Ule Ufalme na lile Tumaini la Ufufuo
“Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake.”—2 Timotheo 4:1.
1. Tukifikiria hesabu ya wanadamu ambao wamepata kuishi, kwa sababu gani tumaini la ufufuo ni la maana sana, lakini ni maulizo gani yanayotokea akilini?
KUNA makadirio yanayotofautiana kati ya bilioni 14 na bilioni 20 juu ya wanadamu wangapi wamepata kuishi. Hata hesabu sahihi iwe nini, mambo mawili ni hakika: (1) Yehova Mungu anajua hesabu kamili ya watu ambao wamepata kuishi, na ana uwezo wa kurudisha kwenye uzima ye yote ambaye anachagua; (2) idadi ya watu wakati huu ulimwenguni isiyopata kuwapo tena ya watu bilioni 4.4 yaelekea ni kisehemu kidogo tu cha jumla ya hesabu ya wanadamu ambao wamepata kuishi. Mkataa (uamuzi) huu hauepukiki: hesabu kubwa zaidi ya wanadamu wamekufa na wanategemea ufufuo ili wawe na tumaini lo lote la wakati ujao. Lakini ni kwa sababu gani walikufa? Na kuna tumaini gani kwamba wataishi tena?
2. Petro alisema nini kuhusu ufufuo wa Kristo na uhusiano Wake na tumaini la ufufuo?
2 Katika mwaka 36 W.K. mtume Petro alisema hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye. . . . Huyo [Yesu Kristo] Mungu alimfufua siku ya tatu, akamjalia kudhihirika, si kwa watu wote, bali kwa mashahidi waliokuwa wamekwisha kuchaguliwa na Mungu, ndio sisi, tuliokula na kunywa pamoja naye baada ya kufufuka kwake kutoka kwa wafu. Akatuagiza tuwahubiri watu na kushuhudia ya kuwa huyu ndiye aliyeamriwa na Mungu awe Mhukumu wa wahai na wafu. Huyo manabii wote humshuhudia, ya kwamba kwa jina lake kila amwaminiye atapata ondoleo la dhambi.”—Matendo 10:34-43.
3. (a) Kwa sababu gani mabilioni mengi sana ya watu wamekufa? (b) Eleza jinsi kifo na ufufuo wa Kristo vilivyo msingi wa tumaini la ufufuo.
3 Ndiyo, sababu ya mabilioni ya wanadamu wafu kulundamana kaburini ni dhambi, tuliyorithi kutoka kwa mtu wa kwanza Adamu. “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote . . . kwa kukosa mtu mmoja mauti ilitawala.” (Warumi 5:12,17) Lakini Kristo alikufa na “akafanywa hai katika roho.” (1 Petro 3:18, NW) Kupitia imani katika damu yake iliyomwagwa, “kila” mtu, kati ya “wahai na wafu,” anaweza kupata “ondoleo la dhambi” na kuokolewa na utawala mkatili wa Mfalme Mauti. Kwa sababu hiyo, wengi wa wanadamu watahitaji ufufuo. Kwa hiyo Paulo anaandika hivi: “Kama vile kifo kilivyoletwa duniani na mtu mmoja [Adamu], vivyo hivyo nako kufufuka katika watu kumesababishwa na mtu mmoja [Yesu].” (1 Wakorintho 15:21, HNWW) Kristo alithibitisha hilo, na kumwambia Martha hivi: “Mimi ndio ufufuo na uzima. Yeye aniaminiye, hata ingawa anakufa, atarudi kwenye uzima.” (Yohana 11:25, NW) Kifo na ufufuo wa Kristo ndio msingi wa tumaini la ufufuo.
Ule “ufufuo wa Kwanza”
4, 5. (a) Yohana aliandika nini juu ya “ufufuo wa kwanza,” na wale wanaoshiriki katika ufufuo huu wanapewa uwezo na cheo gani? (b) Yesu aliwaambia nini wale mitume 11 waaminifu juu ya cheo chao cha wakati ujao?
4 Biblia inaonyesha kwamba Kristo hatahukumu akiwa peke yake “wahai na wafu.” Akieleza juu ya njozi iliyoongozwa kwa roho, mtume Yohana aliandika hivi: “Kisha nikaona viti vya enzi, wakaketi juu yake, nao wakapewa hukumu; nami nikaona [nafsi] zao waliokatwa vichwa kwa ajili ya ushuhuda wa Yesu, na kwa ajili ya neno la Mungu, na hao wasiomsujudia yule mnyama [tengenezo la kisiasa la Shetani], wala sanamu yake, wala hawakuipokea ile chapa katika vipaji vya nyuso zao, wala katika mikono yao; nao wakawa hai, wakatawala pamoja na Kristo miaka elfu. Hao wafu waliosalia hawakuwa hai hata itimie ile miaka elfu. Huo ndio ufufuo wa kwanza. Heri, na mtakatifu, ni yeye aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hao mauti ya pili haina nguvu; bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu.”—Ufunuo 20:4, 6.
5 Wa kwanza kati ya wafalme na makuhani hao wa wakati ujao waliokufa wakiwa mashahidi waaminifu wa Yesu na Babaye, Yehova, walikuwa wale mitume 11 waaminifu. Katika Luka 22:28-30, Yesu anasimulia kuwa hao wameketi juu ya viti vya enzi pamoja naye katika ufalme wake, ili ‘kuwahukumu kabila kumi na mbili za Israeli [zisizo za kikuhani, zinazofananisha wanadamu wengine].’
6. Ni mahakimu washirika wangapi watakaomsaidia Kristo atakapohukumu wahai na wafu, nao wanapata badiliko gani wanapofufuliwa?
6 Maandiko mengine yanaonyesha kwamba pendeleo hilo lisilo la kawaida la kuwa wafalme na makuhani washirika pamoja na Kristo katika ufalme wake ni la “kundi dogo” la Wakristo waaminifu 144,000 peke yao ambao “wamenunuliwa katika wanadamu.” (Luka 12:32; Ufunuo 14:1-4) Wao wanaliacha tumaini lao la kawaida na la asili la kuishi milele duniani ili ‘waungane naye [Kristo] katika mfano wa ufufuo wake.’ (Warumi 6:5, NW) Kuhusu wao, Paulo aliandika hivi vilevile: “Kadhalika na [ufufuo wa] wafu. Hupandwa katika uharibifu; hufufuliwa katika kutokuharibika. . . . Hupandwa mwili wa asili; hufufuliwa mwili wa roho. . . . Nyama na damu haziwezi kuurithi ufalme wa Mungu . . . Sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika.”—1 Wakorintho 15:42-53.
7. Kamusi moja inasema nini juu ya hali ya kutokufa, na Paulo na Petro waliandika nini juu ya tumaini la kimbingu?
7 Kwa kupendeza, kitabu The New International Dictionary of New Testamem Theology kinaonyesha uongo wa wazo lisilo la kimaandiko la kwamba kila mtu ana nafsi isiyokufa, kwa kusema hivi: “Watu wote hawana hali ya kutokufa wakati huu bali ni jambo watakalopata Wakristo wakati ujao. Kulingana na 1 Kor, 15:42, 52 ff., ni baada tu ya badiliko la ufufuo ndipo waamini ‘wanavaa’ vazi la kutokufa. . . . hakuwezi kuwako hali ya kutokufa pasipo kutanguliwa na ufufuo.” Kwa kweli, si Wakristo wote wanaopewa thawabu ya kutokufa, bali wale tu wanaoshiriki katika “ufufuo wa mapema zaidi kutoka kwa wafu.” Wao ‘wamewekewa mbinguni urithi . . . usioharibika na usiochafuliwa na usiofifia.’—Ona Warumi 8:20-22; Wafilipi 3:10, 11; 1 Petro 1:3, 4, NW.
Wakati wa “Ufufuo wa Kwanza”
8. (a) Kulingana na Maandiko, “ufufuo wa kwanza” ulipasa kutokea wakati gani? (b) Eleza maana ya 1 Wathesalonike 4:14-17 na 1 Wakorintho 15:51, 52.
8 Maandiko yanahusianisha huu “ufufuo wa kwanza” na “kuwapo [Kigiriki, parousia]” kwa Kristo. (1 Wakorintho 15:23, NW) Mtume Paulo anaandika hivi: “Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo [kuanza na karne ya kwanza mpaka kuja kwa Kristo kwenye hekalu la kiroho mwaka 1918] watafufuliwa kwanza.” Halafu Paulo anaendelea kusema kwamba Wakristo waliotiwa mafuta ‘wanaosalia hata wakati wa [kuwapo] kwake Bwana,’ na kwa hiyo ambao wanakufa wakati wa parousia, watafufuliwa mara moja na ‘kunyakuliwa katika mawingu, ili kumlaki Bwana hewani’ (1 Wathesalonike 4:14-17) Hawalazimiki ‘kulala’ katika kaburi, wakingojea ufufuo. Wakati wa kufa ‘wanabadilishwa, kwa dakika moja, kwa kupepesa jicho.’—1 Wakorintho 15:51, 52, Revised Standard Version.
9. (a) Kuwapo kwa Kristo kusikoonekana kulianza wakati gani? (b) Ni nini kilichopasa kutokea wakati wa kuwapo kwake, na ni kwa sababu gani Wakristo waliotiwa mafuta wanaokufa wakati wa kuwapo kwa Kristo wanaweza kuonwa kuwa “wenye furaha”?
9 Matukio yanayotimiza unabii mbali-mbali wa Biblia yanaonyesha kwamba kuwapo kwa Kristo, au parousia, kulianza katika mwaka wenye matukio wa 1914. (Mathayo 24:3, 7-14) Ndipo “ufalme wa ulimwengu ulipokuwa ufalme wa Bwana [Yehova] na wa Kristo wake.” Baada ya tukio hilo lenye kutikisa ulimwengu “wakati uliowekwa wa kuwahukumu wafu” ulifika. Kuhukumu na kuthawabisha hao wanaostahili kulianza na wale wanaoshiriki katika “ufufuo wa kwanza” tangu kuja kwa Kristo kwenye hekalu na kuendelea. (Ufunuo 11:15-18, NW) Wakristo hao waliotiwa mafuta wanaokufa wakiwa waaminifu baada ya kusimamishwa kwa ufalme wa Mungu wanaitwa “wenye furaha.” Kwa sababu gani hivyo? Kwa sababu ufufuo wao ni wa mara moja, unaowaruhusu wakati huo huo waanze kazi zao mpya pamoja na Kristo Yesu katika mbingu.—Ufunuo 14:13, NW.
10. Ni kwa sababu zipi ufufuo wa wale 144,000 unaitwa “ufufuo wa kwanza”?
10 Ufufuo wa hesabu yote ya Wakristo watiwa mafuta 144,000 walioitwa kutawala pamoja na Kristo katika mbingu kwa kufaa unaitwa “ufufuo wa kwanza.” Iko hivyo kwa sababu unatangulia kwa wakati ule ufufuo wa kwenye uzima duniani wa wanadamu kwa ujumla, na hao 144,000 wanakuwa “matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-kondoo.” (Ufunuo 14:1, 4, NW; Yakobo 1:18) Jambo hilo linawaweka kwenye cheo cha maana, kwa kuwa hakuna wanadamu wengine ‘wanaoweza kukamilishwa pasipo’ makuhani, wafalme na mahakimu hao 144,000. (Waebrania 11:40b, NW; Ufunuo 22:1, 2) Zaidi ya hayo, huo ni bora zaidi ya ufufuo mwingine wo wote wa kidunia, wale 144,000 wakifufuliwa “kwa mfano wa kufufuka kwake [Kristo]” kwenye uzima usioharibika, hali ya kutokufa wakiwa wana wa kiroho wa Mungu.—Warumi 6:5.
Ufufuo wa Kidunia
11. Ni ufufuo gani mwingine unaotajwa katika Ufunuo, sura ya 20?
11 Ikiwa kuna “ufufuo wa kwanza,” ni jambo la akili kwamba kuwepo ufufuo wa baadaye. Akisimulia yale yatakayotokea wakati wa siku ya hukumu ya mileani (miaka elfu moja) inayotangulia kutajwa katika sura iyo hiyo, mtume Yohana anaandika hivi:
“Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao.”—Ufunuo 20:12.
12, 13. (a) Kwa sababu gani si jambo la akili kusema kwamba wafu waliosalia hawatafufuliwa mpaka baada ya mileani? (b) Basi, ni nini maana ya usemi ‘kuwa hai’ unaotumiwa katika Ufunuo 20:5? (c) Itaamuliwaje ni majina ya nani ambayo mwishowe yataandikwa katika “kitabu cha uzima”?
12 “Wafu” hao ni sawa na wale “wafu waliosalia” wanaotajwa katika mstari wa tano wa sura iyo hiyo, na ambao juu yao inasemwa kwamba “hawakuwa hai, hata itimie ile miaka elfu.” Hiyo haiwezi kumaanisha kwamba hawafufuliwi mpaka baada ya siku ya hukumu ya mileani, kwa sababu wale wanaoshiriki katika “ufufuo wa kwanza” wanapewa uwezo wa ‘kuhukumu’ na watakuwa “makuhani” na ‘kutawala’ wakiwa wafalme pamoja na Kristo kwa “hiyo miaka elfu.” (Ufunuo 20:4-6) Watahukumu na kutawala juu ya nani wakiwa wafalme, na watakuwa makuhani kwa ajili ya nani, iwapo “wafu waliosalia” hawafufuliwi mpaka baada ya mileani?
13 Kwa sababu hiyo, lazima usemi ‘kuwa hai’ uwe unahusu hali itakayokuwapo mwishoni mwa Siku ya Hukumu yenye urefu wa miaka 1,000. Inamaanisha kwamba watu hao ‘wanakuwa hai’ kwa maana ya kwamba mwishowe wanapata ukamilifu wa kibinadamu. Watakuwa katika hali ile ile ya ukamilifu kama walivyokuwa Adamu na Hawa katika bustani ya Edeni. Halafu Yehova ataamuaje wale ambao majina yao yataandikwa katika “kitabu cha uzima”? Itakuwa kwa wanadamu kupata jaribu la mwisho. (Ufunuo 20:7-10, 12, 15) Wale watakaojithibitisha kuwa waaminifu kwa Mungu walipite jaribu la mwisho ‘watahesabiwa haki’ na Yehova mwenyewe na kuingia kwenye “uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu” duniani. (Warumi 8:21, 33) Watapata hakikisho la kimungu la uzima wa milele, tofauti na Adamu, aliyeshindwa na jaribu na hivyo akazuiwa njia ya kwenda kwenye “mti wa uzima” na makerubi waliotumwa na Mungu.—Mwanzo 2:9; 3:22-24.
14. Ufufuo wa watu duniani wakati wa mileani utawaingiza kwenye nafasi nzuri kwa njia zipi?
14 Kwa kuwa “wafu waliosalia” wanafufuliwa wakati wa utawala wa miaka 1,000 wa Kristo watakuwa na nafasi hiyo ya kujithibitisha wanastahili kuandikwa majina yao kwa umilele katika “kitabu cha uzima” cha Yehova na kuishi milele chini ya ufalme wa Mungu, ufufuo wao unawaingiza kwenye nafasi bora zaidi ya zile za wale watu wachache waliofufuliwa katika nyakati za Biblia lakini wakafa tena (1 Wafalme 17:17-24; 2 Wafalme 4:17-37; 13:20, 21; Mathayo 9:18, 23-26; Luka 7:11-15; Yohana 11:38-44; Matendo 9:36-41; 20:7-12) Wanaume na wanawake wa nyakati za kale waliendelea kuwa waaminifu kwa Yehova mpaka kufa ili wapate “ufufuo ulio bora” chini ya ule ufalme, au “mji” wa Masihi.—Waebrania 11:10, 13, 14, 35.
Ufufuo na Hukumu
15, 16. (a) Je! Siku ya Hukumu ni jambo la kuogopa! Eleza. (b) Ni nani atakayehukumu, na kwa msingi gani?
15 Tumekwisha kuona kwamba “wafu waliosalia” wanafufuliwa wakati wa mileani ili ‘wahukumiwe sawasawa na matendo yao’ ya wakati huo. (Ufunuo 20:12) Wazo lenye kuogopesha la siku ya maangamizi wakati ambapo kila mtu aliyepata kuishi atapaswa kutoa jibu kwa dhambi zake za wakati uliopita halina msingi wa Biblia. Maneno yanayozunguka mstari huo yanaonyesha kwamba “vitabu” vya kimungu, au vitabu vya sheria, vitafunguliwa na kwamba wafu waliofufuliwa watahukumiwa “katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao,” yaani, kulingana na utii wao au kutokutii kwao maagizo hayo ya kimungu.
16 Ni nani atakayehukumu? Mtume Paulo aliandika kwamba Kristo Yesu ndiye “atakayewahukumu walio hai na waliokufa,” na wakati uo huo alizungumza juu ya ‘kufunuliwa kwa Kristo na ufalme wake.’ (2 Timotheo 4:1) Watakaoketi kwenye “viti vya enzi” pamoja na Kristo wakati wa ufalme wake wa mileani watakuwa wale mahakimu washirika 144,000. (Luka 22:28-30; Ufunuo 20:4, 6) Paulo aliandika hivi: “Hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu?”—1 Wakorintho 6:2.
17, 18. (a) Je! kuna kupingana ko kote kati ya Yohana 5:29 na Ufunuo 20:12? Eleza. (b) Ni katika maana gani wengine “watatoka . . . kwa ufufuo wa hukumu”?
17 Akizungumza juu ya yale yatakayotokea katika utawala wake wa mileani, ambao pia ni Siku ya Hukumu ya miaka 1,000, Yesu alisema hivi: “Tena Baba hamhukumu mtu ye yote, bali amempa Mwana hukumu yote. . . . Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.”—Yohana 5:22-29.
18 Je! hayo yanapingana na Ufunuo 20:12, ambapo tunasoma kwamba wafu ‘watahukumiwa katika mambo yaliyoandikwa katika vile vitabu,’ vitabu ambavyo ‘havitafunguliwa’ mpaka baada ya mileani? La, sivyo. Maneno ya Yesu katika sura ya tano lazima yafahamike kwa msaada wa ufunuo wake wa baadaye kwa Yohana. (Ufunuo 1:1) “Wale waliofanya mema” na “wale waliotenda mabaya” watakuwa kati ya wale “wafu” ‘watakaohukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake’ aliyofanya baada ya kufufuliwa. (Ufunuo 20:13) Alipokuwa akilinganisha “ufufuo wa uzima” na “ufufuo wa hukumu [Kigiriki, a·naʹsta·sis kriʹseos],” Yesu alikuwa akizungumza juu ya matokeo ya mwisho ya fufuo hizo. Kitabu Thayer’s Greek-English Lexicon kinaeleza a·naʹsta·sis kriʹseos kuwa ufufuo “ukifuatwa na laana.” Mtu huyo hafufuliwi ili alaaniwe moja kwa moja, bali ufufuo wake utafuatwa na hukumu yenye laana akikataa kufuata “mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu” na kwa njia hiyo jina lake likose ‘kuandikwa katika kitabu cha uzima.’ Kisha yeye angekufa “mauti ya pili,” pasipo tumaini lo lote la wakati ujao la kufufuliwa.—Ufunuo 20:14, 15;21:8.
19 na maneno ya chini. (a) Tafsiri moja ya Biblia ya Kifaransa inatafsirije Yohana 5:29, na ni wakati gani tu itakapokuwa wazi kwamba ufufuo ulikuwa wa uzima” au “wa hukumu”? (b) Je! “wenye haki” wanatoka kwa “ufufuo wa uzima” na “wasio haki” kwa “ufufuo wa hukumu,” kama inavyotajwa katika Matendo 24:15? Eleza.
19 Inapendeza kuangalia kwamba kitabu cha Kifaransa Ecumenical Translation (kilichochapishwa na kikundi cha wasomi Wakatoliki na Waprotestanti) kinatafsiri hivi Yohana 5:29: “Wale ambao wamefanya mema watatoka kwa ajili ya ufufuo unaoongoza kwenye uzima; wale ambao wamezoea uovu, kwa ajili ya ufufuo unaoongoza kwenye hukumu.” Ni wakati tu matokeo ya mwisho ya ufufuo wa mtu yatakapokuwa wazi ndipo itakapojulikana kama ufufuo wake ulikuwa “ufufuo wa uzima” au “ufufuo wa hukumu.”a
20. (a) Ni nani watakaohitaji kunywa “maji ya uzima,” na kwa sababu gani? (b) Ni ulizo gani litakalochunguzwa katika makala inayofuata?
20 Wale wafu waliofufuliwa pamoja na “mkutano mkubwa” utakaoiokoka “dhiki ile iliyo kuu” ambayo iko mbele karibu watahitaji kunywa “maji ya uzima,” yaani, wakubali kwa shukrani dhabihu ya ukombozi ya Kristo na mipango mingine yote anayotoa Yehova ili kukomboa wanadamu kutokana na dhambi na kifo. (Ufunuo 7:9, 10, 14, 17; 22:1, 2) Mipango hiyo itasimamiwa na Kristo na washirika wake walio makuhani na mahakimu 144,000 wakati wa Ufalme wa mileani. Lakini je! wafu wote watarudishwa ili wahukumiwe, kutia na watakaoharibiwa na “dhiki ile iliyo kuu” inayokaribia? Makala ifuatayo itazungumza juu ya hilo.
[Maelezo ya Chini]
a Wale wanaofufuliwa kwenye “ufufuo wa uzima” au kwenye “ufufuo wa hukumu” hawapaswi kuonwa ni wale wale sawa na “wenye haki” na “wasio haki” wanaotajwa na Paulo katika Matendo 24:15. Paulo anazungumza juu ya hali ya watu wakati wanapofufuliwa, ikitegemea mwenendo wao kabla ya kufa. “Wenye haki” watapaswa kuendelea na mwendo wao wa kutenda kwa kutii mambo yaliyoandikwa katika vile “vitabu.” Kama sivyo ufufuo wao ungeweza kugeuka uwe “wa hukumu.” Vivyo hivyo, watu wo wote “wasio haki” wakitubu, wakikubali dhabihu ya ukombozi ya Kristo na kutii mambo yaliyoandikwa katika “vitabu” hivyo, ufufuo wao ungeweza kuwa “wa uzima.”
MAULIZO YA KUJIKUMBUSHA
◻ Kristo ni“ufufuo na uzima” kwa njia gani?
◻ Ni nani wanaoshiriki katika “ufufuo wa kwanza,” na watamsaidia Mfalme Yesu Kristo katika utendaji gani?
◻ Kwa sababu gani usemi “ufufuo wa kwanza” unafaa?
◻ Wale “wafu waliosalia” ‘wanakuwa hai’ kwa njia gani baada ya mileani, na ni kwa njia gani ufufuo wao ulivyo bora zaidi ya ule wa watu waliofufuliwa katika nyakati za Biblia kwenye uzima wa kidunia.
◻ Wafu waliofufuliwa watahukumiwa kwa msingi gani, na watahitaji nini ili wakombolewe kutokana na dhambi na kifo?
[Blabu katika ukurasa wa 16]
“Watu wote hawana hali ya kutokufa wakati huu bali ni jambo watakalopata Wakristo wakati ujao. . . . hakuwezi kuwako hali ya kutokufa pasipo kutanguliwa na ufufuo.”—The New International Dictionary of New Testament Theology
[Picha katika ukurasa wa 17]
Biblia inaonyesha kwamba kutakuweko ufufuo wa wengi kwenye uzima juu ya dunia