Mtumikie Yehova kwa Uaminifu-Mshikamanifu
“Kwa mtu mwaminifu-mshikamanifu wewe [Yehova] utatenda katika uaminifu-mshikamanifu.”—2 SAMWELI 22:26, NW.
1. Yehova hutendaje kwa wale walio waaminifu-washikamanifu kwake?
YEHOVA hawezi kulipwa kwa yote anayowafanyia watu wake. (Zaburi 116:12) Zawadi zake za kiroho na kimwili na rehema yake nyororo ni ya ajabu kama nini! Mfalme Daudi wa Israeli la kale alijua kwamba Mungu pia hutenda katika uaminifu-mshikamanifu kwa wale walio waaminifu-washikamanifu kwake. Daudi alisema hivyo katika wimbo aliotunga “siku ile BWANA [Yehova, NW] alipomwokoa mikononi mwa adui zake zote, na mkononi mwa [Mfalme] Sauli.”—2 Samweli 22:1.
2. Ni baadhi ya mambo gani yanayotolewa katika wimbo wa Daudi uliorekodiwa katika 2 Samweli sura 22?
2 Daudi alianza wimbo wake (unaolingana na Zaburi 18) kwa kumsifu Yehova akiwa “Mwandalizi wa Wokovu” kwa kujibu sala. (2 Samweli 22:2-7, NW) Kutoka hekalu lake la kimbingu, Mungu alitenda ili kumkomboa mtumishi wake mwaminifu-mshikamanifu kutoka kwa adui zake wenye nguvu. (Mistari 8-19) Hivyo Daudi alithawabishwa kwa ajili ya kufuatia mwendo mnyoofu na kushika njia za Yehova. (Mistari 20-27) Yaliyotajwa baada ya hayo ni matendo yaliyofanywa kwa nguvu za kupewa na Mungu. (Mistari 28-43) Mwisho, Daudi alitaja ukombozi kutoka kwa wachambuzi wa nyumbani na adui wa mataifa mengine akamshukuru Yehova kuwa “Yule anayemfanyia mfalme wake vitendo vikuu vya wokovu na kumwonyesha mpakwa-mafuta wake fadhili-upendo.” (Mistari 44-51, NW) Yehova aweza kutukomboa pia tukifuatia mwendo mnyoofu na kumtegemea atupe nguvu.
Maana ya Kuwa Mwaminifu-Mshikamanifu
3. Kulingana na maoni ya Kimaandiko, kuwa mwaminifu-mshikamanifu kunamaanisha nini?
3 Wimbo wa Daudi wa wokovu unatupa sisi uhakikishio wenye kufariji: “Kwa mtu mwaminifu-mshikamanifu wewe [Yehova] utatenda katika uaminifu-mshikamanifu.” (2 Samweli 22:26, NW) Kivumishi cha Kiebrania cha·sidhʹ ndicho kinachotumiwa ili kuonyesha “mtu mwaminifu-mshikamanifu,” au “mtu mwenye fadhili-upendo.” (Zaburi 18:25, NW, kielezi-chini) Nomino cheʹsedh ina wazo la fadhili inayojishikamanisha na kitu fulani kwa upendo mpaka kusudi layo kuhusiana na kitu hicho linapotimizwa. Yehova huwaonyesha watumishi wake fadhili ya aina hiyo, sawa na vile wanavyomwonyesha yeye. Uaminifu-mshikamanifu huo mwadilifu, ulio mtakatifu hufasiriwa “fadhili-upendo” na “upendo mwaminifu-mshikamanifu.” (Mwanzo 20:13; 21:23) Katika Maandiko ya Kigiriki, “uaminifu-mshikamanifu” huhusisha wazo la utakatifu na kicho, ambavyo huonyeshwa katika nomino ho·si·oʹtes na kivumishi hoʹsi·os. Uaminifu-mshikamanifu huo hutia ndani uaminifu na ujitoaji na humaanisha kuwa mchaji mwenye bidii na kufanya kwa uangalifu wajibu wote kumwelekea Mungu. Kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova kunamaanisha kushikamana na yeye kwa ujitoaji imara sana hivi kwamba huo unatenda kama gundi yenye nguvu.
4. Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova huonyeshwaje?
4 Uaminifu-mshikamanifu wa Yehova mwenyewe huonyeshwa katika njia nyingi. Kwa mfano, anatekeleza hukumu dhidi ya waovu kwa sababu ya upendo mwaminifu-mshikamanifu kwa watu wake na kwa ajili ya uaminifu-mshikamanifu kwa haki na uadilifu. (Ufunuo 15:3, 4; 16:5) Uaminifu-mshikamanifu kwa agano lake kwa Abrahamu ulimsukuma Mungu kuwa mstahimilivu kuelekea Waisraeli. (2 Wafalme 13:23) Wale walio waaminifu-washikamanifu kwa Mungu wanaweza kutegemea msaada wake hadi mwisho wa mwendo wao mwaminifu-mshikamanifu na wanaweza kuwa na uhakika wa kwamba atawakumbuka. (Zaburi 37:27, 28; 97:10) Yesu aliimarishwa na maarifa ya kwamba akiwa ndiye “mwaminifu-mshikamanifu” mkuu wa Mungu, nafsi yake isingeachwa katika Sheoli.—Zaburi 16:10, NW; Matendo 2:25, 27.
5. Kwa kuwa Yehova ni mwaminifu-mshikamanifu, yeye hutaka nini kwa watumishi wake, na ni swali gani litakalofikiriwa?
5 Kwa kuwa Yehova Mungu ni mwaminifu-mshikamanifu, anataka uaminifu-mshikamanifu kutoka kwa watumishi wake. (Waefeso 4:24) Kwa mfano, ni lazima wanaume wawe waaminifu-washikamanifu ili kustahili kuwekwa rasmi kuwa wazee wa kundi. (Tito 1:8) Ni mambo gani yapaswayo kuwasukuma watu wa Yehova wamtumikie kwa uaminifu-mshikamanifu?
Uthamini kwa Mambo Tunayojifunza
6. Twapaswa kuhisije juu ya mambo ya Kimaandiko ambayo tumejifunza, na twapaswa kukumbuka nini juu ya maarifa hayo?
6 Shukrani kwa mambo ya Kimaandiko ambayo tumejifunza yapaswa itusukume tumtumikie Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Mtume Paulo alimhimiza Timotheo hivi: “Ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:14, 15) Kumbuka kwamba maarifa hayo yalitoka kwa Mungu kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”—Mathayo 24:45-47.
7. Wazee wanapaswa kuhisije juu ya chakula cha kiroho kinachoandaliwa na Mungu kupitia mtumwa mwaminifu?
7 Wazee waliowekwa rasmi ndio wanaopaswa hasa kuthamini chakula cha kiroho chenye kuimarisha kinachoandaliwa na Mungu kupitia mtumwa mwaminifu. Miaka kadhaa iliyopita wazee wachache walikosa uthamini huo. Mtazamaji mmoja alisema kwamba wanaume hao “walikuwa wachambuzi wa makala katika Mnara wa Mlinzi, wasitake kulikubali kuwa . . . njia ya Mungu ya kuwasilisha kweli, wakijaribu sikuzote kuwavuta wengine katika njia yao ya kufikiri.” Hata hivyo, wazee waaminifu-washikamanifu hawajaribu kuwavuta wengine kukatalia mbali chakula chochote cha kiroho kinachoandaliwa na Mungu kupitia mtumwa mwaminifu.
8. Namna gani tusipothamini kikamili jambo fulani la Kimaandiko linalotolewa na mtumwa mwaminifu mwenye akili?
8 Tukiwa Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu, ni lazima sisi sote tuwe waaminifu-washikamanifu kwake na kwa tengenezo lake. Hatupaswi hata kufikiria kugeuka kando kutoka kwa nuru ya Mungu ya ajabu, tukifuatia mwendo wa uasi-imani uwezao kuongoza kwenye kifo cha kiroho sasa na kwenye uharibifu hatimaye. (Yeremia 17:13) Lakini namna gani ikiwa ni vigumu kwetu kukubali au kuthamini kikamili jambo fulani la Kimaandiko linalotolewa na mtumwa mwaminifu? Basi acheni tukiri kwa unyenyekevu mahali tulipojifunzia kweli na kusali ili kupata hekima ya kushughulika na jaribu hilo mpaka lifikie mwisho kwa maelezo wazi yenye kutangazwa kwa chapa kuhusu jambo hilo.—Yakobo 1:5-8.
Thamini Udugu wa Kikristo
9. Yohana wa Kwanza 1:3-6 huonyeshaje kwamba ni lazima Wakristo wawe na roho ya ushirika?
9 Uthamini wa kuhisiwa moyoni kwa ajili ya roho ya ushirika iliyomo ndani ya udugu wetu wa Kikristo hutokeza kichocheo cha kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Kwa kweli, uhusiano wetu na Mungu na Kristo hauwezi kuwa katika hali njema bila roho hiyo. Mtume Yohana aliwaambia Wakristo wapakwa-mafuta hivi: “Hilo tuliloliona na kulisikia, twawahubiri na ninyi; ili nanyi pia mpate kushirikiana [“ushirika,” Diaglott] nasi: na ushirika wetu ni pamoja na Baba, na pamoja na Mwana wake Yesu Kristo. . . . Tukisema ya kwamba twashirikiana naye, tena tukienenda gizani, twasema uongo, wala hatuifanyi iliyo kweli.” (1 Yohana 1:3-6) Kanuni hiyo yawahusu Wakristo wote, tumaini lao liwe ni la kimbingu au la kidunia.
10. Ingawa yaonekana Euodia na Sintike walikuwa na ugumu wa kusuluhisha tatizo la kibinafsi, Paulo aliwaonaje wanawake hao?
10 Jitihada yatakikana ili kudumisha roho ya ushirika. Kwa mfano, yaonekana wanawake Wakristo Euodia na Sintike waliliona kuwa jambo gumu kusuluhisha tatizo lililokuwa kati yao. Hivyo Paulo aliwahimiza “wawe na nia moja katika Bwana.” Aliongeza hivi: “Nataka na wewe pia, mjoli wa kweli; uwasaidie wanawake hao; kwa maana walishindania Injili [habari njema, NW] pamoja nami, na Klementi naye, na wale wengine waliotenda kazi pamoja nami, ambao majina yao yamo katika kitabu cha uzima.” (Wafilipi 4:2, 3) Wanawake hao wenye kumcha Mungu walikuwa wameshindania “habari njema” pamoja na Paulo na wengine, naye alikuwa na uhakika wa kwamba walikuwa miongoni mwa wale ‘ambao majina yao yalikuwa katika kitabu cha uzima.’
11. Mkristo mwaminifu-mshikamanifu akikabili tatizo la kiroho, ingefaa akumbuke nini?
11 Wakristo hawavai nishani ya cheo kuonyesha kile ambacho wamependelewa kufanya katika tengenezo la Yehova na jinsi ambavyo wamemtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu. Ikiwa wana tatizo la kiroho, lingekuwa jambo lenye kukosa upendo kama nini kupuuza miaka yao ya utumishi mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova! Yaelekea, yule aliyeitwa “mjoli wa kweli” alikuwa ndugu mwaminifu-mshikamanifu aliyekuwa na hamu ya kuwasaidia wengine. Ikiwa wewe ni mzee, je, wewe ni “mjoli wa kweli,” aliye tayari kusaidia katika njia ya huruma? Sisi sote na tuyafikirie yale mema ambayo waamini wenzetu wamefanya, sawa na vile Mungu hufikiria, na kuwasaidia kwa upendo wachukue mizigo yao.—Wagalatia 6:2; Waebrania 6:10.
Hakuna Mahali Penginepo Pote pa Kwenda
12. Taarifa za Yesu zilipowasababisha ‘wanafunzi wengi warejee nyuma,’ Petro alichukua msimamo gani?
12 Tutasukumwa kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu pamoja na tengenezo lake tukikumbuka kwamba hakuna mahali penginepo pote pa kwenda ili kupata uhai wa milele. Taarifa za Yesu zilipowasababisha ‘wanafunzi wake warejee nyuma,’ yeye aliwauliza mitume wake hivi: “Je! ninyi mwataka kuondoka?” Petro alijibu hivi: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu.”—Yohana 6:66-69.
13, 14. (a) Kwa nini Dini ya Kiyahudi ya karne ya kwanza ilikosa upendeleo wa kimungu? (b) Shahidi mmoja wa Yehova alisema nini juu ya tengenezo la Mungu lionekanalo?
13 “Maneno ya uzima wa milele” hayakupatikana katika Dini ya Kiyahudi ya karne ya kwanza W.K. Dhambi yayo kuu ilikuwa ya kumkatalia mbali Yesu kuwa Mesiya. Hakuna namna yoyote ya Dini ya Kiyahudi iliyotegemea kikamili Maandiko ya Kiebrania. Masadukayo walikana kuwako kwa malaika na hawakuamini katika ufufuo. Ingawa Mafarisayo hawakukubaliana nao katika mambo hayo, wao walibatilisha Neno la Mungu kidhambi kwa sababu ya mapokeo yao yasiyo ya kimaandiko. (Mathayo 15:1-11; Matendo 23:6-9) Mapokeo hayo yaliwatumikisha Wayahudi na yalikufanya kumkubali Yesu Kristo kuwa jambo gumu kwa wengi. (Wakolosai 2:8) Bidii kwa ajili ya ‘mapokeo ya baba zake’ ilimsababisha Sauli (Paulo), katika ukosefu wake wa maarifa, awe mnyanyasi mkali wa wafuasi wa Kristo.—Wagalatia 1:13, 14, 23.
14 Dini ya Kiyahudi ilikosa upendeleo wa Mungu, lakini Yehova alibariki lile tengenezo lililofanyizwa na wafuasi wa Mwana wake—‘watu wenye juhudi katika matendo mema.’ (Tito 2:14) Tengenezo hilo lingali liko leo, na Shahidi mmoja wa Yehova alisema hivi juu yalo: “Ikiwa kuna jambo ambalo limekuwa lenye umaana zaidi kwangu, jambo hilo limekuwa ni kuendelea kuwa karibu na tengenezo la Yehova lionekanalo. Maono yangu ya mapema yamenifundisha jinsi isivyofaa kutegemea kusababu kwa kibinadamu. Mara akili yangu ilipokuwa imeazimia juu ya hilo, nilipiga moyo konde kubaki karibu na tengenezo hilo jaminifu. Kwani ni kwa njia gani nyingine mtu anaweza kupata upendeleo na baraka ya Yehova?” Hakuna mahali penginepo pote pa kwenda ili kupata upendeleo wa kimungu na uhai wa milele.
15. Kwa nini tushirikiane na tengenezo la Yehova lionekanalo na wale wenye daraka ndani yalo?
15 Mioyo yetu yapaswa itusukume kushirikiana pamoja na tengenezo la Yehova kwa sababu twajua kwamba hilo pekee ndilo huelekezwa na roho yake na ndilo linalojulisha jina na makusudi yake. Bila shaka, wale wenye daraka ndani yalo si wakamilifu. (Warumi 5:12) Lakini ‘hasira za Yehova ziliwaka’ dhidi ya Haruni na Miriamu walipomchambua Musa na kusahau kwamba yeye, si wao, ndiye aliyekabidhiwa daraka la kupewa na Mungu. (Hesabu 12:7-9) Leo, Wakristo waaminifu-washikamanifu hushirikiana na ‘wale wanaoongoza’ kwa sababu hilo ndilo jambo ambalo Yehova hutaka. (Waebrania 13:7, 17) Uthibitisho wa uaminifu-mshikamanifu wetu hutia ndani kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kutoa maelezo ‘yanayowahimiza wengine katika upendo na kazi nzuri.’—Waebrania 10:24, 25.
Kuwa Mwenye Kujenga
16. Tamaa ya kuwafanyia wengine nini yapaswa itusukume tumtumikie Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu?
16 Tamaa ya kuwa mwenye kujenga wengine yapaswa pia ituchochee kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Paulo aliandika hivi: “Ujuzi [maarifa, NW] huleta majivuno, bali upendo hujenga.” (1 Wakorintho 8:1) Kwa kuwa aina fulani ya maarifa iliwafanya waliokuwa nayo wajivune, ni lazima iwe Paulo alikuwa akimaanisha kwamba upendo huwajenga pia wale wanaoionyesha sifa hiyo. Kitabu cha Maprofesa Weiss na English chasema hivi: “Mtu mwenye uwezo wa kupenda kwa kawaida hupendwa yeye mwenyewe. Uwezo wa kunyoosha nia njema na ufikirio katika kila sehemu ya maisha . . . una matokeo yenye kujenga yaonekanayo waziwazi juu ya mtu anayenyoosha hisia hizo na pia juu ya mtu anayezipokea na hivyo huwaletea wote wawili furaha.” Kwa kuonyesha upendo, sisi huwajenga wengine, kama inavyodokezwa na maneno ya Yesu: “Ni heri kutoa kuliko kupokea.”—Matendo 20:35.
17. Upendo hujengaje, nao utatuzuia tusifanye nini?
17 Kwenye 1 Wakorintho 8:1, Paulo alitumia neno la Kigiriki a·gaʹpe linaloonyesha upendo wenye kanuni. Huo hujenga, kwani ni wenye ustahimilivu na fadhili, unastahimili na kuvumilia mambo yote, nao haushindwi kamwe. Upendo huo huondoa hisiamoyo zenye kudhuru, kama vile kiburi na wivu. (1 Wakorintho 13:4-8) Upendo huo utatuzuia tusilalamike juu ya ndugu zetu wasio wakamilifu, sawa na sisi tusivyo wakamilifu. Utatuzuia tusiwe kama wale “watu wasiomcha Mungu” ‘waliojipenyeza ndani’ miongoni mwa Wakristo wa kweli katika karne ya kwanza. Watu hao walikuwa “wanaonyesha kutojali ubwana na wanasema kwa ufidhuli juu ya watakatifu,” yaonekana wakisema mambo ya kudharau watu kama waangalizi Wakristo wapakwa-mafuta waliokuwa wamepewa utukufu fulani. (Yuda 3, 4, 8, NW) Kwa uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova, acheni sisi tusishindwe kamwe na kishawishi cha kufanya lolote linalofanana na hilo.
Mpinge Ibilisi!
18. Shetani angependa kufanya nini kwa watu wa Yehova, lakini ni kwa nini hawezi kufanya hivyo?
18 Maarifa ya kwamba Shetani anataka kuharibu umoja wetu tukiwa watu wa Mungu yapaswa yaongeze azimio letu la kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Shetani angependa hata kuwafutilia mbali watu wote wa Mungu. Lakini Mungu hatamruhusu Shetani awaue wote. Yesu alikufa “ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi.” (Waebrania 2:14) Milki ya Shetani ya kuzoea mamlaka imezuiwa hasa tangu aondoshwe mbinguni baada ya Kristo kuwa Mfalme katika 1914. Na wakati wa Yehova uwadiapo, Yesu atamharibu Shetani na tengenezo lake.
19. (a) Ni onyo gani kuhusu jitihada za Shetani lililotolewa na jarida hili miaka kadhaa iliyopita? (b) Ili kuepuka mitego ya Shetani, tunapaswa tuonyeshe uangalifu gani katika kushughulika na waamini wenzetu?
19 Jarida hili lilionya hivi wakati mmoja: “Kama Shetani, Ibilisi, akiweza kusababisha mchafuko miongoni mwa watu wa Mungu, aweze kusababisha wagombane na kupigana miongoni mwao, au wadhihirishe na kusitawisha nia ya ubinafsi iwezayo kuongoza kwenye uharibifu wa upendo kwa akina ndugu, hapo angeweza kufanikiwa katika kuwaangamiza.” (The Watch Tower, Mei 1, 1921, ukurasa 134) Acheni tusimruhusu Ibilisi aharibu umoja wetu, labda kwa kutushawishi tuchongeane, au tupigane. (Mambo ya Walawi 19:16) Shetani na asitushinde kwa hila zake katika njia ambayo kwayo twadhuru kibinafsi wale wanaomtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu au kufanya maisha yawe magumu zaidi kwao. (Linganisha 2 Wakorintho 2:10, 11) Bali, acheni tutumie maneno ya Petro: “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni [simameni imara dhidi ya, NW] huyo, mkiwa thabiti katika imani.” (1 Petro 5:8, 9) Kwa kusimama imara dhidi ya Shetani, twaweza kudumisha umoja wetu uliobarikiwa tukiwa watu wa Yehova.—Zaburi 133:1-3.
Mtegemee Mungu kwa Sala
20, 21. Kumtegemea Yehova kwa sala kunahusikaje na kumtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu?
20 Kumtegemea Mungu kwa sala kutatusaidia tuendelee kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu. Tunapoona ya kwamba anajibu sala zetu, tunazidi kuvutwa karibu zaidi na yeye. Kumtegemea Yehova Mungu kwa sala kulihimizwa wakati mtume Paulo alipoandika hivi: “Nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.” (1 Timotheo 2:8) Kwa mfano, ni jambo la maana kama nini kwamba wazee wamtegemee Mungu kwa sala! Wonyesho huo wa uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova wakati wanapokutana kuzungumzia mambo ya kundi utasaidia kuzuia majadiliano yasiyo na mwisho na uwezekano wa mifoko ya hasira.
21 Kumtegemea Yehova Mungu kwa sala kunatusaidia tushughulikie mapendeleo katika utumishi wake. Mwanamume mmoja aliyekuwa amemtumikia Yehova Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu kwa miongo mingi angeweza kusema hivi: “Kukubali kwetu kwa nia mgawo wowote tunaopewa katika tengenezo la Mungu la ulimwenguni pote, na kubaki kwetu katika mgawo wetu, bila kutikisika, kwaleta kibali cha Mungu juu ya jitihada zetu nyingi. Hata ikiwa kazi tuliyogawiwa yaonekana kuwa ya hali ya chini, mara nyingi inatokea kwamba bila kazi hiyo kufanywa utumishi mwingine mwingi wa muhimu usingeweza kufanywa. Hivyo ikiwa sisi ni wanyenyekevu na wenye kupendezwa moja kwa moja na kulitukuza jina la Yehova na si letu wenyewe, basi twaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote tutakuwa ‘imara, bila kutikisika, tukiwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Yehova.’”—1 Wakorintho 15:58, NW.
22. Baraka nyingi za Yehova zapaswa kuathirije uaminifu-mshikamanifu wetu?
22 Iwe tunafanya nini katika utumishi wa Yehova, bila shaka hatuwezi kumlipa kwa yale ambayo anatufanyia. Sisi tuko salama kama nini katika tengenezo la Mungu, tukiwa tumezungukwa na wale walio marafiki wake! (Yakobo 2:23) Yehova ametubariki na umoja unaotokana na upendo wa kidugu wenye shina lenye kina kirefu sana hivi kwamba Shetani mwenyewe hawezi kuung’oa. Acheni basi tushikamane na Baba yetu wa kimbingu mwaminifu-mshikamanifu na kufanya kazi pamoja tukiwa watu wake. Sasa na kwa umilele wote, acheni tumtumikie Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu.
◻ Kuwa mwaminifu-mshikamanifu kunamaanisha nini?
◻ Ni baadhi ya mambo gani yapaswayo kutusukuma kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu?
◻ Kwa nini ni lazima tumpinge Ibilisi?
◻ Sala yaweza kutusaidiaje tuwe watumishi wa Yehova waaminifu-washikamanifu?
[Picha katika ukurasa wa 23]
Watumishi wa Yehova waaminifu-washikamanifu hawamruhusu Adui wao aliye kama simba, Ibilisi, avunje umoja wao