova kwa Kushangilia’
23. Badala ya kuruhusu mikazo inayozidi kuongezeka Itawale mawazo yetu, inatupasa tufanye nini?
23 Ingawa Mashahidi wa Yehova wanafurahia baraka nyingi sasa, hawawezi kuiepuka mikazo inayozidi kuongezeka kutokana na mfumo huu wa mambo wa kale. Inakuwa lazima mikazo hiyo ikabiliwe kishujaa huko kazini, shuleni na kwingineko, nayo inaweza kuvunja mtu moyo. Lakini, badala ya kuacha mambo hayo yasiyopendeka yatawale mawazo yetu na kutusumbua-sumbua daima, tunakuwa wenye hekima tukielekeza mawazo yetu kwenye mambo mema yenye kujenga. Ndiyo, badala ya kuvunjika moyo na kuwa na huzuni, acheni ‘tuwe wenye juhudi kwa kazi njema’ kisha tuzifikirie baraka ambazo tumezipata tukiwa watumishi wa Yehova. (Tito 2:14, NW) Halafu tutakuwa wachangamfu kama kwamba tunafurahia karamu inayozidi kuendelea. Ni kama vile Mithali 15:15 inavyoeleza jambo hilo: “Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya; bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.”
24. (a) Maisha yako yanawezaje kuwa na kusudi lenye kuthawabisha? (b) Ni ulizo gani linalotokezwa kwa kufaa?
24 Ni wazi kwamba watu wengi hawafurahii hali yao maishani. Lakini kama wewe unampenda Mungu na kumtii, na unavumilia katika utumishi wake kwa juhudi, maisha yako yana kusudi lenye kuthawabisha. Zaidi ya hilo, kwa msaada wa Yehova, matatizo na mikazo ya maisha yanaweza kuvumiliwa. Basi jipe moyo na uendelee kuzithamini sana baraka ambazo Mungu anakupa unapoendelea kumtumikia Yehova kwa moyo wenye kujaa furaha. (Zaburi 100:2) Lakini ni nini kinachotakwa ili kuendelea kushangilia katika ibada ya Yehova?
Je! Wewe unakumbuka mambo haya?
□ Kwa sababu gani watu wa Yehova hawalemewi kabisa na magumu ya maisha?
□ Maana yake nini kumjua Yehova, na jambo hilo linahusu furaha namna gani?
□ Kazi ya kufanya watu wawe wanafunzi ina uhusiano gani na furaha?
□ Tunawezaje kuendeleza ibada ya kweli kwa furaha?