TARTARO
(Tartaro).
Hali ya kushushwa hadhi kama ya mfungwa gerezani; malaika walioasi katika siku za Noa walitupwa katika hali hiyo.
Neno hilo linapatikana mara moja katika Maandiko kwenye 2 Petro 2:4. Mtume Petro anaandika hivi: “Hakika Mungu hakujizuia kuwaadhibu malaika waliofanya dhambi, bali aliwatupa ndani ya Tartaro, akiwaweka kwenye minyororo ya giza zito ili wawekwe akiba kwa ajili ya hukumu.” Usemi “aliwatupa ndani ya Tartaro” unatokana na kitenzi cha Kigiriki tar·ta·roʹo na hutia ndani neno “Tartaro.”
Andiko la Yuda 6 lenye maneno kama hayo linasema hivi: “Pia malaika ambao hawakubaki mahali pao pa kwanza bali waliacha makao yao yanayowafaa, amewafunga minyororo milele katika giza zito kwa ajili ya hukumu ya ile siku kuu.” Kwa kutaja wakati ambao malaika “waliacha makao yao yanayowafaa,” Petro anazungumzia “roho walio gerezani, ambao mwanzoni hawakuwa watiifu Mungu alipokuwa akingoja kwa subira katika siku za Noa, safina ilipokuwa ikijengwa.” (1Pe 3:19, 20) Hilo linalingana moja kwa moja na simulizi linalopatikana katika Mwanzo 6:1-4 kuhusu “wana wa Mungu wa kweli” walioacha makao yao mbinguni ili kuishi na wanawake kabla ya Gharika na kuzaa nao watoto, uzao ulijulikana kama Wanefili.—Tazama WANEFILI; WANA WA MUNGU.
Kulingana na maandiko hayo ni wazi kwamba Tartaro ni hali wala si eneo fulani hususa, ingawa Petro anasema kwamba viumbe hao wa roho waliokosa kutii wamewekwa kwenye “minyororo ya giza zito,” huku Paulo akisema kwamba wako katika “mahali pa kimbingu,” wakiwa watawala wa ulimwengu wa giza wakiwa majeshi ya roho waovu. (2Pe 2:4; Efe 6:10-12) Giza zito linalotajwa si ukosefu wa nuru halisi bali linatokana na viumbe hao kutokuwa na nuru ya Mungu kwa kuwa ni waasi na wametengwa kutoka katika familia yake, wakiwa na mtazamo wenye giza kuhusu tumaini lao la milele.
Hivyo, Tartaro si sawa na neno la Kiebrania Sheoli au Kigiriki Hadesi, maneno yanayomaanisha kaburi la wanadamu wote kwa ujumla. Hilo linathibitishwa na uhakika wa kwamba ingawa mtume Petro anasema Yesu Kristo aliwahubiria “roho walio gerezani,” alionyesha pia kwamba Yesu alifanya hivyo, si katika siku tatu alizokuwa amezikwa ndani ya Hadesi (Sheoli), bali baada ya kufufuliwa na kutoka Hadesi.—1Pe 3:18-20.
Vilevile, hali ya kushushwa hadhi inayoonyeshwa na Tartaro ni tofauti na “shimo refu lisilo na mwisho” (abiso) ambamo Shetani na roho wake waovu hatimaye watatupwa humo na kukaa kwa kipindi cha miaka elfu moja ya utawala wa Kristo. (Ufu 20:1-3) Ni wazi kwamba malaika waovu walitupwa ndani Tartaro katika “siku za Noa” (1Pe 3:20), lakini miaka 2,000 hivi baadaye tunasoma kwamba walimsihi Yesu “asiwaamuru waende katika shimo refu lisilo na mwisho.”—Lu 8:26-31; tazama ABISO.
Neno “Tartaro” lilitumiwa pia kabla ya Ukristo katika masimulizi ya hekaya za wapagani. Katika kitabu cha mashairi ya Ugiriki cha Homer (Iliad), Tartaro ya wapagani inaonyeshwa kuwa gereza lililo chini ya ardhi ‘lililo mbali chini ya Hadesi kama dunia ilivyo chini mbali na mbingu.’ Ndani ya gereza hilo, miungu wadogo, Cronus na roho wengine walifungwa. Kama tulivyoona, Tartaro inayotajwa katika Biblia si sehemu bali ni hali, hivyo si Tartaro inayotajwa katika masimulizi ya hekaya za Kigiriki. Hata hivyo, Tartaro inayotajwa katika hekaya hizo inaonekana kuwa mahali wanapoishi si binadamu bali viumbe wenye nguvu kuliko wanadamu. Hivyo, kuna ufanani fulani, Maandiko huonyesha kwamba Tartaro si gereza la roho za wanadamu (linganisha Mt 11:23) bali ni la roho waovu wenye nguvu waliomwasi Mungu.
Hali ya kushushwa hadhi kabisa inayowakilishwa na Tartaro ni wonyesho wa mapema wa kutupwa katika abiso kwa Shetani na roho wake waovu kabla ya kuanza kwa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo. Kisha, mwishoni mwa miaka elfu moja wataangamizwa kabisa katika “kifo cha pili.”—Mt 25:41; Ufu 20:1-3, 7-10, 14.