Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 4/15 kur. 15-20
  • Mpate Kuzidi Sana Kuwa na Tumaini!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mpate Kuzidi Sana Kuwa na Tumaini!
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuwa na Maoni ya Kutazama Mbali
  • “Siku ya Kisasi” cha Yehova
  • Ulinzi Katika “Paradiso”
  • Dunia Inafanywa Iwe na Utukufu
  • “Tutaonana Paradiso!”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2018
  • Je, Una Sababu ya Kuamini Kwamba Kutakuwa na Paradiso?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Wenye Shangwe Sasa na Milele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Hakuna Kudhuru Wala Kuharibu Katika Paradiso ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 4/15 kur. 15-20

Mpate Kuzidi Sana Kuwa na Tumaini!

“Basi Mungu wa tumaini na awajaze ninyi furaha yote na amani katika kuamini, mpate kuzidi sana kuwa na tumaini, katika nguvu za [roho takatifu].”—WARUMI 15:13.

1, 2. (a) Paulo alitoa sababu gani ya ‘kuzidi sana kuwa na tumaini’? (b) Unabii wa Isaya unaelekezaje kwenye tumaini hilo?

TUPATE kuzidi sana kuwa na tumaini? Katika ulimwengu wenye giza jingi kama huu, ambamo uhalifu na ukosefu wa adili unatendeka kwenye barabara mbalimbali, ambamo njaa kuu au njaa inayokaribia kuwa kuu imewazunguka watu zaidi ya bilioni moja, na ambamo silaha za nyukilia ziko katika hali ya kuwafyatukia wanadamu wote kwa ghafula, kuna sababu gani ya ‘kuzidi sana kuwa na tumaini’? Muda mfupi tu kabla ya kuisema sala iliyoandikwa juu, mtume Paulo alitaja sababu fulani, akitumia maneno ya Isaya kwa kusema: “Kutakuwako mmoja anayeinuka kuyatawala mataifa; juu yake mataifa yatategemeza tumaini lao.”—Warumi 15:12, NW.

2 Hapo Paulo alikuwa akitumia maneno ya Isaya 11:1-10. Hayo ni matabiri ya watu wale wa mataifa ambao wanamtumainia Yesu, aliyefananishwa na Mfalme Daudi, mwana wa Yese. Katika kueleza habari za Huyo, Mathayo mwandikaji wa Gospeli anatumia pia maneno ya Isaya, kwa kusema: “Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; mpendwa wangu, moyo wangu uliyependezwa naye; nitatia roho yangu juu yake, naye atawatangazia Mataifa hukumu. . . . Na jina lake Mataifa watalitumainia.”—Mathayo 12:18-21; Isaya 42:1, 4.

3, 4. (a) Sasa Yesu ana “jina” gani, na kwa sababu gani? (b) Tutaelewa andiko la Ufunuo 19:10, 11 kuwa na maana gani?

3 Kwa sababu gani mataifa yatumainie jina la Yesu? Ni kwa sababu ya mambo yote yanayosimamiwa na jina hilo. Wakati alipokuwa mwanadamu hapa duniani, Yesu alijifanyia “jina” la kuwa mshika-ukamilifu asiye na kikosa. Wala mateso, wala mashutumu, wala kunyanyaswa-nyanyaswa wala cho chote hakikuweza kumfanya ayumbeyumbe aache kufanya mapenzi ya Mungu kwa ushikamanifu mpaka kifo chenyewe. “Kwa hiyo,” mtume Paulo anaeleza, “Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:9-11.

4 Sasa jina la Yesu linasimamia cheo cha juu ambacho Yehova amempa kwa kumtukuza awe Kuhani Mkuu na Mfalme kwenye “mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Ukuu mbinguni.” Yeye Ndiye anayeitwa “Mwaminifu na Wa-kweli,” ambaye neno lote la unabii linakaza fikira juu ya kuja kwake, “kwa maana ushuhuda wa Yesu ndio roho ya unabii.”—Waebrania 8:1; Ufunuo 19:10, 11.

5. Kwa sababu gani inatupasa, hasa leo, ‘tuzidi sana kuwa na tumaini’?

5 Kwa sababu gani sisi leo ‘tuzidi sana kuwa na tumaini’? Ni kwa sababu neno la unabii linaonyesha kwamba Yesu yuko karibu kuyaondoa madhara yote ambayo Adamu mtenda dhambi aliwaletea wanadamu. “Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.” (Warumi 5:19) Akiwa ndiye Kuhani Mkuu aliyewekwa na Mungu mbinguni, Yesu atatumia ubora wa dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu arudishe wanadamu wote watiifu, kutia ndani mabilioni ya wafu watakaofufuliwa, wafikie ukamilifu wa kibinadamu, wakiwa na taraja la kuishi milele kwa furaha katika dunia-Paradiso. Yesu “sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.” Halafu, wanadamu wote watafurahia ukamilifu wa uzima katika Paradiso hiyo yenye amani.—1 Wakorintho 15:25, 26; Zaburi 72:3, 7; Isaya 33:24.

Kuwa na Maoni ya Kutazama Mbali

6. (a) Ni kwa njia gani tu tunaweza kuwa na maoni ya kutazama mbali kuhusu makusudi ya Mungu? (b) Hilo linaweza kutufaidije?

6 Ni kupitia Biblia tu tunavyoweza kujua kusudi halisi la maisha. Ni Mungu tu, kupitia Neno lake, anayeweza kueleza tulitoka wapi, kwa sababu gani tupo hapa, na ni mambo gani yanayotungoja wakati ujao. (Isaya 46:9, 10; 2 Timotheo 3:16) Biblia inatupa maoni ya kutazama mbali juu ya utimizo wa makusudi ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu. Inatuambia namna tunavyoweza kuwa na ushirika wenye kuchangamsha sana katika kufanya mapenzi yake, tena tuweze kufanya hivyo kwa umilele wote unaokuja!—Zaburi 37:31, 34.

7. “Ishara” ya unabii wa Yesu imetimizwaje?

7 Sasa ile “ishara” ya unabii ambayo Yesu alitaja wakati wa umalizio wa huduma yake ya kidunia imetimizwa kwa njia kubwa sana. Sasa Yesu amekalia kiti chake kitukufu cha ufalme cha kimbingu, naye anayahukumu mataifa ya dunia na kutenganisha watu “kama vile mchungaji anavyotenga kondoo na mbuzi.” Jambo hilo linafanywa kulingana na vile wanavyouitikia ujumbe wa Ufalme unaotangazwa na “ndugu” za Kristo, wale mashahidi wapakwa mafuta wa Yehova ambao wangali wakitumikia Mungu hapa duniani. (Mathayo 24:3-14; 25:31-40, 46, NW ) Lakini je! jambo hilo halimfanyi Yesu alingane cheo na Yehova Mungu, au hata awe mkuu kuliko yeye?

8. (a) Kwa sababu gani Yehova akamfanya Yesu awe Mfalme mwenye kushirikiana naye? (b) Yesu ataonyeshaje anajitiisha kwa Baba?

8 Hapana, kwa maana “kichwa cha Kristo ni Mungu,” ambaye sikuzote ndiye “Mfalme wa milele” na Mwenye Enzi Kuu juu ya uumbaji wake wote. (1 Wakorintho 11:3; 1 Timotheo 1:17; Ufunuo 4:11) Wakati tu uasi ulipochomoza kwa njia mbovu katika Paradiso ya Edeni ndipo Yehova alitangaza kwamba angetokeza Mfalme mshirika—-ule “uzao” wa ahadi—“ili azivunje kazi za Ibilisi.” (Mwanzo 3:15; 1 Yohana 3:8) Lakini, Kristo akiisha kuondolea jina na enzi kuu ya Yehova malawama na kuinua wanadamu wafikie ukamilifu katika ile Paradiso itakayorudishwa duniani, ndipo “atakapompa Mungu Baba ufalme wake,” na Mwana huyo mwenyewe atajitiisha mwenyewe pia kwa Mungu.—1 Wakorintho 15:24-28.

9. (a) Isaya anaielezaje adhama ya Yehova? (b) Maandiko yanaonyesha ni nini kipitio cha kufuata ili kupata wokovu?

9 Akisema juu ya ‘Yehova, mwenye adhama,’ nabii Isaya anakiri hivi: “[Yehova] ndiye mwamuzi wetu; [Yehova] ndiye mfanya sheria wetu; [Yehova] ndiye mfalme wetu; ndiye atakayetuokoa.” Wokovu unatoka kwa Yehova, kupitia Kristo Yesu, na huo ni ukweli ambao ni lazima watu wote wanaotafuta uzima waukubali. (Isaya 33:21, 22; 12:2; Matendo 2:21; 4:12; Warumi 10:13; Ufunuo 7:10) Baada ya kumtaja Yehova kuwa Mwenye Adhama kuliko wote, nabii Isaya anaendelea kuonyesha namna yeye anavyookoa wale wanaompenda, kisha kusudi la kuwaokoa.

“Siku ya Kisasi” cha Yehova

10. Ni hukumu gani inayotamkwa kwenye Isaya 34:1-4, na kwa sababu gani?

10 Mataifa ya kilimwengu yana kumbukumbu la matendo mabaya sana ya utawala mbaya, nayo yameukataa Ufalme wa Mungu wenye uadilifu ulio mikononi mwa Kristo wake. Basi nabii Isaya anasema nayo, akiyaambia hivi: “Karibuni, enyi mataifa, mpate kusikia; sikilizeni, enyi kabila za watu; dunia na isikie, nacho kiijazacho, ulimwengu na vitu vyote viutokavyo. Maana [Yehova] ana ghadhabu juu ya mataifa yote, na hasira kali juu ya jeshi lao lote; amewaangamiza kabisa, amewatoa waende kuchinjwa. Watu wao waliouawa watatupwa nje, na uvundo wa maiti zao utapaa juu, na milima itayeyushwa kwa damu yao. Na jeshi lote la mbinguni litafumuliwa, na mbingu [serikali za kibinadamu ambazo hazikuleta matokeo mazuri] zitakunjwa kama karatsi, na jeshi lao lote litanyauka kama vile jani la mzabibu linyaukavyo na kupukutika, na kama jani la mtini linyaukavyo na kupukutika.”—Isaya 34:1-4.a

11. (a) Kwenye Isaya 34:5-7, Yehova anatangaza nini kuhusu Edomu? (b) Edomu ilikuwa nini, na ni nini chenye kufananishwa nayo wakati wa kisasa?

11 He, ni maneno yenye mkazo hayo! Tena hukumu ambayo Yehova mwenyewe anafuata kutamka baada ya hapo juu ya watu wa Edomu inaogopesha pia: “Maana upanga wangu [utakunywa] na kushiba mbinguni; tazama, utashukia Edomu, na juu ya watu wa laana yangu, ili kuwahukumu.” (Isaya 34:5-7) Taifa la Edomu, ambalo lilikuwa uzao wa Esau ndugu ya Yakobo (jina la pili la Esau likiwa ni Edomu), lilikuwa adui wa muda mrefu wa taifa la Israeli ambalo baba yalo alikuwa Yakobo. Na taifa hilo la Edomu lina ulinganifu wa kisasa. Ulinganifu gani? Ni nani ameongoza katika kutukana na kutesa Israeli wa kiroho wa karne ya 20? Je! si Jumuiya ya Wakristo yenye kuasi imani, kwa kutumia jamii yake yenye kiburi ya viongozi wa kidini? Si kwamba tu viongozi wa kidini wa pande zote mbili waliunga mkono kwa moyo wote vile vita vya ulimwengu viwili vilivyotokea katika karne yetu, bali pia waliongeza hatia yao ya damu kwa kuzifanya serikali za kilimwengu ziwapige marufuku na hata ziwaue Mashahidi wa Yehova, ambao wanawakilisha hapa duniani Yerusalemu, au Sayuni, wa kimbingu.

12. (a) Yehova analetaje malipo juu ya “Edomu”? (b) Ni kwa njia gani Mashahidi wa Yehova wamejitenga na dini za Jumuiya ya Wakristo?

12 Basi nabii wa Mungu anatangaza hivi: “Ni siku ya kisasi cha [Yehova], mwaka wa malipo, ili kushindania Sayuni.” (Isaya 34:8) Matokeo yanakuwaje kwa “Edomu” wa kisasa? Ni uharibifu, kama inavyoonyesha mistari inayofuata kwenye Isaya 34:9-17. Kwa kweli, tangu mwaka wa 1919 ulioifuata vita, dini za Jumuiya ya Wakristo zimekuwa kitu kilichokufa kwa njia ya kiroho, zimekuwa mahali palipoharibiwa pakawa patupu, kulingana na maoni ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu. Hizo ndizo sehemu iliyo kubwa zaidi ya ‘Babeli Mkuu,’ ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo yenye hatia ya umwagaji wa damu, ambayo ilipatwa na anguko kubwa la kiroho baada ya vita ya ulimengu ya kwanza, ikalaaniwa na Yehova. Mashahidi wa Yehova wamejitenga na “Edomu” huyo wa kisasa aliyekwisha kufa kiroho. Wao hawana ushiriki wo wote katika makundi yake yenye kushirikiana katika imani zinazotofautiana, wala katika misukosuko yake ya kisiasa wala katika madhehebu zake mbalimbali zinazojionyesha. Karibuni sana mfumo huo wenye kuasi imani utafagiwa uachwe utupu kabisa, wakati “siku ya kisasi” cha Yehova itakapoijilia dunia yote.—Ufunuo 14:8; 18:2, 4, 24; 19:11-21.

Ulinzi Katika “Paradiso”

13. Isaya anaelezaje tukio la kurudi kutoka “Babeli” ya kisasa?

13 Kwa kutumia mtungo mtamu wa maneno ya kishairi, ndipo Isaya sura ya 35 inapoeleza kurudi kwa mabaki ya Israeli wa kiroho kutoka katika utumwa wa ‘Babeli Mkuu,’ nayo inafikia upeo wa mtungo huo kwa maneno haya: “Na hao waliokombolewa na [Yehova] watarudi, watafikia Sayuni wakiimba; na furaha ya milele itakuwa juu ya vichwa vyao; nao watapata kicheko na furaha, huzuni na kuugua zitakimbia.” Hiyo ni paradiso ya kiroho kweli kweli, nayo inatukumbusha maneno ya Isaya 51:3: “Maana [Yehova ataufariji] Sayuni; [atapafariji] mahali pake palipokuwa ukiwa; [atafanya] jangwa lake kuwa kama bustani ya [Edeni], na nyika yake kama bustani [paradeison (paradiso), Septuagint Version] ya [Yehova].”

14. (a) Paulo alieleza habari ya paradiso gani? (b) Paradiso hiyo inafananishwaje kwenye Isaya 35:1-7, na ni nani anayeweza kushiriki humo?

14 Leo watu wa Yehova waliopakwa mafuta wamekwisha kuingia kweli kweli katika paradiso ya kiroho! Inasimuliwa vizuri sana katika Isaya 35:1-7! Inalinganika na ile ambayo mtume Paulo anasimulia kwenye 2 Wakorintho 12:3, 4, ZSB, kwa wazi akitaja jambo lililompata yeye mwenyewe: “Nami ninajua mutu huyu (kama katika mwili, kama inje ya mwili, sijui: Mungu anajua,) ya kama alichukuliwa juu hata Paradiso, akasikia maneno yasiyoweza kusemwa na yasiyofaa mutu kuyasema.” Lakini leo inafaa kusema habari za paradiso ya kiroho ambayo sasa ipo kati ya mabaki ya Mungu yaliyopakwa mafuta, ambamo pia ‘mkutano mkubwa wa mataifa yote’ umeingia uishiriki! Humo linasitawi kati yao tengenezo lenye ufanisi wa kupendeza sana, ile jamii ya duniani pote ya Mashahidi wa Yehova, iliyoungana kwa umoja katika kifungo cha upendo na katika umoja wa kusudi na tendo. Paradiso ya kiroho kweli kweli!

15. (a) Zaburi 91 inaonyesha nini juu ya paradiso ya kiroho? (b) Ni ulizo gani linalotokezwa juu ya “mkutano mkubwa,” na kwa sababu gani?

15 Maadamu Mashahidi wa Yehova wanaendelea kusitawisha hiyo paradiso ya kiroho, wao hawatapatwa na madhara ya silaha wanazotupiwa na Shetani. (Zaburi 91:1-11) Kwa habari ya mabaki yaliyopakwa mafuta ya Israeli wa kiroho, ule unabii mbalimbali wa Isaya ulio bora unaohusu kurudishwa unatimizwa sasa kwa njia nzuri sana. Lakini hesabu ya wapakwa mafuta hao walio duniani imepungua-pungua ikawa chini ya 10,000—hiyo ikiwa ni asilimia 0.4 ya Mashahidi wote. Hesabu iliyo kubwa zaidi ya makundi 45,000 ya Mashahidi wa Yehova leo haina wapakwa mafuta wo wote katikati yao. Kwa hiyo namna gani juu ya yale mamilioni ya “mkutano mkubwa”? Ni kweli kwamba wao wanazishiriki pamoja na mabaki yaliyopakwa mafuta katika furaha za paradiso ya kiroho. Lakini je! hatulioni tumaini zuri sana walilo nalo la kuwa katika dunia-Paradiso iliyofananishwa katika unabii uo huo mbalimbali?

Dunia Inafanywa Iwe na Utukufu

16. (a) Ni wapi na ni namna gani lazima kusudi la Mungu litetewe kwa kuondolewa malawama? (b) Ni kwa njia gani tu mwanadamu anaweza kustahili kupata uzima katika Paradiso? (c) Jambo hilo tena limewezeshwaje?

16 Kumbuka kwamba ni hapa duniani, katika Edeni, ambapo Paradiso ilipotezwa. Basi, ni hapa ndipo lazima kusudi la Yehova kuelekea dunia na mwanadamu litetewe kwa kuondolewa malawama. Ni lazima dunia ifanywe Paradiso ya duniani pote kwa ajili ya wanadamu, kupatana na kusudi la Yehova la kwanza kabisa. (Mwanzo 1:27, 28) Paradiso ya Kiedeni haikufanyizwa tu na amani iliyokuwa kati ya mtu na wanyama, na upendezi wayo wa kibustani. Mtu aliyefanywa kwa mfano wa Mungu alikuwa safi kiadili, na alipaswa kubaki akiwa hivyo, ili aweze kuendelea kuwa sehemu ya tengenezo kuu la Mungu. Alipaswa kumtii Muumba wake ndipo aweze kubaki akiwa mkamilifu, akiwa bila magonjwa, kifo na elekeo lo lote la kutenda makosa. Adamu alishindwa kubaki akiwa hivyo. Kwa hiyo ili Paradiso ya kidunia irudishwe, ilikuwa lazima mwanadamu mwenye dhambi ainuliwe tena afikie ukamilifu, na jambo hilo lingewezeshwa kupitia dhabihu ya ukombozi wa Yesu.—Warumi 5:12, 18.

17. (a) “Mkutano mkubwa” unapataje ruhusa ya kuingia ndani ya paradiso ya kiroho? (b) Kulingana na Maandiko, wao wanaendelea kutayarishwaje kwa ajili ya uzima wa milele—wapi?

17 Leo, dunia haikaribii hata kidogo kuwa paradiso. Hata hivyo ule “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” umeingia ndani ya paradiso ya kiroho. (Ufunuo 7:9; Yohana 10:16) Kwa njia gani? Ni kwa kuweka maisha yao wakf kwa Yehova, kujipatanisha na matakwa yake na kushirikiana na mabaki wapakwa mafuta ambao wamekwisha kuingizwa ndani ya paradiso ya kiroho tangu mwaka wa 1919 na kuendelea. (Linganisha Ezekieli 38:8-16.) Wakiwa humo wanaendelea kutayarishwa kwa ajili ya uzima katika Paradiso ya kidunia itakayokuwako baada ya ile dhiki itakayotukia kwenye Har–Magedoni. Kwa kadiri dunia inavyohusika, Paradiso itakayorudishwa juu yake itadumu milele, kwa utukufu wa Mungu. Mfalme Daudi alitoa unabii juu ya dunia, akisema: “Bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” Ndiyo, Yesu alisema, “heri wenye upole; maana hao watairithi nchi.”—Zaburi 37:11; Mathayo 5:5.

18. “Utukufu wa [Yehova]” utaonwaje katika Paradiso ya kidunia?

18 Katika Paradiso hiyo ya kidunia, wanadamu wote (kutia ndani wenye kufufuliwa duniani) ambao watatii watumie dhabihu ya ukombozi wa Yesu ili kujifaidi watafurahia baraka kama zile zilizoelezwa na Isaya na manabii wengine kuhusu Israeli wa kiroho. Jambo la kufurahisha ni kwamba ahadi ambayo Yesu alimpa mwivi yule aliyemhurumia kwenye mti wa huko Kalvari itatimizwa kwa njia nzuri sana. (Luka 23:43, NW ) “Utukufu wa [Yehova], ukuu wa Mungu wetu,” utaonwa kwa macho halisi wakati nyika na jangwa zitakapochanua maua, na wakati vipofu, viziwi, vilema na mabubu watakapoponywa. Wakati Paradiso hiyo yenye amani itakapokuwa ikiendelea kupanuka duniani pote, lo, hata “simba atakula majani kama ng’ombe,” kama vile ambavyo bila shaka alikula katika Edeni na katika ile safina ya siku za Noa. Hakuna mtu ‘atakayefanya dhara lo lote wala kusababisha uharibifu wo wote’ katika Paradiso.—Mwanzo 1:29, 30, UV; Isaya 11:6-9, NW; 35:1-7; 65:25, UV.

19. (a) Andiko la Isaya 25:6-8 linatanguliaje kutimizwa? (b) Litatimizwaje pia kuelekea wale watakaoishi duniani?

19 Andiko la Isaya 25:6-8 linaonyesha kwamba paradiso ya kiroho ndiyo inayotangulia kutokea kabla ya ile halisi. Unabii huo umetimizwa kiroho leo katika paradiso ya kiroho, ambamo watu wa Yehova wamefufuliwa wafurahie “karamu” yenye utele. (Linganisha Ezekieli 37:1-6.) Kwa sababu ya kuamini kwao, wamejawa na furaha na amani, nao wamezidi sana katika tumaini la kupata baraka za Ufalme. (Warumi 15:13) Isaya alitabiri hivi: “Bwana [Yehova] atafuta machozi katika nyuso zote.” Unabii huo umepata utimizo mzuri sana kuelekea mabaki wapakwa mafuta, ambao wamerudishwa kwa kuondolewa katika ‘Babeli Mkuu,’ kabla ya Har–Magedoni. Na andiko la Ufunuo 7:17 linatumia maneno ayo hayo kuhusu hali yenye baraka ya “mkutano mkubwa” leo. Zaidi ya hilo, maneno ya Isaya yametumiwa kuhusiana na “nchi mpya,” kwenye Ufunuo 21:3, 4, ambako tunasoma hivi: “Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi katika macho yao,” Katika “nchi mpya” ahadi iliyo nzuri itatimizwa katika Paradiso itakayorudishwa katika dunia itakayokuwa imesafishwa.

20. Kwa sababu gani watumishi wote wa Mungu sasa wana sababu zote za ‘kuzidi sana kuwa na tumaini’?

20 Kwa uhakika, mabaki wapakwa mafuta, pamoja na ule “mkutano mkubwa,” wana sababu zote za ‘kuzidi sana kuwa na tumaini’ wakati matimizo yenye utukufu ya neno la Mungu la unabii yanapoendelea kutimia mbele ya macho yao. Tumaini halitakatishwa tamaa liwe la bure, kwa maana ni lazima ahadi zote zilizo bora za Yehova zije kutimia mwishowe. Basi, acheni ‘tupate faraja iliyo imara, tukimbilie kuyashika matumaini yale yawekwayo mbele yetu.’—Warumi 15:13; Waebrania 6:18. —Kutoka w11/15/83.

[Maelezo ya Chini]

a Ona kitabu Man’s Salvation out of World Distress at Hand! (kilichochapishwa na Sosaiti), kurasa 205-241, ili upate kwa urefu habari nyingine zinazohusu unabii huu.

Wewe Unakumbuka?

□ Sisi tunaweza ‘kuzidi sana kuwa na tumaini’ kwa sababu ya nini kinachohusiana na jina la Yesu?

□ Cheo cha Yesu cha kutukuzwa kinahusianaje na kile cha Yehova?

□ Isaya sura ya 34 inaonyesha nini juu ya “siku ya kisasi” cha Yehova?

□ Tunajifunza nini kutokana na Isaya sura ya 35 na 25:6-8 juu ya “paradiso”?

[Picha katika ukurasa wa 17]

“Ni siku ya kisasi cha [Yehova]”

[Picha katika ukurasa wa 19]

Paradiso ya kiroho inatoa ulinzi wa kutokupatwa na “tauni” ambazo sasa zinawapiga wanadamu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki