Usipinge Shauri la Yehova
“Sikiliza mashauri, ukapokee mafundisho, upate kuwa na hekima siku zako za mwisho.”—Mit. 19:20.
1, 2. (a) Sababu gani watu wazima wanaonekana kama watoto machoni pa Mungu? (b) Sababu gani Yehova ana uwezo wa kutupa shauri lenye hekima?
WEWE una miaka mingapi? Je! wewe una miaka kati ya 13 mpaka 19, au wewe una miaka kati ya 20 na 30? Je! wewe ni wa makamu au wewe unakaribia kuwa na miaka mia moja? Hata uwe umeishi miaka mingapi, bado wewe ni mtoto machoni pa Mungu aishiye milele. Kulingana na maoni ya Yehova ya kwamba miaka 1,000 ni kama siku moja, mtu wa miaka 100 ameishi muda wa saa mbili na dakika 24 tu. (2 Pet. 3:8) Je! yeye anaweza kuwa na hekima sana katika muda huo mfupi namna hiyo hivi kwamba hahitaji shauri kutoka kwa Baba yake anayeishi milele? Je! yeye anakuwa na akili sana hivi kwamba anaweza kutoa uamuzi juu ya shauri hilo na apinge au kukataa yale asiyotaka?
2 Kama vile watoto wanavyohitaji shauri kutoka kwa baba wa kibinadamu mwenye hekima, ndivyo tunavyopaswa kuona uhitaji wa kupata mashauri kutoka kwa Yehova Baba yetu wa mbinguni. Yeye anafahamu sana maisha na magumu yake kuliko sisi. Je! yeye hakuishi muda mrefu sana kuliko sisi? Je! yeye hakuona kizazi baada ya kingine tangu siku za Adamu kikifanya mambo ya upumbavu ambayo yaliwaharibu? Akiwa Muumba wetu, yeye anajua mioyo yetu. Anajua namna maelekeo ya kufikiri kwetu yanavyoweza kuwa mabaya. Anajua udhaifu wetu pamoja na makosa tunayofanya mara nyingi. Yeye anajua matokeo ya mwenendo fulani na kwa hiyo anatuonya juu yake. Kwa kuwa anajua mambo haya, je! yeye hastahili sana kutupa mashauri yenye hekima yanayoweza kutufaidi kimwili, moyoni na kiroho? Kwa sababu nzuri Neno lake lililoandikwa lasema hivi: “Sikiliza mashauri, ukapokee mafundisho, upate kuwa na hekima siku zako za mwisho.” (Mit. 19:20) Shauri la Yehova ndilo shauri bora zaidi tunaloweza kusikiliza.
3. Sababu gani mwanadamu hana uwezo wa kuongoza hatua zake kwa hekima?
3 Kama vile watoto, sisi hatuwezi kuongoza hatua zetu kwa hekima katika njia ya uzima. Tunakuwa na kazi nyingi mno katika maisha yetu ya kila siku na katika tamaa zetu, hivi kwamba hatuwezi kuiona njia ya uzima barabara. Tunahitaji shauri kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni lituonyeshe njia itakayotufaidi. Kama ilivyotajwa katika makala (tungo) iliyotangulia, Yeremia alionyesha kwamba tunahitaji uongozi huu wa kimungu, akisema: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yer. 10:23) Njia yetu katika maisha si yetu tujiongoze kama tupendavyo, kama kwamba tuna uhuru kamili. Yehova ametupa uhuru wa kiasi bila kupita mipaka ya sheria zake za haki na kanuni za Maandiko. Tukipita mipaka hiyo tunajiharibu sisi wenyewe na kuharibu uhusiano wetu naye. Tukikaa ndani ya mipaka hiyo na kwa kuruhusu Yehova aongoze hatua zetu kupitia kwa Neno na tengenezo lake lenye kusonga mbele, tutakuwa wenye ‘hekima mwishoni.’ Wakati ujao utatuletea baraka nyingi.
4, 5. (a) Sana sana ni wakati gani shauri la Yehova linapokuwa lenye maana sana kwetu? Toa mfano wa mtu aliyemgeukia Yehova katika wakati kama huo wa uhitaji.
4 Katika nyakati za taabu Yehova anatuonyesha uamuzi sahihi tunaopaswa kufanya tukimwendea atupe shauri. Anatuonyesha jambo linalofaa tulifanye, kama vile baba mwenye upendo anavyofanya kwa watoto wake wasio na ujuzi na wasiokomaa. Katika nyakati kama hizo Baba yetu wa mbinguni anatutia nguvu. Tunaposhindwa kujua jambo la kufanya, shauri lake linatuongoza. “Maana umekuwa ngome ya maskini, ngome ya mhitaji katika dhiki yake, mahali pa kukimbilia wakati wa tufani, kivuli wakati wa hari.”—Isa. 25:4.
5 Mfalme Yehoshafati wa Yerusalemu alimgeukia Yehova kama ngome alipokuwa na shida. Alipoogopeshwa na jeshi kubwa la adui alimgeukia Yehova akasema: “Ee Mungu wetu, je! hutawahukumu? maana sisi hatuna uwezo juu ya jamii kubwa hii, wanaotujia juu yetu; wala hatujui tufanyeje; lakini macho yetu yatazama kwako.” (2 Nya. 20:12) Kwa hiyo katika taabu yetu leo macho yetu yanapaswa kumwelekea Baba yetu wa mbinguni na masikio yetu yasikilize mashauri yake.
6, 7. (a) Uhitaji wa kutii shauri la Yehova ulikaziwa kwa akina nani, nao waliambiwa nini? (b) Ingekuwaje ikiwa wangepinga shauri lake, nalo hilo ni onyo kwetu namna gani?
6 Uhitaji wa kutii shauri la Yehova na kutolipinga ulikaziwa kwa taifa la Israeli katika siku za Musa. Walipokuwa wamekusanyika chini ya Mlima Sinai, Yehova aliwaambia hivi: “Ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu.” (Kut. 19:5) Kwa kutii sauti yake, maana yake, kutii shauri lake na kufuata maagizo yake, wangejifurahisha uhusiano (urafiki) wa kipekee pamoja na Yehova Mungu. Wangekuwa watu waliobarikiwa, na kufaidika na ukarimu wake.
7 Baadaye, Waisraeli walipokuwa karibu na Nchi ya Ahadi, Musa aliwaonya juu ya yale yangewapata ikiwa wangepinga shauri la Yehova kwa kutosikiliza sauti ya Mungu. “Lakini itakuwa usipotaka kuisikiza sauti ya [Yehova], Mungu wako, usiyaangalie kufanya maagizo yake yote na amri zake, nikuagizazo hivi leo, ndipo zitakapokujia laana hizi zote na kukupata. [Yehova] atakupiga kwa wazimu, na kwa upofu, na kwa bumbuazi la moyoni; utakwenda kwa kupapasa-papasa mchana, kama apapasavyo kipofu gizani, wala hufanikiwi katika njia zako.” (Kum. 28:15, 28, 29) Walionywa kwamba wangepoteza macho ya kiroho nao hawangejua njia ya kufuata ambayo ingewafaidi. Jambo ilo hilo laweza kumpata ye yote katika tengenezo la Yehova anayekataa kusikiliza shauri la Yehova. Yeye pia atapatwa na “bumbuazi la moyoni” naye atapapasa-papasa akitafuta njia ya kufuata asiione. Inapasa wote wanaokuja katika tengenezo la Yehova waendelee kuona uhitaji wao wa maagizo yake yenye kuwaongoza ili waendelee kutembea katika njia iongozayo kwenye wakati ujao utakaowaletea zawadi ya uzima wa milele.
NJIA AMBAZO KATIKA HIZO SHAURI HUTOLEWA
8. (a) Njia moja ambayo katika hiyo Yehova hutoa shauri ni njia gani? (b) Sababu gani tunaweza kusema kwamba shauri lililopewa Waisraeli halikukusudiwa liwe lao peke yao?
8 Zamani sana Mungu aliwaongoza wanaume waaminifu waandike shauri lake katika Maandiko. Neno hili lililoandikwa lina mashauri yake kama ya Baba kwetu sisi tulio watoto wake. Ijapokuwa mengine ya maagizo yake yalielekezwa kwa taifa la Israeli, yanatufaidi sisi pia. “Kwa kuwa yote yaliyotangulia kuandikwa yaliandikwa ili kutufundisha sisi,” asema Paulo, mtume wa Yesu Kristo. (Rum. 15:4) Mungu alilipa taifa la Israeli shauri linalofaa juu ya ibada kwa kuwaambia kwamba walipaswa kumpa ibada ya pekee na kwamba hawapaswi kujichafua kwa kuabudu sanamu au kwa mazoea ya kidini ya kipagani. Kufuata shauri ilo hilo kutahifadhi uhusiano wetu na Yehova Mungu ili usiharibike na kuwa chombo cha kukasirikiwa naye.
9, 10. Njia nyingine ambazo katika hizo twaweza kufaidika na shauri lililotolewa taifa la Israeli ni njia gani?
9 Kwa habari ya mwenendo wa kibinafsi, alitoa maagizo yaliyokuwa kwa faida ya Waisraeli na kwa faida yetu sisi leo. Aliwaonya juu ya kuua wenzao, juu ya kuiba, juu ya uasherati, juu ya kuwa shahidi wa uongo na juu ya mambo mengine mengi. Hekima ya kutii maagizo haya aliyopewa Israeli inaonekana waziwazi. Si lazima tuwe chini ya agano la torati la Israeli ili tuweze kuona kwamba kuna faida kwetu sisi na kwa jamii tunayoishi kati yake tukitii maagizo haya yanayopasa mwenendo wa kibinafsi.
10 Vilevile Neno la Mungu linatufundisha kupitia kwa mashauri ya kipekee waliyopewa watu mmoja mmoja wanaotajwa katika Biblia. Shauri lisemalo, “kutii ni bora kuliko dhabihu,” alilopewa Mfalme Sauli ni shauri linaloweza kutufaidi sisi. (1 Sam. 15:22) Hata tukijinyima mambo gani ili tumtumikie Yehova katika huduma ya Kikristo, ikiwa hatumtii, kujinyima kwetu ni bure tu. Tukikosa kujali shauri lake juu ya mwenendo mwema tunabatilisha (tunafanya yale bure) matendo mema kama vile “dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.” (Ebr. 13:15) Hivyo, shauri la kipekee alilopewa Mfalme Sauli laweza kutufaidi kwa kutufahamisha namna lilivyo jambo la maana sana kumtii Mungu. Hatuwezi kueleza sababu za kutokutii kwa kutoa dhabihu za namna yo yote.
11, 12. Toa mfano wa mashauri waliyotolewa Wakristo wa kwanza yanayotufaa sisi leo. Eleza sababu gani yanafaa.
11 Shauri alilopewa Mkristo Timotheo juu ya kupenda fedha na juu ya hatari inayotokana na kupenda huko bila shaka ni shauri linalotufaa sisi leo kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu wenye kupenda fedha. Aliambiwa hivi: “Maana shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:10) Kupinga shauri hili linalopatikana katika Neno la Mungu kutaleta maumivu na kupoteza imani kama linavyoonya.
12 Waefeso walipewa shauri jema juu ya uhusiano unaofaa kati ya mume na mke pamoja na ule wa watoto na wazazi. Kwa kufuata shauri hili walilopewa Wakristo wa karne ya kwanza, tunaweza kuepuka taabu za ndoa zinazoharibu ndoa katika karne hii ya 20. Linaonyesha njia ya kupata amani na umoja katika uhusiano wa ndoa. Mungu alitoa shauri kama hili kwa watu wa kale, akafanya liandikwe katika Neno lake kwa faida ya watu ambao wangeishi katika vipindi vingine vya wakati. Hivyo, kwa kuliendea Neno lake, tunaweza kupokea shauri lenye hekima kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni.
13. Ni njia gani nyingine ambayo katika hiyo Yehova anatoa shauri?
13 Vilevile Yehova anatutolea shauri kupitia kwa tengenezo lake la kidunia. Kwa kuwa roho yake takatifu inaongoza baraza inayoongoza ya tengenezo hilo, shauri linalotoa linapatana na mapenzi yake. Kupitia kwa vitabu na magazeti ya Sosaiti mashauri yanayofaa yanatolewa juu ya mwenendo wa kipekee, ndoa, ibada, kushika ukamilifu wetu kwa Mungu, uhusiano wetu wa mamlaka za kisiasa za ulimwengu na juu ya mambo mengine mengi. Kupitia kwa mikutano ya kundi, tengenezo la Yehova linatushauri juu ya utumishi tunaomtolea Mungu, maoni yetu juu ya utumishi wetu, juu ya kukomaa kiroho, na vivyo hivyo. Tena nyakati nyingine baraza ya wazee katika kundi inalazimika kutushauri juu ya jambo fulani. Katika njia hizo tengenezo la Yehova linatushauri ili tuendelee kuwa na afya ya kiroho na kuendelea katika kufuata nyayo za Yesu Kristo. Tunasaidiwa tuendelee kuwa na upatano na Yehova. Liwe shauri linatoka katika Biblia au katika tengenezo la Yehova, huwa linatoka kwake na ni kwa faida yetu.
JINSI SHAURI LA YEHOVA LINAVYOPINGWA
14, 15. (a) Watu wengine leo wako kama Kora, Dathani na Abiramu namna gani katika kupinga shauri la Yehova? (b) Jambo lililo la maana kweli kweli ni jambo gani?
14 Kora, Dathani na Abiramu waliposhindana na Musa, walipinga mpango wa Yehova wa mambo. Lilo hilo laweza kusemwa juu ya watu ambao leo wamekuwa sehemu ya tengenezo la Yehova la kidunia, lakini baada ya wakati fulani wakaanza kushindana nalo. Wengine wanakosa kuridhika kwa sababu tengenezo halikubaliani na mawazo yao au na njia wanazodhani linapaswa kufuata. Wengine wanaudhika kwa sababu ya kubadili maoni, au kwa sababu ya maneno yanayotumiwa na kwa sababu ya njia zinazotumiwa na tengenezo la Yehova katika utumishi wake. Mahali pa kusonga mbele na tengenezo na kukubali mabadiliko, wanaudhika. Wengine wanaruhusu upinzani huu uwe jaribu kubwa sana kwao, na kuanguka, wakiurudia ulimwengu ulio na uadui na Mungu.
15 Watu wengine wanatoa ubishi juu ya mambo madogo kama vile mapendeleo ambayo huenda Mungu akawapa au akakosa kuwapa wale watakaofufuliwa katika taratibu yake mpya au Shetani atakuwa na hali gani anapokuwa katika lile shimo refu lisilo na mwisho, na mengine kama hayo. Mambo kama hayo hayana maana kwetu katika wakati huu. Lililo la maana ni kupata kibali ya Yehova na kuwa kati ya wale watakaopata uzima katika taratibu yake mpya. Wakati huo ufikapo tutaona namna Yehova atakavyofanya kwa habari ya mambo ambayo hatuyafahamu vizuri sasa. Inafaa zaidi kungojea tuone litakalotokea wakati huo kuliko kubishana juu ya mambo ya kukisiwa tu.
16. Sababu gani si jambo la kushangaza kwamba watu wengine wanaliacha tengenezo la Yehova leo?
16 Kwamba leo kuna watu wanaoliacha tengenezo la Yehova na wengine wanapigana nalo si jambo linalopaswa kutushangaza. Jambo kama hilo lilifanyika pia katika karne ya kwanza wakati wengine wa mitume bado walikuwa wakiishi. Kwa habari ya watu kama hao waliopinga shauri la Yehova na roho yake katika wakati huo, mtume Paulo alisema hivi: “Mtu awaye yote akifundisha elimu nyingine, wala hayakubali maneno yenye uzima ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala mafundisho yapatanayo na utauwa, amejivuna; wala hafahamu neno lo lote; bali ana wazimu wa kuwazia habari za maswali, na mashindano ya maneno, ambayo katika hayo hutoka husuda, na ugomvi, na matukano, na shuku mbaya; na majadiliano ya watu walioharibika akili zao, walioikosa kweli.”—1 Tim. 6:3-5.
17. (a) Yehova anataka watu wa namna gani katika taratibu yake mpya, nao hawatafanya nini? (b) Yohana anasema nini juu ya wale wanaoondoka kwetu?
17 Namna ya watu ambao Yehova anataka katika taratibu yake mpya ni wale wanaompenda na wanaojaribu kumtii. Hawa hawatapinga mashauri anayotoa kupitia kwa Neno lake na tengenezo lake. Wao hawatahatirisha hali yao ya kiroho kwa kurudisha nyuma maendeleo ya tengenezo lake. Akizungumza juu ya wale wanaoudhika wanapopewa mashauri na kuacha tengenezo au wale wanaoliacha kwa sababu ya mabadiliko linalofanya linapoendelea kusonga mbele, mtume Yohana anasema hivi: “Walitoka kwetu, lakini hawakuwa wa kwetu. Maana kama wangalikuwa wa kwetu, wangalikaa pamoja nasi. Lakini walitoka ili wafunuliwe kwamba si wote walio wa kwetu.” (1 Yohana 2:19) Kama wangalikuwa wanampenda Yehova kweli kweli, wangalikaa karibu na tengenezo lake, wasiruhusu cho chote kiwatenganishe nalo.
18. (a) Sababu gani ni vibaya kubishana juu ya shauri la Yehova? (b) Mahali pake, mtu anapaswa kufanya nini?
18 Njia nyingine tunayoweza kumpinga Yehova nayo ni kubishana juu ya shauri lake. Huenda mtu akafanya kosa au jambo lisilopatana na Neno la Yehova. Akionyeshwa jambo hilo naye akatae kukubali lakini ajaribu kujitetea, yeye anapinga shauri la Yehova. Yeye hajinyenyekezi na kukubali kwamba alifanya kosa. Anapaswa kuungama kosa lake, sana sana anapokutana na halmashauri ya hukumu ya kundi inayochunguza mwenendo wake. Tunaambiwa hivi katika Yakobo 5:16: “Ungameni dhambi zenu ninyi kwa ninyi.” Mtu anapoungama dhambi zake, hawi akitetea kosa lake. Kufanya hivyo kungekuwa kupinga yale ambayo Yehova amesema kwamba ni mema na mabaya.
19, 20. Mtu anawezaje kupinga shauri la Yehova katika njia isiyo ya wazi? Toa mifano namna hili laweza kufanywa.
19 Huenda mtu asibishane juu ya shauri la Yehova waziwazi, lakini huenda akalipinga kwa njia nyingine, kwa kukataa kulifuata. Mungu hutushauri juu ya maisha yetu ya kila siku, kwa mfano, kwa kutuambia tuonyeshe upendo kwa kuwa wastahimilivu, kwa kuwa na adabu, kwa kutoangalia faida zetu wenyewe tu, kwa kutohesabu makosa. Je! sisi tunatii shauri hilo? Au tunalidharau na kulipinga kwa kufanya hivyo? Tengenezo lake linatushauri juu ya kuadibu watoto wetu, juu ya kuwa na funzo letu la kipekee na juu ya kufanya kazi ya kimwili inayopatana na amani tunayofuata. Je! sisi tunatii shauri hili kwa kulitumia katika maisha yetu ya kila siku? Ndiyo sababu likatolewa. Hatufaidiki tukilidharau.
20 Mara kwa mara tengenezo litatushauri juu ya kujiepusha na mashirika mabaya, juu ya kutooa au kutoolewa na watu ambao si watumishi wa Mungu walio wakf, juu ya kufika kwa mikutano ya kundi tukiwa tumechelewa mara nyingi, juu ya kuwa wa kawaida katika utumishi wa Kikristo, na vivyo hivyo. Kudharau mashauri hayo kwa kutoyafuata ni kupinga shauri la Yehova sawasawa kama vile kulibishania. Ndivyo alivyofanya Mfalme Yeroboamu.
21, 22. (a) Eleza namna Yeroboamu alivyolipinga shauri la Yehova. (b) Maoni ya ufalme wa Israeli na wa Yuda juu ya shauri la Yehova yalikuwa maoni gani, naye Yehova alifanya nini?
21 Yeroboamu alipewa shauri kabla taifa la Israeli halijagawanyika kuwa ufalme wa kaskazini na wa kusini. Kwa sababu alipinga shauri hilo kwa kukataa kulifuata, alipoteza baraka za Yehova. Yehova alimwambia hivi: “Tena itakuwa, ukiyasikia yote nitakayokuamuru, na kuenda katika njia zangu, na kutenda yaliyo mema machoni pangu, ili kuzishika amri zangu na hukumu zangu kama Daudi mtumishi wangu alivyotenda, basi, nitakuwa pamoja nawe, nitakujengea nyumba iliyo imara.” (1 Fal. 11:38) Mahali pa kubarikiwa, yeye alikataliwa na Mungu kwa sababu alitenda kinyume cha yale aliyoambiwa na Mungu. Wengi wa watu wa falme hizo mbili za Israeli walikuwa kama Mfalme Yeroboamu. Walikataa kufuata shauri la Yehova. “Kwa sababu waliyaasi maneno ya Mungu, wakalidharau shauri lake Aliye juu.”—Zab. 107:11.
22 Yehova anawezaje kuwapenda watu wanaopinga shauri lake kwa kulibishania au kwa kukataa kulifuata? Yeye anafurahia wale wanaojaribu kufuata maagizo yake. Hao ndio anaobariki, lakini wale wenye shingo ngumu kama Waisraeli walioziba masikio yao yasisikie shauri lake wanajizuia wasipate msaada wake wanapouhitaji. “Mmebatilisha shauri langu, wala hamkutaka maonyo yangu; mimi nami nitacheka siku ya msiba wenu, nitadhihaki hofu yenu ifikapo; ndipo watakaponiita, lakini sitaitika; watanitafuta kwa bidii, wasinione. Kwa kuwa walichukia maarifa, wala hawakuchagua kumcha [Yehova]. Hawakukubali mashauri yangu, wakayadharau maonyo yangu yote.” —Mit. 1:25, 26, 28-30.
LIKUBALI SHAURI LA YEHOVA
23. Yehova na tengenezo lake hutushauri sababu gani?
23 Shauri la Yehova liwe linakuja kupitia kwa Neno lake au kwa tengenezo lake ni lenye faida kwako. Yeye anapendezwa na hali njema yako na wakati wako ujao wa milele. Anafanya taratibu yake mpya kwa ajili yako, nalo shauri lake linatolewa ili likusaidie uendelee kukaa katika njia itakayokuongoza humo. Nalo tengenezo lake la kidunia linapendezwa nawe vivyo hivyo na hali yako njema. Linataka ushike ukamilifu wako kwa Yehova Mungu na kupata kibali yake. Linataka uishi maisha yenye furaha na amani na yenye matokeo sasa, na hata baada ya vita ya Mungu ya Har–Magedoni. Linataka upate zawadi ya uzima wa milele. Kwa hiyo mashauri yote linalokupa yanakusudiwa yakusaidie uufikie mradi huo.
24, 25. Tunapaswa kuwa na maoni gani juu ya shauri la Yehova, nasi tunapaswa kuchukua msimamo gani juu ya hatua ambayo kundi limechukua juu ya rafiki yetu?
24 Likubali shauri la Yehova na ulitegemeze kwa ushikamanifu. Linapokuhimiza utafute mashirika mema, fanya bidii kulifuata. Watie moyo ndugu na dada zako wa kiroho walitii. Ikiwa mashirika mema yalikuwa ya lazima kwa afya ya kiroho ya Waisraeli, je! si ya lazima kwako? Unapolidharau shauri hili unajiumiza mwenyewe.
25 Nyakati nyingine halmashauri ya hukumu ya kundi inalazimika kuchukua hatua juu ya mtu fulani katika kundi. Ijapokuwa huenda mtu huyo akawa rafiki yako sana au mtu wa jamaa yako, usipinge mpango wa Yehova kwa kuungana naye katika kulipinga tengenezo. Hatua iliyochukuliwa ni ya lazima, nayo imechukuliwa kwa faida ya kundi lote. Matukio kama hayo yasiyopendeza yanajaribu upendo wako kwa Yehova na kwa tengenezo lake. Unapojiunga upande mmoja na wale ambao limelazimika kuchukulia hatua unakosa kuonyesha upendo na ushikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake. —1 Kor. 5:9-13.
26. Kwa sababu gani inafaa sikuzote kufuata uongozi wa Yehova?
26 Linaloweza kuonekana kuwa jambo la hekima machoni pako si bora kuliko yale yanayosemwa na Yehova. “Usiwe mwenye hekima machoni pako; mche [Yehova], ukajiepushe na uovu.” (Mit. 3:7) Ujue kwamba faida za kichoyo pamoja na urafiki yanaweza kukupofusha usione yale yanayofaa machoni pa Yehova. Hata ufikie uamuzi gani katika mawazo yako, ufuate uongozi wa Yehova.
27. Tunapaswa kusitawisha maoni gani juu ya shauri la Yehova?
27 Usitafute sababu za kutotii katika mashauri na sheria zake. Unapofanya hivyo, unaonyesha nia ya watu walimwengu wasiotaka kutii sheria bali wanataka kuziepuka kwa sababu zao za kichoyo. Hatupaswi kuwa na nia kama hiyo juu ya shauri la Mungu lenye hekima pamoja na sheria zake za haki. Ikiwa wewe ni mmoja aliyejiweka wakf kwa Mungu, utataka kumtii wala hutatafuta njia za kuepuka mashauri yake na sheria zake. Hutatafuta sababu za kujiepusha na adhabu inayotolewa na tengenezo lake. Ikiwa unataka baraka za Yehova na zawadi zilizoahidiwa, lazima upende sana kufanya yaliyo mema machoni pake.
28. Eleza nyingine za faida tunazopata kwa kutii shauri la Yehova.
28 Kwa kutii shauri la Yehova katika yote unayofanya kila siku, unaweza kujiepusha na taabu zinazoangamiza maisha. Hutasumbuliwa na dhamiri mbaya bali utakuwa na amani ya akili. Hutakuwa na uhusiano mbaya na Yehova na tengenezo lake bali utajua kwamba uhusiano wako na Mungu na tengenezo lake ni mwema. Utatazamia mbele kwa uhakika uhifadhiwe hai uvuke vita inayokuja ya Har–Magedoni Yehova atakapokuwa akifikiliza hukumu yake juu ya waovu. Ukifa kabla ya wakati huo, utakuwa na tumaini hakika kwamba utafufuliwa kwa sababu umekuwa ukifuata uongozi wa Yehova.
29. Tunahimizwa tufanye nini?
29 Lione shauri la Yehova kuwa shauri lililo bora zaidi linaloweza kupatikana. Likubali kwa kulitumia katika maisha yako ya kila siku. Usilipinge kwa kulibishania, kwa kutolitii na kwa kupinga tengenezo la Mungu. Usifuate mfano wa Waisraeli waliopata msiba wa kitaifa kwa kushindwa kusikiliza shauri la Yehova. Mahali pake, fuata mfano wa Yesu Kristo, aliyependezwa na kufanya mapenzi ya Yehova. Kama watoto na majukuu wenye hekima wa Baba yetu wa mbinguni, sikiliza sauti yake na kutii shauri lake jema kila siku ya maisha yako. “Mwanangu usiisahau sheria yangu, bali moyo wako uzishike amri zangu. Maana zitakuongezea wingi wa siku, na miaka ya uzima, na amani.”—Mit. 3:1, 2.
[Picha katika ukurasa wa 16]
“Kutii ni bora kuliko dhabihu”