Kutumikia kwa Uaminifu-Mshikamanifu Pamoja na Tengenezo la Yehova
“Kwa mtu mwenye uaminifu-mshikamanifu utatenda kwa uaminifu-mshikamanifu.”—2 SAMWELI 22:26, NW.
1, 2. Ni vipi baadhi ya vielelezo vya uaminifu-mshikamanifu ambavyo sote twaweza kuona kutanikoni?
JIONI moja saa zikiwa zimesonga sana mzee mmoja atayarisha hotuba kwa ajili ya mkutano wa Kikristo. Angependa kuachia hapo na kupumzika; badala ya hivyo, anaendelea kufanya kazi, akitafuta vielelezo na vielezi vya Kimaandiko vitakavyofikia mioyo na kulitia kundi moyo. Usiku wa huo mkutano, wazazi wawili waliochoka sana katika kutaniko hilohilo wangefurahia kupisha jioni nyumbani; badala ya hivyo, wanawatayarisha watoto wao kwa subira na kwenda mkutanoni. Baada ya huo mkutano, kikundi cha Wakristo chazungumzia hotuba ya yule mzee. Dada mmoja ashawishiwa kutaja kwamba ndugu huyohuyo aliumiza hisia zake wakati mmoja; badala ya hivyo, asema kwa idili juu ya mojawapo ya hoja alizotoa. Je, waona jambo lenye kujitokeza tena na tena katika matukio hayo?
2 Jambo hilo ni uaminifu-mshikamanifu. Yule mzee afanya kazi kwa uaminifu-mshikamanifu ili kutumikia kundi la Mungu; wale wazazi wahudhuria mikutano ya kutaniko kwa uaminifu-mshikamanifu; yule dada awategemeza wazee kwa uaminifu-mshikamanifu. (Waebrania 10:24, 25; 13:17; 1 Petro 5:2) Ndiyo, katika pande zote za maisha, twaona watu wa Mungu wakiwa wameazimia kutumikia kwa uaminifu-mshikamanifu pamoja na tengenezo la Yehova.
3. Kwa nini ni jambo la maana sana kwamba tuendelee kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo la Yehova la kidunia?
3 Yehova autazamapo ulimwengu mfisadi ulio chini, aona uaminifu-mshikamanifu mchache sana. (Mika 7:2) Jinsi moyo wake lazima uwe waitikia kwa shangwe achunguzapo kwa makini uaminifu-mshikamanifu wa watu wake! Ndiyo, uaminifu-mshikamanifu wako mwenyewe humpendeza. Hata hivyo, humchukiza Shetani, yule mwasi wa awali, nao humthibitisha kuwa mwongo. (Mithali 27:11; Yohana 8:44) Tarajia kwamba Shetani atajaribu kudhoofisha uaminifu-mshikamanifu wako kwa Yehova na kwa tengenezo Lake la kidunia. Acheni tufikirie kwa uangalifu njia fulani ambazo kwazo Shetani hufanya hivyo. Hivyo twaweza kuona vizuri zaidi jinsi ya kuendelea kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu hadi mwisho.—2 Wakorintho 2:11.
Kukazia Fikira Kutokamilika Kwaweza Kumomonyoa Uaminifu-Mshikamanifu
4. (a) Kwa nini ni rahisi kuwachambua walio na mamlaka? (b) Kora alithibitikaje kuwa asiye na uaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo la Yehova?
4 Ndugu akiwa katika wadhifa wenye madaraka, makosa yake yaweza kuonekana wazi zaidi. Jinsi ilivyo rahisi kuchambua ‘unyasi ulio katika jicho la ndugu yetu huku tukilipuuza boriti lililo katika jicho letu wenyewe’! (Mathayo 7:1-5) Hata hivyo, kufikiria sana makosa kwaweza kukuza ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu. Kwa kutoa kielezi, fikiria tofauti kati ya Kora na Daudi. Kora alikuwa na madaraka mengi, na labda alikuwa amekuwa mwaminifu kwa miaka mingi, lakini akatamani makuu. Alikuja kuonea uchungu mamlaka ya Musa na Aroni, binamu zake. Ingawa Musa alikuwa msikivu zaidi kati ya watu, kwa wazi Kora alianza kumtazama kwa macho ya kutafuta makosa. Yamkini aliona makosa ya Musa. Hata hivyo, makosa hayo, hayakufanya ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu wa Kora kwa tengenezo la Yehova ustahili. Aliharibiwa kutoka miongoni mwa kutaniko hilo.—Hesabu 12:3; 16:11, 31-33.
5. Kwa nini huenda ikawa Daudi alihisi kushawishiwa kumwasi Sauli?
5 Kwa upande mwingine, Daudi alitumikia chini ya Mfalme Sauli. Sauli ambaye wakati mmoja alikuwa mfalme mzuri, kwa kweli alikuja kuwa mwovu. Daudi alihitaji imani, uvumilivu, na hata werevu ili kusalimika mashambulizi ya Sauli mwenye wivu. Hata hivyo, Daudi alipokuwa na fursa ya kulipiza kisasi, alisema kwamba hilo lilikuwa ‘lisilowazika, kwa maoni ya Yehova,’ kwamba atende tendo la ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu dhidi ya mtu ambaye Yehova alikuwa amemtia mafuta.—1 Samweli 26:11, NW.
6. Hatupaswi kamwe kufanya nini, hata tukiona udhaifu na makosa katika wazee?
6 Baadhi ya wanaoongoza miongoni mwetu waonekanapo kukosea katika hukumu, wasemapo kwa maneno makali, au waonekanapo kuonyesha upendeleo, je, tutalalamika dhidi yao, labda tukichangia roho ya uchambuzi kutanikoni? Je, tutakosa kuhudhuria mikutano ya Kikristo ikiwa njia moja ya kuteta dhidi yao? Kwa hakika la! Sawa na Daudi, hatutaruhusu kamwe makosa ya mwingine yatufanye tukose uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova na kwa tengenezo lake!—Zaburi 119:165.
7. Ni yapi baadhi ya mazoea yenye ufisadi yaliyodhihirika kuhusiana na hekalu katika Yerusalemu, na Yesu alihisije juu ya hilo?
7 Kielelezo kikuu zaidi cha kibinadamu cha uaminifu-mshikamanifu kilikuwa Yesu Kristo, anayefafanuliwa kiunabii kuwa “mwenye uaminifu-mshikamanifu” wa Yehova. (Zaburi 16:10, NW) Kulitumia hekalu la Yerusalemu kwa ufisadi lazima kuwe kulifanya uaminifu-mshikamanifu uwe jambo gumu. Yesu alijua kwamba kazi ya kuhani mkuu na zile dhabihu zilifananisha kimbele huduma yake mwenyewe na kifo chake cha kidhabihu, naye alijua jinsi lilivyokuwa jambo la maana watu wajifunze kutokana na hayo. Kwa hiyo alijawa na ghadhabu ya uadilifu alipoona kwamba hekalu lilikuwa limekuwa “pango la wapokonyaji.” Akiwa na mamlaka yenye kupewa na Mungu, alichukua hatua ya kulisafisha mara mbili.a—Mathayo 21:12, 13; Yohana 2:15-17.
8. (a) Yesu alionyeshaje uaminifu-mshikamanifu kwa mpango wa hekalu? (b) Twaweza kuonyeshaje kwamba twathamini kumwabudu Yehova pamoja na tengenezo lake safi?
8 Hata hivyo, Yesu alitegemeza mpango huo wa hekalu kwa uaminifu-mshikamanifu. Tangu utotoni, alihudhuria zile sikukuu kwenye hilo hekalu na alifundisha humo mara nyingi. Hata alilipa kodi ya hekalu—ingawa kwa kweli hakuwa na wajibu wa kufanya hivyo. (Mathayo 17:24-27) Yesu alimpongeza yule mjane maskini kwa kutumbukiza “riziki yake yote” kwenye sanduku la hazina ya hekalu. Punde baada ya hapo, Yehova alilikataa kabisa hekalu hilo. Lakini hadi wakati huo, Yesu alikuwa mwenye uaminifu-mshikamanifu kwalo. (Marko 12:41-44; Mathayo 23:38) Leo tengenezo la Mungu la kidunia ni bora zaidi kuliko mfumo wa Kiyahudi pamoja na hekalu la mfumo huo. Yakubalika kwamba tengenezo hilo si kamilifu; ndiyo sababu marekebisho hufanywa nyakati nyingine. Lakini halina ufisadi, wala Yehova Mungu haelekei kuweka jingine mahali pa hilo. Tusiruhusu kamwe kutokamilika kokote tunakoona ndani yake kutukasirishe au kutusukume kuwa na mtazamo wenye kuchambua na wa kulalamika. Badala ya hivyo, acheni tuige uaminifu-mshikamanifu wa Yesu Kristo.—1 Petro 2:21.
Kutokamilika Kwetu Wenyewe
9, 10. (a) Mfumo wa mambo wa Shetani hutumiaje kwa faida yake kutokamilika kwetu ili kutushawishi tuingie katika mwenendo wa ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu? (b) Mtu ambaye amefanya dhambi nzito apaswa kufanya nini?
9 Shetani pia hujaribu kuendeleza ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu kwa kutumia kwa faida yake kutokamilika kwetu. Mfumo wake wa mambo hutumia udhaifu wetu mbalimbali kwa manufaa yake, ukitujaribu tufanye lililo kosa machoni pa Yehova. Kwa kusikitisha, kila mwaka maelfu ya watu wanashindwa na ukosefu wa maadili. Baadhi yao huongezea ukosefu huo wa uaminifu-mshikamanifu kwa kuwa na maisha maradufu, wakiendelea katika mwendo wa ukosaji huku wakijifanya kubaki wakiwa Wakristo waaminifu. Akiitikia makala juu ya habari hii katika ule mfululizo wa “Vijana Huuliza . . . ” katika gazeti Amkeni!, mwanamke mmoja kijana aliandika hivi: “Hizo makala zilikuwa simulizi la maisha yangu.” Sirini, alikuwa amekuza urafiki mbalimbali na vijana ambao hawakumpenda Yehova. Tokeo lilikuwa nini? Yeye aandika hivi: “Maisha yangu yalitumbukia shimoni, nikahusika katika ukosefu wa adili na kulazimika kukaripiwa. Uhusiano wangu na Yehova uliharibika, nikapoteza itibari ya wazazi wangu na ya wazee.”b
10 Mwanamke huyo kijana alipata msaada kutoka kwa wazee, akarudia utumishi wenye uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova. Hata hivyo, kwa kuhuzunisha wengi hupatwa na matokeo mabaya zaidi, na wengine hawarudi kamwe zizini. Ni afadhali kama nini kuwa mwenye uaminifu-mshikamanifu na kukinza kishawishi katika ulimwengu huu mwovu! Tii maonyo kutoka katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na la Amkeni! juu ya mambo kama vile mashirika ya kilimwengu na vitumbuizo vyenye kushusha heshima. Na usitumbukie kamwe katika mwenendo wa ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu. Lakini ukifanya hivyo, usiwe kamwe mnafiki. (Zaburi 26:4) Badala ya hivyo, pata msaada. Hilo ndilo kusudi la wazazi na wazee Wakristo.—Yakobo 5:14.
11. Kwa nini lingekuwa kosa kujiona kuwa wabaya hivi kwamba hatuna tumaini, na ni kielelezo gani cha Biblia kiwezacho kutusaidia kusahihisha maoni yetu?
11 Kutokamilika kwetu kwaweza kutuhatarisha katika njia nyingine. Baadhi ya watu wanaofanya tendo la ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu huacha kujaribu kumpendeza Yehova. Kumbuka kwamba, Daudi alitenda dhambi nzito sana. Hata hivyo, muda mrefu baada ya kifo cha Daudi, Yehova alimkumbuka kama mtumishi mwaminifu. (Waebrania 11:32; 12:1) Kwa nini? Kwa sababu hakuacha kamwe kujaribu kumpendeza Yehova. Andiko la Mithali 24:16 lasema hivi: “Mwenye haki huanguka mara saba akaondoka tena.” Kwa hakika, tukiingia katika dhambi ndogondogo—ndiyo kwa kurudia-rudia—kwa sababu ya udhaifu fulani tunaopigana nao, huenda bado tukawa waadilifu machoni pa Yehova tukiendelea “kuondoka”—yaani, kutubu kwa moyo mweupe na kurudia mwendo wa utumishi wenye uaminifu-mshikamanifu.—Linganisha 2 Wakorintho 2:7.
Jihadhari na Njia Zenye Hila za Ukosefu wa Uaminifu-Mshikamanifu!
12. Katika kisa cha Mafarisayo, mtazamo mgumu wa kushika sheria uliongozaje kwenye ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu?
12 Ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu pia hutokea katika njia zenye hila zaidi. Huenda huo hata ukajifanya kuwa uaminifu-mshikamanifu! Kwa kielelezo, labda Mafarisayo wa siku ya Yesu walijifikiria kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu kwa njia kuu.c Lakini walikosa kuona tofauti kati ya kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu na kuwa washikao sheria zilizotengenezwa na watu, wasiopindika, kwa kuwa walikuwa wagumu na wenye kuhukumu kwa ukali. (Linganisha Mhubiri 7:16.) Katika njia hiyo kwa kweli walikosa uaminifu-mshikamanifu—kwa watu waliopaswa kuwa wakiwatumikia, kwa kusudi halisi la Sheria waliyodai kuifundisha, na kwa Yehova mwenyewe. Tofauti nao, Yesu alikuwa mwenye uaminifu-mshikamanifu, kwa kusudi halisi la Sheria, iliyotegemea upendo. Hivyo alijenga na kutia watu moyo, kama tu vile unabii mbalimbali wa Kimesiya ulivyokuwa umetabiri.—Isaya 42:3; 50:4; 61:1, 2.
13. (a) Wazazi Wakristo waweza kukosaje kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu? (b) Kwa nini wazazi waepuke kuwa wakali, wenye kutafuta makosa, au wenye kuchambua kupita kiasi wanapowatia nidhamu watoto wao?
13 Wakristo wenye kiasi fulani cha mamlaka hunufaika sana kutokana na kigezo cha Yesu katika habari hii. Kwa kielelezo, wazazi wenye uaminifu-mshikamanifu wanajua kwamba lazima wawatie watoto wao nidhamu. (Mithali 13:24) Hata hivyo, wanahakikisha kwamba hawawachochei watoto wao kukasirika kwa nidhamu kali inayotolewa kwa hasira au kwa mfululizo wa uchambuzi wa daima. Watoto wahisio kwamba hawawezi kamwe kuwapendeza wazazi wao au wahisio kwamba ibada ya wazazi wao yaonekana tu kuwafanya wazazi waonekane kuwa wenye kutafuta makosa na kuwa wenye kuchambua waweza kuvunjika moyo na, ikisababisha wajitenge na imani ya kweli.—Wakolosai 3:21.
14. Wachungaji Wakristo waweza kuthibitikaje kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu kwa kundi wanalotumikia?
14 Vivyo hivyo, wazee Wakristo na waangalizi wasafirio hukazia uangalifu matatizo na hatari ambazo kundi hukabili. Wakiwa wachungaji wenye uaminifu-mshikamanifu, wao hutoa shauri linapohitajiwa, wakihakikisha kwamba wana mambo yote ya hakika kwanza na kutegemeza wasemayo kwa Biblia na vichapo vya Sosaiti. (Zaburi 119:105; Mithali 18:13) Pia, wanajua kwamba kondoo wanawategemea ili kujengwa na kulishwa kiroho. Kwa hiyo wao hujitahidi kumwiga Yesu Kristo, Mchungaji Mwema. Wao hutumikia kondoo kwa uaminifu-mshikamanifu juma kwa juma katika mikutano ya Kikristo—si kwa kuwaonyesha udhaifu wao, badala ya hivyo, kwa kuwajenga na kutia nguvu imani yao.—Mathayo 20:28; Waefeso 4:11, 12; Waebrania 13:20, 21.
15. Watu fulani katika karne ya kwanza walionyeshaje kwamba walikuwa na uaminifu-mshikamanifu mbalimbali usiofaa?
15 Njia nyingine yenye hila ya ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu ni uaminifu-mshikamanifu usiostahili. Uaminifu-mshikamanifu wa kweli katika maana ya Kibiblia hauturuhusu kuweka uaminifu wetu wa kiraia mbele ya uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova Mungu. Wayahudi wengi katika karne ya kwanza walishikamana kwa ushupavu na Sheria ya Kimusa na mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Hata hivyo, wakati wa Yehova ulikuwa umefika ili aondoe baraka zake kutoka katika taifa hilo lenye kuasi na kuzielekeza kwa taifa la Israeli la kiroho. Kwa kulinganishwa ni wachache tu waliokuwa wenye uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova na ambao walikubali badiliko hilo lenye maana sana. Hata miongoni mwa Wakristo wa kweli, baadhi ya wale Wageuzao watu wafuate dini ya Kiyahudi walisisitiza kuyarudia yale “mambo ya msingi yaliyo dhaifu na yasiyo na maana” ya Sheria ya Musa, ambayo ilikuwa imetimizwa katika Kristo.—Wagalatia 4:9; 5:6-12; Wafilipi 3:2, 3.
16. Watumishi wa Yehova wenye uaminifu-mshikamanifu huitikiaje marekebisho?
16 Kwa kutofautisha, watu wa Yehova katika nyakati za kisasa wamejithibitisha kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu katika nyakati zenye mabadiliko. Nuru ya kweli iliyofunuliwa iendeleapo kung’aa, marekebisho yanafanywa. (Mithali 4:18) Majuzi, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametusaidia kurekebisha uelewevu wetu juu ya neno “kizazi” linalotumiwa kwenye Mathayo 24:34 na juu ya wakati wa kuhukumiwa kwa “kondoo” na “mbuzi” wanaotajwa kwenye Mathayo 25:31-46, na pia juu ya maoni yetu kuelekea utumishi wa kiraia wa aina fulani-fulani. (Mathayo 24:45) Bila shaka waasi-imani fulani wangependezwa ikiwa Mashahidi wa Yehova wengi wangeshikilia sana uelewevu uliotangulia wa habari hizo na kukataa kufanya maendeleo. Hakujawa na itikio lolote la aina hiyo. Kwa nini? Watu wa Yehova ni wenye uaminifu-mshikamanifu.
17. Wapendwa waweza kutahinije uaminifu-mshikamanifu wetu nyakati nyingine?
17 Hata hivyo, habari ya uaminifu-mshikamanifu mbalimbali usiostahili yaweza kutuathiri sisi binafsi. Rafiki mpendwa au hata mshiriki wa familia achaguapo mwendo unaovunja kanuni za Biblia, huenda tukahisi kwamba twagawanyika kati ya uaminifu-mshikamanifu mbalimbali. Kiasili, twahisi tukiwa wenye uaminifu-mshikamanifu kwa washiriki wa familia. Lakini tusiweke kamwe wajibu wetu kwao mbele ya uaminifu-mshikamanifu wetu kwa Yehova! (Linganisha 1 Samweli 23:16-18.) Hatutawasaidia wakosaji kuficha dhambi yao nzito wala kujiunga nao dhidi ya wazee wanaojaribu ‘kuwarekebisha upya katika roho ya upole.’ (Wagalatia 6:1) Kufanya hivyo kungekuwa ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu kwa Yehova, kwa tengenezo lake, na kwa mpendwa. Kwa vyovyote, kumzuia mtenda-dhambi asipokee nidhamu anayohitaji ni, kwa hakika, kuzuia wonyesho wa upendo kutoka kwa Yehova usimfikie. (Waebrania 12:5-7) Pia, kumbuka kwamba “jeraha utiwazo na rafiki ni amini.” (Mithali 27:6) Shauri la wazi, lenye upendo linalotegemea Neno la Mungu laweza kujeruhi kiburi cha mpendwa mkosaji, lakini laweza kuthibitika kuwa lenye kuokoa uhai hatimaye!
Uaminifu-Mshikamanifu Husimama Imara Kujapokuwa Mnyanyaso
18, 19. (a) Ahabu alimtaka Nabothi afanye nini, na kwa nini Nabothi alikataa? (b) Je, uaminifu-mshikamanifu wa Nabothi ulistahili matokeo aliyopata? Fafanua.
18 Nyakati nyingine mashambulizi ya Shetani dhidi ya uaminifu-mshikamanifu wetu ni ya moja kwa moja. Fikiria kisa cha Nabothi. Mfalme Ahabu alipomsonga auze shamba lake la mizabibu, alijibu hivi: “BWANA apishe mbali nikupe wewe urithi wa baba zangu.” (1 Wafalme 21:3) Nabothi hakuwa mkaidi; alikuwa mwenye uaminifu-mshikamanifu. Sheria ya Kimusa iliamuru kwamba Mwisraeli yeyote asiuze mali ya urithi wa ardhi kwa umilele. (Mambo ya Walawi 25:23-28) Kwa hakika Nabothi alijua kwamba mfalme huyu mwovu angeweza kumfanya auawe, kwa kuwa Ahabu tayari alikuwa amemwachilia mke wake, Yezebeli, aue wengi wa manabii wa Yehova! Hata hivyo Nabothi alisimama imara.—1 Wafalme 18:4.
19 Nyakati nyingine uaminifu-mshikamanifu hutoza bei. Yezebeli, akisaidiwa na “watu wasiofaa,” walimsingizia Nabothi uhalifu ambao hakufanya. Tokeo ni kwamba, yeye na wana wake waliuawa. (1 Wafalme 21:7-16; 2 Wafalme 9:26) Je, hilo lamaanisha kwamba uaminifu-mshikamanifu wa Nabothi ulikuwa wenye kosa? La! Nabothi yumo miongoni mwa wanaume na wanawake wengi wenye uaminifu-mshikamanifu walio ‘hai’ katika kumbukumbu la Yehova sasa hivi, wakiwa wamelala salama kaburini hadi wakati wa ufufuo.—Luka 20:38; Matendo 24:15.
20. Tumaini laweza kutusaidiaje kudumisha uaminifu-mshikamanifu wetu?
20 Ahadi hiyohiyo ya ufufuo huwapa uhakikisho watu wa Yehova wenye uaminifu-mshikamanifu leo. Twajua kwamba uaminifu-mshikamanifu wetu waweza kutugharimu sana katika ulimwengu huu. Yesu Kristo alilipia uaminifu-mshikamanifu wake kwa uhai wake, naye aliwaambia wafuasi wake kwamba wangetendewa vivyo hivyo. (Yohana 15:20) Jinsi tumaini lake la wakati ujao lilivyomtegemeza, ndivyo tumaini letu linavyotutegemeza. (Waebrania 12:2) Hivyo, twaweza kuendelea kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu tukabilipo aina zote za mnyanyaso.
21. Yehova awatolea watu wake wenye uaminifu-mshikamanifu uhakikishio gani mbalimbali?
21 Ni kweli kwamba, kwa kulinganishwa ni wachache kati yetu leo wanaopatwa na mashambulio ya moja kwa moja dhidi ya uaminifu-mshikamanifu wetu. Lakini huenda watu wa Mungu wakakabili mnyanyaso zaidi kabla ya ule mwisho kuja. Twaweza kuhakikishaje kwamba twadumisha uaminifu-mshikamanifu wetu? Kwa kuwa wenye uaminifu-mshikamanifu sasa. Yehova ametupatia utume mkubwa—kuhubiri na kufundisha juu ya Ufalme wake. Acheni tuendelee kufanya kazi hiyo muhimu kwa uaminifu-mshikamanifu. (1 Wakorintho 15:58) Tusipokubali kutokamilika kwa kibinadamu kumomonyoe uaminifu-mshikamanifu wetu kwa tengenezo la Yehova na tukijilinda dhidi ya njia zenye hila za ukosefu wa uaminifu-mshikamanifu kama vile uaminifu-mshikamanifu usiofaa, basi tutakuwa tumetayarishwa vizuri zaidi ikiwa uaminifu-mshikamanifu wetu utajaribiwa vikali zaidi. Kwa vyovyote, sikuzote twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova ni mwenye uaminifu-mshikamanifu daima kwa watumishi wake wenye uaminifu-mshikamanifu. (2 Samweli 22:26) Ndiyo, atawalinda watu wake wenye uaminifu-mshikamanifu!—Zaburi 97:10.
[Maelezo ya chinis]
a Yesu alikuwa mwenye moyo mkuu katika kushambulia biashara ya fedha yenye faida kama hiyo. Kulingana na mwanahistoria mmoja, ilikuwa lazima kodi ya hekalu ilipwe kwa sarafu hususa ya kale ya Kiyahudi. Hivyo watu wengi waliolizuru hekalu walilazimika kubadili fedha zao ili walipe hiyo kodi. Wabadili-fedha waliruhusiwa walipize ada iliyowekwa kwa ajili ya kubadili, nao walipata fedha nyingi.
b Ona Amkeni! la Desemba 22, 1993; Januari 8, 1994; na Januari 22, 1994.
c Kikundi chao kilitokana na Wahasidimu, kikundi kilichotokea karne kadhaa mapema ili kushindana na uvutano wa Kigiriki. Wahasidimu walitwaa jina lao kutokana na neno la Kiebrania chasi·dhimʹ, linalomaanisha “wenye uaminifu-mshikamanifu” au “wachaji.” Labda walihisi kwamba maandiko yanayotaja “wenye uaminifu-mshikamanifu” wa Yehova yaliwahusu kwa njia fulani ya pekee. (Zaburi 50:5, NW) Wao, pamoja na Mafarisayo wa baada yao, walikuwa washupavu, walindaji wa herufi ya Sheria waliojiweka wenyewe rasmi.
Ungejibuje?
◻ Twaweza kuepukaje kuruhusu kutokamilika kwa wengine kutufanye tukose uaminifu-mshikamanifu?
◻ Kutokamilika kwetu wenyewe kwaweza kutufanya tukose uaminifu-mshikamanifu katika njia zipi?
◻ Twaweza kukinzaje mwelekeo wa kuwa na uaminifu-mshikamanifu mbalimbali usiofaa?
◻ Ni jambo gani litakalotusaidia kudumisha uaminifu-mshikamanifu wetu hata katika nyakati za mnyanyaso?
[Sanduku katika ukurasa wa 9]
Kutumikia kwa Uaminifu-Mshikamanifu Katika Betheli
“Acheni mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” Ndivyo alivyoandika mtume Paulo. (1 Wakorintho 14:40) Paulo alijua kwamba ili kutaniko litende, kungekuwa na uhitaji wa “mpango,” wa utaratibu. Hali kadhalika leo, lazima wazee wafanye maamuzi juu ya mambo yenye kutumika, kama vile kuwapa washiriki wa kutaniko migawo ya kwenda kwenye mafunzo ya kitabu mahali mbalimbali, kupanga mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani, na kuchunguza kuhubiriwa kwa maeneo. Nyakati nyingine huenda mipango hiyo ikatokeza mitihani ya uaminifu-mshikamanifu. Mipango hiyo si amri zenye kupuliziwa kimungu, nayo haiwezi kupata kibali cha kila mtu mmoja-mmoja.
Je, nyakati nyingine, waona ugumu wa kuwa mwenye uaminifu-mshikamanifu kwa baadhi ya mipango yenye kutumika inayofanywa katika kutaniko la Kikristo? Ikiwa ndivyo, huenda ukaona kielelezo cha Betheli kuwa chenye kusaidia. Zile ofisi zote za tawi 104 za Watch Tower Society kutia na makao makuu ya Marekani,* zinaitwa Betheli, neno la Kiebrania linalomaanisha “Nyumba ya Mungu.” Wajitoleaji wanaoishi na kufanya kazi kwenye majengo ya Betheli wanataka mahali hapo padhihirishe staha na kicho kwa Yehova. Hilo hutaka kila mmoja awe mwenye uaminifu-mshikamanifu.
Mara nyingi, wenye kuzuru Betheli husema juu ya utaratibu na usafi waonao huko. Wafanyakazi ni wenye utaratibu na wenye furaha; usemi wao na adabu zao na hata kuonekana kwao kwadhihirisha dhamiri komavu za Kikristo, ambazo zimezoezwa na Biblia. Washiriki wote wa familia ya Betheli hushikamana kwa uaminifu-mshikamanifu na viwango vya Neno la Mungu.
Kwa kuongezea, Baraza Linaloongoza huwaandalia kijitabu cha maagizo kiitwacho Dwelling Together in Unity, ambacho hutaja kwa fadhili mipango fulani yenye kutumika inayohitajiwa kwa ajili ya familia kubwa kama hiyo ili wafanye kazi vizuri pamoja. (Zaburi 133:1) Mathalani, kinashughulikia vyumba, milo, usafi wa kiafya, mavazi na mapambo, na mambo kama hayo. Washiriki wa familia ya Betheli hutegemeza na kushikamana na mipango hiyo kwa uaminifu-mshikamanifu, hata wakati ambapo labda mapendezi ya kibinafsi yatawaongoza kuelekea upande mwingine. Wanakiona kijitabu hicho cha maagizo kuwa miongozo yenye mafaa inayokusudiwa kuendeleza muungano na upatano, wala si sheria na kanuni ngumu. Waangalizi ni wenye uaminifu-mshikamanifu katika kutegemeza utaratibu huo mbalimbali wenye msingi katika Biblia, nao huutumia katika njia chanya ili kujenga na kutia moyo washiriki wa familia ya Betheli kufuatia utumishi wao mtakatifu wa Betheli.
*Majengo hayo ya kiwanda, ofisi, na makao si hekalu kubwa la kiroho la Mungu, au nyumba yake. Hekalu la kiroho la Mungu ni mpango wake wa ibada safi. (Mika 4:1) Kwa hiyo, si jengo halisi lililo duniani.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Mtu Mwenye Uaminifu-Mshikamanifu na Mshika-Sheria
Nyuma huko katika mwaka wa 1916 kichapo Encyclopædia of Religion and Ethics kilisema kwamba “tofauti hii kati ya mtu mwenye uaminifu-mshikamanifu na mshika-sheria yaweza kupatikana nyakati zote na kila mahali.” Kilieleza hivi: “Kuna mshika-sheria anayefanya aambiwalo, havunji sheria zozote; hushikamana na neno lililoandikwa na liwezalo kusomwa. Kuna mtu mwenye uaminifu-mshikamanifu ambaye hufanya hilo lakini awezaye . . . kutegemewa kwa mengi zaidi, anayeweka akili yake yote katika wajibu wake, anayepatanisha mtazamo wake kulingana na maana halisi ya kusudi linalotumikiwa.” Baadaye, kichapo hichohicho kilionelea hivi: “Kuwa mwenye uaminifu-mshikamanifu kwamaanisha zaidi ya kuwa mwenye kutii sheria. . . . Mtu mwenye uaminifu-mshikamanifu tofauti na mtu mwenye kutii sheria, hutumikia kwa moyo wote na akili yote . . . Hajiruhusu kufanya kimakusudi dhambi ya kutenda, ya kutotenda, au ya kutojua.”