Maagizo ya Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo
Yaliyomo
1. Mkutano wa Huduma na Maisha ya Kikristo utafuata utaratibu ulio kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha kulingana na maagizo yafuatayo. Wahubiri wote wanapaswa kualikwa wajitolee kwa ajili ya migawo ya wanafunzi. Wengine wanaoshirikiana kikamili na kutaniko wanaweza kupewa mgawo ikiwa wanakubali mafundisho ya Biblia na maisha yao yanapatana na kanuni za Kikristo.—be uku. 282.
UTANGULIZI
2. Dakika 1. Kila juma, baada ya wimbo na sala ya kufungua, mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha atatoa maelezo yenye kuchochea hamu kwa ajili ya programu itakayofuata. Mwenyekiti anapaswa kukazia fikira hoja ambazo zitanufaisha kutaniko.
HAZINA ZA NENO LA MUNGU
3. Hotuba: Dakika 10. Kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha kuna kichwa na muhtasari wa mambo makuu mawili au matatu. Hotuba hii inapaswa kugawiwa mzee au mtumishi wa huduma anayestahili. Ikiwa kitabu kipya cha Biblia kimepangiwa katika usomaji wa Biblia wa kila juma, video ya utangulizi wa kitabu hicho itaonyeshwa. Msemaji anaweza kuhusianisha video na kichwa cha hotuba. Hata hivyo, anapaswa kuhakikisha amezungumzia hoja zilizo kwenye daftari. Pia, wakati ukiruhusu, anapaswa kurejelea picha zilizomo na hoja za Kimaandiko, ambazo zimekusudiwa kufanya habari hiyo ieleweke zaidi. Anaweza kutia ndani habari kutoka kwenye marejeo mengine ya ziada maadamu inachangia hoja zilizo kwenye muhtasari.
4. Hazina za Kiroho: Dakika 10. Hii ni sehemu ya maswali na majibu bila utangulizi au umalizio. Inapaswa kushughulikiwa na mzee au mtumishi wa huduma anayestahili. Msemaji anapaswa kuwauliza wasikilizaji maswali yote. Pia, anaweza kuamua ikiwa maandiko yaliyoonyeshwa yanahitaji kusomwa au la. Wale wanaopewa nafasi ya kutoa maelezo wanapaswa kutumia muda usiozidi sekunde 30.
5. Usomaji wa Biblia: Dakika 4. Mgawo huu wa mwanafunzi utashughulikiwa na ndugu. Mwanafunzi anapaswa kusoma sehemu aliyogawiwa bila kutoa utangulizi wala umalizio. Mwenyekiti wa mkutano atapendezwa hasa na kuwasaidia wanafunzi kusoma kwa usahihi, kwa njia inayoeleweka, kwa ufasaha, kukazia maana ipasavyo, ubadilifu wa sauti, kutua ifaavyo, na kusoma kwa njia ya kawaida. Kwa kuwa kila mgawo wa usomaji wa Biblia hutofautiana kwa urefu, mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha anapaswa kuzingatia hasa uwezo wa wanafunzi anapopanga migawo hiyo.
BORESHA HUDUMA YAKO
6. Dakika 15. Sehemu hii ya mkutano imekusudiwa kuwapa wote fursa ya kujizoeza kwa ajili ya huduma na kuboresha uwezo wao wa kuhubiri na kufundisha. Wahubiri wanapaswa kuzungumzia habari iliyo kwenye mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo yaliyo kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha. Hata hivyo, isipokuwa kuwe na maagizo tofauti, wanaweza kuchagua swali, andiko, swali la ziara inayofuata, au kikao kinachofaa hali za eneo lao. Wahubiri watajiamulia ikiwa watatumia au hawatatumia chapisho au video kutoka kwenye Sanduku la Vifaa vya Kufundishia ikiwa jambo hilo halijatajwa kwenye maagizo ya daftari. Ili kusaidia katika huduma, mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo huenda yakatia ndani sehemu ya “Andiko Hili Liko Katika Sanduku la Vifaa vya Kufundishia.” Wanafunzi wanaweza kuamua ikiwa watatumia sehemu hiyo katika migawo yao au la. Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha huonyesha muda hususa kwa ajili ya kila mgawo wa mwanafunzi na, nyakati nyingine, linaweza kuandaa maagizo ya ziada. Wanafunzi hawahitaji kuongezea habari za ziada ili tu kumaliza muda wote wa sehemu yao. Maonyesho fulani yaliyotayarishwa vizuri yanaweza kumalizika dakika moja au zaidi mapema. Ikihitajika, wazee wanaweza kupewa migawo ya wanafunzi. Nyakati nyingine, kwenye ratiba kutakuwa na mazungumzo ya video badala ya video ya mapendekezo. Sehemu hiyo inapaswa kushughulikiwa na mzee au mtumishi wa huduma anayestahili.
7. Video za Mapendekezo ya Kuanzisha Mazungumzo: Video za mapendekezo ya kuanzisha mazungumzo zitaonyeshwa na kuzungumziwa katika kila mwezi. Video hizo zitaonyesha ziara ya kwanza na ziara za kurudia. Sehemu hii itashughulikiwa na mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha.
8. Ziara ya Kwanza: Mgawo huu unaweza kushughulikiwa na ndugu au dada. Msaidizi anapaswa kuwa wa jinsia moja na mwanafunzi au kuwa mshiriki wa familia. Mwanafunzi na msaidizi wanaweza kuketi au kusimama. Mwanafunzi anapaswa kujichagulia salamu inayofaa eneo. Habari iliyo katika pendekezo la kuanzisha mazungumzo kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha inapaswa kutumiwa kama msingi wa mazungumzo.
9. Ziara ya Kurudia ya Kwanza: Mgawo huu unaweza kushughulikiwa na ndugu au dada. Msaidizi hapaswi kuwa wa jinsia tofauti. (km 5/97 uku. 2) Mwanafunzi na msaidizi wanaweza kuketi au kusimama. Mwanafunzi anapaswa kuonyesha jambo tunalopaswa kusema tunapomrudia mtu aliyeonyesha upendezi katika ziara ya kwanza. Habari iliyo katika pendekezo la kuanzisha mazungumzo kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha inapaswa kutumiwa kama msingi wa mazungumzo.
10. Funzo la Biblia: Mgawo huu unaweza kushughulikiwa na ndugu au dada. Msaidizi hapaswi kuwa wa jinsia tofauti. (km 5/97 uku. 2) Mwanafunzi na msaidizi wanaweza kuketi au kusimama. Mgawo huu unapaswa kuonyesha sehemu fupi ya funzo la Biblia ambalo tayari linaendelea. Hakuna haja ya utangulizi wala umalizio isipokuwa mwanafunzi awe anashughulikia kihususa mojawapo ya masomo hayo. Mafungu yote yaliyogawiwa hayahitaji kusomwa kwa sauti, ingawa hilo linaweza kufanywa. Ikiwa habari inatia ndani video, haipaswi kuonyeshwa bali inapaswa kuzungumziwa. Mgawo huu unapaswa hasa kuonyesha ustadi wa kufundisha.
11. Hotuba: Mgawo huu wa mwanafunzi unapaswa kushughulikiwa na ndugu na kutolewa kama hotuba kwa kutaniko.
MAISHA YA MKRISTO
12. Baada ya wimbo, dakika 15 zinazofuata za Maisha ya Mkristo zitatia ndani sehemu moja au mbili ambazo zimekusudiwa kuwasaidia wasikilizaji watumie Neno la Mungu. Isipokuwa kuwe na maagizo tofauti, sehemu hizo zinaweza kugawiwa wazee au watumishi wa huduma wanaostahili. Hata hivyo, sehemu ya mahitaji ya kutaniko inapaswa kushughulikiwa na mzee. Ikiwa sehemu ya mazungumzo ina makala katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha, ndugu aliyegawiwa sehemu hiyo anaweza kutumia maswali ya ziada kukazia mambo makuu ya makala hiyo.
13. Funzo la Biblia la Kutaniko: Dakika 30. Sehemu hii hugawiwa mzee anayestahili. (Ikiwa wazee ni wachache, watumishi wa huduma wanaostahili wanaweza kupewa mgawo huu, ikihitajika.) Baraza la wazee linapaswa kuamua ni nani anayestahili kuongoza Funzo la Biblia la Kutaniko. Wale wanaoidhinishwa wanapaswa kuongoza kwa njia inayofaa ili funzo limalizike kwa wakati, wakazie maandiko ya msingi, na kuwasaidia wote wathamini matumizi ya hoja zinazozungumziwa. Wanaweza kupata kanuni zitakazowasaidia kwa kupitia tena mwelekezo uliochapishwa kuhusu jinsi ya kuongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi. Baada ya kuzungumzia kikamili sehemu iliyoratibiwa kwa ajili ya juma, hakuna haja ya kurefusha funzo. Ikiwa inawezekana, viongozi na wasomaji tofauti-tofauti wanapaswa kutumiwa kila juma. Ikiwa mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha ataelekeza kwamba funzo lifupishwe, kiongozi ndiye atakayeamua jinsi funzo hilo litakavyofupishwa. Anaweza kuamua mafungu fulani yasisomwe.
UMALIZIO
14. Dakika 3. Mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha atapitia hasa mambo muhimu mliyojifunza mkutanoni. Anapaswa pia kupitia kwa ufupi habari za juma linalofuata, labda kwa kutaja swali moja litakalojibiwa. Wakati ukiruhusu, anaweza kutaja majina ya wanafunzi waliogawiwa sehemu za juma lijalo. Isipokuwa kuwe na maagizo tofauti, mwenyekiti atasoma matangazo yoyote muhimu na barua zozote muhimu katika maelezo yake ya kumalizia. Matangazo ya kawaida, kama vile mipango ya utumishi wa shambani na ratiba ya usafi, hayapaswi kusomwa jukwaani bali yawekwe kwenye ubao wa matangazo. Ikiwa muda uliopangiwa sehemu ya umalizio hautoshi kutoa matangazo au kusoma barua, mwenyekiti anapaswa kuwaomba ndugu walio na sehemu katika Maisha ya Mkristo wafupishe sehemu zao ipasavyo. (Ona fungu la 13 na 17.) Mkutano utamalizika kwa wimbo na sala.
BORESHA UWEZO WAKO WA KUSOMA NA KUFUNDISHA
15. Kila mwanafunzi anapaswa kubeba nakala yake ya broshua Kufundisha, iwe ni nakala halisi au ya kielektroniki, katika Mkutano wa Huduma na Maisha. Mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha anapaswa kutumia broshua hiyo kama msingi wa kutoa pongezi na shauri. Kila mwanafunzi anapaswa kufanyia kazi somo linaloonyeshwa katika mabano kando ya mgawo aliopewa kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha. Sehemu ya “Andika Maendeleo Yako” kwenye broshua ni kwa ajili ya matumizi ya mwanafunzi na haipaswi kutiwa alama na mwenyekiti.
KUTOA PONGEZI NA SHAURI
16. Baada ya kila mgawo wa mwanafunzi, mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha ana dakika moja hivi ya kutoa pongezi na shauri linalotegemea broshua Kufundisha. Mwenyekiti anapomkaribisha mwanafunzi kwa ajili ya mgawo, hatatangaza somo. Hata hivyo, baada ya mwanafunzi kumaliza mgawo na kumpongeza ipasavyo, mwenyekiti anaweza kutangaza somo na kutaja kwa nini mwanafunzi alifanya vema katika somo hilo au kueleza kwa fadhili kwa nini mwanafunzi anapaswa kukazia uangalifu zaidi somo hilo hususa. Mwenyekiti anaweza pia kutaja mambo mengine kuhusu onyesho akihisi kwamba kufanya hivyo kutamnufaisha mwanafunzi au wasikilizaji. Shauri la ziada lenye kujenga linalotegemea broshua Kufundisha au kitabu Shule ya Huduma linaweza kutolewa faraghani baada ya mkutano au wakati mwingine, labda kuhusiana na somo alilogawiwa au somo lingine tofauti.—Kwa habari zaidi kuhusu jukumu la mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha na jukumu la mshauri msaidizi, ona fungu la 17, 22, na 23.
WAKATI
17. Hakuna sehemu inayopaswa kupitisha wakati, vilevile maelezo ya mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha hayapaswi kupita wakati. Ingawa muda uliotengwa kwa ajili ya kila sehemu hauna maneno “lisizidi” au “usizidi,” hakuna haja ya kurefusha sehemu ikiwa habari imezungumziwa vya kutosha chini ya muda uliowekwa. Migawo ya wanafunzi inapaswa kukatizwa kwa busara muda unapokwisha. Ikiwa sehemu nyingine za mkutano zimepitisha wakati, mshauri msaidizi anapaswa kutoa shauri la faraghani. (Ona fungu la 23.) Mkutano wote, kutia ndani nyimbo na sala, unapaswa kuchukua muda wa saa 1 na dakika 45.
ZIARA YA MWANGALIZI WA MZUNGUKO
18. Kutaniko linapokuwa na ziara ya mwangalizi wa mzunguko, programu itafuata utaratibu unaoonyeshwa kwenye Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha isipokuwa mambo yafuatayo: Badala ya kufanya Funzo la Biblia la Kutaniko katika sehemu ya Maisha ya Mkristo kutakuwa na hotuba ya utumishi ya dakika 30 itakayotolewa na mwangalizi wa mzunguko. Kabla ya hotuba ya utumishi, mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha atapitia programu iliyomalizika, apitie kifupi programu ya juma linalofuata, asome matangazo yoyote muhimu, asome barua zozote muhimu, kisha amkaribishe mwangalizi wa mzunguko. Baada ya hotuba ya utumishi, mwangalizi wa mzunguko atamalizia mkutano kwa wimbo atakaochagua mwenyewe. Anaweza kumkaribisha ndugu mwingine amalizie kwa sala. Hakuna shule za ziada katika lugha ya kutaniko zinazopaswa kufanywa wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Kikundi kinaweza kufanya mikutano kivyake hata wakati ambapo mwangalizi wa mzunguko anazungukia kutaniko simamizi. Hata hivyo, kikundi kinapaswa kujiunga na kutaniko simamizi wakati wa hotuba ya utumishi ya mwangalizi wa mzunguko.
JUMA LA KUSANYIKO LA MZUNGUKO AU KUSANYIKO LA ENEO
19. Katika juma la kusanyiko la mzunguko au la eneo, hakuna mikutano ya kutaniko inayofanywa. Habari zilizoratibiwa kwa ajili ya mikutano katika majuma hayo zinapaswa kusomwa kibinafsi au kama familia.
JUMA LA UKUMBUSHO
20. Ikiwa Ukumbusho utafanyika katikati ya juma, hakuna Mkutano wa Huduma na Maisha utakaoratibiwa. Bila shaka, mikutano ya utumishi wa shambani inapaswa kufanywa siku hiyo ya Ukumbusho.
MWANGALIZI WA MKUTANO WA HUDUMA NA MAISHA
21. Mzee aliyeteuliwa na baraza la wazee atatumikia akiwa mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha. Ana jukumu la kuhakikisha kwamba mkutano huu umepangwa vizuri na kushughulikiwa kulingana na maagizo haya. Anapaswa kudumisha mawasiliano mazuri pamoja na mshauri msaidizi. Mara tu Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha linapopatikana, mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha atatayarisha migawo ya mkutano wote wa katikati ya juma kwa ajili ya miezi hiyo miwili. (Ona fungu la 2-14.) Hilo linatia ndani sehemu ambazo si za wanafunzi pamoja na sehemu ya mwenyekiti wa katikati ya juma kutokana na wale walioidhinishwa na baraza la wazee na pia sehemu za wanafunzi. Kila mgawo unapaswa kusambazwa angalau majuma matatu kabla ya tarehe ya mgawo. Fomu ya Mgawo wa Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo (S-89) inapaswa kutumiwa kwa ajili ya migawo ya wanafunzi. Mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha anapaswa kuhakikisha nakala ya ratiba ya migawo imewekwa kwenye ubao wa matangazo. Baraza la wazee linaweza kumpa mgawo mzee mwingine au mtumishi wa huduma kumsaidia. Hata hivyo, wazee peke yao ndio wanaopaswa kutumiwa kupanga migawo ambayo si ya wanafunzi.
MWENYEKITI WA MKUTANO WA HUDUMA NA MAISHA
22. Kila juma, mzee mmoja atatumikia akiwa mwenyekiti wa Mkutano wa Huduma na Maisha. (Ikiwa wazee ni wachache, watumishi wa huduma wanaostahili wanaweza kupewa jukumu hili, ikihitajika.) Ana jukumu la kutayarisha maelezo ya utangulizi na umalizio na kuzungumzia video zozote za mapendekezo. Pia ataalika sehemu zote jukwaani, na ikitegemea ukubwa wa baraza la wazee, anaweza kushughulikia sehemu nyingine katika mkutano huo, hasa sehemu zinazohusu kuonyesha video tu bila mazungumzo ya ziada. Maelezo yake baada ya kila sehemu yanapaswa kuwa mafupi sana. Baraza la wazee litaamua ni wazee gani wanaostahili kupewa daraka hili. Wazee hao wanaostahili watakuwa wenyekiti kwa zamu. Ikitegemea hali za kutaniko, mwangalizi wa Mkutano wa Huduma na Maisha anaweza kuwa mwenyekiti mara nyingi zaidi ya wale wazee wengine wanaostahili. Ikiwa mzee anastahili kuongoza Funzo la Biblia la Kutaniko, huenda pia anastahili kuwa mwenyekiti wa mkutano huu. Hata hivyo, tafadhali kumbukeni kwamba, mzee anayetumikia akiwa mwenyekiti anahitaji kutoa pongezi na shauri la upendo litakalowasaidia wale walio na migawo ya mwanafunzi. Mwenyekiti pia ana jukumu la kuhakikisha kwamba mkutano huu unamalizika kwa wakati. (Ona fungu la 14 na 17.) Mwenyekiti akipenda na ikiwa kuna nafasi ya kutosha, maikrofoni nyingine inaweza kusimamishwa jukwaani upande unaofaa kwa ajili ya kualika sehemu mbalimbali huku ndugu aliye na sehemu anapojitayarisha kwenye kinara cha msemaji. Hali kadhalika, mwenyekiti akipenda anaweza kuamua kuketi hapo jukwaani wanafunzi wanaposhughulikia usomaji wa Biblia na kutoa sehemu za Boresha Huduma Yako. Hilo linaweza kuokoa wakati.
MSHAURI MSAIDIZI
23. Ikiwa inawezekana, ingefaa kutumia mzee aliye msemaji mwenye uzoefu atimize daraka hili. Jukumu la mshauri msaidizi ni kuwapa shauri la faraghani, ikihitajika, wazee na watumishi wa huduma kuhusiana na migawo yoyote ya ufundishaji wanayoshughulikia, kutia ndani sehemu za Mkutano wa Huduma na Maisha, hotuba za watu wote, na kuongoza au kusoma katika Funzo la Mnara wa Mlinzi au Funzo la Biblia la Kutaniko. (Ona fungu la 17.) Ikiwa kuna wazee kadhaa kutanikoni ambao ni wasemaji na walimu stadi, basi mzee tofauti anayestahili anaweza kutumikia akiwa mshauri msaidizi kila mwaka. Mshauri msaidizi hahitaji kutoa shauri baada ya kila mgawo.
SHULE ZA ZIADA
24. Ikitegemea idadi ya wanafunzi, makutaniko yanaweza kuwa na shule za ziada kwa ajili ya hotuba za wanafunzi. Kila shule ya ziada inapaswa kuwa na mshauri anayestahili, ikiwezekana mzee. Ikiwa inafaa, mtumishi wa huduma anayestahili kabisa anaweza kupewa jukumu hili. Baraza la wazee linapaswa kuamua ni nani anayeweza kutumikia katika wadhifa huu na ikiwa mgawo huo unapaswa kufanywa kwa zamu. Mshauri anapaswa kufuata utaratibu unaotajwa kwenye fungu la 16. Ikiwa kuna shule ya ziada, wanafunzi wanapaswa kuombwa waende kwenye chumba cha ziada baada ya sehemu Hazina za Kiroho katika Hazina za Neno la Mungu. Wanapaswa kujiunga na wengine kwenye jumba kuu baada ya sehemu Boresha Huduma Yako. Video inapozungumziwa, wale walio kwenye shule ya ziada wanapaswa kutazama au kusikiliza mazungumzo hayo katika chumba hicho, ikiwezekana. La sivyo, mshauri anapaswa kushughulikia video na mazungumzo hayo, akitumia kifaa cha mkononi.
VIDEO
25. Video zilizoteuliwa zitatumika katika mkutano huu. Video za mkutano wa katikati ya juma zitaandaliwa kupitia programu ya JW Library® na kupakuliwa kwenye vifaa mbalimbali. Nyakati nyingine, video za mapendekezo zinaweza kuonyeshwa katika mikutano ya utumishi wa shambani.
© 2022 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
S-38-SW 11/22