Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 10/15 kur. 10-14
  • Wenye Hali Pole Ni Wenye Furaha Kama Nini!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wenye Hali Pole Ni Wenye Furaha Kama Nini!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuchunguza Upole kwa Ukaribu Zaidi
  • Jinsi ya Kusitawisha Upole
  • Faida za Upole
  • Upole Hukuza Furaha
  • Upole​—Unatunufaishaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
  • Jivikeni Upole!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Upole
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Upole Ni Sifa Muhimu Sana ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 10/15 kur. 10-14

Wenye Hali Pole Ni Wenye Furaha Kama Nini!

“Wenye furaha ni wenye hali pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.”—MATHAYO 5:5, NW

1. Ni nini ile hali pole ambayo Yesu alisema juu yayo katika mahubiri yake juu ya mlima?

KATIKA mahubiri yake juu ya mlima, Yesu Kristo alisema hivi: “Wenye furaha ni wenye hali pole, kwa kuwa wao watairithi dunia.” (Mathayo 5:5, NW) Hali hiyo pole, au usikivu, si wonyesho wa juujuu tu wa uanana wa kinafiki, wala si tabia ya kiutu ya kiasili tu. Bali, ni upole wa kweli wa kindani na hali ya kutaka amani inayozoewa hasa katika kuitikia mapenzi na mwongozo wa Yehova Mungu. Watu wenye hali pole kweli kweli huonyesha kwamba wao hupendelea sana kumtegemea Mungu ambako huonyeshwa katika mwenendo wao mpole kuelekea wanadamu wenzao.—Warumi 12:17-19; Tito 3:1, 2.

2. Kwa nini Yesu aliwatangaza wenye hali pole kuwa wenye furaha?

2 Yesu aliwatangaza wale wenye hali pole kuwa wenye furaha kwa sababu watairithi dunia. Akiwa Mwana wa Mungu, mwenye hali pole kikamilifu, Yesu ndiye Mrithi Mkuu wa dunia. (Zaburi 2:8; Mathayo 11:29; Waebrania 1:1, 2; 2:5-9) Lakini akiwa “mwana wa mwanadamu” wa Kimesiya, alipaswa kuwa na watawala washiriki katika Ufalme wake wa kimbingu. (Danieli 7:13, 14, 22, 27, NW) Wakiwa “warithio pamoja” na Kristo, hao wapakwa-mafuta wenye hali pole watashiriki katika urithi wake wa dunia. (Warumi 8:17) Watu wengine wenye hali pole, wenye mfano wa kondoo watafurahia uhai wa milele katika Paradiso katika makao ya kidunia ya Ufalme. (Mathayo 25:33, 34, 46; Luka 23:43) Tazamio hilo huwafanya wawe wenye furaha kweli kweli.

3. Mungu na Kristo waliweka mfano gani kuhusu upole?

3 Mrithi Mkuu mwenye hali pole apokea dunia kutoka kwa Baba yake, Yehova, aliye mfano mkuu wa hali ya upole. Maandiko husema mara nyingi kama nini kwamba Mungu ‘ni wa polepole kukasirika na mwingi katika fadhili-upendo’! (Kutoka 34:6, NW; Nehemia 9:17; Zaburi 86:15) Yeye ana uweza mwingi lakini huonyesha upole mwingi hivi kwamba waabudu wake waweza kumkaribia bila kuogopa. (Waebrania 4:16; 10:19-22) Mwana wa Mungu, aliyekuwa “mpole na mnyenyekevu wa moyo,” aliwafundisha wafuasi wake kuwa wapole. (Mathayo 11:29; Luka 6:27-29) Watumwa hao wa Mungu na wa Mwana wake wenye hali pole, nao, wakaiga na kuandika kuhusu “upole na utaratibu [fadhili, NW] wa Kristo.”—2 Wakorintho 10:1; Warumi 1:1; Yakobo 1:1, 2; 2 Petro 1:1.

4. (a) Kulingana na Wakolosai 3:12, nini kimefanywa na wale ambao kwa kweli ni wenye hali pole? (b) Ni maswali gani yanayostahili ufikirio wetu?

4 Leo, Wakristo wapakwa-mafuta na waandamani wao wa kidunia pia huhitaji kuwa wenye hali pole. Wakiwa wameondolea mbali ubaya, udanganyifu, unafiki, kijicho, na kusengenya kokote, wamesaidiwa na roho takatifu ya Mungu kuwa wapya katika ‘nguvu yenye kutendesha akili zao.’ (Waefeso 4:22-24, NW; 1 Petro 2:1, 2) Wanahimizwa wajivike “moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.” (Wakolosai 3:12) Lakini upole unatia ndani nini hasa? Kwa nini kuna manufaa kuwa mwenye hali pole? Na sifa hiyo yaweza kuchangiaje furaha yetu?

Kuchunguza Upole kwa Ukaribu Zaidi

5. Upole unaweza kuelezwaje?

5 Mtu mwenye hali pole huwa na mwelekeo na tabia ya uanana. Katika tafsiri nyinginezo za Biblia, ni kile kivumishi (adjective) pra·ysʹ kinachotafsiriwa “-sikivu,” “-pole,” “hali pole,” na “-anana.” Katika Kigiriki cha zamani, kile kivumishi pra·ysʹ chaweza kutumiwa kwa upepo au sauti ya uanana. Chaweza pia kutumiwa kwa mtu mwenye neema. Mwanachuo W. E. Vine asema hivi: “Matumizi ya [nomino pra·yʹtes] ni kumwelekea Mungu kwanza na hasa yeye. Ni ile hali ya roho ambayo katika hiyo tunakubali kwamba shughuli Zake pamoja na sisi ni njema, na kwa hiyo bila kubisha au kupinga; inahusiana kwa ukaribu sana na neno tapeinophrosuné [unyenyekevu].”

6. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba upole si udhaifu?

6 Upole si udhaifu. “Kuna uanana katika praus,” kaandika mwanachuo William Barclay, “lakini nyuma ya uanana huo kuna nguvu kama ya chuma.” Nguvu huhitajiwa ili kuwa mwenye hali pole. Kwa mfano, nguvu huhitajiwa ili tuwe wapole tunapokasirishwa au tunaponyanyaswa. Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, mwenye hali pole, aliweka mfano mzuri katika jambo hilo. “Alipotukanwa, hakurudisha matukano; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye [Yehova Mungu] ahukumuye kwa haki.” (1 Petro 2:23) Kama Yesu mwenye hali pole, twaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atashughulika na watukani au wanyanyasi wetu. (1 Wakorintho 4:12, 13) Twaweza kuwa watulivu, kama alivyokuwa Stefano mwenye kunyanyaswa, tukitambua kwamba tukiwa waaminifu, Yehova atatutegemeza naye hatakubali jambo lolote lituletee madhara ya kudumu.—Zaburi 145:14; Matendo 6:15; Wafilipi 4:6, 7, 13.

7. Mithali 25:28 inaonyesha nini kuhusu mtu anayekosa upole?

7 Yesu alikuwa mwenye hali pole, hata hivyo alionyesha nguvu katika kusimama imara kwa ajili ya mema. (Mathayo 21:5; 23:13-39) Yeyote aliye na “akili ya Kristo” atakuwa kama yeye katika jambo hilo. (1 Wakorintho 2:16, NW) Ikiwa mtu si mpole, yeye si kama Kristo. Bali, maneno haya yamfaa: “Asiyetawala roho yake ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.” (Mithali 25:28) Mtu kama huyo anayekosa upole aweza kwa urahisi kuingiwa na fikira mbaya ambazo zingeweza kumfanya atende kwa njia zisizofaa. Ingawa Mkristo mwenye hali pole si dhaifu, bado ajua kwamba “jawabu la upole hugeuza hasira; bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.”—Mithali 15:1.

8. Kwa nini si rahisi kuwa mwenye hali pole?

8 Si rahisi kuwa mwenye hali pole, kwa kuwa tumerithi kutokamilika na dhambi. (Warumi 5:12) Ikiwa sisi ni watumishi wa Yehova, tuna vita pia dhidi ya majeshi ya roho waovu ambayo huenda yakajaribu upole wetu kwa mnyanyaso. (Waefeso 6:12) Na wengi wetu hufanya kazi miongoni mwa wale wenye roho kali bila huruma ya ulimwengu ulio chini ya mwongozo wa Ibilisi. (1 Yohana 5:19) Kwa hiyo twaweza kusitawishaje upole?

Jinsi ya Kusitawisha Upole

9. Ni maoni gani yawezayo kutusaidia kusitawisha upole?

9 Usadikisho wenye msingi wa Biblia kwamba tunatakiwa tuonyeshe upole utatusaidia tusitawishe sifa hiyo. Ni lazima kila siku tujitahidi kusitawisha upole. Kama sivyo, tutakuwa kama watu waonao upole kuwa udhaifu na kufikiri kwamba mafanikio hutokana na kuwa wenye ufidhuli, wagumu, hata wakatili. Kwa vyovyote, Neno la Mungu hulaumu kiburi, na mithali yenye hekima husema hivi: “Mwenye rehema huitendea mema nafsi yake; aliye mkali hujisumbua mwili wake.” (Mithali 11:17; 16:18) Watu huepuka mtu mkali bila huruma asiye na fadhili, hata ikiwa wao hufanya hivyo ili hasa kuepuka kuumizwa na ukatili wake na ukosefu wake wa upole.

10. Ikiwa tutakuwa wenye hali pole, ni lazima tujitiishe kwenye nini?

10 Ili tuwe wenye hali pole, ni lazima tujitiishe kwa uvutano wa roho takatifu au nguvu za utendaji za Mungu. Kama vile Yehova alivyowezesha dunia itokeze mazao, kwa jinsi hiyo hiyo yeye huwezesha watumishi wake watokeze matunda ya roho yake, kutia na upole. Paulo aliandika hivi: “Tunda la Roho ni upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti. Dhidi ya mambo hayo hakuna sheria.” (Wagalatia 5:22, 23, NW) Naam, upole ni mojawapo ya matunda ya roho ya Mungu yanayoonyeshwa na wale wanaompendeza. (Zaburi 51:9, 10) Na upole hutokeza mabadiliko yaliyoje! Kutoa kielezi: Kulikuwako mkora mmoja aitwaye Tony ambaye alipigana, akaibia watu, akaingiza nchini dawa za kulevya kisiri, akaongoza genge la waendeshaji pikipiki, na kupisha wakati fulani gerezani. Hata hivyo, kwa kutwaa maarifa sahihi ya Biblia kwa na msaada wa roho ya Mungu, alibadilika akawa mtumishi wa Yehova mwenye tabia ya upole. Hadithi ya Tony si jambo lisilo la kawaida. Basi, mtu aweza kufanya nini ikiwa ukosefu wa upole umekuwa sehemu kubwa ya utu wake?

11. Sala ina sehemu gani katika kusitawisha upole?

11 Sala ya kutoka moyoni ili kupata roho ya Mungu na kupata tunda layo la upole itatusaidia tusitawishe sifa hiyo. Huenda tukahitaji ‘kuendelea kuomba,’ kama alivyosema Yesu, na Yehova Mungu atatupa tuombacho. Baada ya kueleza kwamba baba za kibinadamu huwapa watoto wao vitu vizuri, Yesu alisema hivi: “Ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu [roho takatifu, NW] hao wamwombao?” (Luka 11:9-13) Sala yaweza kusaidia kufanya upole uwe sehemu ya kudumu ya utu wetu—sifa inayochangia furaha yetu na ile ya washirika wetu.

12. Kwa nini kukumbuka kwamba wanadamu si wakamilifu kutatusaidia tuwe wenye hali pole?

12 Kukumbuka kwamba wanadamu si wakamilifu kwaweza kutusaidia tuwe wenye hali pole. (Zaburi 51:5) Hatuwezi kufikiri au kutenda kikamilifu, hata jinsi watu wengine wasivyoweza kufanya, kwa hiyo twapaswa kwa hakika kuwa na hisiamwenzi na kuwatendea wengine jinsi ambavyo tungependa kutendewa. (Mathayo 7:12) Kutambua kwa-mba sisi sote hufanya makosa kwapasa kutufanya tuwe wenye kusamehe na wenye hali pole katika kushughulika na wengine. (Mathayo 6:12-15; 18:21, 22) Kwa vyovyote vile, je, sisi hatushukuru kwamba Mungu huonyesha upendo na upole kwetu?—Zaburi 103:10-14.

13. Tunaweza kusaidiwaje kusitawisha upole tukikiri kwamba Mungu ameumba wanadamu wawe viumbe wenye hiari ya kuchagua?

13 Kukiri kwamba Mungu ameumba wanadamu wawe viumbe wenye hiari ya kuchagua kwaweza pia kutusaidia kusitawisha upole. Hiyo haimruhusu mtu yeyote kupuuza sheria za Yehova bila kuadhibiwa, lakini inaruhusu kuwe na hali mbalimbali katika ladha za kuchagua mambo, yaliyo mapendezi na yasiyo mapendezi miongoni mwa watu wake. Kwa hiyo acheni tukubali kwamba hakuna yeyote anayelazimishwa kufuata utu fulani wa kipekee ambao huenda tukauona kuwa ndio bora kabisa. Roho kama hiyo itaweza kutusaidia tuwe wenye hali pole.

14. Nini lapasa kuwa azimio letu, kuhusu upole?

14 Kuazimia kutoacha upole kutatusaidia kuendelea kusitawisha sifa hiyo. Kujitiisha kwa uvutano wa roho ya Yehova kulibadili kufikiri kwetu. (Warumi 12:2) Roho ya upole kama ya Kristo hutusaidia sasa ili tujizuie tusishughulike na matendo ya “ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali.” Ni lazima tusiache kamwe upole kwa sababu za kifedha, kijamii au nyinginezo au kwa sababu watu hututukana kuhusu kumhofu Mungu kwetu. (1 Petro 4:3-5) Ni lazima tusiruhusu jambo lolote litufanye tushughulike na “matendo ya mwili,” hivi kwamba tupoteze upole wetu na kushindwa kuurithi Ufalme wa Mungu au kufurahia mibaraka yao. (Wagalatia 5:19-21) Acheni tuthamini sikuzote pendeleo la kuwa wapole wa Mungu, tuwe ni wapakwa-mafuta kwa uhai mbinguni au tuwe ni wenye tumaini la kidunia. Kwa mradi huo, acheni tuzungumzie baadhi ya faida za upole.

Faida za Upole

15. Kulingana na Mithali 14:30, kwa nini ni jambo la hekima kuwa mpole?

15 Mtu mpole ana utulivu wa moyo, akili, na mwili. Hiyo ni kweli kwa sababu yeye hashughuliki na ugomvi, haudhiki na vitendo vya wengine, au hajitesi mwenyewe na wasiwasi mwingi mno. Upole humsaidia adhibiti maoni yake ya moyoni, na hilo lina manufaa ya kiakili na ya kimwili. Mithali moja husema hivi: “Moyo ulio mzima ni uhai wa mwili; bali husuda ni ubovu wa mifupa.” (Mithali 14:30) Ukosefu wa upole huenda ukaongoza kwenye hasira ambayo yaweza kuongeza msukumo wa damu au kusababisha matatizo ya msago wa chakula tumboni, ugonjwa wa pumu, taabu ya macho, na matatizo mengine. Mkristo mwenye hali pole hufurahia faida mbalimbali, kutia na “amani ya Mungu” inayolinda moyo na nguvu zake za akili. (Wafilipi 4:6, 7) Ni jambo la hekima kama nini kuwa mwenye hali pole!

16-18. Upole una tokeo gani juu ya uhusiano wetu na wengine?

16 Sifa ya upole hufanyia maendeleo uhusiano wetu na wengine. Labda wakati mmoja tulikuwa na tabia ya kushurutisha mambo sana mpaka tukapata tulichotaka. Huenda ikawa watu walikasirika kwa sababu yetu kwa kuwa tulikosa unyenyekevu na upole. Chini ya hali kama hizo, isingalipasa kutushangaza ikiwa tulihusika katika ubishani mmoja baada ya mwingine. Hata hivyo, mithali moja husema hivi: “Moto hufa kwa kukosa kuni; na bila mchongezi fitina hukoma. Kama makaa juu ya makaa yanayowaka, na kama kuni juu ya moto; ndivyo mtu mgomvi achocheavyo uadui.” (Mithali 26:20, 21) Ikiwa sisi ni wenye hali pole, badala ya ‘kuongeza kuni juu ya moto’ na kuwakasirisha wengine, tutakuwa na uhusiano mzuri pamoja nao.

17 Mtu mwenye hali pole huelekea kuwa na rafiki wema. Watu hufurahia kushirikiana naye kwa sababu ana mwelekeo chanya (mzuri), na maneno yake ni yenye kuburudisha na ni matamu kama asali. (Mithali 16:24) Hilo lilikuwa kweli kuhusu Yesu, ambaye angeweza kusema hivi: “Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu; kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:29, 30) Yesu hakuwa mkali bila huruma, na nira yake haikuwa yenye kulemeza. Wale waliomjia Yesu walitendewa vizuri na kuburudishwa kiroho. Hali ni hivyo hivyo tunaposhirikiana na rafiki Mkristo mwenye hali pole.

18 Hali pole hutupendekeza kwa waamini wenzetu. Bila shaka, Wakristo wengi katika Korintho walivutwa kwa Paulo kwa sababu aliwasihi “kwa upole na utaratibu wa Kristo.” (2 Wakorintho 10:1) Kwa hakika ni lazima iwe Wathesalonike walimwitikia mtume huyo, kwa kuwa alikuwa mwalimu mpole, na mwanana. (1 Wathesalonike 2:5-8) Hakuna shaka yoyote kwamba wazee Waefeso walikuwa wamejifundisha mengi kutoka kwa Paulo na wakampenda sana. (Matendo 20:20, 21, 37, 38) Je! wewe huonyesha upole unaokupendekeza kwa wengine?

19. Upole unawasaidiaje watu wa Yehova wadumishe mahali pao katika tengenezo lake?

19 Hali ya upole husaidia watu wa Yehova wajitiishe na kudumisha mahali pao katika tengenezo lake. (Wafilipi 2:5-8, 12-14; Waebrania 13:17) Upole hutuzuia tusitafute utukufu, ulio na msingi wa kiburi na ambao humchukiza Mungu. (Mithali 16:5) Mtu mpole hajioni kuwa juu zaidi ya waamini wenzake, naye hajaribu kuwa bora zaidi kwa hasara yao. (Mathayo 23:11, 12) Badala ya hivyo, yeye hukiri hali yake yenye dhambi na uhitaji wake wa uandalizi wa Mungu wa fidia.

Upole Hukuza Furaha

20. Upole una matokeo gani kwenye maisha ya familia?

20 Watumishi wote wa Mungu wapaswa wakumbuke kwamba upole ni tunda la roho yake linalokuza furaha. Kwa mfano, kwa sababu watu wa Yehova huonyesha sifa kama vile upendo na upole, wao wana familia nyingi zenye furaha miongoni mwao. Mume na mke wanaposhughulika katika njia ya upole wenyewe kwa wenyewe, watoto wao wanalelewa katika mazingira yenye utulivu, si katika familia yenye mwelekeo wa maneno na vitendo vya ukali usio na huruma. Baba anapowapa watoto wake shauri katika upole, hiyo ina tokeo zuri kwa akili zao changa, na yaelekea kwamba roho ya upole itakuwa sehemu ya utu wao. (Waefeso 6:1-4) Hali ya upole husaidia waume waendelee kuwapenda wake zao. Inasaidia wake wajitiishe kwa waume wao na husukuma watoto watii wazazi wao. Upole pia hufanya washiriki wa familia wawe na roho ya kusamehe inayochangia furaha.—Wakolosai 3:13, 18-21.

21. Ni nini kiini cha shauri ambalo mtume Paulo alitoa kwenye Waefeso 4:1-3?

21 Familia na watu wenye hali pole hukuza furaha katika makundi ambamo wao hushiriki. Kwa hiyo, watu wa Yehova huhitaji kujitahidi sana kuwa wenye hali pole. Je! wewe unafanya hivyo? Mtume Paulo aliwasihi Wakristo wapakwa-mafuta wenzake watembee kama inavyoustahili mwito wao wa kimbingu, wakifanya hivyo “kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo; na kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha amani.” (Waefeso 4:1-3) Ni lazima pia Wakristo wenye tumaini la kidunia waonyeshe upole na sifa nyingine za kimungu. Huo ndio mwendo unaoleta furaha ya kweli. Wenye hali pole ni wenye furaha kweli kweli!

Ungejibuje?

◻ Kwa nini wenye hali pole ni watu wenye furaha?

◻ Ni nini maana ya kuwa mwenye hali pole?

◻ Upole waweza kusitawishwaje?

◻ Baadhi ya faida za upole ni zipi?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki