USHIKAMANIFU
Katika Maandiko ya Kiebrania, kivumishi kinachotumiwa kufafanua “mtu mshikamanifu,” au mtu aliye na upendo mshikamanifu ni cha·sidhʹ. (Zb 18:25) Nomino cheʹsedh hurejezea fadhili lakini inahusisha mengi zaidi ya wazo la kuwa na wororo au fadhili inayotokana na upendo, ingawa sifa hizo zinahusika. Ni fadhili inayoshikamana na kitu fulani kwa upendo mpaka kusudi lake kuhusiana na kitu hicho litakapotimizwa. Mungu huwaonyesha watumishi wake fadhili ya aina hiyo nao watumishi wake hufanya vivyo hivyo kumwelekea yeye. Kwa hiyo ushikamanifu unaleta wazo la ushikamanifu mtakatifu uliojitoa na wenye uadilifu, na unafafanuliwa kuwa “upendo mshikamanifu.”—Mwa 20:13; 21:23; ona FADHILI.
Katika Maandiko ya Kigiriki nomino ho·si·oʹtes na kivumishi hoʹsi·os huleta wazo la utakatifu, uadilifu, heshima; ujitoaji, kumwogopa Mungu kikweli; kufanya kwa uangalifu wajibu wote kumwelekea Mungu. Inahusisha kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu.
Inaonekana hakuna maneno ya Kiswahili yanayolingana kabisa na maneno ya Kiebrania na Kigiriki, lakini neno “ushikamanifu,” lililo na wazo la ujitoaji na uaminifu, linapotumiwa kuhusiana na Mungu na utumishi wake, linatoa maana inayokaribia sana. Njia bora zaidi ya kuamua maana kamili ya maneno ya Biblia ni kuchunguza jinsi yanavyotumiwa katika Biblia.
Ushikamanifu wa Yehova. Yehova Mungu, Mtakatifu Zaidi, ambaye ni mwadilifu kabisa na sikuzote huwaonyesha upendo mshikamanifu usioyumbayumba wale wanaomtumikia, anawatendea kwa uadilifu na kweli hata maadui zake naye anategemeka kabisa. Kitabu cha Ufunuo kinasema hivi kumhusu: “Matendo yako ni makuu na ya ajabu, Yehova Mungu, Mweza-Yote. Njia zako ni za uadilifu na za kweli, Mfalme wa umilele. Ni nani ambaye kwa kweli hatakuogopa wewe, Yehova, na kulitukuza jina lako, kwa kuwa wewe peke yako ni mshikamanifu?” (Ufu 15:3, 4) Kwa sababu Yehova ameshikamana kabisa na uadilifu na haki, na pia kwa sababu upendo wake kwa watu wake unamfanya achukue hatua inayohitajika ya kihukumu, malaika mmoja alichochewa kusema hivi: “Wewe, Ambaye uko na uliyekuwako, Mshikamanifu, wewe ni mwadilifu, kwa kuwa umetoa hukumu hizi.”—Ufu 16:5; linganisha Zb 145:17.
Yehova ni mshikamanifu kwa maagano yake. (Kum 7:9) Kwa miaka mingi alilionyesha taifa la Israeli subira na rehema kwa sababu ya agano lake pamoja na rafiki yake Abrahamu. (2Fa 13:23) Aliwasihi hivi Waisraeli kupitia Yeremia nabii wake: “‘Rudi, Ee Israeli mwasi,’ asema Yehova. ‘Sitakutazama kwa hasira, kwa maana mimi ni mshikamanifu.’” (Yer 3:12) Walio washikamanifu kwake wanaweza kumtegemea kikamili. Daudi alisema hivi alipomwomba Mungu msaada katika sala: “Kwa mtu mshikamanifu unatenda kwa ushikamanifu; kwa mtu asiye na lawama, mtu hodari, unatenda bila lawama.” (2Sa 22:26) Daudi aliwasihi Waisraeli wageuke mbali kutoka kwa mambo mabaya na kufanya yaliyo mema, “Kwa maana Yehova anapenda haki, naye hatawaacha washikamanifu wake. Watalindwa sikuzote.”—Zb 37:27, 28.
Wale walio washikamanifu kwa Yehova watakuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye, na Yehova atawasaidia kubaki waaminifu hadi mwisho, nao wanaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atawakumbuka hata wapatwe na hali gani. Anailinda njia yao. (Met 2:8) Analinda uhai wao au nafsi zao.—Zb 97:10.
Yesu Kristo. Alipokuwa duniani, Yesu Kristo aliimarishwa sana kwa kutambua kwamba Mungu alikuwa ametabiri kuwa nafsi yake haingeachwa katika kaburi kwa sababu alikuwa “mshikamanifu” sana kwa Mungu. (Zb 16:10) Katika siku ya Pentekoste, 33 W.K., mtume Petro alielekeza unabii huo kwa Yesu, aliposema: “[Daudi] aliona mapema na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika Kaburi wala mwili wake haukuona uharibifu. Mungu alimfufua, Yesu huyu, na sisi sote ni mashahidi wa jambo hilo.” (Mdo 2:25-28, 31, 32; linganisha Mdo 13:32-37.) Kikieleza kuhusu andiko la Matendo 2:27, kitabu The Expositor’s Greek Testament kinasema kwamba neno la Kiebrania cha·sidhʹ (linalotumiwa katika Zb 16:10) “linamaanisha mtu ambaye anapokea upendo mshikamanifu wa Yehova, si yule aliye wa kimungu au anayemwogopa Mungu tu.”—Kilichohaririwa na W. R. Nicoll, 1967, Buku la II.
Ushikamanifu Ambao Mungu Anataka. Yehova anataka watumishi wake wawe washikamanifu. Ni lazima wamwige. (Efe 5:1) Mtume Paulo aliwaambia Wakristo kwamba ‘wanapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.’ (Efe 4:24) Alipopendekeza kwamba sala itolewe katika kutaniko, alisema: “Basi ninatamani kwamba kila mahali wanaume waendelee kusali, wakiinua mikono yenye ushikamanifu, bila hasira wala mabishano.” (1Ti 2:8) Ushikamanifu ni sifa muhimu sana kwa mwanamume ambaye anataka kustahili kuwekwa rasmi kutumikia akiwa mwangalizi katika kutaniko la Mungu.—Tito 1:8.