SIRI TAKATIFU
Ile tofauti kubwa kati ya siri takatifu ya Mungu na siri za dini za mafumbo, kwanza kabisa, ni habari zilizomo: Siri ya Mungu ni habari njema wala si uwongo au udanganyifu ulioundwa na mwanadamu. (Yoh 8:31, 32, 44; Kol 1:5; 1Yo 2:27) Pili, waliochaguliwa waelewe siri takatifu ya Mungu wamefungwa na wajibu wa kuifanyia tangazo na mwenezo mkubwa zaidi iwezekanavyo, wala si kuiweka siri. Kama yanayotangulia yanavyoonyesha, hilo linafunuliwa na matumizi ya Biblia ya semi kama vile ‘kuhubiriwa,’ ‘kujulishwa,’ ‘kudhihirishwa,’ na pia ‘kutangazwa,’ ‘kusema,’ kuhusiana na “siri takatifu ya habari njema.” Wakristo wa kweli walijizatiti sana kutangazia “uumbaji wote ulio chini ya mbingu” habari njema hizi zenye kuleta uelewaji wa ile siri takatifu. (1Ko 2:1; Efe 6:19; Kol 1:23; 4:3, 4) Mungu huamua ni nani wasiostahili naye huzuia uelewaji huo usiwafikie. Mungu hapendelei anapofanya hivyo; Mungu hawafungulii uelewaji wa siri yake takatifu kwa sababu ya “ugumu wa mioyo yao.”—Efe 4:17, 18.
Huangazia Kristo. Kwa kuwa “kutoa ushahidi kumhusu Yesu ndilo kusudi la unabii,” ni lazima iwe “siri takatifu ya Mungu” inaangazia Kristo. (Ufu 19:10; Kol 2:2) “Siri takatifu” zote za Mungu zinahusiana na Ufalme wa Kimasihi. (Mt 13:11) Mtume Paulo anawaandikia hivi Wakristo wenzake: “Hazina zote za hekima na za ujuzi zimefichwa kwa uangalifu ndani yake,” na “ni katika yeye kwamba ujazo wote wa sifa ya Mungu hukaa kimwili.”—Kol 2:2, 3, 9.
Paulo alisema kujihusu kuwa amepewa usimamizi-nyumba juu ya “siri takatifu za Mungu.” (1Ko 4:1) Anazungumza juu ya uelewaji alio nao “katika siri takatifu ya Kristo.” (Efe 3:1-4) Anaeleza kwamba hii siri takatifu ni hekima iliyofichwa ambayo ilipangwa mapema na Mungu kabla ya hii mifumo ya mambo. (1Ko 2:7) Kujulishwa kwa hili fumbo, au “siri takatifu za Mungu,” kulianza na unabii wa Yehova mwenyewe kwenye Mwanzo 3:15. Kwa karne nyingi wanaume wa imani waliutazamia “uzao” wa ahadi ukomboe jamii ya wanadamu kutoka katika dhambi na kifo, lakini haikueleweka wazi huo “uzao” ni nani hasa na ni jinsi gani hasa “uzao” huo ungekuja na kuleta ukombozi. Ilifanywa kuwa wazi baada ya Kristo kuja na ‘kuangaza nuru juu ya uzima na kutoweza kuharibika kupitia habari njema.’ (2Ti 1:10) Hapo ndipo ujuzi wa fumbo la ‘uzao wa mwanamke,’ ulipoanza kueleweka.
Ufalme wa Kimasihi. Katika maandishi ya Paulo anatoa maono kamili ya ufunuo wa siri takatifu ya Kristo. Kwenye Waefeso 1:9-11 anasema Mungu alijulisha “siri takatifu” ya mapenzi yake, na kusema hivi: “Ni kulingana na upendezi wake mwema alioukusudia ndani yake mwenyewe kwa ajili ya usimamizi wa mambo kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi, yaani, kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyo mbinguni na vitu vilivyo duniani. Ndiyo, katika yeye, katika muungano pamoja na yeye ambaye tulihesabiwa pia kuwa warithi, kwa kuwa tuliagizwa kimbele kulingana na kusudi lake yeye anayetenda mambo yote kulingana na jinsi mapenzi yake yanavyoshauri.” Hii “siri takatifu” inahusisha serikali, Ufalme wa Mungu wa Kimasihi. “Vitu vilivyo mbinguni,” anavyorejezea Paulo, ni wanaotazamia kuwa warithi wa Ufalme huo wa kimbingu wa Kristo. “Vitu vilivyo duniani” vitakuwa ni raia zake wa kidunia. Yesu aliwatajia wanafunzi wake kwamba siri takatifu ilihusiana na Ufalme alipowaambia hivi: “Ninyi mmepewa siri takatifu ya ufalme wa Mungu.”—Mk 4:11.
Inatia Ndani Kutaniko. Ujuzi wa siri takatifu una sehemu nyingi ndani yake. Mtume alitoa habari zaidi alipoeleza kwamba siri takatifu inatia ndani kutaniko, ambalo Kristo ni Kichwa chake. (Efe 5:32; Kol 1:18; Ufu 1:20) Hawa ndio warithi-washirika wake, ambao anashiriki Ufalme pamoja nao. (Lu 22:29, 30) Wametwaliwa kutoka miongoni mwa Wayahudi na vilevile Watu wa Mataifa. (Ro 11:25; Efe 3:3-6; Kol 1:26, 27) Sehemu hii ya “siri takatifu” haingeweza kufanywa iwe wazi hadi Petro alipoelekezwa amtembelee Kornelio, Mtu wa Mataifa na kuwaona watu wa nyumba hii ya watu wa mataifa wakipokea karama za roho takatifu, katika 36 W.K. (Mdo 10:34, 44-48) Akiwaandikia Wakristo walio Watu wa Mataifa, Paulo aliwaambia hivi: “Mlikuwa bila Kristo, . . . wageni kwa maagano ya ahadi, wala hamkuwa na tumaini na mlikuwa bila Mungu katika ulimwengu. Lakini sasa katika muungano na Kristo Yesu ninyi ambao wakati mmoja mlikuwa mbali sana mmekuja kuwa karibu kupitia damu ya Kristo.” (Efe 2:11-13) Kupitia shughuli za Mungu pamoja na kutaniko, “serikali na mamlaka zilizo katika mahali pa kimbingu” zingekuja kuijua “hekima ya Mungu ya namna nyingi sana.”—Efe 3:10.
Katika njozi ya Ufunuo aliopewa Yohana, kutaniko hilo linaonyeshwa kuwa na washiriki 144,000 ‘walionunuliwa kutoka kati ya wanadamu wakiwa matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.’ Wanasimama pamoja na Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, juu ya Mlima Sayuni, hapo pakiwa ni mahali ambapo linasimama “jiji la Mungu aliye hai, Yerusalemu la mbinguni.” “Kiti cha ufalme cha Yehova” kilisimamishwa katika jiji la kidunia la Yerusalemu la kale na wafalme wa nasaba ya Daudi wakiketi juu yake; pia hekalu la Yehova lilikuwa hapo. Yesu Kristo amewekwa juu ya kiti cha ufalme katika Yerusalemu la kimbingu, na wafuasi wake watiwa-mafuta walio washikamanifu wanaushiriki utawala wake wa Ufalme. (Ufu 14:1, 4; Ebr 12:22; 1Nya 29:23; 1Pe 2:4-6) Mojawapo kati ya zile sehemu za shughuli za Mungu kuhusiana na kutaniko hilo ni ufufuo wao kwenye uzima usioweza kufa na hali ya kutoharibika wakati wa kuwapo kwa Kristo, na jambo hilo lenyewe ni “siri takatifu.”—1Ko 15:51-54.