UPOLE
Kitabu A New Testament Wordbook, cha William Barclay, kinasema hivi kuhusu kivumishi pra·ysʹ: “Katika Kigiriki cha kale, neno hilo linapendeza sana. Kuhusu vitu linamaanisha ‘wororo.’ Kwa mfano, linaweza kutumiwa kurejelea upepo mwanana au sauti tulivu. Kuhusu watu linamaanisha ‘mpole’ au ‘mwenye neema’. . . . Neno praus linatia ndani wororo lakini wororo wenye nguvu za chuma . . . Si wororo usio thabiti, au hisia za upendo zisizo na msingi wowote, au kukaa kimya tu.” (London, 1956, uku. 103, 104) Kamusi ya Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words inasema nomino pra·yʹtes “haionyeshwi na ‘tabia ya nje tu ya mtu; wala na uhusiano wake na wengine; haihusiani na mtazamo wake wa asili. Badala yake ni neema inayotoka ndani ya nafsi; na inaonyeshwa kwanza hasa kumwelekea Mungu. Ni mtazamo unatufanya tukubali kwamba anashughulika nasi vizuri, na hivyo hatubishani naye wala kumpinga; inahusiana kwa ukaribu na neno tapeinophrosunē [unyenyekevu], na inategemea kabisa sifa hiyo.’”—1981, Buku la 3, uku. 55, 56.
Katika tafsiri mbalimbali za Biblia neno pra·ysʹ limetafsiriwa kuwa “upole,” “tabia-pole,” “uanana,” na “wororo.” (KJ, AS, NW, NE) Hata hivyo, kulingana na maelezo ya Barclay yaliyotajwa awali, neno pra·ysʹ lina uzito kuliko wororo na, linapotumiwa kuhusu watu, linamaanisha upole, neema.
Ingawa Yehova havumilii dhambi na uovu, kwa upendo ameandaa njia ya kumfikia kupitia dhabihu ya fidia na huduma za kikuhani za Yesu Kristo. Kwa hiyo, waabudu wa Yehova na watumishi wake wanaweza kumkaribia bila woga. (Ebr 4:16; 10:19-22; 1Yo 4:17, 18) Yesu alimwakilisha Yehova Mungu kikamili sana hivi kwamba alisema: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” Alisema hivi pia: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole [Kigr., pra·ysʹ] na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu. Kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Yoh 14:9; Mt 11:28-30) Hivyo, Yehova Mungu anaweza kufikiwa na wote wanaompenda, naye huwasaidia kuwa na upole, uhakika mkubwa, na nguvu kwa wale anaowapenda.
Sifa Yenye Nguvu. Upole au roho ya upole si sifa ya watu walio dhaifu. Yesu Kristo alisema: “Mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni.” (Mt 11:29; 2Ko 10:1) Hata hivyo, Yesu alikuwa na nguvu nyingi sana kutoka kwa Baba yake, naye alitetea ukweli kwa uthabiti; alitenda na kuzungumza kwa uhuru mkubwa alipolazimika kufanya hivyo.—Mt 23:13-39; linganisha na 21:5.
Mtu huwa mpole kwa sababu ana imani na ana nguvu. Si rahisi kwake kupoteza usawaziko au busara. Ukosefu wa upole husababishwa na kutojiamini, kuvunjika moyo, kukosa imani na tumaini, au hata kukata tamaa. Methali inamfafanua hivi mtu ambaye si mpole: “Kama jiji lililobomolewa, lisilo na ukuta, ndivyo alivyo mtu asiyeweza kuidhibiti hasira yake.” (Met 25:28) Yuko wazi na hana ulinzi dhidi ya mawazo yoyote yasiyofaa, ambayo yanaweza kumfanya atende mambo yasiyofaa.
Sifa ya Tunda la Roho. Upole ni tunda la roho takatifu ya Mungu, nguvu zake za utendaji. (Gal 5:22, 23) Kwa hiyo, Mungu ndiye Chanzo cha upole, na lazima mtu amwombe roho yake na kusitawisha sifa hiyo ya tunda la roho ili awe na upole wa kweli. Kwa hiyo, mtu hawezi kuipata kwa nguvu zake mwenyewe, anaweza kuipata kwa kumkaribia Mungu.
Ukosefu wa upole husababisha msisimko usiofaa, ukali, kutojizuia, na ugomvi. Badala yake, Mkristo anashauriwa adumishe umoja na amani kwa “unyenyekevu wote na upole.”—Efe 4:1-3.
Wivu na ugomvi ukiruhusiwa kutia mizizi na kukua, utatokeza vurugu za kila aina. Kwa upande mwingine, upole utazuia mambo hayo yasitokee kati ya wafuasi wa Kristo. Kwa hiyo, mwandishi wa Biblia Yakobo anawahimiza wenye hekima na uelewaji kutanikoni wawe na ‘mwenendo mzuri’ kwa kuonyesha “upole unaotokana na hekima,” “hekima inayotoka juu.”—Yak 3:13, 17.
Mara nyingi neno “upole” katika Biblia linatajwa pamoja na neno “roho,” kwa mfano, “upole wa roho” au “roho ya upole.” Kwa hiyo, upole wa kweli si sifa inayoonyeshwa tu kwa nje, kwa muda mfupi tu au nyakati fulani; badala yake ni sehemu ya utu au tabia ya mtu. Mtume Petro anazungumzia ukweli huo anaposema: “Kujipamba kwenu kusiwe kwa nje—kusuka nywele na kuvaa mapambo ya dhahabu au mavazi bora—bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika mapambo yasiyoharibika ya roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—1Pe 3:3, 4.
Mtume Paulo aliandika hivi: “Jivikeni . . . upole,” na mtu akisoma kijuu-juu anaweza kufikiri ni sifa ya nje tu; lakini katika muktadha huohuo anahimiza hivi: “Mjivike utu mpya, ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mpya kulingana na mfano wa Yule aliyeuumba.” (Kol 3:10, 12; Efe 4:22-24) Kwa kweli, hilo linaonyesha kwamba upole ni tabia ambayo mtu anapata hasa kwa kusitawisha tunda la roho ya Mungu kupitia ujuzi sahihi na kutumia ujuzi huo, wala si sifa ambayo anarithi kiasili.
Sifa Muhimu kwa Waangalizi. Paulo alipomwandikia kijana Timotheo barua yenye mwongozo kuhusu jinsi ya kulitunza kutaniko, alimwagiza hivi kuhusu kushughulikia hali ngumu: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, mwenye uwezo wa kufundisha, anayejizuia anapokosewa, akiwafundisha kwa upole wale wasio na mwelekeo unaofaa. Huenda Mungu akawasaidia kutubu.” (2Ti 2:24, 25) Tunaona uhusiano kati ya upole na subira katika andiko hilo. Mwangalizi anatambua kwa nini anahitaji kushughulikia hali hiyo ngumu: Mungu ameiruhusu, basi akiwa mwangalizi lazima aishughulikie kwa njia itakayomnufaisha mtu au watu wanaohusika. Lazima avumilie hali hiyo ngumu hadi itakaposuluhishwa, bila kuhangaika kupita kiasi.
Mwangalizi mwingine, Tito, aliyeishi Krete, aliagizwa pia awakumbushe ndugu zake Wakristo “wawe na usawaziko, wakionyesha upole wote kwa watu wote.” Ili kukazia umuhimu wa upole, Paulo alimkumbusha Tito upendo mkubwa na rehema za Mungu alizoonyesha kupitia Mwana wake, zinazomchochea Mkristo aache njia ya zamani yenye hila na chuki na kufuata njia mpya inayoongoza kwenye uzima wa milele.—Tit 3:1-7.
Paulo anawaambia hivi tena watu wakomavu kiroho kutanikoni, akiwakumbusha jukumu lao: “Hata mtu akichukua hatua isiyofaa kabla hajajua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo kwa roho ya upole. Lakini kila mmoja wenu aendelee kujiangalia, kwa kuwa ninyi pia mnaweza kujaribiwa.” (Gal 6:1) Wanapaswa kukumbuka jinsi ambavyo Mungu ameshughulika nao. Hivyo, hawatamkaripia kwa ukali mkosaji bali watajitahidi kumrekebisha kwa roho ya upole. Hilo litakuwa na matokeo mazuri sana kwa wote wanaohusika.
Upole husaidia kushughulika na hali ngumu au na mtu mwenye hasira, lakini ukali hufanya hali iwe mbaya zaidi. Methali moja inasema: “Jibu la upole hutuliza hasira, lakini neno kali huchochea hasira.” (Met 15:1) Upole unaweza kuwa na nguvu sana. “Kwa subira kamanda hushawishiwa, na ulimi laini unaweza kuvunja mfupa.”—Met 25:15.
Sifa Muhimu Tunapotiwa Nidhamu. Sulemani anataja kanuni nyingine inayohusiana na upole au utulivu. Inahusu mwelekeo tunaoweza kuwa nao wa kuasi tunaporekebishwa au tunapoadhibiwa na mtu mwenye mamlaka. Tunaweza kukasirika sana hivi kwamba tuache kujitiisha, na kuacha mara moja mgawo wetu. Lakini Sulemani anaonya hivi: “Hasira ya mtawala ikiwaka dhidi yako, usiondoke mahali pako, kwa maana utulivu huzuia dhambi kubwa.” (Mhu 10:4; linganisha na Tit 3:2.) Mtazamo mzuri wa utulivu na upole tunapotiwa nidhamu hutusaidia kuepuka hasira zaidi kutoka kwa mwenye mamlaka na pia kuboresha utu wetu kwa kudhibiti hasira yetu na kubaki mahali petu, au sehemu yetu, huku tukifuata ushauri tuliopewa.
Ni muhimu hasa kufanya hivyo ikiwa mtawala huyo ni Yehova Mungu na ikiwa nidhamu inatolewa na wale waliopewa mamlaka naye. (Ebr 12:7-11; 13:17) Hilo linahusu pia uhusiano wetu na wale ambao Mungu amewaruhusu wawe na mamlaka ya kutawala katika ulimwengu. (Ro 13:1-7) Hata mtawala huyo akimwamuru vikali Mkristo aeleze sababu ya tumaini alilo nalo, Mkristo anapaswa kujibu “kwa upole na heshima kubwa,” huku akitanguliza kwa uthabiti utii wake kwa Mungu.—1Pe 3:15.