Mamilioni ya Walio Hai Sasa Hawatakufa Kamwe Wamalizike Katika Dunia Yetu
“Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapojufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele.”—YOHANA 11:25, 26.
1. Mtu asipokufa kamwe aondoke kwenye dunia yetu, hiyo ingekuwa na maana gani kwa mtu huyo mwenye kupendelewa?
MTU asipokufa kamwe hata siku moja, hiyo ingekuwa na maana ya kwamba huyo mwenye kupendelewa hivyo angebaki akiwa hai akiwa mwanamume au mwanamke asiyeweza kufa hapa duniani mpaka milele! Kukata maneno hivyo ni jambo la akili nzuri, sivyo? Na je! si kukata maneno hivyo kunapatana na maneno yaliyopo juu aliyoyasema Yesu Kristo zaidi ya karne 19 zilizopita? Ndivyo!
2, 3. (a) Maandiko ya Kiebrania yanatolea watu tumaini gani? (b) Mifumo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo ina tazamio gani kwa ujumla?
2 Maandiko ya Kiebrania yaliyo matakatifu, kuanzia Mwanzo mpaka Malaki, hayatolei watu tumaini lo lote la kuishi mbinguni, na kwa hiyo Wayahudi walioyafuata sana Maandiko hayo hawakuwa na tumaini lo lote au tamaa yo yote ya kuishi mbinguni. Lakini Maandiko ya Kiebrania yanatolea watu tumaini la kupata uzima wa milele. (Zaburi 37:29; Ayubu 14:13-15) Kuwa na uzima wa milele duniani chini ya Ufalme wa Masihi aliyeahidiwa kulikuwa tumaini na tazamio la kikawaida kwa Myahudi ye yote wa asili aliyetahiriwa.
3 Lakini, kwa ujumla hilo silo tazamio la mifumo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo. Wao wanaamini na kufundisha kwamba sisi wanadamu tuna nafsi isiyoweza kufa ndani ya mwili wetu wenye kufa na kwamba wakati tunapopatwa na kifo kisichoepukika nafsi hiyo inaachwa huru na kukimbilia makao ya kiroho yasiyoonekana. Huko nafsi hiyo inapitishwa kwenye hukumu kisha Mungu anaiweka ama katika mbingu zenye raha nyingi au katika mahali pa adhabu ya mateso yasiyofikia mwisho ikiwa mtu mwenyewe hakuwa Mkristo mwaminifu. Nayo maoni ya ujumla ya Jumuiya ya Wakristo ni kwamba dunia, jua, mwezi na nyota vitachomwa vimalizike, viharibiwe, katika moto wenye kuteketeza ulimwengu mzima.
4. Kwa sababu gani kutokufa kamwe kwa mtu atoke kwenye dunia yetu kusingeelekea kuwa habari njema kwa watu wengi wanaoifikiria hali ya sasa ya dunia?
4 Kulingana na maoni hayo ya kidini, haingeweza kamwe kuwa kweli kwamba “mamilioni ya walio hai sasa hawatakufa kamwe wamalizike katika dunia yetu. Lakini, huenda watu wengi wakauliza, Ni akina nani wangetaka kuishi juu ya sayari yenye kupigwa kwa wingi na njaa kubwa-kubwa, magonjwa ya kipuku, matetemeko ya ardhi, vita, chuki za kimataifa na za kikabila, pamoja na lundo kubwa la silaha za vita ya nyukilia ambazo zinatisha kumaliza kabisa kuwapo kwa mwanadamu duniani? Kama maafa makubwa namna hiyo yangeipata dunia yetu bila kufikia mwisho, watu wengi wenye fikira nzuri wangetaka kuondoka duniani—hata kwa kufa!
Kusudi la Kwanza Kabisa kwa Dunia
5. Hali ya dunia ilikuwa namna gani wakati Mungu alipoweka jamii ya kibinadamu juu yake, na Mungu anajisikiaje kuelekea wanadamu?
5 Lakini, pale pale mwanzoni mwa kuwako kwa mtu, Muumba aliipa jamii ya kibinadamu dunia ili iwe makao yao ya milele. Wakati huo ilikuwa ‘dunia njema’ kweli kweli. Masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji yanatuambia kwamba, baada ya Muumba kutayarisha hali za kidunia kwa ajili ya mwanamume na mwanamke wa kwanza na kuwaweka juu ya dunia, ‘Mungu aliona kila kitu alichokifanya, na tazama, ni chema sana.’ (Mwanzo 1:31) Kama dunia isingalionekana kuwa njema sana machoni pa Muumba, yeye asingaliwaweka kamwe watoto wake wa kibinadamu hapa. Mwandikaji mwenyewe aliyeyaandika masimulizi ya uumbaji anasema hivi juu ya Mungu Muumba: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Mungu Mweza Yote hana kumbukumbu la kazi au utendaji ambao aliufanya vibaya hata astahili kuomba mtu ye yote radhi (msamaha). Akiwa Baba mwema, yeye alipenda wanadamu mwanzoni. Na angali anapenda wanadamu.—Yohana 3:16.
6, 7. Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba uumbaji wa Mungu wa dunia na mwanadamu anayeikaa hautakuja kuwa kazi-bure?
6 Jambo la kufurahisha ni kwamba tendo la Mungu kuumba dunia na mwanadamu anayeikaa halitakuwa kazi-bure. Alipokuwa akiwekea mwanamume na mwanamke wa kwanza mradi wenye kumheshimu mbele yao, Mungu aliwapa Adamu na Hawa ruhusa ya kuzaa watoto wakamilifu na kujaza dunia kwa watoto hao. Waliagizwa pia waitiishe dunia iwe Paradiso ya dunia nzima na kutawala viumbe vyote duniani vilivyo vya cheo cha chini. (Mwanzo 1:28) Jambo la kusikitisha ni kwamba, baada ya miaka zaidi ya 6,000 ya kuwako kwa wanadamu na kupata ujuzi, wanadamu hawakufanya waliloagizwa wafanye. Kuongezea ubaya huo, sasa wanadamu wanatokeza tisho la kujifagilia mbali wenyewe kwa njia iliyo ya jeuri kupita zote ya kutumia vifaa vya kuchukiza ambavyo wamejitengenezea. Lakini ingawa wanadamu wamejitia wenyewe katika hali ya kushindwa kwa kiasi kikubwa, hilo halikumfanya Mungu Muumba awe ameshindwa.
7 Kusudi la kwanza kabisa ambalo Mungu alikuwa nalo kuhusu dunia yetu litatimizwa. Tuna uhakikisho wa Mungu wa kuonyesha ndivyo itakavyokuwa! (Isaya 55:11) Kwenye Mhubiri 1:4 Biblia inasema hivi: “Kizazi huenda, kizazi huja; nayo dunia hudumu daima.” Na kwenye Isaya 45:18 Mungu Muumba anajiita “aliyeiumba dunia na kuifanya,” kisha anaongeza hivi: “Ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni [Yehova], wala hapana mwingine.” Nayo hakika ‘itakaliwa na watu’ katika wakati wake Mungu, iwe na jamii kamilifu ya wanadamu, wenye kupendelewa kwa kupewa zawadi ya uzima wa milele!
8, 9. (a) Kwa sababu gani kusudi la Mungu la kutaka dunia ikaliwe na watu halipingwi na uhakika wa kwamba mbingu za sasa na dunia ya sasa vitapitilia mbali? (b) “Mbingu mpya” na “dunia mpya” ni nini, na Biblia inatoa ahadi gani juu yavyo?
8 Maneno hayo yaliyotangulia yanayoonyesha uhakikisho wa kusudi la Mungu hayapingwi na mtume Petro wakati anapotuonya kwamba mbingu na dunia zilizopo sasa zitapitilia mbali. Hapana, kwa maana baada tu ya kutukumbusha juu ya tukio hilo la mwisho la wakati ujao, ambalo sasa linakaribia sana kutokea, yeye anaendelea kusema: “Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:10-13, NW) Ahadi ya Mungu ya kuleta hizo mbingu mpya na dunia mpya imehifadhiwa katika Isaya 65:17. Kuhusu muda ambao zitakaa, tunaambiwa hivi katika Isaya 66:22: “Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema [Yehova], ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.”
9 Ah, ndiyo, mbingu mpya na dunia mpya zitaendelea kuwapo mbele za Yehova; zitasimama imara, zitadumu, wala hazitakwisha! “Dunia mpya” ni jamii ya wanadamu wenye uadilifu watakaoikaa dunia itakayokuwa imesafishwa, dunia ambayo Muumba aliifanya “ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) “Mbingu mpya,” ambazo ni wakuu wapya wa kimbingu wenye uadilifu, zitakuwa ndizo zenye kuitunza dunia itakayosafishwa pamoja na wakaaji wayo wenye uadilifu. Basi, kwa uhakika Yehova Mungu hatakuwa ameiumba dunia yetu “ukiwa.” Bado itakuwa na wakati wa kumtakasa kuwa ndiye Mfanyi!
Kuokoka Hata Kuingia Katika “Dunia Mpya”
10, 11. (a) Katika matabiri yao, wachunguzi wa mambo ya ulimwengu hawafikirii jambo gani, na kwa hiyo sisi tunaweza kuokoka nini, kisha tuingie katika nini? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na uokokaji wa Noa na jamaa yake kupitia ile Gharika?
10 Maoni ambayo wanafunzi wa mambo ya ulimwengu wanatoa kwa ujumla hayaonyeshi tumaini lo lote la kwamba wanadamu wataokoka wakiwa hapa duniani waingie ndani ya mfumo mpya wa mambo ulio bora. Ni shukrani kwa sababu mawazo yao siyo mawazo ya Muumba dunia, wala njia zao sizo njia zake. (Isaya 55:8-11) Mawazo yao hayategemei lile lililotukia duniani zamani za kale katika siku za yule mwanamume Noa. Makombora yote ya nyukilia na silaha nyingine za mataifa zenye milipuko mikubwa si kitu zikilinganishwa na nguvu nyingi zilizomiminwa chini. wakati huo kutoka angani na Gharika ya dunia nzima ili kuukomesha ulimwengu huo wa kale wenye jeuri. Kwa rehema Yehova Mungu aliye Muumba alifanya maandalizi ili jamaa ya kibinadamu iuokoke mwisho huo wenye msiba wa ulimwengu wa wakati huo, ili waendelee kuwapo duniani.
11 Waokokaji wa kibinadamu wa ulimwengu huo wa kale walikuwa wanane, yaani, Noa na mkeye, na wanao watatu na wake zao. Jamii yetu ya kibinadamu ilipewa mwanzo mpya wa uadilifu kupitia nafsi nane hizo. (2 Petro 2:5; 3:6) Hicho ni kielelezo cha jambo litakalotukia karibuni. (Mwanzo 9:1-7) Kinaonyesha kwamba, sawasawa na vile Noa na jamaa yake walivyouokoka mwisho wa ulimwengu katika siku zao, hata sisi tunaweza kuuokoka mwisho wa ulimwengu huu tuingie ndani ya mfumo mpya wa mambo unaokaribia sana!
12, 13. (a) Kwa sababu gani mamilioni ya watu leo hawauogopi mwisho wa mfumo huu wa mambo ya kale? (b) Sala aliyotufundisha Mwana wa Adamu inatupa uhakikisho unaohusu nini juu ya dunia yetu halisi?
12 Mamilioni ya watu waliopo duniani leo wanathamini kwamba “mbingu mpya” na “dunia mpya” ziko hapa hapa tu mbele yetu Wao wanajua hawauogopi mwisho wa ulimwengu wa sasa ulio wa kale, hata utatokea kama kwamba ni moto wenye kufunika mbingu hata dunia. Wao wanajua kutokana na Neno linalotegemeka la Muumba wa vitu vyote kwamba dunia yetu halisi itaokoka sawasawa na vile ilivyookoka wakati ulimwengu wa kwanza ulipokwisha siku za Noa babu yao. Mtunga zaburi mwenye kuongozwa na Mungu alitoa maelezo haya juu ya dunia yetu: “Mbingu ni mbingu za [Yehova], bali nchi amewapa wanadamu.”—Zaburi 115:16.
13 “Wanadamu” walifanywa ili wawe wa duniani, si wa mbinguni, na duniani ndipo Muumba aliwapa ruhusa ya kupakaa. Hapa duniani ndipo yule Mwalimu Mkuu aliyejiita “Mwana wa Adamu” alipofunzia wanafunzi wake kumpelekea Muumba sala, akisema: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litukuzwe, ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 24:37; 6:9, 10) Ili sala hiyo ijibiwe na “Msikiaji wa sala” kupitia kuja kwa Ufalme wake wa kimbingu, ni lazima dunia yetu halisi iuokoke mwisho unaokaribia wa mfumo wa mambo ya sasa uliohukumiwa maangamizi. (Zaburi 65:2, NW) Wanadamu waokokaji watafanya mapenzi ya Baba wa kimbingu wakiwa juu ya dunia hii sawasawa na vile malaika wa mbinguni wanavyoyafanya mapenzi hayo.
14. Ni akina nani watakaoianza “dunia mpya,” na dunia mpya hiyo itapanuliwa namna gani?
14 Basi watendaji wa mapenzi ya Mungu wana tazamio zuri ajabu la kuwa katika dunia itakayosafishwa! Waokokaji wa kibinadamu wa ulimwengu huu wa sasa, ambao wanatazamia kumtolea Baba wa kimbingu utumishi usio na mwisho katika dunia-Paradiso, ndio watakaoianza “dunia mpya’’ wakiwa chini ya “mbingu mpya” za Kimasihi. Baadaye “dunia mpya” hiyo iliyoahidiwa itapanuliwa kupitia kufufuliwa kwa wanadamu-wafu waliokombolewa ambao watalazimika kutenda mambo ya uadilifu. (Yohana 5:28, 29) Kwa sababu hiyo, sisi tunaotazamiwa kuwa waokokaji wa mwisho wa ulimwengu huu tutafanya nini?
15, 16. (a) Mtume Petro alionyesha ni mwendo gani unaofaa kufuatwa na wanaotazamiwa kuwa waokokaji wa mwisho wa ulimwengu huu? (b) Noa alikuwa mtu wa namna gani katika siku zilizoitangulia Gharika, na yeye na jamaa yake walipata malipo gani?
15 Hilo ni ulizo zuri. Miaka zaidi ya 1,900 iliyopita mtume Petro alionyesha linalopasa kuwa jibu la ulizo hilo, wakati alipoandika hivi: “Kwa kuwa vitu vyote hivyo vitafumuliwa hivyo, ninyi yawapasa kuwa watu wa namna gani katika vitendo vitakatifu vya mwenendo na matendo ya utawa, mkingojea na kukaribisha akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo kupitia kwayo mbingu zikiwa katika moto zitafumuliwa na vitu vya asili vikiwa na moto mwingi sana vitayeyuka!” (2 Petro 3:11,12, NW) Ikiwa ilifaa mtume huyo aliyeongozwa na Mungu aandike maneno hayo miaka 1,900 iliyopita katika siku zile za usitawi mkubwa wa Milki ya Kiroma, inafaa zaidi sana Mashahidi wa Yehova waambiwe maneno hayo ya kuwahimiza wakati wa hizi siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Huku “kuwapo kwa siku ya Yehova” kutafikia upeo wakati “dunia na kazi zilizomo” zitayeyuka kama kwamba zimo katika nyungu ya kuyeyushia vitu.—2 Petro 3:10 NW.
16 Katika siku za kumalizia kabla ya mwisho wa ulimwengu uliokuwako kabla ya Gharika, “Noa alikuwa mtu mwenye uadilifu. Yeye alijithibitisha mwenyewe kuwa asiye na kosa kati ya watu wa rika lake. Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli.” (Mwanzo 6:9 NW) Kutembea kwa Noa kwa njia hiyo akiwa ndiye kichwa cha jamaa yake ndogo kulifanya wakawekwa hai na Mungu aliyetembea naye. Noa na jamaa yake walipotoka nje ya safina ya wokovu wakiwa hai, walitumiwa kuanza mfumo mpya wa mambo ya uadilifu wakiwa chini ya baraka ya Yehova Mungu. Ndipo Mungu alipofanya agano na waokokaji hao wa Gharika asilete tena kamwe Gharika ya dunia nzima juu ya jamii ya wanadamu duniani.—Mwanzo 9:8-17.
17. Noa alipewa onyo kwa kadiri gani, na ni hali gani inayolingana na hiyo siku hizi?
17 Noa alipewa onyo la kutosha juu ya mvua nzito ambayo ingemwaga maji mengi ya kuweza kuigharikisha dunia yote. Hata Mashahidi wa Yehova wa karne hii ya 20 wamepewa kwa kadiri iyo hiyo onyo la mwisho wa ulimwengu huu. Onyo hilo linaitegemea Biblia iliyoongozwa na Mungu na pia linategemea utimizo wa unabii mbalimbali wa Biblia yenyewe unaoonyesha wazi kwamba sisi tunakaribia kikomo cha mfumo huu wa mambo ya jeuri.
Kukaribisha Wafu Wawe Tena Duniani
18. Leo mamilioni ya Mashahidi wanafurahia sana njozi gani ya mapema ya kufufuliwa kwa wafu wa kidunia kama inavyoelezwa katika Ufunuo?
18 Leo mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ‘wanaotembea pamoja na Mungu’ wanafurahia sana kile kinachotangulia kuonyeshwa katika njozi kwenye Ufunuo 20:11-14 (ZSB), ambapo tunasoma hivi: “Nikaona kiti cha ufalme, kikubwa, cheupe, naye anayeketi juu yake, dunia na mbingu zikakimbia uso wake; na pahali pao hapakuonekana. Nikaona wafu, wakubwa na wadogo, wamesimama mbele ya Mungu, na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, kilicho cha uzima; na wafu wakahukumiwa katika mambo haya yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao. Bahari ikatoa wafu waliokuwa ndani yake; Mauti na Hadeze zikatoa wafu waliokuwa ndani yao. Wakahukumiwa kila mutu kwa kadiri ya matendo yake. Mauti na Hadeze zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii ndiyo mauti ya pili, hili ziwa la moto.”
19. Wanadamu-wafu watafufuliwa warudie dunia iliyo katika hali gani, nao watatendewaje kuwapa mwanzo mpya wa maisha?
19 Wale watakaofufuliwa kwa wafu kulingana na unabii huo wa Biblia hawatarudi wawe katika dunia isiyo na wakaaji. Mamilioni ya mashahidi walio wakf na waliobatizwa wa Yehova wanatazamia kuokoka wakati mbingu na dunia za kale za mfano zitakapoondoka mbio, ili wawakaribishe wafu watakaofufuliwa katika dunia itakayokuwa ikiendelea kulimwa iwe Paradiso ya ulimwenguni pote. (Luka 23:43, NW) Mfumo mpya wa mambo utakuwa unaendelea kufanyika wakati huo. Waokokaji wa mwisho wa ulimwengu huu wa kale watakuwa wamekwisha kufanya kwa upendo matayarisho ya kutosha ya kurudi kwa wanadamu-wafu waliokombolewa.
20. Ni maagizo gani yaliyotolewa na Yesu baada ya yeye kufufua Lazaro na binti ya Yairo kutoka kwa wafu yanayoonyesha mambo ambayo waokokaji watalazimika kuyafanyia yale mabilioni yatakayo fufuliwa?
20 Mamilioni hayo ya waokokaji watakumbuka namna Yesu alivyoamuru Lazaro afunguliwe vitambaa vya maziko na wale walioshuhudia mwujiza wa kufufuliwa kwake, mara tu baada ya Yesu kumfufua huyo Lazaro rafiki yake mpendwa huko Bethania, karibu na Yerusalemu. Vivyo hivyo, wakati Yesu alipofufua binti ya Yairo mtawala wa Kiyahudi kutoka kwa wafu, yeye ‘aliamuru binti huyo apewe chakula.’ (Luka 8:55; Yohana 11:44) Bila shaka maagizo yatatoka mbinguni kuwaagiza waokokaji wafanye maandalizi ya kuyafaa mabilioni ya wanadamu-wafu wenye kurudi.
21, 22. (a) Ni kwa shughuli gani waokokaji watasaidia wafu watakaofufuliwa ili wazitumie kwa ukamili faida za kifo cha Kristo? (b) Kwa sababu gani ile “dunia mpya” itakuwa na uadilifu tangu pale pale mwanzoni?
21 Kutakuwa pia na kazi kubwa ya kuwapa watu elimu. Jambo hilo linapatana na kusudi la kimungu kwa wanadamu-wafu wenye kurudi watumie kwa ukamilifu faida za dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo. Ni kwa kufanya hivyo tu wataweza kuruhusiwa waishi katika dunia iliyo mfano wa Edeni, wakiwa na ukamilifu wa kibinadamu. Tayari “mkutano mkubwa” wa wanaotazamiwa kuwa waokokaji wa ‘dhiki kubwa’ wanajitayarisha kushiriki katika shughuli hiyo ya elimu iliyo nzuri sana. Wao binafsi wamezitumia faida za kifo cha dhabihu cha “Mwana-kondoo wa Mungu,” Yesu Kristo. (Yohana 1:29) Hilo ndilo linaloonyeshwa katika Ufunuo 7:9-14 ambapo, kati ya mambo mengine, inasemwa hivi juu yao: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Kwa hiyo, kwa sababu ya kupokea faida za ukombozi wa Kristo, wao wanafananishwa kuwa ‘wamevikwa mavazi meupe.’
22 Juu ya huo “mkutano mkubwa,” inasemwa hivi pia kwa maana ya mfano: “Wanamtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufunuo 7:15, NW) Wakati wa ‘dhiki kubwa’ iliyo hapa mbele tu, wao hawatanyang’anywa mavazi yao meupe, bali wataendelea bila kuyumba-yumba kutolea Yehova Mungu utumishi mtakatifu wakiwa chini ya ulinzi wake. (Ufunuo 7:17) Wakiwa katika ‘mavazi yao meupe’ ya mfano, watakuwa ndio sehemu ya kwanza ya ile “dunia mpya,” hivi kwamba “uadilifu utakaa” ndani yake tangu pale pale mwanzoni.—2 Petro 3:13, NW.
Maulizo ya Kujikumbusha
◻ Watu wa kale na wa sasa wamekuwa na maoni gani juu ya uzima?
◻ Kusudi la Mungu kwa dunia ni nini na Biblia inathibitishaje jambo hilo?
◻ Lililopata Noa na jamaa yake linatupaje uhakika wa kwamba mamilioni ya walio hai sasa hawatakufa kamwe?
◻ Ni nani watakaokaribisha wafu wenye kurudi, na hao watafanyiwa maandalizi gani?
[Picha katika ukurasa wa 11]
Noa na jamaa yake waliiokoka Gharika. Mamilioni ya watu watauokoka mwisho wa ulimwengu huu
[Picha katika ukurasa wa 12]
Kama vile Lazaro alivyokaribishwa alipokuwa hai tena, ndivyo waokokaji wa Har–Magedoni watakavyokaribisha wafu wenye kurudi