Elekeza Fikira Kwenye Neno la Kiunabii la Mungu!
Mambo Makuu Kutoka Petro ya Pili
NENO au ujumbe wa kiunabii wa Yehova, ni kama tamaa ing’aayo katika mahali pa giza, na Wakristo wa kweli wahitaji kwa uangalifu sana kulielekezea fikira zao. Hilo si jambo rahisi walimu bandia wanapojaribu kuendeleza uasi-imani. Lakini linawezekana kwa msaada wa kimungu. Na ni lazima tuambatane kwa imara na neno la Mungu ikiwa tutaokoka ile siku ya Yehova inayokaribia kasi.
Barua ya pili ya mtume Petro yenye pumzi ya Mungu yaweza kutusaidia kuelekeza fikira zetu kwenye neno la kiunabii la Mungu. Petro aliandika waraka huu labda kutoka Babuloni katika 64 W.K. hivi. Katika barua yake yeye atetea ukweli wa Mungu, aonya Wakristo wenzi juu ya kuja kwa siku ya Mungu kama mwivi, na asaidia wasomaji wake wasipotoshwe na kosa la watu wakaidi-sheria. Kwa kuwa siku ya Yehova inakaribia juu yetu, tunaweza kufaidika sana kutokana na maneno ya Petro yaliyoongozwa na Mungu.
Tumaini Katika Neno la Kiunabii
Sisi tulio Wakristo, tunahitaji kujitahidi ili tuonyeshe sifa za kimungu na ni lazima tuelekeze fikira kwenye neno la kiunabii. (1:1-21, NW) Ili kuepuka kuwa wasiotenda ama wasiozaa matunda, tunahitaji ‘kugawa kwenye imani yetu nguvu ya wema, maarifa, kujidhibiti, uvumilivu, ujitoaji kimungu, shauku ya kidugu, na upendo.’ Petro alipomwona Yesu akigeuka sura na kusikia Mungu akinena juu ya Kristo katika kipindi kile, neno la kiunabii lilihakikishwa zaidi. (Marko 9:1-8) Tunahitaji kuelekeza fikira kwenye neno hilo lenye kupuliziwa kimungu.
Jilindeni Dhidi ya Waasi-Imani
Kwa kuelekeza fikira kwa uangalifu sana kwenye neno la kiunabii la Mungu, tunaweza kujilinda dhidi ya waasi-imani na wafisadi wengine mmoja mmoja. (2:1-22) Petro alionya kwamba walimu bandia wangeingia kundini. Hata hivyo, Yehova angetekeleza hukumu nzito dhidi ya waasi-imani hawa, hata kama alivyohukumu wale malaika wasiotii, ulimwengu uliokana Mungu wa siku ya Noa, na majiji ya Sodoma na Gomora. Hao walimu bandia huchukia mamlaka iliyotoka kwa Mungu na hushawishi walio dhaifu kujiunga nao katika kutenda mabaya. Ingalikuwa bora kwa waasi-imani hawa kutokujua “njia ya haki, kuliko kuijua, kisha kuiacha ile amri takatifu waliyopewa.”
Siku ya Yehova Inakuja!
Tukiwa wale wanaoelekeza fikira kwenye neno la kiunabii katika siku za mwisho hizi, ni lazima tusijiruhusu kuvutwa na wadhihaki wanaofanyia mzaha ujumbe juu ya kuwapo kwa Kristo. (3:1-18, HNWW) Wao husahau ya kwamba yule Mungu ambaye amekusudia kuharibu mfumo huu wa mambo aliuharibu ule ulimwengu wa kabla ya Gharika. Saburi ya Yehova haipasi kuonwa kuwa upolepole, kwa kuwa ataka watu watubu. Mfumo huu utaharibiwa katika “Siku ile ya Mungu [Yehova, NW]” na mahali pao patachukuliwa na “mbingu mpya na dunia mpya ambayo imejaa uadilifu.” Kwa hiyo, tunapaswa kufanya yote tuwezavyo tuwe ‘safi kabisa, bila hatia mbele ya Mungu, na kuwa na amani naye.’ Badala ya kuongozwa vibaya na walimu bandia, na tukue katika maarifa ya Yesu Kristo.
Acheni tuingize maneno ya Petro moyoni. Usishindwe kamwe kujilinda dhidi ya walimu bandia. Ishi ukiwa na ufahamu wa kwamba siku ya Yehova inakuja karibuni. Na sikuzote elekeza fikira kwenye neno la kiunabii la Mungu.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 31]
Kutupwa Katika Tartaro: Yehova “hakuwaachilia malaika waliokosa, bali aliwatupa shimoni [Tartaro, NW], akawatia katika vifungo vya giza, walindwe hata ije hukumu.” (2 Petro 2:4) Hiyo si ile Tartaro ya kihekaya inayofananishwa katika Iliad ya Homer kuwa mahali chini ya ardhi ambapo miungu bandia wadogo, Kronosi na roho wengine wa Titani, walifungwa. Tartaro ya Kibiblia ni ile hali ya kushushwa iliyo kama kufungwa ambamo Mungu aliwatupa malaika wasiotii katika siku ya Noa. (Mwanzo 6:1-8; 1 Petro 3:19, 20; Yuda 6) ‘Giza zito’ latokea kwa kukataliwa kwao na Mungu kutoka kwenye mwangaza wa kiroho wakiwa waliotupwa kutoka familia yake. Wakiwa wale waliowekwa kwa ajili ya hukumu yake nzito, wana mtazamo wenye giza tu. Tartaro ni kitangulizi tu cha kutiwa katika abiso kwa Shetani na roho waovu wake kabla ya Utawala wa Yesu wa Miaka Elfu. Uharibifu wao utatukia baada ya Utawala wa Yesu wa Mileani.—Mathayo 25:41; Ufunuo 20:1-3, 7-10, 14.
[Picha]
Zeu aliwarusha miungu wadogo katika Tartaro ya kihekaya
[Hisani]
National Archaeological Museum, Athens, Greece