Kutoka Katika Taabu ya Ulimwengu Kuingia Katika “Nchi Mpya” Yenye Amani
(Funzo la Kitabu)
1. Ni kwa sababu gani Nuhu na jamaa yake walihifadhiwa wakati “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu” wa wakati huo ulipokwisha, na ni kwa sababu gani kuokoka kwao ni kwenye maana kwetu?
HAPO kale katika historia ya kibinadamu “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu” ulikwisha! Babu yetu sote aliokoka mwisho huo wa “ulimwengu” huo. Babu yetu huyu alikuwa Nuhu mwana wa Lameki. Nuhu pamoja naye, mkewe na wanawe watatu na binti-wakwe watatu, aliokoka kwa sababu ya kuwa upande wa haki. Hili latufanya sisi sote leo kuwa wazao wa watu hao wanane waliookoka mwisho wa ulimwengu. Mwisho wa ulimwengu ulikuja kwa namna ya gharika ya dunia yote, ambayo wanadamu hawataiona tena kamwe. Nuhu akaitwa “muhubiri wa haki.” Habari ya Biblia inasema: “Noa akatembea pamoja na Mungu.” Huyu Ndiye ambaye upande wake Nuhu alisimama wakati wa hatari ya ulimwengu ya wakati wake. Ndiyo sababu yeye na jamaa yake walihifadhiwa katika safina kubwa mno ambayo aliunda kwa kutii amri ya Mungu ajihifadhi mwenyewe na jamaa yake.—2 Petro 2:5; Mwa. 6:9, ZSB; Ebr. 11:7.
2. (a) Nani watakaookoka mwisho wa “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu” ambao sasa uko mbele ya wanadamu, na kuna msingi gani wa kuwa na hakika hiyo? (b) Ni “mbingu” gani watakazoona zikiharibiwa kana kwamba kwa moto?
2 Tena, wanadamu wanakutana na mwisho wa “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu.” Bila kujali wale wanaodhihaki wazo hilo kubwa, kuna watu wengi wanaosimama upande wa haki, kama vile Nuhu alifanya kabla ya kuja gharika ya mwaka wa 2370 K.W.K. Nuhu alikuwa mmojawapo wa mashahidi wa kwanza wa Yehova. Jambo hili ni lenye maana sana kwa wakati wetu wenye hatari. Katika njia gani? Katika njia hii: Kama vile Nuhu alivyolindwa na Mungu, mashahidi wa Kikristo wa Yehova wa leo watauokoka mwisho unaokuja wa “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu.” Katika dunia watajionea wenyewe ikionyeshwa kwamba, “[Yehova] anajua namna gani kuokoa watawa katika majaribu na kuweka wasio haki katika hali ya azabu hata siku ya hukumu,” kama 2 Petro 2:9, ZSB inavyosema. Watahifadhiwa kama jamii katika “siku ya Mungu, kwa sababu yake, mbingu zikiungua zitayeyushwa, na viumbe vya asili vitayeyuka kwa moto mukali.” “Na inchi na kazi zilizo ndani yake zitateketezwa.” (2 Pet. 3:12, 10, ZSB) Wataziona “mbingu” zinazoonekana za kiserikali zikiteketezwa kwa njia yenye moto ambayo wakati huo Mungu mwenye kufanya miujiza atatumia. Wataisikia kelele kubwa ya kutoweka milele kwa “mbingu” hizo zenye kuteketea. Vitu “vya asili” vinavyokamatana na taratibu hii ya ulimwengu ya mambo “vitayeyuka,” kwa sababu ya kupatwa na moto mkali usiovumilika.
3. Onyesha vitu “vya asili” ni nini ‘vitakavyoyeyuka’ wakati huo, kulingana na 2 Petro 3:12.
3 Vitu “vya asili,” ambavyo ni sehemu ya hewa ya mfano ya taratibu hii ya mambo inayotoweka, havitaweza kuvumilia ule moto wenye kujaribu. Ile nia ya kilimwengu ya kwamba wanadamu wanaweza kuitawala dunia bila kumtegemea Mungu haitavumilia jaribu hilo lenye moto. Tamaa ya mwili na tamaa ya macho na kujivunia kwa mtu mali yake, kama mambo makuu yenye choyo ya taratibu hii ya mambo, itakuwa yenye muda mfupi kama “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu.” Yatateketea katika jaribu lenye moto la siku ya hukumu ya Yehova. “Mafundisho ya kwanza yaliyo manyonge, yenye upungufu,” yaani, makisio, filosofia, mazoea na kawaida za dini zenye udhaifu ambayo kwa hayo wanadamu wametafuta kupata wokovu wao wenyewe na kujionyesha wenyewe kuwa wenye haki, “mafundisho” hayo yatayeyuka katika jaribu kali lenye moto. Yataonekana kuwa hayana nguvu, hayafai, ni ya ovyo kabisa. (1 Yohana 2:15-17; Gal. 4:9) Vitu hiyo “vya asili” vitatoweka kwa sababu si hewa, si anga la asili ambalo waabudu wa Mungu duniani wamepaswa waishi chini yake.
4. “Inchi na kazi zilizo ndani yake” zitakazoharibiwa katika “siku ya Mungu” yenye moto, ni nini?
4 Vitu visivyoweza kuteketezwa na moto havitapatikana katika “inchi na kazi zilizo ndani yake” wakati wa hiyo “siku ya Mungu” yenye moto mkubwa. Vitaonekana kuwa vyenye kuteketezwa kwa moto kama “mbingu” na vitu “vya asili.” Jamii ya kibinadamu kama msingi ulio hai wa taratibu ya mambo ambayo mungu wake amekuwa Shetani Ibilisi itaangamizwa kwa kutekelezwa kwa hukumu za Mungu zenye haki. Katika njia hii ulimwengu mzima utakoma, ule “ulimwengu wa wale wasioogopa Mungu” unaolingana na ulimwengu ule katika gharika ya Nuhu. Kazi ambazo jamii hii ya kibinadamu ya duniani isiyomwogopa Mungu imesimamisha hazitaiokoa, hazitakuwa mahali pake penye usalama. Wonyesho mkali wa hasira ya Mungu, ghadhabu na lawama lake utateketeza mambo haya yote.
5, 6. (a) Wakati huo, inaelekea hali hiyo itaonekanaje kwa waabudu wa Yehova mwenyewe duniani? (b) Ni kwa njia gani peke yake wo wote wataokoka wakati huo wa taabu, na wanaweza kupata kutia moyo gani katika Zaburi ya 46?
5 Kwa kuwa “mbingu” na “viumbe vya asili” vya mfano na “inchi na kazi zilizo ndani yake” vitaharibiwa, huenda ikaonekana kwa waabudu wa Yehova watakaokuwa katika taabu hii ya ulimwengu isiyo na mfano kwamba ulimwengu mzima unaharibika-haribika karibu yao. Ndiyo, kana kwamba ardhi yenyewe inatikisika chini ya miguu yao. Huenda mwendo wa matukio hayo ukawa wenye kuogofya kwa watazamaji wa kidunia. Itakuwa wazi kwamba ni kwa mwujiza peke yake wa Mungu Mwenye Nguvu Zote watu wo wote walio katika mwili duniani wanaweza kuokoka. Ni kwa kumtumainia kabisa Yehova Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote peke yake watazamaji wa kidunia hawataogopa. Zaburi ya hekaluni ya wana wa Kora, waliookoka uharibifu wenye moto wa baba yao mwenye kuasi na Walawi wenzake wenye kiburi imeandikwa kwa ajili ya tukio hilo lenye kutetemesha:
6 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema. Mataifa yalighadhibika, falme zikataharuki; alitoa sauti yake, nchi ikayeyuka. [Yehova] wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.”—Zab. 46:1-7.
7, 8. Katika mistari inayofuata ya Zaburi hiyo, ni uhakikisho gani unaouona kuonyesha kwamba watakuwako waokokaji wa mageuzo makubwa ya ulimwengu?
7 Kuonyesha kwamba ingewezekana waweko wenye kuokoka mageuzo hayo yenye kuogofya sana katika ulimwengu wa asili, waandikaji wa zaburi (wana wa Kora) wanaendelea kusema, kwa maneno yao yafuatayo:
8 “Njoni myatazame matendo ya [Yehova], jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari [ya vita]. Acheni [Basi, na], mjue ya kuwa Mimi ni Mungu, nitakuzwa katika mataifa, nitakuzwa katika nchi. [Yehova] wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.”—Zab. 46:8-11, UV; NE; Hes. 16:1-35; 26:10, 11; 27:2, 3; Yuda 11.
9. (a) Ikiwa Yehova atakuwa kimbilio letu wakati huo, yatupasa tufanye nini sasa? (b) Waebrania 12:26-29 inatukumbusha tukio gani la kale wakati inaposema juu ya kuharibiwa kwa “mbingu” na “nchi”?
9 Kupata kimbilio kwa Yehova Mungu wakati wa msukosuko huo wa ulimwengu kunataka tumkimbilie Yeye mapema, hata sasa. Uwezo wake wa kutikiswa kwa “mbingu” na “nchi” hata kuharibiwa ulionyeshwa katika mwaka wa 1513 K.W.K., wakati wa kutikisisha Mlima Sinai pindi ya kuwapa wana wa kale wa Israeli Amri Kumi. (Kut. 20:1-18) “Sauti yake iliitetemesha nchi wakati ule; lakini sasa ameahidi akisema, Mara moja tena nitatetemesha si nchi tu, bali na mbingu pia. Lakini neno lile, Mara moja tena, ladhihirisha kuhamishwa vile viwezavyo kutetemeshwa, kama vitu vilivyoumbwa, ili vitu visivyoweza kutetemeshwa vikae. Basi kwa kuwa [sisi watu wa Israeli wa kiroho] tunapokea ufalme usioweza kutetemeshwa, na tuwe na neema, ambayo kwa hiyo tumtolee Mungu ibada ya kumpendeza, pamoja na unyenyekevu na kicho; maana Mungu wetu ni moto ulao.”—Ebr. 12:26-29; Hag. 2:6, 7.
10. (a) Wakati huo wa tetemeko kubwa, nini kitakachodumu, kama wonyesho wa nini? (b) Je! kuna lo lote ambalo Shetani na mashetani zake wataweza kufanya wazuie uharibifu wa “mbingu” na “nchi” za taratibu mbovu ya sasa ya mambo?
10 Ziacheni “mbingu” na “nchi” za kubandia tu zitikiswe hata ziondolewe kabisa katika uharibifu wenye moto wakati wa “siku ya Mungu,” lakini ufalme wa Kimasihi wa Mungu kupitia kwa Mwanawe wenye kushinda vitani utadumu. Kama wonyesho wa Enzi Kuu yake ya Ulimwengu Wote isiyotikisika, utadumu kwa ushuhuda Wake wa milele kama Bwana Mwenye Enzi Kuu wa wote. Shetani Ibilisi, “mtawala wa ulimwengu huu,” na malaika zake wote za kishetani wametawala kwa muda mrefu “mbingu” na “nchi” hii ya kubandia tu ya taratibu mbovu ya sasa ya mambo. Lakini, ijapokuwa uwezo wao usio wa kibinadamu, hawataweza kuzuia “mbingu” na “nchi” isitikiswe hata kuvunjika vipande vipande na kufutiliwa mbali itoke katika ulimwengu wote. “Wakati mchache” ambao katika huo hawa “pepo wabaya katika ulimwengu wa roho” wamezuiliwa hapa katika ujirani wa dunia utakuwa umekwisha. Mara baada ya ushindi wa milele wa Yehova Mungu kupitia kwa Yesu Kristo katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni, Shetani Ibilisi na malaika zake za kishetani watakamatwa na kufungwa katika minyororo na kutupwa katika shimo refu mbali na ujirani wa dunia hii.—Ufu. 20:1-3.
11. Je! mashahidi wa Yehova watakaookoka watajua kwamba kufungwa na kutupwa kwa Shetani na mashetani zake katika shimo refu kumetukia?
11 Ijapokuwa kufungwa huko katika minyororo na kutupwa kwa Shetani na malaika zake za kishetani katika shimo refu hakutaonekana na macho ya mashahidi wa Yehova watakaookoka, na inaelekea bila kusikika kwa masikio yao ya asili, wataona matokeo yake yenye kuokoa. Haitasemwa tena kwamba ‘Shetani ametuzuia,’ wakati tutakapokuwa tunataka kutimiza kazi ya ujenzi mpya katika dunia safi baada ya kufungwa katika shimo refu kwa pepo hao wabaya ambao sasa inatupasa tushindane mweleka na kupigana nao kwa silaha za kiroho. (1 The. 2:18; Efe. 6:12-18) Kushindana mweleka na kupigana huko kwa kiroho kutakuwa jambo la zamani kwao wakati wa utawala wa Kristo wa miaka elfu.—Ufu. 20:1-6; Rum. 16:20.
“MBINGU MPYA NA DUNIA MPYA”
12. Wakati hao, ni mambo gani yaliyotabiriwa na Danieli na Yesu Kristo yatakuwa unabii uliotimizwa?
12 Ee, siku hiyo yenye baraka, siku tunayotazamia kwa shauku sana! Ndipo utakapokuwa umetimizwa unabii—ule ambao nabii Danieli alitabiri aliposema: “Kwa wakati ule Mikaeli [Kristo aliyetukuzwa] atasimama, yule mukubwa anayesimama kwa ajili ya wana wa watu wako: na kutakuwa na wakati wa taabu kama usivyokuwa mbele tangu wakati taifa lilipokuwa hata wakati ule.” Alipokuwa akitoa unabii wake juu ya “mwisho wa taratibu ya mambo,” akitumia maneno hayo ya Danieli, Yesu Kristo aliongeza maneno haya: “Wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.”—Dan. 12:1, ZSB; Mt. 24:3, NW, 21, 22, UV; Marko 13:19, 20.
13. Mabaki na waabudu wenzao watakuwa na ufahamu gani, pendeleo gani lenye maana sana, wakiisha kuokoka taabu hiyo ya ulimwengu?
13 Hali ya kimwili na yenye mazingira ambayo katika hiyo mabaki yenye uaminifu ya Israeli wa kiroho na “mkutano mkubwa” wa waabudu wenzao wenye ushikamanifu watatoka katika taabu mbaya hiyo ya ulimwengu ambayo haijapata wanadamu ni jambo ambalo bado latazamiwa kuonwa na kufahamika. Lakini, lo! inachangamsha kama nini kufahamu kwamba mwisho Taratibu Mpya ya Mungu yenye haki imeanza! Lo! pendeleo lenye maana sana kuona hasa aliyoona mzee mtume Yohana zamani katika njozi tu! “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya; kwa maana mbingu za kwanza na dunia ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena.” (Ufu. 21:1, ZSB) Unabii wa Yehova ambao hata katika siku za kale za nabii Isaya ulitoa tumaini la jambo hilo utatimizwa: “Tazama, mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya, na maneno ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini mufurahi, na mushangilie daima, kwa ajili ya hivi ninavyoumba.”—Isa. 65:17, 18, ZSB.
14. (a) Wakristo katika kame ya kwanza walionaje ahadi ya “mbingu mpya na dunia mpya”? (b) Ni kwa sababu gani shauku za mashahidi wa Kikristo wa Yehova juu ya ahadi hiyo zinakuwa nyingi sasa?
14 Hata Wakristo wa karne ya kwanza walitaja ahadi hiyo ya Mungu asiyesema uongo. Wakiwa na maoni ya Waisraeli wa kiroho, walijitia nguvu katika uvumilivu wao wa Kikristo kwa kutazamia kutimizwa kwa ahadi ya Mungu yenye maana sana. Katika kutofautisha masimulizi ya kuyeyushwa kwa “mbingu,” “vitu vya asili,” na “dunia na kazi zilizomo” ambayo ameandikia wapokeaji wa barua yake, mtume Petro anaongeza maneno yenye kuchangamsha hivi: “Lakini ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi yake, na katika hizi haki itakaa.” (2 Pet. 3:13, NW) Leo mashahidi wa Kikristo wa Yehova wa karne hii ya 20 wanatazamia pia mbingu mpya na dunia mpya izo hizo. Wanajua kwamba wanaishi katika siku za mwisho za “mbingu zilizo sasa, na dunia.” Kile kizazi kilichotazamiwa kisipite mpaka “hayo yote” yaliyotabiriwa na Yesu Kristo yametimia kimeendelea kuishi tangu mwisho wa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 na kimeona karibu “hayo yote” yakitimia. (Mt. 24:3, 34) Hivyo sasa shauku zao zinakuwa nyingi!
15. Imetupasa sote tushughulike sana na shughuli gani?
15 Kuna sababu zaidi kuliko zamani kwa mashahidi wa Kikristo wa Yehova wa “kizazi hiki” kuwa na shughuli nyingi sana “katika mwenendo mtakatifu na utauwa” na hasa kuwa na shauku sana ya ‘kutazamia hata ije siku ya Mungu, na kuihimiza’ ambayo katika hiyo taratibu ya kale isiyo haki itayeyushwa katika uharibifu. (2 Pet. 3:11, 12) Siku hiyo ni ya lazima. Ni lazima ije ili itayarishe kutimizwa kwa ahadi ya Mungu yenye maana sana ya “mbingu mpya na dunia mpya,” ambayo katika hiyo haki itakaa. Inakaribia siku wakati kuumba kupya huko kulikoahidiwa kutakapoyapamba makao ambayo kwa muda mrefu yameharibiwa na kuwapo kwa mbingu na dunia zisizo za haki alizofanyiza Ibilisi. Lo! wakati huo utakuwa wenye kupendeza kama nini kuishi duniani!
16. (a) Ufalme huo wa Kimasihi wa mbinguni utakuwa na maana gani kwa wakaaji wa dunia? (b) Utakuwa wonyesho wa Yehova wa nini kwa wanadamu?
16 Utawala wa Bwana Yesu Kristo pamoja na kundi lake tukufu la “bibi-arusi” utaleta wakati usio na kizuizi wa utawala wenye haki na amani na furaha kwa wakaaji wa dunia. Ufalme huo wa mbinguni wa Kimasihi utakuwa mahali pa utawala mbaya wa mashetani na watu ambao umetawala wanadamu bila huruma kwa miaka hii elfu sita iliyopita. Serikali hiyo ya Kimasihi itachukua mahali pa “mbingu” mbovu za kale. Utakuwa wonyesho wa upendo mwingi wa Yehova Mungu kwa mwanadamu aliyeumbwa kama “mwana wa Mungu,” katika mfano na sura ya Mungu mwenyewe. (Mwa. 1:26-28; Luka 3:38, NW) Yehova Mungu aliupenda ulimwengu wa wanadamu sana hata kwa hasara yake akamtoa Mwana wake mzaliwa wa pekee awe Mfalme katika serikali hiyo ya Kimasihi.—Yohana 3:16.
17. Waokokaji wa Har–Magedoni watakuwa na tumaini gani mbele, na sasa wanafurahia hali gani?
17 “Vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni itakapokuwa imekwisha kupita na “pepo wabaya” wa Shetani na mashetani zake watakapokwisha kufungwa katika shimo refu, waokokaji wenye kupendelewa duniani watafurahi sana wakijua ya kwamba zile “mbingu mpya” zenye kuumbwa na Mungu zilizotazamiwa kwa muda mrefu zinatawala kweli kweli juu yao. Watakapoitazama nchi safi itakayotapakaa mbele yao, watajawa na roho ya upainia. Lo! kuna miaka elfu ya kufanya kazi katika nchi yote! Tumaini la paradiso ya dunia yote liko mbele yao. Tayari wanafurahia paradiso ya kiroho kwa roho na kibali ya Mungu. Walihifadhiwa katika paradiso hii ya kiroho wakati wa uharibifu mkubwa ulioyeyusha taratibu ya kale ikaharibiwa, kana kwamba katika safina ya kuokokea. Ndiyo sababu “dunia mpya” iliyoahidiwa na Mungu inaanza nao. Furaha wee, wao wenyewe ndicho kiini cha “dunia mpya,” jamii mpya ya kibinadamu, ulimwengu mpya wa watu wenye kumwabudu Mungu!
18. Huo ndio wakati wa utimizo wa ahadi gani yenye maana sana iliyoandikwa katika Ufunuo 21:3, 4?
18 Huu ndio mwanzo wa utimizo wa yale ambayo mtume Yohana alisikia yakitangazwa kutoka mbinguni: “Tazama, hema ya Mungu ni pamoja na watu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake, na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao, atakuwa Mungu wao. Naye atapangusa kila chozi katika macho yao; wala mauti haitakuwa tena; wala maombolezo, wala kilio, wala uchungu hautakuwa tena; kwa maana maneno ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufu. 21:3, 4, ZSB.—Kutoka Kitabu Man’s Salvation, sura ya 19.