Je! Sikuzote Wewe Unapata Maana?
KAKA mkubwa alikuwa na hasira yenye ghadhabu nyingi. Chombo cha kuonyesha ghadhabu yake kilikuwa ndugu yake mdogo. Na kisababishi chayo? Ndugu yake alikuwa amepewa utambuzi ambao yeye mwenyewe alikuwa amenyimwa. Hasira yake ilipoendelea kukua, mtu mwenye hekima aliyefahamiana naye alimshauri azuie hasira yake. La sivyo jambo baya lingetukia. Lakini mwanamume huyo alipuuza shauri hilo jema. Badala yake, kwa huzuni, yeye alimwua ndugu yake mdogo.
Mwanamume huyo alikuwa Kaini, mwana mkubwa wa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. Kaini alimwuua nduguye mdogo Abeli Yehova alipoikubali dhabihu ya Abeli na kuikataa ya Kaini. Mtu mwenye hekima aliyefahamiana naye hakuwa mwingine ila Yehova Mungu, aliyetoa shauri hilo lenye upendo aiilolikataa Kaini. Kama matokeo, mauaji ya kukusudia yakaingilia jamaa hiyo changa ya kibinadamu. Na Kaini alihukumiwa kuishi maisha yake marefu yaliyobaki kama mtu aliyetupwa nje ya jamaa na kukataliwa. Ni matokeo yenye kuhuzunisha kama nini kutokana na kushindwa kupata maana ya shauri!—Mwanzo 4:3-16.
Karne nyingi baada ya Kaini, Mfalme Daudi wa Israeli alifanya uzinzi pamoja na Bathsheba, mke wa Uria Mhiti, na mwanamke huyo akawa na mimba. Daudi alijaribu kushughulikia tatizo hilo kwa kumhimiza Uria aingie ndani kwa mkewe. Alipokataa, Daudi alipanga Uria afie uwanjani mwa vita na kisha akamwoa Bathsheba kuzuia asiuawe kwa kuwa mzinzi. Nabii wa Mungu alimjia Daudi na kumwonyesha uzito wa jambo alilokuwa amefanya. Upesi Daudi alifahamu maana ya shauri hilo. Hivyo, ijapokuwa kwa muda uliobaki wa maisha yake yeye alitaabishwa na matokeo ya uhalifu huo, Yehova alikubali toba yake ya moyo wote.—2 Samweli 11:1–12:14.
Mifano hii miwili ya matokeo ya kweli inaonyesha umaana wa kusikiliza shauri. Inaweza kuleta tofauti kati ya kufaulu na kushindwa, furaha na huzuni, hata uzima na kifo. Si ajabu kwamba Biblia husema: “Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri.” (Mithali 12:15) Ingawa si rahisi kusikiliza shauri. Kwa sababu gani? Tunaweza kusitawishaje mwelekeo unaofaa kama ule wa Mfalme Daudi katika habari hii na kuepuka mfano mbaya wa Kaini?
Unyenyekevu Unasaidia
Mara nyingi sana watu wanaona ni vigumu kusikiliza shauri kwa sababu hawawezi kukubali uhakika wa kwamba wanahitaji msaada. Au ikiwa wanahitaji, hawawezi kuona ni kwa sababu gani wanapaswa kukubali shauri kutoka kwa mtu huyu. Kwa kweli, hicho ni kiburi, na kufikiri kidogo kunaweza kusaidia kushinda hilo. Kwa mfano, Paulo alisema hivi: “Wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Warumi 3:23) Hilo latuambia kwamba kila mtu anahitaji shauri mara kwa mara. Linatuambia pia kwamba hata wale wanaotutolea shauri wanapungukiwa. Hakuna aliyeachiliwa. Kwa hiyo usiache makosa unayofahamu ya mtu yakuzuie wewe kukubali msaada wo wote ambao yeye anaweza kuutoa.
Yesu alikazia uhitaji wa kupigana na kiburi alipowaambia wafuasi wake hivi: “Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 18:3) Watoto wachanga wanahisi usalama wakati wazazi wao wanapowashauri na kuwaongoza. Je! wewe unahisi vivyo hivyo unaposhauriwa na mtu fulani, ukitambua kwamba shauri hilo linathibitisha upendo na hangaikio la mtu huyo kwako? (Waebrania 12:6) Mfalme Daudi, ambaye nia yake yenye unyenyekevu ya kukubali shauri ilimfungulia Yehova njia ya kukubali toba yake, alisukumwa kuandika hivi: “Ikimpasa mwadilifu kupiga mimi, ingekuwa fadhili za upendo; na ikimpasa kukaripia mimi, ingekuwa mafuta kichwani.”—Zaburi 141:5, NW.
Mwelekeo kama huo wenye upole unaweza kutusaidia sisi wakati shauri tunalopokea linapogusa yale maeneo ambapo hakuna kanuni zilizowekwa. Kwa mfano, ikiwa tunashauriwa kwamba kujipamba kwetu na njia ya kuvalia kunakwaza wengine kundini, ingehitaji unyenyekevu halisi kupata maana. Ingawa hivyo, kufanya hivyo kungekuwa kufuata shauri la upole la mtume Paulo: “Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.”—1 Wakorintho 10:24.
Kwa furaha, Yehova ameandaa Biblia, inayojaa shauri lililo bora zaidi. Kwa kweli, neno “shauri” katika namna yalo mbalimbali linapatikana humo zaidi ya mara 170. Pia, yeye anaandaa wachungaji wenye upendo kutusaidia kutumia shauri hilo. Mpango wa jamaa ni mwandalio mwingine kutoka kwa Yehova wa kutupatia usaidizi wa upendo kwa njia ya shauri kutoka kwa wazazi wanaojua madaraka yao. Acheni sisi kwa kunyenyekea sikuzote tusikilize shauri hilo.
‘Uwe Mwepesi wa Kusikia’
Yakobo 1:19 hushauri hivi: “Kila mtu na awe mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema; wala wa kukasirika.” Hasa hilo ni kweli tunapopokea shauri. Kwa sababu gani? Kwa jambo moja, je! si kweli kwamba mara nyingi sisi tunajua makosa yetu, na haitushangazi kabisa wakati rafiki anayehangaikia anapotuonyesha makosa hayo na kutoa shauri? Hakika inafanya iwe rahisi kwa wote wanaohusika ikiwa tunafahamu kwa haraka jambo analojaribu kusema na kukubali kwa unyenyekevu msaada huo wa upendo.
Wakati rafiki anapotukaribia akiwa na shauri, inatupasa kukumbuka kwamba huenda yeye akawa mwenye fadhaa sana. Si rahisi kutoa shauri. Pengine huyo anayekuja kuwa mshauri amefikiria sana maneno au njia itakayotumiwa. Huenda mzee akaanza mazungumzo kwa kutusifu sisi kwa ajili ya jambo fulani la utumishi wa Kikristo ambalo katika hilo tumekuwa tukifanya vizuri. Lakini jambo hilo halipasi kutufanya tutie shaka makusudio yake anapoendelea kutoa shauri. Yule anayetoa shauri huenda kwanza akasema katika njia isiyo ya moja kwa moja, akijaribu kutokuwa mwenye busara au kutoboa mambo wazi. Kuwa kwetu wenye fahamu ya kutosha kupata maana upesi kutamsaidia mshauri katika kazi yake ngumu na pengine kutuondolee kuudhika.
Nyakati nyingine mshauri huenda akatumia kielelezo au mfano kutusaidia tupate maana. Kijana mmoja alikuwa bado hajakuwa mtenda makosa mazito, lakini alikuwa akifuata mwendo wenye kosa. Katika kumpa sababu, mwanamume Mkristo wa umri mkubwa zaidi alichukua rula iliyokuwa kwenye dawati. Akiipinda rula hiyo mikononi mwake, aliuliza: “Nikiipinda rula hii hivi, bado ninaweza kupima mstari ulionyooka kwayo?” Kijana huyo alipata maana. Yeye alikuwa amekuwa akijaribu kupinda kanuni zifaane na tamaa zake mwenyewe. Mfano huo ulimsaidia afuate shauri la hekima la Mithali 19:20, NW: “Sikiliza shauri na kupokea nidhamu.”
Kutambua Shauri Lisilo la Moja kwa Moja
Ufahamu kama huo unaweza kutusaidia sisi tunufaike na shauri lisilo la moja kwa moja, hata bila ya mtu mwingine kuingilia. Jambo hilo lilitukia kwa habari ya kijana mmoja mwanamume katika Ureno. Yeye alikuwa akijifunza Biblia na akapokea nakala ya kitabu Kupata Faida Zote za Ujana Wako. Siku chache tu baadaye, yeye alifichua kwamba tayari alikuwa amekisoma kitabu hicho mara tatu na alikuwa amesaidiwa nacho. Katika njia gani? Hivi ndivyo kijana huyo alivyosema:
“Mimi sikuwa na tumaini lo lote halisi kwa wakati ujao, lakini sura ya 2 [“Sababu Unaweza Kuutazamia Wakati Ujao Ukiwa na Hakika”] imeyapa maisha yangu maana. Vilevile, mimi nimepiga punyeto kwa miaka kadha sasa; hakuna ye yote aliyepata kuniambia kwamba jambo hilo halimpendezi Mungu na kwamba linaumiza mimi. Baada ya kusoma sura ya 5 [“Punyeto na Ngono za Wanaume kwa Wanaume na Wanawake kwa Wanawake”], mimi nilifanya uamuzi kutoendeleza zoea hilo. Sura ya 7 [“Mavazi na Sura Huonyesha Ulivyo Wewe”] ilinisaidia kuthamini sura yangu mwenyewe, na kama unavyoweza kuona, tayari nimenyolewa.”
Yeye aliendelea hivi: “Kwa miaka mingi mimi nimekuwa nikivuta sigareti. Sura ya 15 [“Je! Dawa za Kulevya Zinaleta Maisha Bora?”] ilinyoosha mimi katika jambo hilo. Mimi nimetoa sala kwa Yehova, na tangu Jumapili sijavuta sigareti nyingine. Wajua, kwa muda fulani nimekuwa nikifanya ngono na msichana rafiki yangu, lakini sura ya 18 [“Je! Ni Busara Kutofanya Ngono Kabla ya Kufunga Ndoa?”] ilivuta fikira zangu kwenye maoni ya Mungu juu ya habari hiyo. Tayari nimesema naye juu ya jambo hilo, naye aliamua kumaliza uhusiano wetu.”
Ni furaha kama nini kuona mabadiliko kama hayo katika muda mfupi hivyo katika maisha ya kijana! Ni nini lililowezesha hilo? Uhakika wa kwamba yeye aliweza kutambua yale aliyosoma kuwa shauri lililomhusu yeye binafsi.
Kutii Shauri Kunaleta Manufaa
Shauri—liwe linatujia kwa njia isiyo ya moja kwa moja kupitia Biblia au vichapo vya Biblia, au moja kwa moja kutoka rafiki—linaweza kunufaisha. Jambo hilo linaonwa kutokana na jambo lililoonwa na baba mmoja aliyetafuta msaada kutoka kwa wanaume wazee kiroho katika kundi lake kwa sababu mwanaye wa miaka 18 hakuwa akiitikia jitihada zake za kumpa nidhamu. Wazee hao Wakristo kwa upendo walizungumza kwa kumpa sababu baba huyo, ambaye alikuwa na bidii kwa ajili ya kumtumikia Mungu lakini kwa wazi alihitaji usawaziko zaidi katika kushughulika na jamaa yake.
Alisomewa maneno ya Paulo: “Na ninyi, akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Baba huyo aliombwa kufikiri hivi: Je! ile njia aliyokuwa amejaribu kumtia moyo mwanaye, hata kama alikuwa akimaanisha mema, ilikuwa kwa kweli ikimwudhi kivulana huyo? Je! kilikuwa kisa cha kutazamia mwana huyo afuate bidii ya baba yake kwa ajili ya mikutano ya Kikristo na utumishi bila ya kujaribu kupanda upendo kwa mambo hayo katika moyo wake? Je! yeye alikuwa amemsaidia mwanaye ‘ajifunze kumwogopa Yehova Mungu wake’?—Kumbukumbu 31:12, 13.
Baba huyo alisikiliza shauri hilo na akalitumia. Matokeo yakawaje? Mwanaye wa miaka 18 sasa anahudhuria mikutano ya Kikristo, na baba anaongoza funzo la Biblia la kila juma pamoja naye. Na kama vile baba huyo alivyoeleza, “Sasa sisi tuna uhusiano mzuri zaidi wa baba na mwana.” Ndiyo, wote wawili baba na mwana walipata maana ya shauri.
Hakuna shaka kwamba sisi sote tunafanya makosa na tunahitaji shauri mara kwa mara. (Mithali 24:6) Tukipata maana na kutii shauri lenye hekima, tutafurahia baraka nyingi. Miongoni mwazo itakuwa ile baraka yenye thamani kubwa zaidi ya yote: kusitawisha na kudumisha uhusiano wa kibinafsi, wenye maana pamoja na Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo, Yehova. Hivyo, tutaitikia maneno haya ya Mfalme Daudi: “Mimi nitambariki Yehova, ambaye amenipa mimi shauri.”—Zaburi 16:7, NW.