Angalia Unabii kwa Makini
“Sisi tunalo neno la unabii lililohakikishwa zaidi; nanyi mnafanya vizuri katika kuliangalia kama taa inayong’aa mahali penye giza.”—2 PETRO 1:19.
1. Ni mambo gani ya kustaajabisha ambayo Yesu alifunua wazi, kulingana na Mathayo 16:21-28?
HUDUMA ya Yesu ya kidunia ilikuwa ikikaribia kumalizika. Akiwa karibu na Filipi ya Kaisaria, kaskazini ya Galilaya, huyu “Mwana wa Adamu” alikuwa amewapasha wanafunzi wake habari za kwamba kifo chake kilikuwa kikikaribia na kwamba angerudi katika utukufu wa Baba yake. Halafu akawaambia hivi: “Amin, nawaambieni, Pana watu katika hawa wasimamao hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata watakapomwona Mwana wa Adamu akija katika ufalme wake.” (Mathayo 16:21-28) Hilo lingeweza kuwa na maana gani?
2. (a) Maneno ya Yesu yalitimizwaje katika njozi iliyoonwa na Petro, Yakobo na Yohana? (b) Huo ulikuwa unabii wa tukio gani lenye utukufu?
2 Karibu siku sita baadaye, Yesu alimchukua Petro, Yakobo na Yohana wakapanda mlima mrefu, labda Hermoni wa ule mfululizo wa vilima vilivyoungana vinavyoelekeana na Lebanoni. Hapo palitukia jambo la kustaajabisha! Yesu aligeuzwa sura wakiwa wanamtazama, akawa na sura yenye mng’ao wa kushangaza. Katika njozi, Musa na Eliya walionekana wakiongea naye. Kwa sababu gani Musa na Eliya? Kwa kufaa, Yesu anatambulishwa wazi katika Maandiko kuwa “Nabii yule” aliyetangulia kufananishwa na Musa. Na kazi inayofanana na ile ya Eliya inahusianishwa sana na Ufalme wa Mungu ambamo Yesu anatawala. (Matendo 3:22, 23, NW; Kumbukumbu la Torati 18:15-19; Malaki 4:5, UV ) Basi, ilifaa wakaonekana hapo wakiwa pamoja na Yesu katika njozi hiyo ya kuja kwake katika fahari ya utukufu wa Ufalme wake wa wakati ujao.—Mathayo 17:1-5.
3. Ni maneno gani ya Yehova yaliyoukazia umaana wa njozi hiyo?
3 Pia, ilifaa sauti ya Yehova ikasikiwa kutoka mbinguni, ikisema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” Naye Mungu akaongeza maneno haya: “Msikieni [msikilizeni, NW ] yeye.”
4. (a) Kwa sababu gani tukio hilo linapasa kutuvuta sisi leo? (b) Andiko la 2 Petro 1:19 linamaanisha ‘neno la unabii’ gani?
4 Tukio hilo la kuogopesha liliwaacha mitume wakiwa na maoni gani? Linapasa kuwa na matokeo gani juu yetu leo? Karibu miaka 30 baadaye, bado Petro aliweza kuikumbuka tamasha hiyo pamoja na mng’ao wayo wote. “Kwa hiyo,” yeye akasema, “sisi tunalo neno la unabii lililohakikishwa zaidi.” “Neno la unabii gani”? Ni ule unabii mbalimbali, kama Danieli 7:13, 14, ambao sasa ulihakikishwa kuwa kweli na lile tukio la kugeuka sura—unabii mbalimbali juu ya kuja kwa Mwana wa Adamu katika utukufu wa mamlaka ya Ufalme!—2 Petro 1:16-19; ona pia Isaya 9:6, 7.
5. Ni maongezeo gani ya maana yaliyofanywa kwa “neno” hilo?
5 Kufikia wakati huo “neno la unabii” lilikuwa limekwisha kutia ndani unabii mbalimbali uliotolewa na Yesu Kristo mwenyewe pia. Kati ya unabii huo ulikuwako ule unabii wa Ufalme wake juu ya “umalizio wa mfumo wa mambo,” ambao pia ulimwonyesha “Mwana wa mtu akija juu ya mawingu ya mbingu pamoja na mamlaka na utukufu mkuu” katika wakati wa taabu kubwa ya ulimwengu ambayo haijapata kuwa na kifano. (Mathayo 24:3-14, 30, 31, NW ) Baadaye, “neno la unabii” lingetia ndani unabii mbalimbali wa Ufalme wenye mkazo mwingi ambao Yesu Kristo aliyetukuzwa alimfunulia mtume Yohana mzee, kama ule ulioandikwa kwenye Ufunuo 1:12-16; 5:5-10; 11:15-17 na 14:14,15.
Angalia kwa Makini!
6. Kwa sababu gani neno hilo la unabii linapasa kuwa na mkazo mkubwa zaidi kwetu leo?
6 Ikiwa Petro na wenzake walivutwa sana na njozi hiyo ya unabii, yapasa kutuvuta sisi leo kwa njia kubwa zaidi! Kwa kuwa sasa Mwana wa Adamu amekwisha kufika katika utukufu wake, akalie kiti chake cha Ufalme chenye utukufu katika mbingu, kwa uhakika huu ndio wakati wa ‘kumsikiliza yeye’! Inatufaa kabisa tuliangalie neno la unabii, “kama taa inayong’aa mahali penye giza,” tuliruhusu limulike mioyo yetu.—2 Wakorintho 4:6.
7. (a) Paulo anakaziaje umaana wa unabii? (b) Ni kwa sababu gani, hasa, inatupasa sisi tuutii leo?
7 Mtume Paulo pia alikazia uhitaji wa kuingiza ujumbe wa unabii ndani ya mioyo yetu. Aliwaandikia Wakristo Waebrania kwamba “zamani za kale [Mungu] alinena pindi nyingi na kwa njia nyingi na babu [zao] kupitia manabii,” lakini ‘kwenye mwisho wa zile siku (za mfumo wa mambo ya Kiyahudi)’ alisema nao kupitia Mwana. Neno hilo la unabii lililosemwa na Yesu lilikuwa na umaana mkubwa sana. Kama lingetiiwa, lingeongoza watu kwenye wokovu. Paulo alisema, “Ndiyo sababu ni lazima kwetu tuyaangalie zaidi kuliko kawaida mambo yaliyosikiwa na sisi.” (Waebrania 1:1-4; 2:1, NW ) Sasa, kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo [wa ulimwengu wote],” tuna sababu kubwa zaidi ya kusikiliza maneno ya Yesu.—Mathayo 24:3, 35, NW; linganisha Isaya 55:6-11.
8. Neno la unabii linapasa kutuchocheaje, na faida itakuwa nini?
8 Na ikaziwe kwamba kuangalia kwetu kwa makini lile neno la unabii hakupasi kuwa na kusudi la kujipatia maarifa tu. Sivyo kabisa! Neno hilo linapasa lituchochee tutende kulingana na maarifa hayo, litutendeshe mapenzi ya Mungu, na hasa sasa, “katika sehemu ya mwisho ya zile siku.” (Isaya 2:2, 3, NW ) Akimwambia Yehova Mungu, mtunga zaburi anasema hivi: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.” Neno hilo linatuwezesha tuendelee kutembea katika nuru ya ukweli na katika uhusiano wa kindani pamoja na Mungu wetu. Linatulinda tusipeperuke kamwe tuurudie ulimwengu wa Shetani. (Zaburi 119:105; Ayubu 29:3,4) Ili tupate faida ya huduma kutokana na neno hilo la unabii, ni lazima tusitawishe hali yenye kina kirefu ya kuipenda Biblia, kuingiza ujumbe wote wa Biblia ndani sana ya mioyo yetu. Hivyo sikuzote tutachochewa kufanya mapenzi ya Mungu na kuendelea kujiweka katika upendo wake.—Marko 12:29-31; 1 Yohana 4:16; Yuda 20, 21.
Violezo vya Unabii
9. (a) Kwa sababu gani tunasema kwamba kumbukumbu la maandishi ya Biblia si historia iliyokwisha kazi? (b) Ni siku gani ya kisasi inayofananishwa humo?
9 Biblia inaeleza kwa urefu upotovu wa Israeli wa kale. Na sababu ni nini? Ili “kuwa onyo kwa sisi ambao miisho ya mifumo ya mambo imefika juu yetu.” Jambo hilo linapasa kukaza ndani yetu woga wa kimungu, tusije tukakuza “moyo mbovu wa kutokuamini, kwa kujitenga na Mungu aliye hai.” (1 Wakorintho 10:11, NW; Waebrania 3:12; Ayubu 28:28, UV ) Kumbukumbu la maandishi ya Biblia si historia iliyokwisha kazi! Lina violezo vya unabii na maamuzi rasmi yanayoonyesha kwamba Yehova Mungu atalipa kisasi tena lakini kwa kipimo kikubwa zaidi ya vile alivyofanya siku za Israeli waasi-imani. Adhabu ya Mungu juu ya taifa hilo lenye kurudi nyuma katika mwaka wa 607 K.W.K., na tena katika mwaka wa 70 W.K., ni mfano wa namna hasira yake iliyo kali sana itakavyomwagwa hivi karibuni juu ya Jumuiya ya Wakristo hasa. Inafaa tulitii neno hilo la unabii! —Yeremia 7:28, 32-34; Mathayo 24:3-22.
10, 11. (a) Ni ulinganifu gani unaotusaidia tufahamu kwamba kweli hizi ndizo “siku za mwisho”? (b) Ni kwa njia gani, hasa, madhehebu za Jumuiya ya Wakristo zimetimiza unabii huu?
10 Ni jambo lisiloweza kufanyiwa ubishi kwamba tumekwisha kuingia katika “siku za mwisho” za mfumo wa Shetani wa utawala wa ulimwengu. Ukilinganisha hali ya ulimwengu leo na maneno ya mtume Paulo kwenye 2 Timotheo 3:1-5, 13 utaufahamu waziwazi uhakika huo. Na hasa kati ya madhehebu zilizo na mvurugo za dini za Jumuiya ya Wakristo ndiko tunakoona watu “wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake.” Wao hawana ujumbe wa kweli wa wokovu.—Linganisha Mathayo 7:21-23.
11 Madhehebu zile nyingi zilizo katika Jumuiya ya Wakristo zinapatana sana na maelezo yaliyotolewa na nabii wa Yehova, wakati aliposema hivi: “Watu wangu hawa wametenda maovu mawili; wameniacha mimi [Yehova Mungu], niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavujayo, yasiyoweza kuweka maji.” (Yeremia 2:13) Ni kweli kama nini kwamba madhehebu za Jumuiya ya Wakristo zimemwacha Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu na kanuni za uadilifu zilizoonyeshwa wazi katika Neno lake! Hata yanachukia kutaja jina lake. Badala yake, yamechimba “mabirika yavujayo,” wakageukia falsafa na makisio ya wanadamu na kufanya siasa pamoja na ulimwengu. Katika nchi nyingi makanisa yazo yanafifia kwa kukosa kuungwa mkono kwa sababu watu hawapati ndani ya makanisa hayo maji ya ukweli yenye kuburudisha. Lakini, pana tofauti kati ya wale wanaotumikia Yehova kwa uaminifu kwa sababu wana wingi wa burudisho la kiroho.—Isaya 55:1, 2; 65:13,14.
Yanayosemwa na Viongozi wa Ulimwengu
12. Kwa sababu gani ni kazi bure kuwatumaini viongozi wa kibinadamu kwa wokovu?
12 Si Biblia tu inayotoa onyo la uharibifu wa ulimwengu. Katibu-mkuu wa sasa wa Umoja wa Mataifa ametangaza kwamba kwa mara ya kwanza katika historia ya kibinadamu sisi sasa “tuko kati ya ukingo mwembamba wa kupata maangamizi makubwa sana na wa kupata wokovu.” Katika taarifa ya ukumbusho iliyoandikwa huko nyuma mwaka wa 1958, Harry Truman aliyekuwa Rais wa United States (Amerika) alisema hivi: “Sasa sisi tumeelekewa na uharibifu wa jumla. . . . Uharibifu huo umekaribia sana isipokuwa kama viongozi wakuu wa ulimwengu watauzuia.” Lakini katika muda wa miaka 25 iliyopita, je! hao “viongozi wakuu” wamechukua hatua ya kuzuia uharibifu wa jumla? Badala ya kufanya hivyo, sasa wanaendelea kutumia dola zaidi ya milioni moja (shilingi zaidi ya milioni 13) kwa dakika moja kutengeneza silaha zilizo za kiibilisi zaidi za kuangamiza watu. Habari za “viongozi wakuu” hao ndizo zilizoandikwa hivi na mtunga zaburi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.”—Zaburi 146:3.
13, 14. (a) Viongozi wa kidini wameelekeza watu kwenye tumaini gani la uongo? (b) Kulingana na Isaya, tumaini lililo la kweli kweli ni tumaini gani?
13 Hali hiyo yenye msiba ni jambo lisiloweza kuondolewa na mataifa. Hata ule unaoitwa Umoja wa Mataifa kwa jina umekuwa makao ya kufanyia magombano ya wafuasi wao badala ya kuwa shirika la kuongezea amani na usalama. Papa Paulo wa 6 na hata Papa John Paul wa Pili alienda kwenye makao ya Umoja wa Mataifa kwa kufanyiwa sherehe zenye utukuzo mwingi. Wao walilitangaza baraza hilo kuwa ‘tumaini la mwisho la upatani na amani’ kwa wanadamu. Lakini je! ndivyo lilivyo?
14 Katika neno lake la unabii, Yehova anataja lile tumaini lililo la kweli kweli. Alimwagiza Isaya atabiri kuzaliwa kwa mwana anayekuwa “Mwana-Mfalme wa Amani.” Huyo ni Kristo Yesu, aliyetangulia kufananishwa na Mfalme Daudi wa kale. Unabii unaendelea kusema hivi juu ya Yesu: “Kwa wingi wa utawala huo wa mwana-mfalme na kwa amani hakutakuwako mwisho, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuusimamisha kwa imara na kuuendeleza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanza sasa na kuendelea na mpaka wakati usiojulikana. Ile ile juhudi ya Yehova wa majeshi itafanya hili.” (Isaya 9:6, 7, NW ) Lakini ni kwa njia gani juhudi ya Yehova italeta ‘amani isiyo na mwisho’?
“Ufalme wa Mungu U Karibu”
15. Yesu alikaziaje tumaini la Ufalme?
15 Yeye aliye mkuu kuliko Daudi, Yesu Kristo, alitabiri juu ya vita vya jumla na taabu kuu ambazo zingetokezwa na vita hivyo vya karne yetu ya 20. Aliyatabiri matukio ya kuogofya, dhiki ya mataifa, tazamio lenye kuogopesha la mambo yanayokuja juu ya dunia. Halafu alisema: “Basi mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia. . . . Mwonapo mambo hayo yanaanza kutokea, tambueni ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.” (Luka 21:10,11, 25-31) Ufalme wa Mungu! Huo ndio utatuzi wa matatizo ya wanadamu. Muda wote wa miaka iliyopita, je! sisi hatukuwa tukisali Ufalme huo uje? Hivyo ndivyo Yesu alivyotufundisha kufanya, akisema: “Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.
16. Ni katika maana gani Ufalme wa Mungu “umekaribia”?
16 Neno la unabii linatuambia kwamba sasa “ufalme wa Mungu u karibu.” Lakini katika maana gani? Danieli nabii wa Mungu anaeleza. Baada ya kueleza habari za falme, au serikali, za wanadamu zenye kuwako “wakati wa mwisho,” yeye anasema hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Danieli 12:4; 2:44) Kwa hiyo dunia haitateketezwa na maangamizi makuu ya silaha za nyukilia zenye kuharibu wanadamu wote walio hai. Bali, Ufalme wa Mungu ndio utakaofagia watu na mataifa yenye uovu yatoke usoni pa dunia yetu, ili kutayarisha serikali ya kudumu ya duniani pote yenye kuongozwa na “Mwana-Mfalme wa Amani.”—Isaya 9:6, NW.
Kisasi cha Mungu Kinalipwa
17. Ile kelele yenye kusema “Kuna amani na slama”! itakuwa kiishara cha jambo gani?
17 Unabii mbalimbali wa Biblia unaelekeza fikira kwenye siku zetu. Unaonyesha mambo yatakayotokea baada ya muda mfupi tu. “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Neno la unabii linaonyesha kile kinachoitwa ‘tumaini la mwisho kwa amani’ ya wanadamu ati, yaani Umoja wa Mataifa, kuwa mnyama-mwitu mwenye rangi nyekundu. He, huenda shirika hilo likatunga kwa uongo namna fulani ya amani ya wasiwasi tu kisha lishiriki kupiga kelele yenye kusema “Kuna amani na salama”!-—kupatana na mkataba walo na kwa utimizo wa unabii ulio kwenye 1 Wathesalonike 5:3. Lakini hapo ndipo Yehova atatumia maarifa ya kuziongoza “pembe” za kijeshi za Umoja wa Mataifa ziteketeze dini ya uongo, ‘Babeli Mkuu,’ ambayo madhehebu za Jumuiya ya Wakristo ndizo sehemu yake yenye malawama mengi zaidi. Halafu, wakati “pembe” hizo zitakapogeuka zipigane na Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, kwa kushambulia mashahidi wapenda amani wa Yehova, upanga wa Mungu wenye kuua utayashukia mataifa hayo na majeshi yao, “wala hakika hawataokolewa.”—Ufunuo 17:3-6, 12-17.
18. (a) Kulingana na neno la unabii, itakuwaje kwa yale mataifa yanayoshambulia watu wa Mungu? (b) Mwishoni, ni kwa njia gani Mungu atamaliza mambo?
18 Silaha za nyukilia za mataifa hazitawalinda kwa njia yo yote wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi,” lile pigano la Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Ikiwa silaha hizo zilizotengenezwa ili kumaliza halaiki ya watu kwa njia ya kuogopesha sana zitatumiwa kwa kadiri fulani, zitasaidia tu kufanya mataifa yaangamizane. Katika siku za Mfalme Yehoshafati wa Yuda aliyekuwa mwema, makundi ya adui yalisonga mbele yashambulie watu wa Mungu walioonekana kama kwamba hawakuwa na ulinzi. Lakini kupitia nabii wake, Yehova aliwaambia hivi: “Msiogope, wala msifadhaike kwa ajili ya jeshi kubwa hili; kwani vita si yenu bali ni ya Mungu.” Yehova aliwatega mtego adui hao, hata “wakajitia kuharibu kila mtu mwenziwe,” mpaka wote wakaangamizwa kabisa. (2 Mambo ya Nyakati 20:15-23; linganisha pia Waamuzi 7:22; Ezekieli 38:21-23; Zekaria 14:13.) Matokeo ya mwisho yataongozwa na ‘Mfalme wa wafalme’ aliyewekwa na Mungu pamoja na majeshi yake ya malaika, ambao watawamaliza adui zake fyu, hata yule wa mwisho atakayebaki akitanga-tanga bila kujua kwa kwenda. Pia Shetani na mashetani wake watafungwa katika shimo refu lisilo na mwisho.—Ufunuo 19:11-16, 21; 20:1-3.
19. (a) Ni somo gani tunalopaswa kuchukua kutokana na Mwanzo 18:23-33? (b) Ni nani peke yao watakaoachiliwa wakati wa ile “dhiki kubwa”?
19 Lakini, je! si jambo la kugutusha kwamba Yehova atauharibu mfumo huu mzima wa ulimwengu, kisha isirudishwe hata sehemu moja ya mfumo wenyewe? Labda wengine wanajisikia kama vile Abrahamu alivyojisikia juu ya Sodoma na Gomora, kwamba ikiwa watu waadilifu 50 tu, au 45, au 30, au 20, au hata 10 wangeweza kupatikana huko katika ulimwengu, basi “Mhukumu ulimwengu wote” hapaswi kuufagilia mbali ulimwengu wote. (Mwanzo 18:23-33) Lakini neno la unabii linaeleza wazi kwamba ulimwengu wa Shetani umejawa na udhalimu juu chini na kwamba utakung’utwa fyu! (Yeremia 25:31-33; Sefania 3:8) Mwili wa pekee utakaookoka hiyo “dhiki kubwa” utakuwa, kama Yesu mwenyewe alivyosema, ule “mwili” ambao ni wapakwa mafuta walio wakf aliowachagua na pia wenzi wao wenye mfano wa kondoo. Hakuna watu wengine wanaohesabiwa kuwa waadilifu machoni pa Yehova.—Mathayo 24:21,22, NW; 25:31-33,46; Yohana 10:16; Habakuki 3:1, 2,12,13, UV.
20. Ni lazima sisi Mashahidi wa Yehova tuwe macho kufanya nini wakati wa siku hizi za mwisho kabisa?
20 Neno la unabii la Yehova ‘linafanya haraka’ likienda likapate utimizo kamili, Inatupasa sisi tuendelee ‘kulingojea.’ (Habakuki 2:3) Basi, acheni sisi Mashahidi wa Yehova tutangaze kwa ujasiri “siku ya kisasi cha Mungu wetu” na tuwe ‘wasema-wazi’ kama mitume wa Yesu katika kuwafariji waombolezaji kwa habari njema za wokovu, (Isaya 61:1, 2, UV; Matendo 4:8-13, 18-20, NW ) Acheni tuwe macho, pia katika kutii maneno haya ya Yesu: “Jiangalieni ili mioyo yenu isije ikalemewa na kula kupita kiasi na kunywa kupita kiasi na masumbufu ya maisha, na kwa ghafula siku ile iwafyatukie kama mtego. Kwa maana itawajilia wote wale wanaokaa juu ya uso wa dunia. Endeleeni kukesha, basi, wakati wote mkifanya dua ili ninyi mpate kufaulu katika kuyakimbia mambo haya ambayo yamekusudiwa yatukie, na katika kusimama mbele ya Mwana wa mtu.”—Luka 21:34-36, NW.
Wewe Ungejibuje?
□Tunajifunza somo gani kutokana na 2 Petro 1:16-19 na kutokana na maandiko yanayohusiana na hilo?
□ Tunapata faida gani kwa ‘kuliangalia neno la unabii’?
□ Ni nini kinachotabiriwa kuwa karibu, na kwa sababu gani haitupasi kuogopa?
□ “Siku ya kisasi” cha Mungu inapokaribia, inatupasa tuwe tunafanya nini?
[Picha katika ukurasa wa 13]
“Vita si yenu bali ni ya Mungu”