KUJIZUIA
Kudhibiti, au kuzuia mwenendo, usemi, au mawazo ya mtu. (Mwa 43:31; Es 5:10; Zb 119:101; Met 10:19; Yer 14:10; Mdo 24:25) Maneno ya Kiebrania na ya Kigiriki yanayohusiana na kujizuia kihalisi yanamaanisha kuwa na uwezo wa kujidhibiti au kujiweza. Kujizuia ni mojawapo ya sifa ya ‘tunda la roho ya Mungu’ (Gal 5:22, 23); na ingawa Yehova ana nguvu nyingi anaonyesha sifa hiyo kila wakati. Badala ya kuwaangamiza mara moja watenda dhambi, ameruhusu wakati upite ili wapate fursa ya kuacha njia zao mbaya na hivyo kupata kibali chake.—Yer 18:7-10; 2Pe 3:9.
Hata hivyo, Yehova hakujizuia kutekeleza hukumu yake ilipothibitika kwamba wale aliowapa wakati wa kutubu hawakuwa tayari kukubali rehema zake. Mfano mmoja ni wale walioharibu jiji la Yerusalemu. Walikosa kutambua kwamba Yehova aliwaruhusu watawale Israeli ili kuwaadhibu Waisraeli kwa sababu ya kukosa uaminifu, nao wakawatendea bila huruma na kuwaadhibu kupita kiwango ambacho Mungu alitaka. (Linganisha Isa 47:6, 7; Zek 1:15.) Yehova aliliona hilo kimbele, na kupitia nabii Isaya, alitabiri wakati ambapo angeacha kujizuia kuwaadhibu waharibifu hao. Alisema hivi: “Nimenyamaza kwa muda mrefu. Niliendelea kukaa kimya na kujizuia. Kama mwanamke anayezaa, nitalia kwa uchungu, nitahemahema, na kutweta wakati uleule. Nitaiharibu milima na vilima na kukausha kabisa majani yake yote.”—Isa 42:14, 15.
Kristo Yesu pia alijizuia. Akieleza kuhusu jinsi watumishi wa nyumbani walivyohitaji kujitiisha chini ya mabwana wao, mtume Petro aliandika hivi: “Kwa kweli, mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. . . . Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa kutukana. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali alijikabidhi mkononi mwa Yule anayehukumu kwa uadilifu.”—1Pe 2:21-23.
Katika “siku za mwisho” ukosefu wa sifa ya kujizuia ungekuwa jambo moja ambalo lingewatambulisha wale ambao si Wakristo wa kweli. (2Ti 3:1-7) Hata hivyo, kwa kuwa Wakristo ni waigaji wa Mungu na wa Mwana wake (1Ko 11:1; Efe 5:1), wanapaswa kujitahidi kusitawisha sifa ya kujizuia katika mambo yote. (1Ko 9:25) Mtume Petro alisema hivi: ‘Ongezeni kwenye imani yenu wema wa adili, kwenye wema wenu wa adili ujuzi, kwenye ujuzi wenu kujizuia, kwenye kujizuia kwenu uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu ujitoaji-kimungu, kwenye ujitoaji-kimungu wenu upendo wa kindugu, kwenye upendo wenu wa kindugu upendo. Kwa maana mambo hayo yakiwa ndani yenu na kufurika, yatawazuia msiwe wasiotenda ama wasiozaa matunda kuhusiana na ujuzi sahihi kumhusu Bwana wetu Yesu Kristo.’—2Pe 1:5-8.
Wale hasa wanaotumikia wakiwa waangalizi katika makutaniko ya Kikristo wanapaswa kuwa na sifa ya kujizuia. (Tit 1:8) Ili waangalizi washughulikie vizuri matatizo ndani ya kutaniko lazima wawe na mazoea ya kuzuia maneno na matendo yao. Mtume Paulo alimshauri Timotheo hivi: “Isitoshe, kataa mabishano ya kipumbavu na ya kijinga, ukijua kwamba hayo hutokeza mapigano. Kwa maana mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote, mwenye uwezo wa kufundisha, anayejizuia anapokosewa, akiwafundisha kwa upole wale wasio na mwelekeo unaofaa.”—2Ti 2:23-25.
Kukosa kujizuia katika hali fulani kunaweza kuharibu rekodi nzuri ya utumishi mwaminifu na kumwingiza mtu katika matatizo ya kila aina. Kisa cha Mfalme Daudi kinaonyesha jambo hilo. Ingawa alikuwa mshikamanifu kwa ibada ya kweli na alipenda kanuni zenye uadilifu za sheria ya Mungu (linganisha Zb 101), Daudi alifanya uzinzi na Bath-sheba, kisha akaagiza mume wake Uria awekwe mbele ya mashambulio makali zaidi ya kivita, mahali ambapo lazima angeuawa. Matokeo yalikuwa kwamba Daudi alipatwa na matatizo mengi katika familia yake kwa miaka mingi iliyofuata. (2Sa 12:8-12) Kisa chake pia kinatuonyesha kwamba ni jambo la hekima kujiondoa katika hali inayoweza kukufanya ukose kujizuia. Daudi angeweza kuondoka kwenye dari la nyumba yake ya kifalme, lakini aliendelea kumtazama Bath-sheba alipokuwa akioga na akaanza kumtamani.—2Sa 11:2-4.
Vivyo hivyo, ili mtu asiyeweza kujizuia ajilinde na hatari ya kufanya uasherati, ingekuwa vema afunge ndoa yenye heshima badala ya kubaki mseja. Kuhusiana na hilo, mtume Paulo alisema hivi: “Ikiwa hawawezi kujizuia, acheni wafunge ndoa, kwa maana ni bora kufunga ndoa kuliko kuwaka tamaa.”—1Ko 7:9, 32-38.