Sura 5
Mifano Yenye Kutegemeka Inayoonyesha Utakavyokuwa Wakati Ujao wa Wanadamu
1. Ni kwa nini nyakati zote unabii wa Biblia unathibitika kuwa sahihi?
TUNA sababu nzuri za kuwa na hakika ya mambo ambayo Biblia inatuambia juu ya wakati ujao. Mambo yake ya unabii hayategemei makisio ya wanadamu ambao wamechunguza mielekeo fulani kisha wakatoa matabiri. “Hakuna unabii wa Andiko unaotokana na fasiri yo yote ya mtu binafsi. Kwa maana unabii haukuletwa wakati wo wote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu wakati walipoongozwa kwa roho takatifu.” (2 Petro 1:20, 21, New World Translation) Kwa sababu ya hilo, unabii wa Biblia umethibitika kuwa sahihi katika kila jambo.
2. Toa mifano ya mambo ya unabii juu ya mambo ya ulimwengu.
2 Ilitabiri juu ya kutokea na kuanguka kwa serikali za ulimwengu kwa kuzitaja majina—Babuloni, Umedi na Uajemi na Ugiriki. Mapema karibu karne mbili, ilitangaza jinsi Babuloni ungeanguka na ikataja jina la mwenye kuushinda. Hilo lilitimizwa katika mambo yote. Ilitabiri kwamba mji wa Babuloni mwishowe ungekuwa ukiwa, usipate kukaliwa tena kamwe. Hali hiyo inaendelea mpaka wakati wetu. (Danieli 8:3-8, 20-22; Isaya 44:27–45:2; 13:1, 17-20) Mataifa mengine yasiyotajwa majina katika Biblia yalisimuliwa mapema waziwazi sana hata watu wenye kujua mambo wanaweza kuyatambua vyepesi.
3. Je! kuna mambo ya unabii yasiyoelezwa kwa namna ya matabiri?
3 Lakini, na ifahamike kwamba kuna habari nyingi za unabii kuliko moja katika Biblia. Tumekwisha ona hilo kuhusiana na miujiza ya Yesu, iliyokuwa ishara za ajabu za mambo ambayo wanadamu wataona chini ya Ufalme wa Mungu. Vifungu vingine vya Maandiko visivyotumia usemi unaoonekana kama utabiri vina mambo ya unabii pia.
MIFANO YA UNABII YENYE KUVUTIA SANA
4. Tunawekwaje tayari tuone maana ya kiunabii ya Torati ya Musa?
4 Kwa mfano, kitabu cha Biblia cha Waebrania, kinafungua macho yetu kwenye umaana wa kiunabii wa mambo ambayo msomaji wa vivi hivi tu huenda akayaona kuwa historia tu. Kinafunua kwamba “torati [ya Musa ina] kivuli cha mema yatakayokuwa.”—Waebrania 10:1.
5. Ni nini kinachoonyesha kwamba huenda vitu vikatoa mfano wa jambo lililo kubwa zaidi?
5 Mara nyingine vitu vilitumiwa viwe mifano ya unabii. Kwa mfano, kwa habari ya ile hema takatifu iliyojengwa na Musa kwa mwelekezo wa Yehova, pamoja na utumishi mbalimbali uliofanywa humo, mwandikaji aliyeongozwa na Mungu wa barua kwa Waebrania anaeleza kwamba ilikuwa “mfano na kivuli cha mambo ya mbinguni.” Ilifananisha hekalu kuu la kiroho la Yehova, ambalo Patakatifu Zaidi Sana pako mbinguni. Hivyo, “Kristo akiisha kuja, aliye kuhani mkuu wa mambo mema yatakayokuwapo, kwa hema iliyo kubwa na kamilifu zaidi, isiyofanyika kwa mikono, maana yake, isiyo ya ulimwengu huu, wala si kwa damu ya mbuzi na ndama, bali kwa damu yake mwenyewe aliingia mara moja tu katika Patakatifu, akiisha kupata ukombozi wa milele [kwa ajili yetu]. . . . Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi; bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu.” (Waebrania 8:1-5; 9:1-14, 24-28) Faida kubwa zinawajia Wakristo kutoka kwa mambo halisi ya kiroho yanayosimuliwa hapa, na kuthaminiwa kwa mambo hayo kumepasa kuonekane katika mwendo wetu wa maisha.—Waebrania 9:14; 10:19-29; 13:11-16.
6. Watu wanatoa maana gani ya unabii katika (a) Wagalatia 4:21-31? (b) Mathayo 17:10-13?
6 Pia watu wanaotajwa katika Maandiko walikuwa mifano ya unabii. Katika Wagalatia 4:21-31 mfano wa hilo wenye masimulizi marefu umeelezwa kwa habari ya Sara, mke wa Abrahamu, (ambaye anasemwa kuwa analingana na “Yerusalemu wa juu”) na Hajiri mjakazi (anayeshirikishwa na “Yerusalemu wa sasa”) na watoto wao. Katika habari nyingine Yesu alisaidia wanafunzi wake wafahamu kwamba nabii Eliya alikuwa mfano wa Yohana Mbatizaji, ambaye, kama Eliya, alikuwa asiyeogopa kufichua mazoea ya kidini yenye udanganyifu.—Mathayo 17:10-13.
7. Ni kwa njia gani Yesu Kristo alifananishwa na (a) Sulemani? (b) Melkizedeki?
7 Sulemani, mwenye sifa sana kwa sababu ya hekima yake na ufanisi na amani ya utawala wake, alikuwa mfano wa kufaa wa Yesu Kristo. (1 Wafalme 3:28; 4:25; Luka 11:31; Wakolosai 2:3) Ijapokuwa masimulizi yaliyo katika kitabu cha Mwanzo juu ya kukutana kwa Abrahamu na Melkizedeki ni mafupi, Zaburi 110:1-4 inaonyesha kwamba hayo, pia, yamejaa maana, kwa sababu Masihi angekuwa “kuhani hata milele, kwa mfano wa Melkizedeki,” yaani, angepokea ukuhani wake kwa kuwekwa moja kwa moja na Mungu wala si kwa sababu ya jamaa ambayo katika hiyo angezaliwa. Baadaye, barua kwa Waebrania inaeleza zaidi hilo na inashirikisha uthamini wa kweli hizo na kukomaa kwa Kikristo, sifa ya maana kwa wale wanaotaka kumpendeza Mungu.—Waebrania 5:10-14; 7:1-17.
8. (a) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba mambo yanayowapata watu maishani yanaweza kuwa ya unabii? (b) Je! ni lazima kila jambo la hayo liwe mfano wa kitu fulani katika utimizo?
8 Ni wazi kwamba mifano ya kiunabii inahusu mambo mengi kuliko cheo tu cha watu. Inatia ndani pia mambo yanayowapata watu maishani. Pindi moja viongozi wa kidini walipoonyesha kutoamini kwao, Yesu aliwaambia: “Kizazi kibaya na chenye uzini kinatafuta alama, lakini hakitapewa alama, ila alama ya Yona nabii; kwani kama Yona alivyokuwa siku tatu muchana na usiku katika tumbo la samaki mukubwa, vivyo hivyo Mwana wa watu atakuwa siku tatu muchana na usiku katika moyo wa inchi.” (Mathayo 12:38-40, Zaïre Swahili Bible; Yona 1:17; 2:10) Ingawa hivyo, Yesu hakusema kila jambo katika maisha ya Yona lilifananisha yale ambayo yangempata yeye mwenyewe. Alipopewa mgawo na Yehova, Yesu hakutoroka, kama Yona alivyokuwa amejaribu kukimbilia Tarshishi. Lakini kama Yesu alivyoonyesha, yaliyompata Yona katika tumbo la samaki mkubwa yalitiwa katika maandishi ya Biblia kwa sababu yalitumika kutoa maelezo ya kiunabii juu ya kifo na ufufuo wa Yesu mwenyewe.—Mathayo 16:4, 21.
9. (a) Ni mambo gani ya unabii ambayo Yesu alieleza katika vipindi vya historia viwili? (b) Kwa kuongozwa na Mungu, Petro alitaja mambo gani zaidi yenye maana?
9 Pia vipindi vya historia fulani vinatoa mifano ya kiunabii yenye kutuvutia sana. Alipokuwa akisema juu ya wakati wenye kutangulia kufunuliwa kwake mwenyewe katika mamlaka ya Ufalme, Yesu aliulinganisha na vipindi vingine viwili wakati hukumu ilipotekelezwa juu ya watu waovu. Alisema juu ya “siku za Noa” na “siku za Loti” kuwa zenye maana, hasa zikikazia jinsi wakati huo watu walivyokuwa na shughuli nyingi sana za mambo ya kila siku ya maisha. Alituomba sana tuchukue hatua ya haraka na tusirudi nyuma kwa kutamani sana vitu vilivyoachwa nyuma, kama alivyokuwa amefanya mkeye Loti. (Luka 17:26-32, Zaïre Swahili Bible) Mambo zaidi yenye maana yanatajwa katika barua ya pili ya Petro iliyoongozwa kwa roho ya Mungu. Kutokutii kwa malaika kabla ya Gharika kunatajwa, halafu utendaji wa Noa wa kuhubiri, kusumbuka kwa Loti kwa sababu ya maisha ya anasa yenye kuvunja sheria ya watu wa Sodoma, uhakika wa kwamba kukatiliwa mbali kwa waovu kwa wakati wake Mungu kulikuwa kukiweka mfano wa mambo yatakayokuja, na ule ushahidi wa kwamba Mungu anaweza kuokoa watumishi wake waaminifu, na bila shaka atawaokoa.—2 Petro 2:4-9.
10. Kwa kulinganisha maneno ya Yeremia na ya Ufunuo, onyesha kwamba mambo ya unabii yanayotimizwa yaweza kuwa na ubora zaidi wa unabii?
10 Mambo ya unabii yanapotimizwa, haina maana kwamba sasa yanakuwa historia tu. Mara nyingi taarifa ya mapema ya mambo yaliyopasa kutukia na jinsi yalivyotimizwa ni unabii wa matukio yaliyo makubwa hata zaidi ya wakati ujao. Hilo liko hivyo kwa habari ya mambo yaliyoandikwa juu ya Babuloni wa kale, milki ambayo kwa kutokeza ilikuwa ya kidini na ambayo uvutano wayo bado unaonekana kuzunguka ulimwengu wakati wetu. Ijapokuwa Babuloni uliangushwa na Wamedi na Waajemi mwaka wa 539 K.W.K., kitabu cha Ufunuo, kilichoandikwa mwishoni mwa karne ya kwanza W.K., kinatumia usemi wa nabii Yeremia na kinaelekeza bado kwenye matumizi ya wakati ujao wa mambo ya unabii, kuhusiana na Babuloni Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo. Ili uone mifano ya hilo, linganisha Ufunuo 18:4 na Yeremia 51:6, 45; Ufunuo 17:1, 15 na 16:12 na Yeremia 51:13 na 50:38; Ufunuo 18:21 na Yeremia 51:63, 64.
11. Kushughulika kwa Yehova na falme za Waisraeli waasi na Yuda zilipokosa imani, kuna maana gani ya kiunabii? Kwa nini?
11 Kwa jinsi kama hiyo, kushughulika kwa Yehova na ufalme wa Israeli wa makabila kumi na kushughulika kwake na wafalme na makuhani wa ufalme wa Yuda wa makabila mawili ni jambo la unabii. Mambo yote hayo ya unabii yaliyohusu falme hizo za kale na yalivyotimizwa, yakawekwa katika Maandiko, yanatoa picha iliyo wazi sana ya jinsi Mungu atakavyoshughulika na Jumuiya ya Wakristo ya siku hizi, inayojidai pia kumtumikia Mungu wa Biblia lakini inavunja sana amri zake za uadilifu.
12. Sisi binafsi tunafaidikaje na masimulizi hayo?
12 Kwa hiyo, masimulizi hayo yote ni yenye maana leo. Yanatusaidia tufahamu jinsi Mungu anavyoziona hali za wakati wetu na linalotupasa sisi binafsi tufanye ili tuje tuokoke dhiki kubwa inayokuja. Kwa njia hiyo tunasaidiwa tuthamini zaidi sana uhakika wa kwamba “Kila andiko . . . lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki.”—2 Timotheo 3:16, 17.
JE! YOTE YALIPANGWA KIMBELE?
13. Twajuaje kwamba Mungu hakuchochea watu wafanye dhambi ili mifano ya unabii iweze kutolewa?
13 Kwa sababu ya yote hayo, je! tufahamu kwamba mwenendo wote wa watu na mataifa yaliyoandikwa katika Biblia ulipangwa kimbele na Mungu ili uwe na maana ya kiunabii? Ni wazi kwamba Mungu mwenyewe alishughulika na watumishi wake zamani kwa jinsi fulani ili atoe mfano wa mambo makubwa zaidi aliyokuwa akifikiria kufanya wakati ujao. Lakini vipi vitendo vya wanadamu? Wengine kati yao walifanya dhambi nzito-nzito. Je! Mungu aliwachochea wazifanye ili akamilishe maandishi ya Biblia? Yakobo, mwandikaji Mkristo wa Biblia anajibu: “Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu.” (Yakobo 1:13) Mungu hakuwafanya watende makosa ili aweze kutoa mifano ya unabii.
14. (a) Yehova anajuaje yatakayofanywa wakati fulani ujao na wanadamu, au hata na Shetani? (b) Ni kwa njia gani maarifa ya Yehova juu yake mwenyewe na kusudi lake yanahusika katika unabii wa Biblia?
14 Usisahau kwamba Yehova ni Muumba wa wanadamu. Yeye anajua tulivyofanyizwa na kinachofanya watu watende wanavyotenda. (Mwanzo 6:5; Kumbukumbu la Torati 31:21) Yeye aweza kutabiri bila kukosea yatakayowatokea watu wanaoishi kupatana na kanuni zake za uadilifu na yatakayowatokea wale wanaojaribu kupuuza uhitaji wao wa Mungu au wanaozuia njia zake. (Wagalatia 6:7, 8) Yeye anajua kwamba Ibilisi ataendelea kutumia mbinu zake kama zile alizotumia zamani. Yehova anajua pia atakayofanya yeye mwenyewe zikitokea hali fulani fulani, kwamba yeye atatenda kupatana na sifa zake zilizo bora za haki, kutopendelea watu, upendo na rehema, ambazo ameonyesha nyakati zote. (Malaki 3:6) Kwa kuwa makusudi ya Yehova ni hakika yatatimizwa, yeye anaweza kutabiri yatakayotokea na hatua atakazochukua ili ayatimize. (Isaya 14:24, 27) Hivyo angeweza kuchagua matukio kutoka maisha ya watu mmoja mmoja na mataifa moja moja na kuagiza hayo yatiwe katika Biblia ili yawe mifano ya yatakayotokezwa na wakati ujao.
15. Mtume Paulo alikaziaje kwamba masimulizi ya Biblia si historia tu?
15 Kwa kufaa, basi, baada ya kusimulia matukio kutoka historia ya Israeli, mtume Paulo aliwaambia Wakristo wenzake hivi: “Basi mambo hayo yakaendelea kuwapata wao yawe mifano, nayo yaliandikwa yawe onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.” (1 Wakorintho 10:11, New World Translation) Na kwa kundi la Kikristo katika Roma aliandika hivi: “Yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi; ili kwa saburi na faraja ya maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Warumi 15:4) Tunapothamini hivyo kwamba masimulizi ya Biblia si historia tu, tunaweza kuanza kupata kwayo mifano ya ajabu inayoonyesha utakavyokuwa wakati ujao wa wanadamu.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 41]
MIFANO YA KIUNABII—Inaelekeza Kwenye Nini?
Siku za Noa
Hema
Mfalme Sulemani
Yona Katika Tumbo la Samaki kwa Siku Tatu
Kuanguka kwa Babuloni