Siri Takatifu Yakunjuka
“Siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ni kubwa bila shaka.”—1 TIMOTHEO 3:16, NW.
1. Ni siri gani yenye kuelezwa kwenye 1 Timotheo 3:16?
JE! MAFUMBO hukuvutia wewe? Je! wewe huona shangwe kuchunguza siri? Walio wengi kati yetu hufanya hivyo! Basi, jiunge nasi tuchunguzapo moja ya siri zilizo kubwa kupita zote—siri iliyofungwa kufuli ndani ya Neno la Mungu kwa maelfu ya miaka. Siri takatifu hii huathiri sana maisha zetu, za wakati uliopo na wakati ujao. Hiyo ni ‘ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu,’ ambayo twaelezwa kwenye 1 Timotheo 3:16, NW. Lo, jinsi twapasWa kuwa wenye shukrani kwa Yehova, “afunuaye siri,” kwa kutujulisha kwa neema siri hii tukufu mno na fasiri yayo!—Danieli 2:28, 29.
2. (a) Ni lini Yehova aliponena kwanza juu ya siri takatifu, na aliahidi nini wakati huo? (b) Ni maswali gani ambayo yataka kujibiwa?
2 Yehova alinena kwanza juu ya siri takatifu baada ya Nyoka kuwa amemdanganya Hawa, na Adamu akawa amemfuata katika uasi. Ndipo Mungu akaahidi kwamba “mbegu,” au uzao, ungeponda kichwa cha Nyoka. (Mwanzo 3:15, NW) Ni nani Mbegu huyu? Angeshindaje Nyoka? Je! yeye angetetea ukweli wa Mungu na kusudi Lake kuelekea dunia hii?
3. Unabii wa kimungu uliandaa vidokezi gani juu ya utambulisho na utendaji wa yule Mbegu?
3 Kwa wakati wake, unabii wa kimungu ulifunua vidokezi kuhusu utambulisho na utendaji wa Mbegu huyo wakati ujao. Yeye angekuwa mzao wa Abrahamu, angerithi ufalme wa Daudi, na angeitwa Mwana-Mfalme wa Amani. ‘Kwa wingi wa utawala wake wa kimwana-mfalme na kwa amani kutakuwa hakuna mwisho.’ (Isaya 9:6, 7, NW; Mwanzo 22:15-18; Zaburi 89:35-37) Lakini kama vile Warumi 16:25 hutaarifu, siri takatifu hiyo ‘ilisitirika kwa zamani za milele.’
Kutatua Lile Fumbo
4. Siri takatifu ilianzaje kukunjuka katika 29 W.K.?
4 Mwishowe, baada ya mileani nne, mnurisho ulitokea ghafula! Katika njia gani? Katika 29 W.K., Yohana alibatiza Yesu wa Nazareti katika Mto Yordani, na kutoka mbinguni sauti ya Mungu ikajulisha wazi hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mathayo 3:17) Ah, huyu hatimaye akawa ndiye yule Mbegu aliyeahidiwa! Ile siri takatifu ilikuwa imeanza kukunjuka katika nyuso zayo zote zilizo tukufu, kutia na lile jambo la ujitoaji kimungu.
5. “Ujitoaji kimungu” ni nini, nao huathirije wale wanaouzoea?
5 Sisi twaelewaje “ujitoaji kimungu”? Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, usemi huu wapatikana mara 20 tu, zaidi ya nusu ya mara hizo katika barua mbili za Paulo kwa Timotheo. Kichapo Insight on the Scriptures hueleza maana ya “ujitoaji kimungu” kuwa “kicho, ibada, na utumishi kwa Mungu, pamoja na uaminifu-mshikamanifu kwa enzi kuu yake ya ulimwengu wote mzima.” Kicho hutoka ndani ya moyo wenye kukaribia Mungu, kwa hofu nyingi ya kustahi fahari yake, umilele wake, na wingi wa uumbaji wake mtukufu, pamoja na ushukuru kwa ajili ya zawadi za kiroho na kimwili ambazo humimina juu ya wanadamu wenye kuthamini. Kweli kweli, kila mmoja wetu ambaye huzoea ujitoaji kimungu aweza kusema, kama vile mtunga zaburi kwenye Zaburi 104:1: ‘Ee nafsi yangu, umhimidi Bwana [Yehova, NW]. Wewe, Bwana [Yehova, NW], Mungu wangu, umejifanya mkuu sana; umejivika heshima na adhama.”
6. (a) Waabudu wa Yehova watofautianaje na wakaa-vitini wa Jumuiya ya Wakristo? (b) Paulo alisema nini kwenye Warumi 11:33, 34, na hivyo ni maswali gani yenye kutokezwa?
6 Ujitoaji wetu kwa Mungu ni lazima ujionyeshe, nao hufanya hivyo kupitia vitendo. Kwa habari hii, waabudu wa Mungu wa kweli, Yehova, ni tofauti sana na wakaa-vitini wa makanisa yenye kufifia ya Jumuiya ya Wakristo. Kwa watu wengi duniani, dini—ikiwa wangali wana dini—ni kawaida tu, kisetiri ambacho huvaliwa kuwafanya waonekane watakatifu huku wakiishi maisha yenye upatano na ulimwengu mfisadi uwazungukao. Hata hawajui Mungu ni nani. Kwa uhakika, watu kama hao wahitaji kutii maneno ya Paulo kwenye Matendo 17:23, NW, aliposema hivi kwa Waathene walioheshimu mno ‘Mungu Asiyejulikana’: “Kile mnachotolea ujitoaji kimungu bila kujua, hicho ndicho mimi nawatangazia nyinyi.” Kuhusu Mungu huyo mkuu, Paulo apaaza sauti hivi kwenye Warumi 11:33, 34, NW: “O kina cha mali ya Mungu na hekima na maarifa! Jinsi hukumu zake hazichunguziki na zenye kupita uwezo wa kuchunguza ni njia zake! Kwa maana ‘ni nani amepata kujua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake?’ “Basi, ni jinsi gani sisi huja kujua njia za Mungu? Ni kupitia kujifunza ile ‘siri takatifu ya ujitoaji kimungu.’ Lakini twafanyaje hivyo?
7. Kwa nini yaweza kusemwa kwamba “siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ni kubwa bila shaka”?
7 Kwenye 1 Timotheo sura ya 3, mtume Paulo atoa kwanza muhtasari wa mambo yatakwayo kwa watumishi katika nyumba ya Mungu, ambayo yaelezwa katika 1Ti 3 mstari wa 15, NW, kuwa “kundi la Mungu aliye hai, nguzo na tegemezo la ukweli.” Halafu Paulo aongeza hivi, katika 1Ti 3 mstari 16, NW: “Siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ni kubwa bila shaka.” Kubwa kweli kweli kwa sababu Yehova alituma Mwana wake mzaliwa pekee duniani ili afungue kufuli ya siri hii, kuonyesha ujitoaji kimungu ni nini kikweli na jinsi ulivyo wa maana sana, tegemeo la ibada ya kweli. Siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu yadhihirishwa na mwendo wa maisha ya Yesu hapa duniani. Ni lazima wote wapendao Yehova wajenge imani yao na maisha zao juu ya Kristo, aliyetoa kielelezo cha ujitoaji kimungu. Basi, ni jinsi gani Yesu alionyesha wazi siri takatifu ya ujitoaji kimungu?
Nyuso Sita
8. (a) Ni nini zile nyuso sita za siri takatifu ambayo Paulo aeleza kwenye 1 Timotheo 3:16? (b) “Yeye” ambaye adhihirishwa ni nani?
8 Kwa uvuvio wa kimungu, Paulo ajibu swali hilo. Kwenye 1 Timotheo 3:16, NW, yeye aeleza nyuso sita za siri takatifu hii, akisema hivi: “Yeye [1] alidhihirishwa katika mnofu, [2] alijulishwa wazi kuwa mwadilifu katika roho, [3] aliwatokea malaika, [4] alihubiriwa kote miongoni mwa mataifa, [5] aliaminiwa katika ulimwengu, [6] alipokewa juu katika utukufu.” Ni nani “Yeye” huyu mwenye kudhihirishwa? Kwa uwazi, “Yeye” ni yule Mbegu aliyeahidiwa, Yesu, aliyekuja kufanya mapenzi ya Mungu. Yeye ni kitovu cha siri takatifu, akiifanya iwe “kubwa” kweli kweli.
9. Kuna uthibitisho gani kwamba 1 Timotheo 3:16 haipasi kusomwa hivi: ‘Mungu alidhihirika katika mnofu’?
9 Wanautatu hujaribu kuchafua uelewevu wa siri takatifu hii kwa kusema kwamba “Yeye” kwenye 1 Timotheo 3:16, NW, ni Mungu mwenyewe. Wao hufanya msingi wa kusema hivyo uwe Biblia ya King James, ambayo husomwa kwamba, “Mungu alikuwa dhahiri katika mnofu.” Hata hivyo, hati za Kigiriki zenye kutegemeka zaidi husema nini? Kwa upatani, hizo hutumia kijina “Yeye” badala ya “Mungu.” Sasa wachambuzi wa maandishi wakubali kwamba kuingizwa kwa “Mungu” katika andiko hili ni kosa la waandishi. Hivyo, tafsiri za karibuni zaidi, kama vile American Standard Version, The New English Bible, na New World Translation, husomwa kwa usahihi hivi: ‘Yeye [au, Yeye ambayej alidhihirishwa katika mnofu.’ Si Mungu mwenyewe aliyetokea “katika mnofu,” hapana. Bali, ni Mwana wake mpendwa aliye kiumbe wa kwanza, ambaye kwa habari zake mtume Yohana aliandika hivi: “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema [fadhili zisizostahilika, NW] na kweli.”—Yohana 1:14.
‘Kadhihirishwa Katika Mnofu’
10. (a) Sehemu ya kwanza ya ile siri takatifu ilikujaje kuonekana wazi kwenye ubatizo wa Yesu? (b) Kwa nini Yesu akawa “Adamu wa mwisho”?
10 Sehemu ya kwanza ya siri takatifu ilikuja kuwa wazi kwenye ubatizo wa Yesu: Yesu “alidhihirishwa katika mnofu” akiwa Mwana wa Mungu mpakwa-mafuta. Yehova Mungu alikuwa amehamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni akautia katika tumbo-uzazi la Mariamu ili Yesu aweze kuzaliwa katika mnofu akiwa binadamu mkamilifu. Hivyo, kama vile 1 Wakorintho 15:45-47 huonyesha, Yesu akawa Adamu wa pili, au “wa mwisho,” nafsi kamilifu ya kibinadamu yenye kulingana barabara na Adamu wa kwanza. Kwa kusudi gani? Timotheo wa Kwanza 2 5, 6 humtaja “Adamu wa mwisho” kuwa “Mwanadamu, Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.” Kwa msingi huu wa kisheria wa dhabihu kamilifu ya kibinadamu, Yesu hupatanisha lile agano jipya kuelekea wanadamu 144,000 ambao huwa warithi washirika pamoja naye katika Ufalme wake.—Ufunuo 14:1-3.
11. Manufaa za dhabihu ya ukombozi ya Yesu zanyooka kufikia nani?
11 Je! wengine pia wangenufaika na kifo cha Yesu cha dhabihu? Ndiyo bila shaka! Yohana wa Kwanza 2:2 hutaarifu kwamba Yesu Kristo “ni [dhabihu ya] kipatanisho kwa dhambi zetu [yaani, dhambi za Wakristo wapakwa-mafuta kama Yohana]; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” Hivyo manufaa za ukombozi wa Yesu huenea kufika mbali kupita Wakristo wapakwa-mafuta 144,000 kufikia ulimwengu wote wa aina ya binadamu. “Umati mkubwa” ambao wako hai sasa na maelfu ya mamilioni watakaofufuliwa katika dunia Paradiso watapokea uhai wa milele kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya ukombozi ya Yesu. Tayari, kama ilivyosemwa kwa unabii kwenye Ufunuo 7:9, 10, umati mkubwa umeosha majoho yao na kuyafanya meupe kwa kujizoeza imani katika damu iliyomwagwa ya Mwana-Kondoo, Yesu Kristo. Wao wahesabiwa kuwa waadilifu kwa habari ya urafiki pamoja na Mungu. Kwa shangwe, wao wajifunza zile nyuso mbalimbali za siri takatifu na kuonyesha ujitoaji kimungu kupatana na kielelezo cha Yesu!
Nyuso Nyingine
12. Ni jinsi gani Yesu “alijulishwa wazi kuwa mwadilifu katika roho”?
12 Sasa, namna gani sehemu ya pili iliyo kwenye 1 Timotheo 3:16, NW? Yesu “alijulishwa wazi kuwa mwadilifu katika roho.” Lakini jinsi gani? Ni kwa Yehova kuinua Mwanaye mshika-uaminifu-maadili kutoka kwa wafu akawe na uhai wa roho. Hiyo ilikuwa sawa na Yehova kujulisha wazi kwamba Yesu alikuwa mwadilifu kabisa na mwenye kustahiki migawo zaidi iliyotukuka. Kama vile Warumi 1:4 yaeleza jambo hilo, Yesu ‘alijulishwa wazi kuwa Mwana wa Mungu kulingana na roho ya utakatifu kwa njia ya ufufuo kutoka kwa wafu.” Akithibitisha hilo, Petro atuambia hivi katika barua yake ya kwanza, sura ya 3, mstari wa 18, NW: “Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kwa habari ya dhambi, mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu, kwamba awaongoze nyinyi kwa Mungu, akiuawa katika mnofu, bali akafanywa kuwa hai katika roho.” Je! kielelezo cha Yesu cha ujitoaji kimungu kinakuongoza wewe kwa Mungu?
13. Yesu aliyefufuliwa aliwatokea malaika gani, na ni ujumbe wa aina gani ambao aliwahubiria?
13 Akiendelea na 1 Timotheo 3:16, NW, ndipo Paulo arejezea sehemu ya tatu ya siri takatifu, akisema kwamba Yesu “aliwatokea malaika.” Malaika hao wangeweza kuwa nani? Kuhusu Yesu, sasa ‘akiwa amefanywa kuwa hai katika roho,’ Petro aandika hivi kwenye 1 Petro 3:19, 20, NW: “Katika hali hii pia alikwenda zake na kuwahubiri roho walio gerezani, ambao hapo kwanza walikuwa wasiotii wakati saburi ya Mungu ilipokuwa ikingojea katika siku za Noa.” Kulingana na Yuda 6, roho hao walikuwa “malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu” katika mbingu. Walivaa miili ya kimnofu ili wapate shangwe ya ngono isiyo halali pamoja na wanawake. Gharika ilipolazimisha malaika hao kurudi katika makao ya kiroho, walitupwa katika Tartaro, hali ya kushushwa kabisa. (2 Petro 2:4) Yesu aliyefufuliwa aliwahubiri. Lakini je! huo ulikuwa ujumbe wa wokovu? Sivyo kabisa! Bali, Yesu alishutumu uovu wao kuwa kinyume kabisa cha ujitoaji kimungu. Wowote wa watu wa Mungu ambao huchezea ukosefu wa adili kingono leo wapaswa wapate onyo kutokana na hukumu iliyotangazwa juu ya malaika hao!
14. Ilikuwaje hata habari njema zikaanza ‘kuhubiriwa miongoni mwa mataifa’?
14 Sehemu ya nne ya 1 Timotheo 3:16 ni kwamba Yesu “alihubiriwa miongoni mwa mataifa.” Hilo limetimizwaje? Kabla tu ya kukamatwa kwake, Yesu aliwaambia mitume hivi: “Amin, Amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya, kwa kuwa mimi naenda kwa Baba.” (Yohana 14:12) Muda mfupi baada ya hapo, kwenye Pentekoste 33 W.K., Yesu alimimina roho takatifu juu ya wanafunzi wake, na zile habari zenye kugutusha za kwamba “Yesu huyo Mungu alimfufua” zikaanza kuhubiriwa kwa Wayahudi. Baadaye, Wasamaria pia walikubali neno la Mungu na wakaanza kupokea roho takatifu. (Matendo 2:32; 8:14-17) Kisha, katika 36 W.K., Petro akahubiria Kornelio na wengine waliokusanyika katika nyumba yake. Hivyo, habari njema zikaanza ‘kuhubiriwa miongoni mwa mataifa,’ yaani, miongoni mwa wasio Wayahudi, ambao pia walipakwa mafuta kwa roho takatifu.
15. Ni nini chenye kuthibitisha kwamba Wakristo wa kame ya kwanza walikuwa wamejifunza vizuri ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu?
15 Kama ilivyoripotiwa kwenye Matendo 12:24, “neno la Bwana [Yehova, NW] likazidi na kuenea.” Matendo 17:6 yasimulia kwamba kaskazini mwa Ugiriki wapinzani walipaaza sauti, kama vile wafanyavyo huko hata leo hii: “Watu hawa walioupindua ulimwengu wamefika huku nako.” Katika muda wa miaka 30 tangu hapo, Paulo angeweza kuandika akiwa Roma kwamba habari njema zilikuwa ‘zimehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:23, NW) Wakristo wa wakati huo walikuwa wamejifunza vizuri ile siri takatifu ya ujitoaji kimungu. Lo, waliitumia kwa bidii iliyoje! Sisi pia na tujifunze siri hiyo na kuitumia katika siku hii ya upeo wa kuhubiri Ufalme!
16. Sehemu ya tano ya ile siri takatifu ilikuwa nini, na ni utendaji gani uliofanya ionekane wazi?
16 Kwa kuitikia kuhubiri huko kwa karne ya kwanza, sehemu ya tano ya siri takatifu ya 1 Timotheo 3:16 ikaonekana wazi sana. Yesu sasa “aliaminiwa ulimwenguni.” Hiyo ilitokea kwa sababu ya ujitoaji kimungu ulio kama wa Kristo wa wamisionari wenye bidii, kutia na Paulo na Timotheo. Walipeleka habari njema ndani ya Esia Ndogo na Ulaya, labda hata mbali kufikia Hispania, na ndani ya Afrika Mashariki kwa kinywa cha Mwethiopia aliyebatizwa, huku Petro akitumikia katika Babuloni.
17. Kwa nini Yesu aaminiwa kotekote katika ulimwengu wa ki-siku-hizi?
17 Namna gani siku yetu? Tangu 1919 mabaki wapakwa-mafuta wamekuwa wakionyesha ujitoaji kimungu ulio kielelezo chema. Wapakwa-mafuta hao wamejenga imara juu ya msingi wa imani uliowekwa na Yesu. Hasa tangu 1935 wamechukua hatua zaidi ya kukusanya umati mkubwa, ambao washangilia tazamio la kupita “dhiki kubwa” na kuona shangwe ya uhai wa milele katika dunia paradiso. (Ufunuo 7:9, 14) Hivyo, zile habari njema zenye kuelekeza fikira kwa Yesu zaaminiwa kotekote katika ulimwengu wa ki-siku-hizi. Sasa Mashahidi wa Yehova zaidi ya 3,700,000 wanahubiri na kusitawi kuzunguka tufe lote wakiwa katika ujitoaji kimungu!
18. Ni jinsi gani Yesu ‘alipokewa juu katika utukufu’?
18 Uso mmoja zaidi wa siri takatifu hiyo wabakia, ule wa sita: Yesu “alipokewa juu katika utukufu.” Wakati wa zile siku 40 baada ya kuhuishwa katika roho, Yesu alijivika-vika miili ya kimnofu, akiwatokea wanafunzi wake na kuwaambia “mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu.” Halafu akapaa mbinguni. (Matendo 1:3, 6-9) Hivyo sala yake, iliyoandikwa kwenye Yohana 17:1-5, ilijibiwa: “Baba, . . . mtukuze Mwanao, ili Mwana wako naye akutukuze wewe . . . Mimi nimekutukuza duniani . . . Na sasa, Baba, unitukuze mimi pamoja nawe, kwa utukufu ule niliokuwa nao pamoja nawe kabla ya ulimwengu kuwako.”
19. Ni lazima iwe ilitokeaje Yesu aliporudi mbinguni?
19 Ni lazima iwe kulikuwa na ushangilio mkubwa sana Yesu aliporudi mbinguni! Mapema zaidi, wakati Yehova alipoweka misingi ya dunia, ‘wana wote wa Mungu walipiga kelele kwa furaha.’ (Ayubu 38:7) Ni lazima vikosi hivyo vya malaika viwe vilijawa na shangwe nyingi mno kumpokea tena miongoni mwao Bingwa huyo mwenye kutetea enzi kuu ya Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu!
20. Kwa nini Yesu amerithi jina tukufu jinsi hiyo, naye alifanya nini alipokuwa angali duniani?
20 Kwenye Waebrania 1:3, 4, Paulo asema hivi juu ya Yesu mwenye ushindi: “Akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu; amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao.” Kristo alipokea iina hilo kwa sababu ya kushinda kwake ukosefu wa uadilifu. Mwana huyu wa Mungu alikuwa ameanzisha kweli kweli kijia cha ujitoaji kimungu hapa duniani. Pia alikuwa ameweka kigezo kwa wengine wote watakaofikia uhai wa milele. Yesu akiwa ametukuzwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu katika mbingu, siri takatifu ya huu ujitoaji kimungu ilifunuliwa katika sehemu zayo zote.
Wewe Ungeitikiaje?
◻ “Ujitoaji kimungu” ni nini?
◻ Yesu ‘alidhihirishwaje katika mnofu’ na baada ya hapo ‘akajulishwa wazi kuwa mwadilifu katika roho’?
◻ Yesu aliwatokea malaika gani, na akiwa na ujumbe gani?
◻ NijinsiganiKristoamehubiriwa miongoni mwa mataifa’ na ‘akaaminiwa katika ulimwengu’?
◻ Ni lini Yesu ‘alipopokewa juu katika utukufu,’ na baada ya kufanya nini kuhusu ujitoaji kimungu?