Zishikeni Sana “Habari Njema”!
“Mnaushika sana, isipokuwa, kwa kweli, mlikuwa waamini bila kusudi.”—1 Kor. 15:2, NW.
1. Kwa sababu gani Paulo alitoa hoja kwa bidii juu ya ufufuo?
MTUME Paulo anaimalizia barua yake aliyowaandikia Wakorintho kwa mazungumzo ya ufundi juu ya ufufuo. Ni kwa sababu gani alitoa hoja za ufufuo kwa bidii hivyo? Ilikuwa kwa kusudi la wakati wake. Wakristo hao Wakorintho walikuwa wamezungukwa na ulimwengu wenye pupa, uliopotoka, na wengine walikuwa hata wametumbukia katika mitego ya Shetani. Paulo hakutaka ndugu zake wapendwa wawe “waamini bila kusudi,” kwa maana kufanya hivyo kungemaanisha uharibifu kwao. Mahali pake, alitaka wawe imara katika “habari njema” alizowatangazia.
2. (a) Kwa sababu gani sisi leo tunapaswa kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya “habari njema”? (b) Ufufuo unafungamanishwaje na “habari njema”?
2 Vivyo hivyo leo, tunaishi katika ulimwengu usiomjua Mungu. Kwa hiyo, sisi ambao ‘tunamtumaini Mungu aliye hai’ lazima tufanye kazi kwa bidii na kujikaza kwa ajili ya “habari njema.” (1 Tim. 4:10) Hizi “habari njema” sasa zinaelekeza fikira juu ya “ufalme wa Bwana wetu [Yehova] na wa Kristo wake.” Ni kupitia ufufuo Kristo Yesu na wafalme washirika wake 144,000 wanaupata ufalme huo, mlima Sayuni wa kimbinguni. Vilevile, ni kupitia ufufuo kwamba walio wengi sana kati ya wanadamu watayapokea makao ya kidunia ya Ufalme huo. (Ufu. 11:15; 14:1; 20:12) Kwa hiyo, ufufuo ni sehemu ya maana sana ya “habari njema.”
TUMAINI LA UFUFUO
3. Fundisho la ufufuo linapinganaje na lile la nafsi isiyokufa?
3 Basi, ni nini tumaini la ufufuo? Hilo si tumaini ambalo msingi wake ni dhana (wazo) la kutokufa kwa nafsi, kama inavyofundishwa na milki ya ulimwengu ya dini ya uongo, ndani na nje ya Jumuiya ya Wakristo. La, ni tumaini la nafsi yenye kufa! Neno “ufufuo” (Kigiriki, a·naʹsta·sis) linaonekana mara 40 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Linamaanisha kuwa hai tena. Ili kufufuliwa tena kuingia kwenye uzima, lazima kwanza mtu awe mfu, kwa maana uhai ni kinyume cha kifo—Kum. 30:19, 20; Isa. 38:17-19.
4. Ni nini kinachoonyesha kwamba Wayahudi wa kwanza waliamini ufufuo wa kidunia wala si nafsi isiyokufa?
4 Katika Maandiko ya Kiebrania, hakuna fundisho la kutokufa kwa wanadamu. Wazo hilo lilikuwa geni kabisa kwa Wayahudi. Hata hivyo, kuna vionyesho vingi kwamba wao waliuamini ufufuo wa kidunia. Kwa wazi hiyo ndiyo sababu walidhani kwamba Yesu alikuwa ‘Yohana Mbatizaji, Eliya, Yeremia au nabii mwingine’ aliyekuwa ameinuka.—Mt. 16:14
5. Kupatana na kusudi la Mungu, Ibrahimu na watumishi wa Mungu wengine wa kale walitazamia nini?
5 Baada ya kusimulia mwendo wa uaminifu wa Habili, Henoko, Noa na lbrahimu na nyumba yake, mtume Paulo atuambia hivi: “Hawa wote wakafa katika imani, wasijazipokea zile ahadi bali wakaziona tokea mbali na kuzishangilia, na kukiri kwamba walikuwa wageni na wasafiri juu ya nchi.” Wao walitazamia ufufuo ambao ungekuwa duniani chini ya utawala wa ‘mji wenye misingi halisi’—ufalme wa Mungu kupitia Masihi. Alipojaribiwa kuhusiana na kumtoa Isaka, Ibrahimu mwaminifu alitambua ‘Mungu aweza kumfufua hata kutoka [kwa wafu].’ Vilevile, Ibrahimu aliiamini ahadi ambayo Mungu alimpa kwamba “katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.” Ni jambo la akili kwamba walio wengi kati ya watu wa mataifa wangehitaji kufufuliwa ili wafurahie baraka hizo kupitia “uzao” huo.—Mwa. 22:18; Ebr. 11:4-19.
6. Maneno ya Ayubu na ya wana wa Kora yanaonyesha nini juu ya ufufuo huo?
6 Baadaye, Ayubu aliyeendelea kuwa mkamilifu aliuliza hivi: “Mtu akifa atakuwa hai tena?” Ayubu aliamini kwamba mtu angeweza kuishi tena. Na alionyesha imani hiyo kwa kumwuliza Mungu amfiche katika Sheol (kaburi la kawaida la wanadamu) na kumkumbuka baada ya wakati uliowekwa. (Ayubu 14:13-15) Katika Zaburi 45:16, NW, wana wa Kora walitabiri kwamba Masihi angekuwa na “wana” ambao angewaweka wawe “wana wa kifalme katika dunia yote,” wakati wa utawala wake wa mileani. “Wana” hao wangetia “babu” zake wenye kustahili ambao angekuwa kwao baba kupitia ufufuo kwa wafu.—Mt. 1:1-16; Luka 3:23-38.
7. (a) Maandishi ya manabii yanaungaje mkono tumaini la ufufuo wa kidunia? (b) Kwa sababu gani ufufuo wa Danieli na wengine utakuwa “ufufuo ulio bora”?
7 Manabii walioongozwa kwa roho ya Mungu vilevile walizungumza juu ya ufufuo, ambao waliufahamu kuwa wa kidunia. (Isa. 25:8; 26:19; Hos. 13:14) Alipokuwa akikaribia kifo, Danieli mwenye umri mkubwa alipokea ahadi hiyo: “Wewe utapumzika, walakini utasimama kwa ajili ya fungu lako mwishoni mwa siku hizo.” (Dan. 12:13, NW) Danieli, ambaye ‘kwa imani . . . [hata] alifunga vinywa vya simba,’ alitazamia “ufufuo ulio bora.” Huo ungekuwa ufufuo kwenye uzima chini ya ufalme wa Mungu uliosimamishwa, tofauti na yaliyotimizwa na Eliya, Elisha, Yesu na mitume katika kuwafufua watu ambao baadaye walikufa tena.—Ebr. 11:33, 35.
8. Wajumbe wa Yohana na Martha pia walikuwa na maoni gani juu ya ufufuo?
8 Baada ya Yesu kuanza huduma yake, mbatizaji aliyekuwa mfungwa, Yohana, alipeleka wajumbe wakamwulize Yesu kama ndiye aliyekuwa Masihi kweli kweli. Baada ya kufanya maponyesho zaidi ya kimwujiza, Yesu aliwaambia: “Nendeni mkamweleze Yohana hayo mliyoyaona na kuyasikia; vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, maskini wanahubiriwa habari njema.” (Luka 7:19-23) Hivyo, Yesu alikuwa akithibitisha kwamba ndiye aliyekuwa Masihi na pia alikuwa akijenga imani katika yale ambayo angetimiza kupitia ufalme wake hata kuwafufua wafu. Watu hao walifahamu kuwa huo ulikuwa ufufuo juu ya dunia. Ndivyo na Martha, wakati baadaye alipomwambia Yesu juu ya Lazaro mfu: “Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.”—Yohana 11:24.
UFUFUO WA KIMBINGUNI
9. Lazaro aliwezaje kupokea tumaini la ufufuo wa kimbinguni?
9 Kama Yesu hangemfufua Lazaro wakati huo, tumaini lake lingekuwa la kidunia kwa hakika. Walakini Yesu aliufanya mwujiza huo wa kumrudisha Lazaro kwa muda kutoka kwa wafu. Bila shaka, Lazaro aliokoka na akaipita siku ya Pentekoste, 33 W.K., na hiyo ingemaanisha angepokea kibali ya ziada kutoka kwa Bwana yake. Kwa maana katika siku hiyo ya Pentekoste angezaliwa kwa roho ya Mungu awe na tumaini la uzima wa kimbinguni, pamoja na taraja la ufufuo wa kimbinguni mbele yake. Nafasi hiyo ilifunguliwaje?
10. Ni maoni gani yenye makosa yaliyotokea katika siku za Paulo, walakini yeye alithibitishaje kwamba yalikuwa yenye makosa?
10 Katika barua yake ya kwanza aliyowaandikia Wakristo wa Korintho, mtume Paulo anazungumza juu ya ufufuo. Wengine katika kundi huko walikuwa wakibisha kwamba “hakuna ufufuo wa wafu.” Kwa wazi walikuwa wamechukua maoni ya kwamba Wakristo waliokuwa wakiishi wakati huo walikuwa wamepata namna fulani ya “ufufuo” wa kiroho, na pengine wengine walikuwa wakiunganisha jambo hilo na falsafa (filosofia) ya Plato ya kutokufa kwa nafsi. Hata maelezo ya kindani ya maoni yao yenye makosa yawe yalikuwa nini, Paulo aliona inafaa ‘kuwanyosha’ kwa kutoa hoja ya ufundi kwa ajili ya fundisho la kweli juu ya ufufuo, na kuweka mkazo juu ya ‘habari njema ambazo kupitia hizo walikuwa wakiokolewa.’—1 Kor. 15:1, 2, 12, NW.
11. “Habari njema” zinahusianaje na tumaini la ufufuo?
11 “Habari njema” hizo ni nini? Msingi wake ni Kristo. Kati ya ‘mambo ya kwanza’ ya umaana Paulo anatia uhakika wa kwamba Kristo alikufa, akazikwa, akafufuliwa, na kwamba alitokea, kwanza Kefa (Petro) kisha akatokea mara mbalimbali watu mia tano na wengine zaidi na mwishowe kwa Paulo mwenyewe. Kweli kweli, Kristo alikuwa amefufuliwa katika roho! (1 Pet. 3:18) Kama ambavyo Paulo alikazia mara mbili, matukio hayo yenye kuchochea yalikuwa ‘yanalingana na Maandiko,’ yakithibitisha yote ambayo neno la Yehova lilikuwa limetabiri kumhusu Masihi. Imani yetu ingekuwa bure kama isingalikuwa imetiwa nanga kwa uhakika wa kwamba Yesu Kristo alikuwa amefufuliwa.—1 Kor. 15:3-8, 17, NW.
“KILA MTU KATIKA MAHALI PAKE PENYE UTARATIBU’’
12. Kristo anakuwa “matunda ya kwanza” kwa njia gani?
12 Baadaye sana, mtume huyo anahusianisha ufufuo pamoja na makusudi ya Ufalme ya Yehova. Akiwa na uhakika Paulo anatangaza hivi: “Sasa Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu, matunda ya kwanza ya wale ambao wamelala katika mauti.” Ikiwa Kristo ni “matunda ya kwanza” basi, lazima vilevile kuwe wengine wanaofufuliwa, “walakini kila mtu katika mahali pake penye utaratibu.” Lazima wengine wangojee mpaka wakati wa “kuwapo” kwa Kristo akiwa na uweza wa Ufalme, wakati mkombozi, Yesu Kristo, anapoanza ‘kuwafanya hai’ wale ‘wanaokufa’ au wale ambao wamekufa kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa kutoka kwa Adamu.—1 Kor. 15:20-23, Kingdom Interlinear.
13. Ufufuo unafanywaje kulingana na “cheo”?
13 Baada ya Kristo, watakaofufuliwa ‘katika mahali pao penye utaratibu panapofaa’ watakuwa wale 144,000 ambao ni warithi wa Ufalme waliotiwa mafuta, ambao wamefuata hatua za Yesu mpaka kufa. Ufufuo huo unaanza “wakati wa kuwapo [Kigiriki, parousia] kwake,” ambako kulianza katika mwaka wa 1914 wenye matukio ya maana. Wachache wanaosalia wa “ndugu” za kiroho wa Kristo wangali wanatumikia duniani, na hawa pia watafufuliwa “katika cheo” hicho, “katika kufumba kwa jicho” wakati wa kifo chao cha kibinadamu. Hivyo “Israeli [ya kiroho] ya Mungu” yote itakusanywa pamoja kwenye ufalme wa kimbinguni—1 Kor. 15:22, 23, 50-52; Ebr. 2:10-13; Ufu. 7:4-8; Gal. 6:16.
14. Paulo anauonyeshaje ufufuo wa kimbinguni?
14 Mtume huyo anaonyesha vizuri kwa njia ya mfano kufa na kufufuliwa kwa Wakristo waliozaliwa kwa roho. Anafanya hivyo kwa kufananisha na kifo cha nafaka ya ngano au ya nyinginezo, ambayo katika hiyo mmea mpya unachipuka. Ndiyo, mwili ‘unaopandwa kuharibika’ ‘unafufuliwa katika kutokuharibika’ kama mwili wa kiroho wenye utukufu ‘unaofana na mfano wa Adamu wa mwisho’—Bwana Yesu Kristo.—1 Kor. 15:35-49, NW.
15. “Ufufuo ulio bora” unatokea wapi, na ni nani wanaotiwa ndani?
15 Hata hivyo, je.’ wale 144,001, kutia Kristo, ndio wa pekee kufufuliwa katika utaratibu unaofaa? Hapana kabisa! Kwa maana Waebrania 11:40 inatuambia kwamba ufufuo wao ni “kitu kilicho bora,” makao ya kiroho ya kimbinguni. Ni bora kuliko nini? Ni bora zaidi ya makao wanayopata wale wanaofufuliwa katika ufufuo unaofuatia katika utaratibu huo! Lazima ufufuo utie wale watakaofanywa kuwa “wana wa kifalme katika dunia yote,” na wale ambao kwa kufaa watakuwa kati ya wa kwanza kufufuliwa duniani baada ya ushindi kamili wa Yehova kwenye pigano la Har–Magedoni. Hivyo wataweza kuchukua kazi zao walizogawiwa katika “dunia mpya”—jamii ya kitheokrasi ya watu wa Mungu katika dunia iliyosafishwa. Wao ni ufufuo ulio bora,” kwa maana unatokea chini ya ufalme wa Mungu, pamoja na taraja la uzima wa milele kwa wale waliofufuliwa. Katika kipindi hicho cha wakati twatazamia kuwapata Wakristo waaminifu waliojiweka wakf ambao leo wana tumaini la kidunia na wanaokufa kutokana na visababisho mbalimbali kabla ya kuja kwa “dunia mpya.”—Isa. 32:1; Ufu. 16:14, 16; 21:1, 3, 4, NW.
KIKUNDI CHENYE PENDELEO
16. Ni kikundi gani kingine kinachofurahia pendeleo pekee, na hawa wanashiriki mapendeleo gani?
16 Hata hivyo, kuna kikundi kimoja ambacho kimependelewa sana-sana. Na hao ni nani? Wao ndio ule “mkutano mkubwa” ambao mtume Yohana anasimulia kwa maelezo mengi katika Ufunuo 7:9-17. Tumaini lao ni uzima wa milele katika “dunia mpya.” Wakiwa kikundi wanaipita ile “dhiki iliyo kuu” pasipo kufa kamwe. Ni pendeleo lenye thamani kama nini ambalo wao wanafurahia kama matokeo ya ‘kufua mavazi yao na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo’! Katika kipindi hicho cha mwisho chenye maana zaidi kabla ya “siku za mwisho” wakati ambapo ushuhuda wenye kuvuma pote lazima utolewe kwa mataifa na watu wa dunia, huu “mkutano mkubwa,” wenye hesabu ya zaidi 2,300,000 kwa sasa, unaonekana ukitoa huo “utumishi mtakatifu” katika nyua za kidunia za mpango wa ibada wa Yehova. Huu “mkutano mkubwa” haupatwi na “hari” [joto lenye kuchoma] ya hukumu ya kimungu. Kwa sababu gani? “Kwa maana huyo Mwana-Kondoo [Yesu Kristo], aliye katikati ya kiti cha enzi [cha kimbinguni], atawachunga, naye atawaongoza kwenye chemchemi ya maji yenye uhai, na Mungu atayafuta machozi yote katika macho yao.”
17. (a) Ni furaha gani inayongojea “mkutano mkubwa”? (b) Mwujiza wa ufufuo utasongaje kufikia mwisho wake?
17 Bila shaka “mkutano mkubwa” utakuwa wenye furaha utakapokuwa ukisonga na kuingia kwenye dunia iliyosafishwa na kuwakaribisha watu waaminifu waliofufuliwa. Kisha, vilevile, katika wakati wake Mungu na katika mpango wa utaratibu, mabilioni ya wanadamu katika “makaburi ya ukumbusho” watatoka kuingia katika dunia kupitia ufufuo wa watu wote. (Yohana 5:28, 29, NW; Ufu. 20:12) Jamii ya “dunia mpya” inapoanza kufanya kazi, na Kristo na watawala wenzake wanapotumia faida za dhabihu yake ya ukombozi katika kuwaponyesha wanadamu na kuwainua katika ukamilifu wa akili na mwili kutakuwa na shangwe kama nini kati ya jamaa za wanadamu zenye furaha na umoja!—Isa. 65:17, 18; 2 Pet. 3:13.
18. Kusudi bora la Mungu juu ya dunia yetu litafikiaje ukamilisho walo kamili?
18 Miaka elfu moja itapita kama siku moja, kwa maoni ya Yehova. (2 Pet. 3:8) Kisha dunia itajawa na wanadamu wakamilifu kama ambavyo Yehova alikusudia hapo kwanza alipomwumba mwanadamu miaka 7,000 kutangulia hapo. “Siku” yake ya miaka 7,000 ya mapumziko itakuwa imefikia mwisho wake, na haitakuwa imekuwa kazi bure, kwa maana makusudi yake makuu kuelekea dunia yatakuwa yametimizwa. Halafu sasa kutafuata nini?
19. Ni jambo gani litakalotokea baada ya “adui ya mwisho’’ kubatilishwa?
19 Mtume Paulo anatuambia hivi: “Halafu, mwishowe, wakati [Kristo] anampa Mungu wake na Baba ufalme, wakati amebatilisha serikali zote na mamlaka zote na uwezo [unaopinga]. Kwa maana lazima yeye atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka adui zote chini ya miguu yake. Kwa kuwa adui ya mwisho, kifo, atabatilishwa. . . . ndipo Mwana mwenyewe pia atakapojitiisha kwa Yeye aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe mambo yote kwa kila mtu.” (1 Kor. 15:24-28, NW) Kisha Shetani atafunguliwa kama inavyosimuliwa katika Ufunuo 20:7-10, ajaribu ukamilifu wa kila mtu mmoja mmoja kati ya wanadamu waliofanywa wawe wakamilifu. Kisha yeye, na wote watakaomfuata, watavurumishwa kwenye “ziwa la moto” la mfano, linalofananisha uharibifu wa milele.
20. Ni taraja gani tukufu watakalokabili wanadamu wakati siku ya kupumzika ya Mungu ifikiapo mwisho?
20 Sasa siku ya Mungu ya ‘kustarehe na kuacha kazi yake’ kuhusiana na uumbaji wa kidunia ikiwa imekwisha, bila shaka yeye ataanza kazi mpya ambazo zitaendelea mpaka umilele wote. Hakutakuwa wakati wa kuchosha kamwe wakati wakaaji wenye furaha wa dunia, wenye kufurahi sikuzote katika nguvu mpya za ujana wanaposhiriki katika utendaji wo wote watakaogawiwa na Mungu kusudi waufanye.—Mwa. 2:3; Isa. 66:22.
JAMBO LA UMAANA SANA
21. Tunawezaje kufaidika na hoja ya Paulo katika 1 Wakorintho 15?
21 Ni lazima ‘tushike sana habari njema kutia tumaini zayo la ufufuo, kwa maana ufufuo ni wa maana sana kwa watumishi wote wa Mungu. Wanaume na wanawake waaminifu wa nyakati za kale waliuamini ufufuo wa kidunia, na waliutazamia. (Ebr. 11:13-16) Kristo Yesu alifufuliwa akiwa “matunda ya kwanza” ya ufufuo huo, kama ilivyoshuhudiwa na mamia ya mashahidi waliojionea kwa macho. Wakristo waliotiwa mafuta, na kuzaliwa kwa roho wamehubiri “katika kuumba kote kuliko chini ya mbingu,” katika siku za mitume na katika nyakati za kisasa, hata kwamba “habari njema” zinazohusu ufufuo zilizunguka dunia nzima. (Kol. 1:23, NW) Na watiwa mafuta waliobaki wanapoendelea kuumaliza mwendo wao wa kidunia ili wapate zawadi yao ya kimbinguni, “mkutano mkubwa,” pia kwa mara nyingine wenye tumaini la uzima wa milele duniani umetangaza “habari njema” za ufalme huo.—Mt. 24:14, NW.
22. Paulo anatoa onyo gani la kumalizia katika barua yake, na kwa nini tuna kila sababu kulifuta?
22 Vikundi hivyo vyote ni vyenye pendeleo kama nini vinapofikia miradi yavyo, kila kimoja katika utaratibu wacho wenyewe, au cheo! Kweli kweli, sisi leo tuna kila ya sababu ya kufuata onyo linalofuata la Paulo: “Mwendelee kukesha, msimame imara katika imani, tendeni kiume, iweni wenye nguvu. Mambo yenu yote na yafanywe kwa upendo.” (1 Kor. 16:13, 14, NW) Kwa njia hiyo tutakuwa waamini wa kusudi jema.
Je! Unaweza kujibu yafuatayo?
◼ Ni nini kinachoonyesha kwamba wanaume na wanawake wa imani katika nyakati za kwanza walitazamia ufufuo duniani?
◼ Baada ya Kristo aliye “matunda ya kwanza,” ni wangapi wengine wanaoshiriki, “kila mtu katika mahali pake penye utaratibu,” katika ufufuo wa kimbinguni?
◼ Ufufuo duniani unatokea wakati gani na katika vikundi gani?
◼ Jamii moja sana-sana imependelewaje kupata uzima duniani bila kufufuliwa?
◼ Sisi sote tunapaswa kufanya nini ili tusiwe “waamini bila kusudi”?
[Picha katika ukurasa wa 14]
“Habari njema” zinahusu hasa ufalme wa Mungu kupitia Kristo, tumaini la kurudishwa kwa paradiso duniani