Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 10/15 kur. 15-20
  • Jivikeni Upole!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jivikeni Upole!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wachungaji Wenye Hali Pole Wahitajiwa
  • Upole Huongoza Mshauri Mwenye Hekima
  • Thamani ya Wingi wa Washauri
  • Kutoa Ushahidi kwa Upole
  • Upole Wahitajiwa kwa Wote
  • Wenye Hali Pole Ni Wenye Furaha Kama Nini!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Onyesheni “Upole Wote Kuelekea Watu Wote”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Upole Ni Sifa Muhimu Sana ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Upole​—Unatunufaishaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2020
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 10/15 kur. 15-20

Jivikeni Upole!

“Kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.”—Wakolosai 3:12.

1-3. Kwenye Wakolosai 3:12-14, mtume Paulo alisema nini kuhusu upole na sifa nyinginezo za kimungu?

YEHOVA huwapa watu wake mavazi ya ufananisho yaliyo bora kabisa. Kwa kweli, ni lazima wote wanaotaka upendeleo wake wajivike vazi lenye nyuzi ngumu za upole. Sifa hiyo ni yenye kufariji kwa sababu inapunguza mahangaiko katika hali zenye taabu. Inalinda pia, kwa kuwa inakinga ugomvi.

2 Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wapakwa-mafuta hivi: “Kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu.” (Wakolosai 3:12) Hali ya neno la Kigiriki linalofasiriwa “jivikeni” huonyesha utendaji unaotakiwa ufanywe kwa hima. Wapakwa-mafuta walioteuliwa, watakatifu, wapendwao na Mungu, walipaswa wasikawie kujivika sifa kama vile upole.

3 Paulo aliongeza hivi: “Mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama Bwana alivyowa-samehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.” (Wakolosai 3:13, 14) Upendo, upole, na sifa nyinginezo za kimungu huwezesha Mashahidi wa Yehova “wakae pamoja, kwa umoja.”—Zaburi 133:1-3.

Wachungaji Wenye Hali Pole Wahitajiwa

4. Wakristo wa kweli huvaa vazi la ufananisho lililofumwa kwa sifa zipi?

4 Wakristo wa kweli hufanya bidii ‘kuvifisha viungo vyao vilivyo katika nchi, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya, na kutamani,’ na wao hujitahidi kuvua vazi lolote la zamani lenye uzi wa hasira, ghadhabu, uovu, matukano, na matusi. (Wakolosai 3:5-11) Wao huvua “utu wa zamani” (kihalisi, “mtu wa zamani”) na kujivika “utu mpya” (au, “mtu mpya”), vazi linalofaa. (Waefeso 4:22-24, Kingdom Interlinear) Vazi lao mpya, lililofumwa kwa huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu, lawasaidia wasuluhishe matatizo na kuishi maisha za kumhofu Mungu.—Mathayo 5:9; 18:33; Luka 6:36; Wafilipi 4:2, 3.

5. Ni nini kuhusu kufanya kazi kwa kundi la Kikristo kinacholifanya iwe shangwe kuwa sehemu yalo?

5 Watu wanaoonwa kuwa wenye kufanikiwa katika ulimwengu huu mara nyingi ni wagumu, hata wakatili. (Mithali 29:22) Ni tofauti yenye kuburudisha kama nini miongoni mwa watu wa Yehova! Kundi la Kikristo halitendi kazi kama vile watu wengine huendesha biashara—katika njia stadi lakini yenye ukatili ambayo huenda ikafanya watu wakose furaha. Badala ya hivyo, ni shangwe kuwa sehemu ya kundi. Sababu moja ni kwamba hali ya upole ni sehemu ya hekima inayoonyeshwa na Wakristo kwa ujumla na hasa na wanaume wenye sifa za kuwafundisha waamini wenzao. Naam, shangwe hutokana na maagizo na shauri linalopewa na wazee waliowekwa wanaofundisha “katika upole wa hekima.”—Yakobo 3:13.

6. Kwa nini ni lazima wazee Wakristo wawe wenye hali pole?

6 Roho, au mwelekeo wenye kutawala wa watu wa Mungu unataka kwamba wanaume wenye kukabidhiwa uangalizi kundini wawe wenye hali pole, wepesi kukubali maoni ya wengine, na wenye uelewevu. (1 Timotheo 3:1-3) Watumishi wa Yehova ni kama kondoo waanana, si kama mbuzi wakaidi, nyumbu wenye vichwa vigumu, au mbwa-mwitu wakali. (Zaburi 32:9; Luka 10:3) Wakiwa wenye mfano wa kondoo, wanahitaji kutendewa kwa upole na wororo. (Matendo 20:28, 29) Naam, Mungu huwatazamia wazee kuwa wapole, wenye fadhili, wenye upendo, na wenye saburi kuelekea kondoo wake.—Ezekieli 34:17-24.

7. Wazee wapaswa kufunzaje wengine au kusaidiaje walio wagonjwa kiroho?

7 Akiwa “mtumwa wa Bwana,” mzee apaswa “kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, mvumilivu; akiwaonya kwa upole wao washindanao naye, ili kama ikiwezekana, Mungu awape kutubu na kuijua kweli.” (2 Timotheo 2:24, 25) Wachungaji Wakristo wapaswa waonyeshe ufikirio mwororo wanapojaribu kusaidia walio wagonjwa kiroho, kwa kuwa kondoo ni za Mungu. Wazee hawapaswi kuwatendea kama vile mtu aliyeajiriwa kuchunga angefanya bali wanahitaji kuwa wenye hali pole, kama Mchungaji Mwema, Yesu Kristo.—Yohana 10:11-13.

8. Ni jambo gani lililotukia kwa Musa mwenye hali pole, na kwa nini?

8 Huenda nyakati nyingine mzee akaona ni vigumu kudumisha roho ya upole. “Musa, alikuwa mpole sana zaidi ya wanadamu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hesabu 12:3) Hata hivyo, Waisraeli walipopatwa na upungufu wa maji huko Kadeshi, waligombana na Musa na kumlaumu kwa kuwaongoza kutoka Misri hadi kwenye jangwa lenye ukame. Yajapokuwa yote ambayo Musa alikuwa amevumilia, yeye alisema bila kufikiri, kwa ukali usio na huruma. Yeye na Haruni walisimama mbele ya watu na kuelekeza fikira kwao wenyewe, Musa akisema hivi: “Sikieni sasa, enyi waasi; je! tuwatokezee maji katika mwamba huu?” Kisha Musa akaupiga ule mwamba kwa fimbo yake mara mbili, Mungu naye akafanya ‘maji mengi’ yatoke kwa ajili ya watu na wanyama wao. Yehova alichukizwa kwa sababu Musa na Haruni hawakuwa wamemtukuza, kwa hiyo Musa hakupewa pendeleo la kuwaongoza Waisraeli kuingia Bara Lililoahidiwa.—Hesabu 20:1-13; Kumbukumbu la Torati 32:50-52; Zaburi 106:32, 33.

9. Upole wa mzee waweza kujaribiwaje?

9 Upole wa mzee Mkristo huenda pia ukajaribiwa katika njia mbalimbali. Kwa mfano, Paulo alimwonya Timotheo kwamba kungeweza kutokea mtu ambaye “amejivuna” na “ana wazimu wa kuwazia habari za maswali, na mashindano ya maneno.” Paulo aliongeza hivi: “Katika hayo hutoka husuda, na ugomvi, na matukano, na shuku mbaya; na majadiliano ya watu walioharibika akili zao, walioikosa kweli.” Mwangalizi Timotheo hakupaswa atende kwa ukali usio na huruma bali alitakiwa ‘ayakimbie mambo hayo,’ naye alipaswa ‘afuate haki, utauwa [ujitoaji kimungu, NW], imani, upendo, saburi, upole.’—1 Timotheo 6:4, 5, 11.

10. Tito alipaswa kuyakumbusha makundi kuhusu nini?

10 Ingawa wazee wanahitaji kuwa wapole, ni lazima wawe imara kwa ajili ya mema. Tito alikuwa hivyo, akiwakumbusha wale walioshiriki na makundi katika Krete “wasimtukane mtu ye yote, wasiwe wagomvi, wawe wema, wakionyesha upole wote kwa watu wote.” (Tito 3:1, 2) Kuonyesha kwa sababu gani Wakristo wapaswa wawe wenye hali pole kwa wote, Tito alipaswa aelekeze fikira kwenye jinsi Yehova alivyokuwa amekuwa mwenye fadhili na mwenye upendo. Mungu hakuwa amewaokoa waamini kwa sababu ya vitendo vyovyote vya uadilifu ambavyo walikuwa wamefanya bali ilikuwa kulingana na rehema yake kupitia Yesu Kristo. Upole na saburi za Yehova humaanisha wokovu kwetu pia. Kwa hiyo, kama Tito, wazee wa siku hizi wapaswa kuyakumbusha makundi yajitiishe kwa Mungu, yakimwiga kwa kuwatendea wengine kwa njia ya upole.—Tito 3:3-7; 2 Petro 3:9, 15.

Upole Huongoza Mshauri Mwenye Hekima

11. Kulingana na Wagalatia 6:1, 2, shauri lapasa litoleweje?

11 Vipi ikiwa kondoo wa ufananisho amekosa? Paulo alisema hivi: “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi mlio wa Roho [wenye sifa za kiroho, NW] mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe. Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:1, 2) Shauri huwa na matokeo zaidi likitolewa kwa roho ya upole. Hata kama wazee wanajaribu kumshauri mtu ambaye amekasirika, wanapaswa waonyeshe kujidhibiti, wakitambua kwamba “ulimi laini huvunja mfupa.” (Mithali 25:15) Mtu mwenye utu mgumu kama mfupa aweza kulainishwa na maneno yenye upole, na ugumu wake waweza kulainika.

12. Roho ya upole husaidiaje mshauri?

12 Yehova ni Mkufunzi mwenye hali pole, na njia yake ya upole ya kufundisha ina matokeo katika kundi. Hilo ni kweli hasa wakati wazee wanapoona ni lazima wawashauri wale wanaohitaji msaada wa kiroho. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “N’nani aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima.” Upole unatokana na heshima na shukrani kwa ajili ya “hekima itokayo juu,” pamoja na utambuzi wenye kiasi wa hali za kupungukiwa kwa mtu mwenyewe. Roho ya upole na unyenyekevu humlinda mshauri asiseme maneno yenye kuvunja na kukosa na hufanya shauri lake liwe rahisi kukubalika.—Yakobo 3:13, 17.

13. “Upole wa hekima” huathirije jinsi shauri linavyotolewa?

13 “Upole wa hekima” humzuia mshauri asiwe mwenye kusema waziwazi bila kufikiri au mwenye ukali usio na huruma. Hata hivyo, hangaiko juu ya urafiki au kupata kibali cha mtu halipasi kumsukuma mzee aseme mambo ambayo yamebuniwa kupendeza badala ya kutoa kwa upole shauri la waziwazi lenye msingi wa Neno la Mungu. (Mithali 24:24-26; 28:23) Shauri alilopokea Amnoni kutoka kwa binamu yake lilitosheleza tamaa yake, lakini lilimgharimisha uhai wake. (2 Samweli 13:1-19, 28, 29) Kwa hiyo, ni lazima wazee wa siku hizi wasipunguze umaana wa kanuni za Biblia ili kutuliza dhamiri ya mtu, kwa kuwa kufanya hivyo kwaweza kuhatarisha uhai wake. Kama Paulo, wazee hawapaswi wajiepushe na kuwaambia wengine “shauri lote la Mungu.” (Matendo 20:26, 27, NW; 2 Timotheo 4:1-4) Mshauri Mkristo mkomavu huonyesha hofu ya kimungu naye hutoa shauri lenye uadilifu akiwa na upole wa hekima.

14. Kwa nini mzee apaswa awe mwangalifu asiwafanyie wengine maamuzi ambayo wanapaswa wajifanyie?

14 Upole pamoja na hekima ya kimungu zitamzuia mzee asifanye madai yenye ukali usio na huruma. Yeye apaswa atambue kwamba si jambo la hekima wala haifai kwake kumfanyia mtu mwingine uamuzi ambao apaswa ajifanyie mwenyewe. Kama mzee aliwafanyia wengine maamuzi, jukumu ya matokeo ingekuwa juu yake naye angeshiriki lawama kwa matokeo yoyote mabaya. Mzee aweza kuelekeza fikira kwenye yale ambayo Biblia husema, lakini kama hakuna sheria ya Kimaandiko kuhusu jambo hilo, uchaguzi na dhamiri ya mtu mwenyewe yapasa iamue kile atakachofanya au kutofanya. Kama Paulo alivyosema: “Kila mtu atalichukua furushi lake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5; Warumi 14:12) Hata hivyo, mwenye kuuliza aweza kusaidiwa kufanya uamuzi ulio sahihi kwa mzee kumwuliza maswali yanayosaidia mtu huyo asababu juu ya maandiko yanayohusika na miendo tofautitofauti ambayo anaweza kufuata.

15. Ni nini chapasa kufanywa ikiwa mzee hajui jibu la swali fulani?

15 Kama mzee hajui jibu la swali fulani, yeye hapaswi kujibu ili tu asipoteze sifa. Upole wa hekima ungemzuia asikisie na labda kutoa jibu lisilo sahihi ambalo lingeweza kusababisha taabu baadaye. Kuna “wakati wa kunyamaza, na wakati wa kunena.” (Mhubiri 3:7; linganisha Mithali 21:23.) Mzee apaswa “kunena” wakati tu anapojua jibu la swali au amefanya uchunguzi wa kutosha kutoa jibu sahihi. Ni jambo la hekima kutojibu maswali ya kukisia tu.—Mithali 12:8; 17:27; 1 Timotheo 1:3-7; 2 Timotheo 2:14.

Thamani ya Wingi wa Washauri

16, 17. Kwa nini inafaa kwa wazee kuomba shauri kwa wazee wengine?

16 Sala na kujifunza zitasaidia wazee wajibu maswali na kushughulikia matatizo magumu, lakini inapasa kukumbukwa kwamba “kwa wingi wa washauri jambo fulani linatimizwa.” (Mithali 15:22, NW) Kuomba shauri kwa wazee wengine kunatokeza mkusanyo wa hekima wenye thamani. (Mithali 13:20) Si wazee wote walio na ujuzi au maarifa ya Biblia yaliyo sawa. Kwa hiyo, upole wa hekima wapasa kumsukuma mzee mwenye ujuzi mdogo zaidi afanye shauri na wazee wenye maarifa na ujuzi mwingi zaidi, hasa wakati jambo lenye uzito linapohitaji kushughulikiwa.

17 Wazee wanapoteuliwa kushughulikia jambo lenye uzito, wao waweza kutafuta msaada kwa usiri. Musa aliteua “watu walio na uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu,” ili wamsaidie kuhukumu Waisraeli. Ingawa walikuwa wazee, hawakuwa na maarifa na ujuzi mwingi kama wa Musa. Kwa hiyo, “mashauri magumu wakamletea Musa, lakini kila neno dogo wakaliamua wenyewe.” (Kutoka 18:13-27) Basi, ikiwa lazima, wazee wanaoshughulikia kesi ngumu leo wanaweza kwa kufaa kutafuta msaada wa waangalizi wenye ujuzi, ingawa wanafanya uamuzi wa mwisho wao wenyewe.

18. Katika kushughulikia mambo ya kihukumu, ni mambo gani yenye kukata maneno yanayohakikisha kwamba maamuzi sahihi yatafanywa?

18 Mishnah ya Kiyahudi husema kwamba katika Israeli idadi ya wale waliofanyiza mahakama ya kijiji ilibadilika kulingana na uzito wa kesi. Kuna thamani ya kweli katika wingi wa washauri, ingawa wingi wa watu peke yake hauhakikishi usahihi, kwa sababu watu wengi waweza kukosa. (Kutoka 23:2) Mambo yenye kukata maneno yanayohakikisha kwamba maamuzi sahihi yatafanywa ni Maandiko na roho ya Mungu. Hekima na upole zitawasukuma Wakristo wajitiishe kwa hayo.

Kutoa Ushahidi kwa Upole

19. Upole unawasaidiaje watu wa Yehova kuwatolea wengine ushahidi?

19 Upole pia huwasaidia watumishi wa Mungu watoe ushahidi kwa watu wenye mielekeo tofautitofauti. (1 Wakorintho 9:22, 23) Kwa sababu Yesu alifundisha akiwa na upole, watu wanyenyekevu hawakumhofu, kama vile walivyowahofu viongozi wa kidini wakali bila huruma. (Mathayo 9:36) Bila shaka, njia zake za upole zilivutia “kondoo,” si “mbuzi” waovu. (Mathayo 25:31-46; Yohana 3:16-21) Ingawa Yesu alitumia maneno makali katika kushughulika na wanafiki wenye mfano wa mbuzi, ni lazima Mashahidi wa Yehova wawe wenye upole wanapotangaza ujumbe wa hukumu za Mungu leo kwa sababu hawana ule mwono-ndani na ile mamlaka aliyokuwa nayo Yesu. (Mathayo 23:13-36) Wanaposikiliza ujumbe wa Ufalme unaohubiriwa kwa upole, ‘wale walio na mwelekeo wenye kufaa kwa ajili ya uhai wa milele wanakuwa waamini,’ kama watu wenye mfano wa kondoo waliomsikiliza Yesu walivyokuwa.—Matendo 13:48, NW.

20. Mwanafunzi wa Biblia hunufaikaje anapofundishwa kwa upole?

20 Matokeo mazuri hupatikana kwa kutoa ushahidi na kuwafunza wengine kwa upole na kwa kuwavutia kwa msingi wa kufikiri kuzuri, kanuni za Biblia, na kweli. “Mtakaseni Kristo Bwana mioyoni mwenu,” akaandika Petro. “Mwe tayari sikuzote kumjibu kila mtu awaulizaye habari za tumaini lililo ndani yenu; lakini kwa upole na kwa hofu.” (1 Petro 3:14, 15) Mwanafunzi anayefundishwa katika njia ya upole aweza kukaza fikira kwenye habari badala ya kukengeushwa fikira au labda hata kukwazwa na njia ya ukali usio na huruma, ya kubishana. Kama Paulo, wahudumu wanaofunza kwa upole waweza kusema hivi: “Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe.” (2 Wakorintho 6:3) Hata wapinzani nyakati nyingine huwaitikia kwa upendelevu wale wanaofunza kwa upole.

Upole Wahitajiwa kwa Wote

21, 22. Upole hunufaishaje watu wote wa Yehova?

21 Ni lazima upole wa Kikristo usiwe wa kujifanya tu ili kuwavutia wale walio nje ya tengenezo la Yehova. Sifa hiyo ni ya muhimu pia katika mahusiano miongoni mwa watu wa Mungu. (Wakolosai 3:12-14; 1 Petro 4:8) Makundi hujengwa kiroho wakati wazee na watumishi wa huduma wenye hali pole wanapofanya kazi pamoja kwa upatano. Kuonyesha upole na sifa nyinginezo za kimungu ni jambo la muhimu kwa kila mmoja wa watu wa Yehova kwa sababu kuna “sheria moja” kwa wote.—Kutoka 12:49; Mambo ya Walawi 24:22.

22 Upole unachangia amani na furaha ya watu wa Mungu. Kwa hiyo, unapasa kuwa sehemu ya uzi wa sifa zinazofanyiza vazi linalovaliwa na Wakristo wote nyumbani, kundini, na penginepo. Naam, watumishi wote wa Yehova wanahitaji kujivika upole.

Ungejibuje?

◻ Kwa nini ni lazima wazee Wakristo wawe wenye hali pole?

◻ Upole humwongozaje mshauri mwenye hekima?

◻ Ni nini thamani ya wingi wa washauri?

◻ Kwa nini kuna manufaa kutoa ushahidi kwa upole?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Watu wa Yehova ni wenye mfano wa kondoo na huhitaji kutendewa kwa upole

[Hisani]

Garo Nalbandian

[Picha katika ukurasa wa 19]

Upole huwezesha watu wa Yehova watoe ushahidi kwa watu wenye mielekeo tofautitofauti

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki