Hakuna Kudhuru Wala Kuharibu Katika Paradiso ya Kiroho
Makala hii ni ya kutumia kwa mafunzo ya kitabu ya kundi
1. Ni sifa gani za adili zinazoonyeshwa na yeye aliye Mfalme juu ya paradiso ya kiroho?
IMESEMEKANA kwamba uadilifu wa serikali yo yote ya kibinadamu waonyesha watu wenyewe wanaotawalwa walivyo. Haya ndiyo yamekuwa maoni yanayotolewa na wanasiasa wenyewe wa ulimwengu. Walakini, hivyo sivyo ilivyo miongoni mwa wale ambao sasa wanaikaa paradiso ya kiroho ambayo Yehova Bwana Mwenye Enzi Kuu amewasimamishia waabudu wake duniani. Kama Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote, Ndiye ameweka mtawala wao, Mfalme wao, juu yao. Hawakuchagua na kumtawaza Mfalme wao juu yao wenyewe, Mfalme wa mfano wao wenyewe na ambaye angekuwa mwenye kuachilia maisha yao ya kufuata vitu vya kimwili, yenye choyo na yenye dhambi. Badala yake, wale walio katika paradiso ya kiroho wanataka Mfalme mwenye mfano wa Yehova Mungu, nao wanataka wawe kama Mfalme wao aliyepewa na Mungu. Kiadili na kidini, wanataka kuwa walivyo kwa sababu ya alivyo Mfalme wao mwenye kumwogopa Mungu. Ndiyo, wao wanataka waonyeshe Mfalme wao wa Kimasihi alivyo kwa jinsi wao wenyewe walivyo, kwa heshima yake.
2, 3. Isaya 11:6-8 yasimulia kwa usemi gani mabadiliko ya utu yanayotokezwa katika raia za Mfalme wa Kimasihi?
2 Utu wa Mfalme wa Kimasihi wageuza katika njia bora na yenye kujenga, nyutu za raia zake walio katika paradiso ya kiroho. Unabii wa Isaya waelekeza kwenye upande huo. Mara akiisha kusimulia sifa na matendo ya Mfalme wa Kimasihi aliyeinuliwa na Yehova Mungu, nabii Isaya aendelea kusema hivi:
3 “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. Ng’ombe na dubu watalisha pamoja; watoto wao watalala pamoja; na simba atakula majani kama ng’ombe. Na mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia mkono wake katika pango la fira.”—Isa. 11:6-8.
4. (a) Ni jambo gani lisilo la kawaida juu ya simulio hilo, hasa juu ya wanyama-mwitu? (b) Je! hali hizo zimepata kuwako duniani wakati wo wote?
4 Katika mfano huo wa ajabu wa unabii, jambo fulani limegeuza sana wanyama, hasa wanyama-mwitu wa kondeni. Wanyama-mwitu hawawindi na kuwatafuna tena wanyama wa kufugwa. Wamekuwa wapole na wasiodhuru, wakiacha njia zao za kula nyama wakiwa wenye kula mboga au majani. Kwani, hivyo ndivyo ilivyokuwa katika dunia, ndiyo, katika Bustani ya Edeni, kabla Yehova Mungu hajamweka mwanamume na mwanamke mkamilifu humo. Na hata wajapoumbwa katikati ya dunia yenye kusongamana wanyama, Adamu na Hawa hawakuogopa kuumizwa nao, na wote wawili pia walikuwa wenye kula mboga. Hivyo ni kwa sababu gani mgeuzo huo katika wanyama wafananishwa katika unabii? Ni kwa sababu gani tunapewa kwa unabii mfano huu wa hali ya kutodhuru na yenye usalama?
5. Kwa wazi ni nini lililo kusudi la simulio hili lenye kupendeza?
5 Kwa wazi ni ili kufananisha yanayotukia katika jamii ya kibinadamu wakiwa chini ya utawala wa Hakimu-Mfalme wa Kimasihi, Yesu Kristo aliyetawazwa katika mbingu. Lakini bila shaka mambo yasingekuwa njia moja katika wanyama na njia nyingine katika wanadamu. Bila shaka njia moja yapaswa itoe mfano wa ile nyingine. Sehemu ya chini yapaswa ionyeshe mfano wa sehemu iliyo juu zaidi. Wapaswa uhusiano wa kiparadiso uenee miongoni mwao.
6. (a) Mgeuzo huo umetukia wapi, na tangu wakati gani? (b) Ni nini linalosababisha badiliko hilo?
6 Mgeuzo huo wa tabia za asili za muda mrefu haujatukia katika wanyama. Hapana, hata ijapo Mfalme wa Kimasihi amekuwa akitawala katika mbingu tangu mwisho wa Majira ya Mataifa katika mwaka wa 1914 W.K. Walakini, mgeuzo huo wa tabia zilizo katika wanyama ulikusudiwa uonyeshe mfano wa mgeuzo unaotukia katika jamii ya kibinadamu. Kupatana na kusudi hilo, mgeuzo huo kama ulivyotabiriwa na unabii juu ya wanyama umetukia kweli katika paradiso ya kiroho ya waabudu waliorudishwa wa Yehova. Jambo hili limekuwa hivyo tangu kukombolewa kwao katika Babeli Mkuu mwenye hatia ya damu, kuanzia mwaka wa 1919 W.K. Mgeuzo huu watukia kwa sababu ya utendaji wa “roho ya [Yehova],” na pia ni kwa sababu wakaaji wa paradiso ya kiroho wanatawalwa na Mfalme wa Kimasihi ambaye juu yake “roho ya [Yehova]” imekaa.—Isa. 11:1, 2.
7, 8. (a) Ni tabia za namna gani ambazo wengi ambao sasa wamo katika paradiso ya kiroho walikuwa nazo zamani na ni nini lililosababisha hili? (b) Waefeso 2:1-3 lahusu sawasawa wale walio katika paradiso ya kiroho kwa njia gani?
7 Si wote wale wanaokaa sasa katika paradiso ya kiroho ya kibali ya Mungu walikuwa wenye amani zamani kama mwana-kondoo au mwana-mbuzi au ng’ombe au kinono (mnyama mnono) mwenye kufugwa. Wengi, yaelekea umati mkubwa, walikuwa na tabia kama zile za mbwa-mwitu au chui au simba mdogo mwenye manyoya au dubu mkali au fira au nyoka mwingine mwenye sumu. Hasa hivyo, tangu ulimwengu ulipoingia ambacho kimeitwa “Kizazi chenye Jeuri” katika mwaka wa 1914, mwaka ulioonyeshwa kwa kutokea kwa vita ya kuenea dunia yote, vita ya ulimwengu. Hii haikuleta maendeleo katika tabia na maelekeo ya watu wote. Hata adili nzuri zilianza kupungua kwa kadiri zilivyo leo. Wale wote wanaokaa katika paradiso ya kiroho wanaweza kuambiwa sawasawa kama lilivyoambiwa kundi la Kikristo katika Efeso, Asia Ndogo, miaka 1900 iliyopita:
8 “Mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.”—Efe. 2:1-3.
9, 10. Mtume Paulo alieleza nini juu ya njia ya zamani ya maisha ya wale waliokuwa katika makundi ya Kikristo katika Korintho na Rumi?
9 Akieleza waziwazi namna washiriki wa kundi la Kikristo katika Korintho, Ugiriki walivyokuwa watu wa ulimwengu hapo zamani, mtume Paulo aliwaandikia hivi: “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti, wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi. Na baadhi yenu mlikuwa watu wa namna hii; lakini mlioshwa, lakini mlitakaswa, lakini mlihesabiwa haki katika jina la Bwana Yesu Kristo, na katika [roho ya] Mungu wetu.”—1 Kor. 6:9-11; tazama pia Wakolosai 3:5-8.
10 Pia, wakati alipokuwa akionya Wakristo wasizirudie njia zao za zamani za ulimwengu, mtume Paulo aliliandikia kundi katika Rumi, Italia hivi: “Tukiujua wakati, kwamba saa ya kuamka katika usingizi imekwisha kuwadia; kwa maana sasa wokovu wetu u karibu nasi kuliko tulipoanza kuamini. Usiku umeendelea sana, mchana umekaribia; basi na tuyavue matendo ya giza, na kuzivaa silaha za nuru. Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu. Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake.”—Rum. 13:11-14.
11. (a) Wengi wale ambao sasa wamo katika paradiso ya kiroho walionyeshaje wakati mmoja tabia kama zile za wanyama wakali? (b) Ni jambo gani lililotokeza badiliko katika nyutu zao?
11 Hivyo, yaelekea sana kwamba wengi wa wale zaidi ya milioni mbili wanaofurahia paradiso ya kiroho ya mpango wa Mungu leo, hapo zamani iliwapasa na bado yawapasa wapambane na tabia za ukali, maelekeo ya kinyama, yanayohusiana na wanyama wakali wanaotajwa katika Isaya 11:6-8. Katika muda huu wa vita vya ulimwengu, wengine kati ya wakaaji hao walishiriki kwa halisi mapigano hayo ya ulimwengu na vita vidogo-vidogo vya katikati, na kwa kweli walitenda kama wanyama-mwitu wenye njaa katika kuua au katika kutafuta kuua wanadamu wenzao. Wakaaji wengine walikuwa katika shughuli au matendo yanayofanya iwe kazi yao ya kutumia udhaifu wa mateka yao kwa faida ya kichoyo, pasipo kujali kwamba wanaumiza mateka yao kimwili na kimoyoni. Lakini sasa kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova wamebadili utu. Mfalme wake aliyewekwa wa paradiso ya kiroho, Mfalme wa Kimasihi ambaye juu yake roho ya Yehova imekaa, haruhusu kuwindana huko kwa kinyama ndani ya kao hili la kiroho la waabudu wa Yehova. (Efe. 4:20-24; Kol. 3:10, 11) Upendo wa ndugu wa Kikristo waenea katika Paradiso hiyo.
12. Maneno ya Yesu, kama yalivyoandikwa katika Mathayo 18:1-4 yanahusuje wale waliomo katika paradiso ya Kiroho?
12 Hivyo, kwa njia ya mfano, mbwa-mwitu mpole hulala pamoja na mwana-kondoo, pia chui pamoja na mwana-mbuzi, ndama na kinono na simba mdogo mwenye manyoya huchangamana pamoja wakati wo wote. Badala ya dubu kujilisha ng’ombe na wachanga wake, dubu na ng’ombe na wachanga wao hujilisha pamoja majani. Hata simba aonwa akila majani kama ng’ombe. Maneno haya ya Yesu Kristo Mfalme yamefuatwa katika paradiso ya kiroho: “Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni. Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.” (Mt. 18:1-4) Hivyo sasa iko kana kwamba mtoto mdogo ni kiongozi wa wanyama-mwitu wa kondeni.
13. Ni matumizi ya kanuni gani ya Maandiko yamewasaidia wafikie hali iliyotabiriwa na nabii Isaya, na namna gani hivyo?
13 Jambo linalosaidia katika hali hii yenye amani na ukosefu huu wa kuwindana kinyama katika paradiso ya kiroho ni kwa vile wakaaji wake huishi kwa kanuni ya kwamba wao si sehemu ya ulimwengu huu. (Yohana 15:19; 17:14-16) Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ya 1914 hadi 1918 W.K., wengine kati ya mabaki ya Israeli wa kiroho walikubali kufanya utumishi usio wa kupigana katika majeshi yenye kupigana, na kwa njia hiyo wakawa na hatia ya damu kwa sababu ya kushiriki kwao lawama la kijamii la damu iliyomwagwa katika vita. Walakini, katika 1939, mwaka ambao katika huo Vita ya Ulimwengu ya Pili ilitokea, mabaki wote wa Israeli wa kiroho na pia wote wale wa “mkutano mkubwa” wa wenzao walio mfano wa kondoo walijitangaza wenyewe kupendelea kutokuwamo kabisa katika mapigano yote ya kilimwengu, bila kujali taifa. Kuchapwa kwa makala “Kutokuwamo” katika toleo la Novemba 1, 1939, la The Watchtower kulionyesha maoni yao. Tangu wakati huo hawajaacha maoni haya wakati wo wote. Pia, kwa kupatana na haya hawakujitia kamwe au hata kushiriki siasa za taifa lo lote, ambazo pamoja nazo kuna maneno mengi sana yenye kukashifu na uchochezi wa uadui mwingi sana na chuki zenye kugawanya.
14. Ni tunda gani linalositawishwa katika paradiso ya kiroho, na hili lashirikije kutimiza yale yaliyotabiriwa katika Isaya 11:6-8?
14 Tunda la roho ya Yehova husitawishwa, kupatana na shauri la mtume Paulo: “Tunda la roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza. Juu ya mambo hayo hakuna sheria. Zaidi ya hayo, wale walio wa Kristo Yesu waliutundika mwili pamoja na nyege na tamaa zake. Ikiwa sisi tunaishi kwa roho, na tuendelee pia kutembea kwa utaratibu kwa roho. Na tusiwe wenye kujikuza wenyewe, tukiamsha kushindana mmoja na mwenzake, kuoneana kijicho.” (Gal. 5:22-26, NW) Kwa vile hakuna mashindano, kujikuza kwa makuu juu ya wengine, hakuna kusengenya kwenye kuleta uchungu au kinyongo. Ni kama kwamba nyoka mwenye sumu, hata fira, anajiona salama na kuchagua kutotumia sumu yake, ili mtoto anyonyaye acheze penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa karibuni apate kutia mkono wake katika pango la fira au nyoka mwenye sumu.
—Kutoka Kitabu Man’s Salvation Out of World Distress at Hand!, sura ya 11, yaendelea katika toleo litakalofuata.