Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • su sura 4 kur. 30-37
  • Aina ya Maisha Watakayokuwa Nayo Waokokaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Aina ya Maisha Watakayokuwa Nayo Waokokaji
  • Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KINACHOFUNULIWA NA KUSUDI LA AWALI LA MUNGU
  • YANAYOFUNULIWA NA HUDUMA YA YESU
  • Mamilioni ya Walio Hai Sasa Hawatakufa Kamwe Wamalizike Katika Dunia Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
    “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
  • Miujiza ya Yesu Unaweza Kujifunza Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Kutazama Baadhi ya Miujiza ya Yesu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
su sura 4 kur. 30-37

Sura 4

Aina ya Maisha Watakayokuwa Nayo Waokokaji

1. Kwa nini “siku ya [Yehova]” inayokuja haitaacha dunia iwe magofu yenye ukiwa? (Isaya 45:18)

IJAPOKUWA “siku ya [Yehova]” inayokuja itakuwa yenye kutia woga mwingi, haitaacha dunia ikiwa magofu isikaliwe. Matokeo yayo hayatakuwa kama yale ya uharibifu mkubwa wa vita ya nyukilia, unaoogopwa kuwa ungevuruga hali ya mazingira na kufanya waokokaji wapatwe na matokeo mabaya sana kutokana na mnururisho wenye sumu. Badala ya yeye aiharibu dunia isikaliwe na wanadamu, Muumba atakuja “kuwaharibu hao waiharibuo [dunia].”—Yoeli 2:30, 31; Ufunuo 11:18.

2. Ni nini kinachotupa uhakika wa kwamba Yehova ataokoa waaminifu katika dhiki kubwa?

2 Akili za watumishi waaminifu wa Yehova hazina shaka hata kidogo kwamba Mungu aweza kuwaokoa bila kujali majeshi yenye kuharibu ambayo ataruhusu kuwazunguka. Wanajua kwamba Sodoma na Gomora, miji yenye adili mbovu ilipoharibiwa kwa ‘kiberiti na moto kutoka mbinguni,’ malaika za Yehova walimwokoa Loti na binti zake wawili. (Mwanzo 19:15-17, 24-26) Wanajua pia kwamba wazaliwa wa kwanza wa Misri yote walipoharibiwa siku za Musa, malaika wa Yehova wa kuharibu alizipita nyumba za Waisraeli, nyumba zile zilizotiwa alama kwa damu ya mwana-kondoo wa kupitwa. (Kutoka 12:21-29) Ndivyo itakavyokuwa wakati hasira kali ya uharibifu wa ile dhiki kubwa itakapotokea. Yehova atawaokoa wale ambao wamemfanya yeye kuwa kimbilio lao.—Zaburi 91:1, 2, 14-16; Isaya 26:20.

3. Kwa nini idadi kubwa mno ya mizoga haitahatirisha afya ya waokokaji?

3 Ni kweli kwamba uso wa dunia utajawa na wale watakaouawa na Yehova, kwa sababu uharibifu huo utakuwa mkubwa. Lakini hakuna ajuaye kumpita Mungu jambo linalohitajiwa kufanywa ili kuilinda afya ya waokokaji. Anatuambia kwamba ataalika ndege wa mbinguni na wanyama wa kondeni kwenye “chakula cha jioni kikuu” chake na kwamba watashiba minofu ya wale watakaouawa. (Ufunuo 19:17, 18, New World Translation; Ezekieli 39:17-20) Sehemu ambayo hawawezi kula anaweza kuiondoa kwa njia nyingine. Kusudi la Mungu kwa dunia kama lilivyosemwa katika Edeni ndipo litasonga mbele likapate utimizo.

KINACHOFUNULIWA NA KUSUDI LA AWALI LA MUNGU

4. Ni mwanzo wa aina gani ambao Yehova aliwapa watu wawili wa kwanza, na kwa nini hilo ni lenye kutupendeza kwa njia ya pekee?

4 Kinachoonyesha yanayotumainiwa wakati ujao na waokokaji wa dhiki kubwa kinapatikana katika aina ya mwanzo ambao Yehova aliipa jamaa ya kibinadamu katika Edeni. Katika kuitayarisha dunia iwe makao ya wanadamu, Muumba alimeesha mboga nyingi, pia samaki, ndege na wanyama wa nchi kavu wengi kwa namna nyingi zenye kupendeza. “Jehova Mwenyiezi Mngu akafanya busitani huko upande wa mashariki, katika Edeni; akamweka huko huyo Adamu aliyekuwa amemfinanga.” (Mwanzo 2:8, The Old Testament in Swahili, Mombasa) Lakini Mungu hakuifanya dunia yote kuwa paradiso kisha akaitunza iwe shamba la starehe kwa mwanadamu. Badala yake, Yehova aliwapa watu wawili wa kwanza mwanzo mzuri ajabu, akawabariki na kuwapa mgawo wa kazi. Aliweka mbele yao kazi ambazo zingewawezesha watumie uwezo wao wote waridhike na mambo ambayo wangetimiza. Hiyo ingejaza maisha zao maana. Lo! walikuwa na mgawo wenye kuvutia kama nini! Kulea watoto ili waonyeshe sifa za kimungu, waipanue Paradiso ifike kwenye miisho ya dunia na kuitunza ikiwa imejaa viumbe hai! Kama Adamu na Hawa wangeendelea kuheshimu enzi kuu ya Yehova, hawangekufa kamwe. Wangefurahia uzima mkamilifu duniani milele.—Mwanzo 1:26-28; 2:16, 17.

5. Hivyo, ni mataraja gani yatakayokuwa mbele ya waokokaji wa dhiki kubwa?

5 Bila shaka, hali zitakazokuwapo duniani mara baada ya dhiki kubwa hazitakuwa kama zile zilizokuwa katika Edeni. Lakini kusudi la awali la Mungu kwa dunia na wanadamu litaendelea bila kubadilika. Ni lazima Paradiso ienee dunia yote, jamii ya kibinadamu ndiyo itaitunza, nao wote watakuwa wenye umoja katika ibada ya Mungu wa kweli. Mbele yao watakuwa na nafasi ya kuishi milele, wafurahie uhuru mtukufu wa watoto wa Mungu.—Luka 23:42, 43; Ufunuo 21:3, 4; Warumi 8:20, 21.

6. (a) Vifaa vyo vyote vya kivita vitageuzwa viwe vya kazi gani? (b) Kwa nini hakuna mtu ambaye atakuwa na njaa tena wakati wo wote?

6 Bila shaka, kwanza magofu ya mfumo wa kale yatahitaji kuondolewa. Vifaa vya kivita vitakavyosalia vitageuzwa viwe vya matumizi ya amani. (Ezekieli 39:8-10; linganisha Mika 4:3.) Bila shaka mazao yatakayokuwa bado yamo mashambani yatavunwa ili yaliwe na waokokaji. Ndipo mbegu zitakapopandwa na mavuno mapya yakivunwa, ahadi hii itatimia: “Dunia yenyewe hakika itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.” (Zaburi 67:6, New World Translation; linganisha Kumbukumbu la Torati 28:8.) Wachoyo na wenye kuleta migawanyiko wa mfumo wa kale wakiisha kuondoka, hakuna mtu ye yote atakayelazimika tena kulala usiku akiwa na njaa.—Zaburi 72:16.

7. Uchaguzi wa Yehova wa Mfalme mpya wa dunia unaonyeshaje hekima na upendo wa Mungu?

7 Huo utakuwa ulimwengu wenye watu wanaothamini umaana wa kuwa na mwelekezo na baraka ya Yehova. Na hiyo itatolewa kwa jinsi itakayoonyesha hekima na upendo wa Mungu mwenyewe. Yeye ambaye Yehova amempa mgawo wa kuwa Mfalme mpya wa dunia ni Mwanaye mwenyewe, Yesu Kristo. Biblia inafunua kwamba kupitia yeye Mungu aliiumba dunia na aina mbalimbali zote za uhai ulio juu yayo. (Wakolosai 1:15-17) Mwana wa Mungu anafahamu kwa ukamili kinachotakwa ili kuendeleza uhai hapa duniani, naye ana upendo wa pekee kwa vitu vinavyohusu wanadamu.—Mithali 8:30, 31.

8. Ni itikio gani kwa enzi kuu ya Yehova ambalo Kristo atasaidia raia zake za kidunia wasitawishe?

8 Zaidi ya yote, Mwana huyo anategemeza kwa ushikamanifu enzi kuu ya Yehova. Kwa habari ya Yesu ilitabiriwa hivi: “Juu yake roho ya Yehova itatulia, na roho ya hekima na ya ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumwogopa Yehova; na yeye atafurahia kumwogopa Yehova.” (Isaya 11:2, 3, New World Translation) Atasaidia raia zake wa kidunia wafurahie namna iyo hiyo kupatanisha maisha zao na njia za Yehova. Chini ya umaliki wake, waokokaji wa dhiki kubwa watarudishwa kwenye aina ya maisha ambayo Mungu alikusudia wanadamu wakati wazazi wetu wa kwanza walipopewa Edeni iwe makao yao.

YANAYOFUNULIWA NA HUDUMA YA YESU

9. (a) Ni nini baadhi ya matokeo yenye kuhuzunisha ya dhambi iliyorithiwa? (b) Miujiza ya Yesu inatoa tumaini gani?

9 Lakini, ili tufurahie aina hiyo ya maisha, tunahitaji kuondolewa matokeo yenye kuhuzunisha ya dhambi. Sisi sote tumerithi dhambi kutoka kwa Adamu, aliyepoteza ukamilifu wake alipopuuza enzi kuu ya Yehova kwa njia ya kuasi. Matokeo ya dhambi yanaonekana kwa njia mbalimbali. Inaweza kutokeza ugonjwa, kasoro za mwili, pia elekeo la kufikiri na kusema na kutenda mambo kwa nia zilizo na makosa. Hatimaye inatokeza kifo. (Warumi 5:12; 6:23) Wakati wa huduma yake ya kidunia, Yesu alifanya miujiza mingi iliyoonyesha atakayofanya ili aletee faraja wale walio raia za Ufalme wa Mungu.

10. Kwa nini ni jambo la akili kwamba Yesu angeweza kufanya miujiza inayowashinda wanasayansi kufanyiza tena?

10 Lakini watu fulani wanapoyasoma masimulizi ya Biblia yenye kusisimua juu ya Yesu, wanaonyesha shaka. Kwa nini? Kwa sababu tunaishi katika ulimwengu ambamo kutia shaka kumependwa sana na wengi. Huenda wenye kutia shaka wakahisi kwamba ili miujiza iwe yenye kusadikika, wanasayansi wamepaswa wawe na uwezo wa kuifanyiza tena au kuieleza. Lakini kwa nini wanasayansi wanaendelea kutumia kiasi kikubwa cha mapesa wakichunguza habari? Kwa sababu kuna mambo mengi wasiyoyafahamu. Linalohusika hasa katika mwelekeo wetu kwenye huduma ya Yesu ni utayari wa kukubali kujiingiza kwa kimungu katika mambo ya kibinadamu.

11. Katika Matendo 2:22, ni semi gani zinazotumiwa kueleza miujiza ya Yesu, nayo inaonyesha nini?

11 Akihutubia umati uliokuwa Yerusalemu mwaka wa 33 W.K., mtume Petro alisema juu ya Yesu kuwa “mtu aliyedhihirishwa kwenu na Mungu kwa miujiza na ajabu na ishara, ambazo Mungu alizifanya kwa mkono wake.” (Matendo 2:22) Kama Petro alivyoonyesha, miujiza hiyo ilikuwa kazi zenye nguvu, si kazi ambazo wanadamu wengine wangeweza kurudia kuzifanya wala kuzieleza, bali ni ushahidi wa kwamba nguvu za Mungu zilikuwa zikitenda kazi kupitia Yesu. Ilikuwa “ishara” za kwamba yeye alikuwa Masihi kweli kweli, Mwana wa Mungu mwenyewe. Pia ilikuwa “ajabu,” mambo yaliyoelekeza kwenye matukio yenye kuchangamsha moyo ya wakati ujao.

12. (a) Kwa nini unaona yale masimulizi juu ya kusafishwa kwa watu waliokuwa na ukoma kuwa yenye kutia moyo? (b) Ni jambo gani juu ya Yesu kuponesha mwenye kupooza lililofaa kuangaliwa hasa?

12 Soma masimulizi ya Injili katika Biblia, na unaposoma, kumbuka kwamba miujiza iliyofanywa na Yesu inatoa mwonjo wa yale ambayo atafanyia wanadamu watakaoishi duniani chini ya Ufalme wa Kimasihi wa Mungu. Huo utakuwa wakati ambao watu wenye magonjwa yenye kuharibu umbo la mtu kama ukoma watasafishwa—kama Yesu alivyosafisha wakoma kumi alipokuwa akielekea Yerusalemu mwaka wa 33 W.K. Yeye alionyesha kwamba anaweza kusaidia watu kama hao na kwamba kweli anataka kufanya hivyo. (Luka 17:11-19; Marko 1:40-42) Wengi wamepooza. Hata wao wataponeshwa—kama mwenye kukaa kitandani kwa sababu ya kupooza ambaye Yesu aliponesha, akashirikisha tendo hilo na lile la kusamehe dhambi za mtu huyo.—Marko 2:1-12.

13. Eleza muujiza mmoja wa Yesu unaotoa tumaini kwa (a) vipofu, (b) viziwi na walio na kasoro ya usemi, (c) watu ambao wametibiwa na madaktari wasipate nafuu. (d) Unajuaje kwamba Yesu ataweza kuponesha aina zote za magonjwa na udhaifu?

13 Macho yaliyopofuka yatafunguliwa, masikio yasiyosikia yatafunguliwa na wale walio na kasoro za usemi watafunguliwa ndimi zao—kama Yesu alivyofanya mambo hayo kwa watu waliokuwa Galilaya na Dekapoli katika karne ya kwanza. (Mathayo 9:27-30; Marko 7:31-37) Madaktari hawawezi kuponesha watu wengi leo. Ndiyo iliyokuwa hali ya mwanamke katika Kapernaumu ambaye “alikuwa amesumbuliwa sana na waganga wengi. Na, ingawa alikuwa amekwisha tumia mali yake yote hakupata nafuu.” Lakini Yesu alimponesha, na ataponesha wengi walio kama yeye. (Marko 5:25-29, Habari Njema kwa Watu Wote) Kama alivyoonyesha alipoponesha “magonjwa yote na udhaifu wa kila aina” wakati wa huduma yake Galilaya, kansa, ugonjwa wa moyo, maleria, kichocho, hayatakuwa magumu mno kuponesha.—Mathayo 9:35.

14. Masimulizi juu ya Yesu kufufua wafu yanaonyeshaje ufufuo utakavyomaanisha kwa waokokaji?

14 Huo utakuwa pia wakati wa nafasi kwa wafu—si wale watakaoharibiwa na Mungu katika dhiki kubwa, bali kwa mabilioni ya wengine ambao wamekufa katika karne zote—waishi tena, wawe na mataraja ambayo hawakupata kamwe kuwa nayo mbele yao. Hilo litakuwa na maana gani kwa waokokaji? Karibu na kijiji cha Naini, Yesu alikausha machozi ya huzuni ya mama-mjane kwa kurudisha mwanaye pekee kwenye uzima. Katika Kapernaumu alileta msisimuko mkubwa kwa wazazi wa msichana mdogo kwa kumwamsha katika wafu mtoto wao. (Luka 7:11-16; Marko 5:35-42) Je! ungependa kuwapo wakati wapendwa wako watakaporudi kutoka kwa wafu? Hilo litakuwa jambo lenye kusisimua kuonwa na waokokaji watakaoingia katika “dunia mpya.”

15. (a) Mafundisho ya Yesu yanaonyeshaje aina ya watu watakaoishi duniani wakati huo? (b) Ni kwa njia gani tunaweza sasa kuwa na mwonjo wa aina hiyo ya maisha?

15 Wakati huo maisha hayatakuwa marudio ya masikitiko ya moyo na huzuni zinazolemea watu sasa mara nyingi sana. Hilo linaonyeshwa si na miujiza tu ya Yesu bali pia na mafundisho yake, kwa sababu ni wale tu walio wanafunzi wake kweli kweli ndio watakaookoka waingie katika “dunia mpya.” (Yohana 3:36) Alifundisha wafuasi wake waweke faida za kiroho mbele ya shughuli za kimwili, wamtegemee Yehova, wamtumainie Yeye awape mwongozo na kuwa wenye kuthamini baraka Zake. Kwa neno na kwa mfano, Yesu alikazia umaana wa upendo na unyenyekevu, kuwajali sana watu wengine na kujitoa kwa ajili yao. Tayari, wale wanaokuwa wanafunzi wa Kristo na wanaofuata kweli kweli kanuni hizo wanapata burudisho kubwa la nafsi zao, nao wanaburudisha wengine. (Mathayo 11:28, 29; Yohana 13:34, 35) Huo ni mwonjo tu wa aina ya maisha yatakayofurahiwa na wale watakaokuwa bado hai wakati ulimwengu wa sasa usio na upendo utakapoondoka. Ukitenda kwa hekima sasa, maisha hayo yanaweza kuwa yako.

[Sanduku\Picha katika ukurasa wa 33]

KUSUDI LA AWALI LA MUNGU KWA WANADAMU

Kuijaza dunia wanadamu wenye kuonyesha sifa za kimungu

Kupanua Paradiso duniani pote na kuitunza pamoja na uhai wa wanyama

Kufurahia uzima duniani milele

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki