Taratibu Mpya Inayokuja Inayotegemezwa na Roho Takatifu
(Funzo la Kitabu)
1. Yajapokuwapo maneno ya Mhubiri 1:9, sababu gani taratibu inayokuja ambayo inategemezwa na roho takatifu itakuwa jambo jipya kweli kweli?
TUSEMAPO juu ya taratibu mpya inayokuja inayotegemezwa na roho takatifu, twaweza kusema kweli kweli: “Tazama, ni jambo jipya.” Hata Mfalme Sulemani hataweza kutumia ile kanuni yake aliyoisema: “Jambo jipya hakuna chini ya jua.” (Mhu. 1:9, 10) Usemi huu wa Sulemani umekuwa ukitumika mpaka wakati huu kwa habari ya namna ya maisha ya wanaume na wanawake na kwa habari ya kuinuka na kuanguka kwa serikali zilizofanywa na wanadamu. Walakini taratibu ya mambo ambayo Muumba wa mbingu na dunia ataleta hapa hivi karibuni litakuwa jambo jipya kweli kweli, jambo ambalo halijapata kuonekana katika wakati wo wote uliotangulia katika historia yote ya wanadamu.
2. Kwa sababu gani ni jambo ambalo lingetazamiwa kwamba taratibu mpya iliyoahidiwa ingetegemezwa na roho takatifu?
2 Roho takatifu ndiyo itakayokuwa ikitegemeza hiyo taratibu mpya inayokuja. Na kwa sababu gani isiwe hivyo? Ndiyo iliyoongoza wale waliyoiandika Biblia, nacho kitabu hiki kilichoongozwa na roho hiyo ya Mungu kinatoa habari nyingi njema kuhusu hiyo taratibu mpya yenye amani kwa wanadamu ambao wamechoka kuona taabu. Itakapokuwa mwishowe imekwisha kuletwa katika kizazi hiki, wale wote watakaoifurahia watasema hivi kwa furaha: “Hii ni mpya!” Yehova, Mungu mwenye nguvu zote, atakuwa ametimiza ahadi yake kwa wanadamu: “Tazama, Nayafanya yote kuwa mapya.”—Ufu. 21:5.
3. (a) Ni mambo gani mapya ambayo kitabu cha Ufunuo kinasema juu yayo? (b) Ni kwa sababu gani taratibu mpya ya Mungu haitakuwa kazi iliyobandikwa-bandikwa viraka?
3 Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia kinazungumza juu ya mambo mapya, “jina jipya,” “wimbo mpya,” “mbingu mpya na nchi mpya,” na “Yerusalemu mpya.” (Ufu. 2:17; 12; 5:9; 14:3; 21:1, 2) Haya ni mambo yenye kusisimua kuyafikiria na kuyazungumza. Naye mtu anapothamini hali ya mambo mapya ambayo wanadamu wamewekewa akiba, yanamsukuma ‘amwimbie Yehova wimbo mpya.’ (Zab. 96:1; 98:1; 144:9; 149:1) Taratibu yake mpya haitakuwa kazi ambayo imebandikwa-bandikwa viraka, kutengeneza upya taratibu ya kale ya wanadamu, kujaribu kuhifadhi sehemu kubwa iwezekanavyo ya taratibu hiyo ya kale na kuweka tu viraka vipya juu yake, hivyo kuitumia ile taratibu ya kale ya wanadamu kama msingi. Hilo halingeweza kufanya kazi. Yesu Kristo mwenyewe alisema hivi:
“Hakuna akataye kiraka cha vazi jipya na kukitia katika vazi kuukuu; na kama akitia, amelikata lile jipya, na kile kiraka cha vazi jipya hakilingani na lile vazi kuukuu. Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama akitia, na ile divai mpya itavipasua vile viriba, divai yenyewe itamwagika, na viriba vitaharibika. Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya.”—Luka 5:36-38.
4. Ni kwa sababu gani Yerusalemu wa kale uliojengwa upya hautashiriki sehemu yo yote katika hiyo Taratibu Mpya?
4 Kulingana na mfano huu, yale ambayo Mungu ametabiri kwa ajili ya wanadamu, yatakuwa mambo mapya kabisa. Yerusalemu wa kale katika Mashariki ya Kati hautashiriki sehemu yo yote ya mambo haya. Mungu alipotoa hukumu Yake juu yake katika mwaka 70 W.K., yeye aliruhusu Yerusalemu wa siku za Yesu uharibiwe. Yerusalemu ambao umepata kujengwa tangu wakati huo haukujengwa kwa amri Yake wala na watu wake waliokubaliwa. (Yohana 4:21) Yerusalemu Mpya ndio jambo lenyewe! Huu hautakuwa mji uliojengwa hapa duniani, katika makao ya ule Yerusalemu wa kale. Yerusalemu Mpya ni wa kimbinguni. Jambo peke yake tuwezalo kufanya ni kuchunguza tu maelezo yake kama vile yanavyotolewa katika Ufunuo 21:9 mpaka 22:3, nasi tutaona kwamba, kwa sababu ya ukubwa na hali yake, haungeweza kamwe kuenea katika eneo la Yerusalemu wa kale. Katika maelezo yaliyoongozwa na Mungu, Yerusalemu Mpya unaitwa “Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo.”
5. Yerusalemu Mpya unafananishwa na nani, nalo jambo hilo linalinganaje na usemi katika Zekaria 9:9?
5 “Nami nikauona ule mji mtakatifu,” asema mtume Yohana, “Yerusalemu Mpya, kama bibi-arusi aliyekwisha kupambwa kwa mumewe.” (Ufu. 21:2) Kama vile Yerusalemu Mpya unavyofananishwa hapa na mwanamke, bibi-arusi, mke, ndivyo na Yerusalemu wa kale ulivyofananishwa na mwanamke. Kwa mfano, Yesu alipoingia Yerusalemu akiwa amempanda mwana-punda Nisani 9 (Machi 27), mwaka 33 W.K., kama kwamba alikuwa mfalme-mwekwa aliyekuwa akipanda kwenda kutawazwa, unabii wa Zekaria 9:9 ulitimizwa: “Furahi sana, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, Mfalme wako anakuja kwako; amempanda punda, naam, mwana-punda, mtoto wa punda.”—Mt. 21:4, 5.
6. Yerusalemu Mpya utakuwaje ukilinganishwa na ule mji wa kale kwa habari ya uzuri, nao unashukaje kutoka mbinguni kwa Mungu?
6 Yerusalemu wa kale wa kidunia uliitwa “mji huu ndio ulioitwa, Ukamlifu wa uzuri.” (Omb. 2:15; Zab. 48:1, 2; 50:2) Hata hivyo, kwa habari ya uzuri na utukufu, huangeweza hata kidogo kulingana na Yerusalemu Mpya wa kimbinguni. Mji huu mpya wenye utukufu washuka “kutoka mbinguni kwa Mungu.” Katika njia gani? Katika njia ya kwamba baraza hii mpya ya kiserikali inatoka kwa Mungu nayo hupeleka uwezo na mamlaka yake kutoka mbinguni kufika hapa duniani, kwa faida ya milele ya wanadamu.—Ufu.21:2.
7. Huo mji mtakatifu, Yerusalemu Mpya, ni “mke wa Mwana-Kondoo” katika njia gani?
7 Mji huo mtakatifu ni “Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo” katika njia gani? Katika njia ya kwamba washiriki wake ni kundi la wanafunzi watiwa mafuta wa Kristo, warithi wake wa shirika katika ufalme wa Kimasihi. (Efe. 5:25-27; 2 Kor. 11:2; Ufu, 19:7, 8; 22:17) Kwa habari ya kila mmoja wa hawa, Yesu aliyetukuzwa alisema hivi: “Nami nitaandika juu yake jina la Mungu wangu, na jina la mji wa Mungu wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu mwenyewe, lile jipya.” (Ufu. 3:12) Washiriki wa “bibi-arusi” ni Waisraeli wa kiroho, walio katika lile agano jipya, nao hesabu yao ni 144,000. Yesu Kristo anawajenga juu yake, yeye mwenyewe akiwa ule “mwamba,” nao mitume wake 12 wakaa juu yake wakiwa kama mawe ya msingi mdogo uliojengwa juu yake.—Mt. 16:18; Ufu. 7:4-8; 14:1-5; 21:14.
8. Ni kwa sababu gani warithi wa shirika wa Kristo 144,000 watakuwa baraza ya watawala iliyo jipya kabisa?
8 Wale warithi washirika 144,000 pamoja na Bwana-arusi Yesu Kristo hawatatia ndani wanasiasa walimwengu wo wote, hata wafalme wa kisiasa na wa kidini waliotawala katika Jumuiya ya Wakristo. Wao ni baraza iliyo tofauti kabisa ya watawala, kitu kipya kabisa. Kwa kuwa wao hawana tena hali ya kibinadamu, wana ‘hali ya kimungu.’ Wao ni “kiumbe kipya.” (1 Pet. 1:4, HNWW; 2 Kor. 5:17) Wao wametimiza matakwa ya mwanafunzi duniani ya kuingia katika ufalme wa kimbinguni. Wao walipata ‘kuzaliwa mara ya pili,’ ‘wakazaliwa kwa maji na kwa roho,’ ‘wakazaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu.’ (Yohana 1:12, 13; 3:3, 5) Wanafunzi wa Kristo waliozaliwa kwa roho wanasoma hivi katika Warumi 6:5, 8: “Kwa maana kama tulivyounganika naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika tutaunganika katika mfano wa kufufuka kwake. Lakini tukiwa tulikufa pamoja na Kristo, twaamini ya kuwa tutaishi pamoja naye.”
9. Ufufuo wa Kristo ulikuwa wa namna gani, na ambao wale warithi wake wa shirika 144,000 watafufuliwa kwa mfano wake na kuunganishwa pamoja naye?
9 Ni nini “mfano wa kufufuka kwake”? Basi, Kristo alifufuliwaje? Katika 1 Petro 1:18, NW, tunaambiwa hivi: “Kristo alikufa mara moja tu kuhusu dhambi, mtu mwenye haki kwa wasio haki, ili apate kuongoza ninyi kwa Mungu, yeye akauawa katika mwili, lakini akifanywa hai katika roho.”
10. (a) Kusudi la Mungu katika ‘kutayarishia’ Mwanawe Yesu mwili wa nyama hapa duniani ilikuwa kusudi gani? (b) Ili Yesu apate kuishi tena baada kuuawa katika mwili kwa habari ya dhambi, ingempasa afufuliweje?
10 Kwa kumtuma Mwana wake mwenyewe kwa mfano wa mwili wenye dhambi, Mungu alikuwa amemtweza Mwanawe, akimfanya “mdogo punde kuliko malaika.” (Rum. 8:3; Ebr. 2:7-9; Zab. 8:5) Walakini Mungu hakukusudia kwamba Mwanawe pekee aendelee kuwa kiumbe cha mwili wa nyama na damu milele, kilicho cha hali ya chini kuliko malaika. Mungu alikusudia kumtukuza zaidi sana kuliko malaika kwa sababu ya uaminifu wake mpaka kufa katika mwili. Kwa hiyo mwili mkamilifu wa kibinadamu ambao Mungu ‘alimtayarishia’ Yesu duniani kwa mwujiza ndio mwili ambao Yesu alimtolea Mungu mara moja tu katika dhabihu. Ulitolewa ili wanadamu wapate kuula kama chakula; kama vile alivyosema Yesu: “Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.” (Ebr. 10:1-10; Yohana 6:51) Hivyo, baada ya yeye ‘kuuawa katika mwili,’ ikiwa Yesu angefufuliwa apate kuishi tena, angalipaswa ‘kufanywa hai katika roho,’ kama Mwana wa kiroho wa kimbinguni wa Mungu.
11. Ili wanafunzi wa Kristo waliozaliwa kwa roho wapate kuwa katika mfano wa ufufuo wake, lazima ‘wafanywe hai’ katika nini, nalo hilo Iapatanaje na 1 Wakorintho 15:42-54?
11 Kama vile ilivyokuwa kwa Yesu Kristo, wanafunzi wake waliozaliwa kwa roho lazima wawe ‘waaminifu mpaka kufa’ katika mwili. (Ufu. 2:10) Ili wapate kuunganishwa pamoja naye “katika mfano wa kufufuka kwake,” wao pia, kama vile yeye, wangepaswa ‘kufanywa hai katika roho,’ kama viumbe vya kiroho. Katika 1 Wakorintho 15:42-54, twasoma juu ya namna ya ufufuo wao:
“Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutoharibika; hupandwa katika aibu; hufufuliwa katika fahari; hupandwa katika udhaifu; hufufuliwa katika nguvu; hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho: Ikiwa uko mwili wa asili, na wa roho pia uko. Ndivyo ilivyoandikwa, Mtu wa kwanza, akawa nafsi iliyo hai; Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha. Lakini hautangulii ule wa roho, bali ule wa asili; baadaye huja ule wa roho. Mtu wa kwanza atoka katika nchi, ni wa udongo. Mtu wa pili atoka mbinguni. Kama alivyo yeye wa udongo, ndivyo walivyo walio wa udongo; na kama alivyo yeye wa mbinguni, ndivyo walivyo walio wa mbinguni. Na kama tulivyoichukua sura yake yule wa udongo, kadhalika tutaichukua sura yake yeye aliye wa mbinguni.
“Ndugu zangu, nisemayo ni haya, ya kuwa nyama na damu haziwezi kuurithi ufalme wa Mungu; wala uharibifu kurithi kutokuharibika. Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika, kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika. Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa. Basi huu uharibikao utakapovaa kutokuharibika, na huu wa kufa utakapovaa kutokufa, hapo ndipo litakapokuwa lile neno lililoandikwa, Mauti imemezwa kwa kushinda.”
UFUFUO MPYA
12. (a) Kwa kuwa ufufuo wa wale 144,000 unafanana na ufufuo wa Kristo, hilo laonyesha kwamba Kristo alipata ufufuo wa namna gani? (b) Ni kwa sababu huu ni ufufuo mpya, nalo ni jambo gani linaloufanya kuwa “ufufuo wa kwanza”?
12 Ufufuo wa namna hiyo kwenye kutokuharibika na kutokufa katika “mwili wa roho,” ndio unaoitwa katika Warumi 6:5 “mfano wa kufufuka kwake.” Hii inamaanisha kwamba Yesu Kristo mwenyewe alipata ufufuo wa namna hiyo, si kwenye uzima katika mwili wa asili uharibikao na wenye kufa ulio mdogo punde kuliko wa malaika, bali katika mwili wa kiroho na kama “roho yenye kuhuisha.” (1 Kor. 15:45) Sasa twaweza kufahamu sababu gani, baada ya kufufuka kwake, ilimpasa Yesu kuchukua umbo la kibinadamu pamoja na mavazi ili apate kuonekana na wanafunzi wake wakati wa zile siku 40 mpaka alipopaa kurudi mbinguni. Huu ni ufufuo mpya kweli kweli, usioonekana kwa macho ya kibinadamu. Umetangulia kufufuliwa kwa wanadamu wote kunakokuja. Vilevile ni wenye maana sana. Kwa hiyo unaitwa “ufufuo wa kwanza.” Ndio unaoitwa na mtume Paulo “ufufuo wa mapema.” Warithi wa shirika pamoja na Kristo 144,000 wanashiriki katika huo. (Flp. 3:11, NW) Hao ndio wanaosemwa habari zao katika Ufunuo 20:4-6, NW:
“Nao wakawa hai wakatawala pamoja na Kristo kwa miaka elfu. . . . Huu ndio ufufuo wa kwanza. Mwenye furaha na mtakatifu ni ye yote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hawa mauti ya pili haina mamlaka, lakini watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala kama wafalme pamoja naye kwa hiyo miaka elfu.”
13. Ufufuo huo wa kwanza utatoa tengenezo la kiserikali la namna gani kwa ajili ya faida ya wanadamu, nalo linaitwaje katika 2 Petro 3:13?
13 Hivyo, washiriki wa “Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo,” wanapata namna ile ile ya ufufuo kama Bwana-arusi, Yesu Kristo. Je! sisi tunafahamu na kuthamini hasa ni jambo gani litakalotokezwa na ufufuo huo? Unatoa baraza ya watawala wasioweza kuharibika wala kufa kwa faida ya wanadamu wote. Hakuna mtawala ye yote wa kidunia aliyepata kuwa na kutokufa huko. (1 Tim. 6:15, 16) Yesu Kristo na wafalme-makuhani wenzi wake 144,000 watakuwa bora kuliko serikali yo yote ya kidunia ambayo wanadamu wamepata kuwa nayo katika muda wa miaka elfu sita ya kuwapo kwao. Itakuwa serikali ya namna bora na iliyo ya juu zaidi ambayo Mungu angeweza kuwapa wanadamu. Itachukua mahali pa serikali zote za kibinadamu ambazo zimekuwa chini ya uongozi wa hila wa Shetani Ibilisi na mashetani zake. Mungu ataitumia ilete juu ya dunia taratibu yake mpya, kwa kuwa itakuwa “mbingu” mpya za kiserikali.—2 Pet. 3:13.
14. (a) Lazima jambo gani litokee kwa “mbingu” za kale zilizopo zilizo juu ya wanadamu? (b) Ni katika njia gani serikali hiyo mpya itakuwa “mbingu” katika njia halisi?
14 “Mbingu” za kiserikali zilizofanyizwa na wanadamu lazima ziondolewe, pamoja na Shetani Ibilisi mtegemezaji wazo, aliye “mkuu wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31) Zinakaribia uharibifu wazo katika “dhiki ile iliyo kuu” itakayofikia upeo wa uharibifu wake katika Har–Magedoni, wakati ambapo “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” itakapomletea ushindi mkuu Yehova, Mwenye Enzi Kuu wa mbingu na dunia. (Ufu. 16:14-16; 19:11-21; Dan. 2:44) Hizo “mbingu” mpya za kiserikali lazima zipate kuwa na mamlaka na kutawala pasipo upinzani. Lazima ziwe za kimbinguni, si kwa njia ya mfano tu, bali pia katika njia halisi, kwa kuwa na washiriki ambao ni watawala wa kiroho walio na ‘hali ya kimungu’ na kuwa wasioweza kufa wala kuharibika. (1 Pet. 1:4, HNWW) Macho yetu yatakuwa yenye kubarikiwa kweli kweli wakati tutakapoona kwa njia halisi yale ambayo mtume Yohana alipata kuona katika njozi, Maelezo yake ni yenye kuvutia sana:
“Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; kwa maana mbingu za kwanza na nchi ya kwanza zimekwisha kupita, wala hapana bahari tena. Nami nikauona mji ule mtakatifu, Yerusalemu mpya, ukishuka kutoka mbinguni kwa Mungu, umewekwa tayari, kama bibi-arusi aliyekwishwa pambwa kwa mumewe. Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja, nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.—Ufu. 21:1-4.—Kutoka Holy Spirit—The Force Behind the Coming New Order, Sura ya 9.