Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 7/1 kur. 11-18
  • Kuridhika na Tengenezo la Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuridhika na Tengenezo la Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUPATA FURAHA KATIKA MIGAWO YETU
  • HESHIMA KWA MAMLAKA YA KITHEOKRASI
  • KURIDHIKA NA KWELI ILIYOFUNULIWA
  • Kuepuka Roho ya Manung’uniko
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Sababu kwa Nini Fungu la Mlalamikaji Si Lenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Je, Kulalamika kwa Namna Zote Ni Kubaya?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Jitahidi Kuwaona Wengine Kama Yehova Anavyowaona
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 7/1 kur. 11-18

Kuridhika na Tengenezo la Yehova

“Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.”​—Yohana 6:68.

1. Kwa sababu gani viumbe vya Yehova vyaweza kuwa na uhakika kamili naye?

YEHOVA anatawala na amekuwa akitawala kila kitu katika ulimwengu wote. Uwezo wake mwingi umezidumisha nyota, jua, mwezi na sayari katika mizunguko yake na ni yeye ambaye kwa njia ya upendo ameidumisha na kuihifadhi dunia iwe makao ya mwanadamu. Kila jambo afanyalo ni kamilifu kabisa na kwa sababu hii viumbe vyake vyaweza kuutumaini kabisa utawala wake wa enzi kuu uangalizi wenye rehema.

2. (a) Yehova anatumiaje sifa zake? (b) Kwa nini basi wengine wananung’unika, na wanang’unikia nani, na kwa kweli, wao wanung’unikia nani?

2 Kwa kuwa yeye ni mwenye nguvu zote na mwenye kuona yote, Yehova anatumia sifa zake zisizo na kipimo za upendo, hekima, haki ya hukumu na nguvu katika njia iliyosawazika kabisa anaposhughulika na viumbe vyake. Yeye hatumii kamwe haki yake ya hukumu kupita kiasi bila kuichanganya na upendo na rehema. Yeye hatumii vibaya nguvu zake zisizo na kipimo kamwe, bali kila wakati anazitumia kwa upendo na hekima. Yeye hajipingi kamwe, wala yeye habadiliki katika njia anayozitumia sifa zake. Kwa kuwa hii ni kweli, kwa nini vingine vya viumbe vyake nyakati nyingine vinang’unikia mipango yake na njia zake za kufanya mambo? Mara nyingi huwa ni kwa sababu ya kutokuelewa njia ambazo Yehova anatumia ili atimize makusudi yake, au ni kwa sababu ya kuwa na maoni mabaya juu ya njia ambazo katika hizo Yehova anashughulika na viumbe vyake. Walakini, ingawa ni kweli kwamba huenda mara nyingi ikawa hatujui sababu kwa nini Yehova hufanya mambo fulani, kunung’unika kwetu kungeonyesha kwamba tunakosa tumaini na imani katika Yehova Mungu na katika uwezo wake wa kutimiza mambo katika njia yake na wakati wake. Hili ni kosa nzito sana. Kama miaka 3,500 iliyopita, wakati watu wa Mungu Israeli walipokuwa wakisafiri jangwani katika sehemu ya kusini ya Palestina, walianza kunung’unikia waangalizi wao, Musa na Haruni, kuhusu ukosaji wa chakula. Musa aliwajulisha uzito wa roho yao ya manung’uniko aliposema: “Manung’uniko yenu hayakuwa juu yetu sisi, ila juu ya [Yehova].”​—Kut. 16:8.

KUPATA FURAHA KATIKA MIGAWO YETU

3. Ni nini kinachowafanya wengine wanung’unikie kazi yao ya kuhubiri?

3 Ndugu wengine leo ambao wamekuwa katika kweli kwa miaka kadha huenda wakaanza kuonyesha roho ya kutokuridhika kama ile iliyoonyeshwa na Waisraeli wa siku za Musa. Kwa miaka mingi wamekuwa wakiwaambia rafiki zao na jirani zao kwamba vita ya Har–​Magedoni iko karibu sana. Bila shaka wameenda katika nyumba zile zile wakiwa na ujumbe ule ule wa ufalme wa Mungu mara nyingi. Lakini sasa, wanaona kwamba vita ya Har–​Magedoni yapaswa ije upesi na wanaanza kukosa subira kwa sababu Mungu hamalizi uovu mara moja. Wanaanza kunung’unika.

4, 5. (a) Eleza habari ya Biblia kuhusu kilichotokea wakati Yona alipowahubiri Waninawi. (b) Kosa kubwa la Yona lilikuwa lipi, na Yehova alimfundishaje somo la rehema?

4 Linaweza kuwa jambo nzuri kwa ndugu hawa wakikumbuka nabii Yona, aliyepewa mgawo wa kuhubiri watu wa Ninawi katika karne ya tisa K.W.K. Ujumbe wake ulikuwa wa kushtua: “Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa.” (Yona 3:4) Watu wa mji huo waliposikia hivyo walitubia uovu wao mara moja na wakamrudia Yehova. Hata mfalme alijivika nguo za kuombolezea na akawaagiza watu wote wafunge na kumwomba Mungu awarehemu. Alisema: “Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha hasira yake kali, ili tusiangamizwe?” (Yona 3:9) Kwa sababu ya toba hii na unyenyekevu wa watu wengi, Yehova hakuuleta uharibifu ulioahidiwa baada ya siku arobaini. Je! Yona alionaje juu ya jambo hili?

5 Maandishi yaliyoongozwa na Mungu yanatuambia hivi: “Lakini jambo hili lilimchukiza Yona sana, naye akakasirika.” (Yona 4:1) Yona alikuwa na maoni yasiyosawazika ya kichoyo kuhusu hali hii yote. Wakati ambao maisha ya makumi ya maelfu ya watu ilikuwa hatarini, yeye alikuwa akijifikiria zaidi, akifikiri kwamba amepoteza sifa kwa sababu unabii wake haukutimia. Bila subira alitaka uharibifu wa Ninawi uje upesi baada ya siku 40, na kwa sababu hii alisahau sifa ya rehema. Alipokuwa akiwaza-waza juu ya manung’uniko yake bila furaha chini ya jua kali, Yehova alifanya mmea mkubwa ukue ili umpe kivuli. Lakini, siku iliyofuata, alimfanya nyungunyungu aukaushe mmea huo, na mara hiyo Yona akaanza kunung’unika tena. Katika wakati huu uliofaa Yehova alikazia somo lile kwa Yona kwa kusema: “Wewe umeuhurumia mtango, ambao hukuufanyia kazi, wala kuuotesha; uliomea katika usiku mmoja, na kuangamia katika usiku mmoja; na mimi, je! haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambao ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto; tena wamo wanyama wa kufugwa wengi sana?”​—Yona 4:10, 11.

6. Petro alikuwa na maoni gani kuhusu rehema ya Mungu, na sisi tunawezaje kuepuka kuwa na nia ya kutokusubiri, na kunung’unika katika utumishi wetu?

6 Ndiyo, Yehova ni mwenye huruma na mwingi wa fadhili za upendo, na wakati wo wote auruhusuo kabla ya kuwaangamiza waovu wote katika Har–​Magedoni ni wonyesho wa ajabu wa subira yake. “[Yehova] hakawii kuitimiza ahadi yake, . . . bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9) Maoni ya juu namna gani ya mambo! Kwa kuelewa maoni ya Yehova kuhusu jambo hili na kwa kuiga sifa zake zisizo na kifani, hatutakosa subira kamwe, lakini tutaridhika kumngojea yeye na wakati wake uliowekwa. Tutaendelea kuhubiri kwa kusudi la upendo, tukitumia vizuri kila nafasi inayotolewa na Yehova tuwasaidie watubu. Kwa kufanya hivyo tutakuwa na furaha katika utumishi wetu na tutaepuka kuwa wanung’unikaji wasio na furaha.

7. Eleza namna roho ya manung’uniko inavyoweza kukua akilini mwa mmisionari.

7 Huenda ndugu akatumwa katika mgawo wa kigeni kama mmisionari halafu aanguke katika mtego wa kunung’unika. Namna gani? Kwa kuwa na maoni ya kwamba kila kitu katika nchi yake mpya kinapaswa kuwa kama ilivyo katika nchi ya kwao. Huenda akatazamia hali ya maisha na starehe ziwe kama zile alizozifurahia katika Shule ya Biblia ya Gileadi katika mji wa New York. Akiona kwamba mambo hayako hivyo, anaanza kukosa furaha na kutokuridhika. Ndipo roho hii ya kutoridhika inapoenea upesi katika mambo mengine, kama vile desturi, lugha na tabia za watu wa nchi anamoishi. Yeye anaanza kulaumu haya na mambo mengine madogo ambayo anaona kwamba si sawa. Mengine ya mambo haya huenda yasihusiane na kazi ya kuhubiri habari njema za Ufalme, lakini hata hivyo anakuwa na mdomo mkubwa anapoyanung’unikia mambo ambayo kwa kawaida hangeyanung’unikia katika nchi yake, kwa kuwa sasa anakuwa na roho ya kutoridhika. Ndugu kama huyo hatafurahia mgawo wake kamwe maadamu roho hii inaendelea.

8. Ni nani katika nyakati za zamani waliokosa kutosheka na hali yao ya maisha, na je! kweli wao walikuwa na sababu ya kunung’unika?

8 Hii inatukumbusha mkutano uliochangamana wa wakimbizi waliotoka nchi ya Misri wasafiri pamoja na Waisraeli jangwani miaka 1,500 kabla ya wakati Yesu alipokuwa hapa duniani. Walikuwa wamekuwa wakisafiri zaidi ya mwaka mmoja chini ya uongozi wa Yehova walipoanza kunung’unika. Hawakuwa wameona njaa, wala viatu vyao na nguo zao havikuwa vimewapasukia katika safari yao. Walikuwa na mahitaji yao ya kuwatosha ya kila siku. Hata hivyo, hawakutosheka. Walianza kulinganisha maisha yao ya kuhama-hama na maisha yao ya hapo kwanza katika Misri, na kwa sababu hii, hata Waisraeli walijiunga nao wakilia: “Twakumbuka huko Misri bure; na yale matango, na matikiti, na mboga, na vitunguu saumu; lakini sasa roho zetu zimekauka; hapana kitu cho chote; hatuna kitu cha kutumainia isipokuwa hii mana tu.” (Hes. 11:5, 6) Ukosefu wa shukrani namna gani kwa mipango ya Yehova ya mkate wa mwujiza kutoka mbinguni!

9. Mtume Paulo ni mfano namna gani kwa wamisionari na mapainia wa pekee wa kisasa, na watajiepusha na nini wakimwiga?

9 Badala ya kuiga mkutano uliochangamana usio na shukrani pamoja na Waisraeli hawa, tunapaswa kujaribu kuwa kama mtume Paulo, aliyeishi chini ya hali mbalimbali na katika nchi nyingi mbalimbali. Akitaja mambo mbalimbali aliyoyaona akiwa mmisionari, aliwaambia Wakristo Wafilipi hivi: “Nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo. Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.” (Flp. 4:11-13) Po pote alipokwenda Paulo alikuwa amejifunza kujipatanisha na hali za huko na kufuraha na kuridhika katika mgawo wo wote aliopewa na Yehova. Wamisionari na mapainia leo wanaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wake mzuri hivyo wajiepushe na shida na maumivu ya moyo yatokanayo na kuwa mnung’unikaji asiye na furaha katika mgawo wake.

HESHIMA KWA MAMLAKA YA KITHEOKRASI

10. Kwa nini wengine wanaona ugumu wa kuheshimu mamlaka ya kitheokrasi, na hii inaweza kuongoza kwenye matokeo gani?

10 Kwa kuwa Yehova anawatumia wanaume wasiokamilika wamwakilishe katika tengenezo lake la kidunia, inakuwa vigumu kwa wengine kutambua na kuheshimu mamlaka ya kitheokrasi. Wao wanakosa kuona uhakika wa kwamba Yehova ndiye anawaweka na wanaanza kuona mwanadamu tu aliye dhaifu na asiyekamilika. Badala ya kuheshimu cheo alicho nacho ndugu, wanung’unika upesi anapofanya kosa dogo kwa sababu ya kutokamilika kulikorithiwa. Hili ni kosa zito sana na linaweza kuongoza kwenye ubaya mwingi na kutokuridhika katika kundi la watu wa Yehova.

11. (a) Na manung’uniko gani Waisraeli zaidi ya 250 waliyofanya kuhusu Musa na Haruni jangwani, yakitokeza suala gani? (b) Yehova alionyeshaje hasira yake kwa sababu ya wajumbe wake waliowekwa kukosa kuheshimiwa namna hii?

11 Mamia mengi ya miaka iliyopita, kikundi cha wanaume zaidi ya 250 kilifanya kosa kama hilo la kuwa na maoni kama hayo juu ya wajumbe wa Yehova Musa na Haruni. Wanaume hawa walijiona kwamba wao pia walikuwa wanastahili kuliangalia taifa la Israeli sawasawa kama hawa wawili na kwa hivyo “wakakusanyika kinyume cha Musa na Haruni, na kuwaambie, Ninyi inawatosha, kwa kuwa mkutano wote ni mtakatifu, kila mmoja miongoni mwao, [Yehova] naye yu kati yao; n’nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa [Yehova]?” Kwa hivyo walishtaki makosa Musa na Haruni kuwa wanajifanya mabwana juu ya kundi. Dathani na Abiramu, wawili katika kundi hili, baadaye walimwambia Musa kwamba alikuwa ‘akijikuza mwenyewe awe mkuu juu yao.’ Je! hiyo ilikuwa kweli? Je! Musa na Haruni walikuwa wamejiweka wenyewe katika vyeo vya uangalizi kwa sababu za kichoyo, au ni Yehova aliyekuwa amewaweka katika vyeo hivyo? Siku iliyofuata taifa zima lilijulishwa jibu kutoka kwa Yehova mwenyewe. Kwa kuipasua ardhi na kwa moto, Yehova aliwaangamiza waasi hao pamoja na jamaa zao, hivyo akathibitisha maneno ya Musa: “Kwa jambo hili mtajua ya kwamba [Yehova] amenituma, ili nifanye kazi hizi zote; kwa kuwa mimi sikuzifanya kwa akili zangu mwenyewe.” Na tusiyafanye makosa kama hayo yenye kuleta mauti kamwe kwa kuwanung’unikia wajumbe waliowekwa na Yehova!​—Hes. 16:3, 13, 28.

12. Kuna hatari gani kwa kuwaona watumishi waliowekwa katika njia ya kimwili, na Yehova alionyeshaje hivyo katika maneno aliyomwambia Samweli, katika 1 Samweli 16:7?

12 Kama ilivyokuwa kwa waasi hao wasio na heshima wakati mrefu uliopita, hakuna ndugu ye yote leo atakayefurahia kuridhika na tengenezo la Yehova maadamu anaendelea kuwa na maoni ya kimwili au ya kibinadamu kuelekea watumishi waliowekwa. Wataendelea kuona udhaifu wa mtumishi na watanung’unika waziwazi kwa sababu ya njia anayotumia kushughulika na mambo, wakiona kwamba labda wao wenyewe wangeweza kuyafanya vizuri zaidi. Hata hivyo, ni vizuri kukumbuka amri aliyoitoa Yehova kwa nabii wake Samweli, aliyeagizwa amtie mafuta mfalme atakayefuata katika Israeli. Samweli alimtazama Eliabu mara moja, mmoja wa wana wa Yese, akawa na hakika kwamba huyu ndiye aliyekuwa amechaguliwa na Yehova kwa sababu ya sura yake yenye kuvutia. Walakini, Yehova alimwonya Samweli: “Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; [kwa] maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali [Yehova] huutazama moyo.” (1 Sam. 16:7) Wakijua hivyo, Wakristo wote walio wakf watamheshimu mtu aliyewekwa na Yehova, hata ingawa kwa kuonekana nje nje tu au kulingana na maoni ya kilimwengu haonekani kuwa aliyestahili zaidi.

13. Ni kitu gani kinachoongeza furaha ya mtumishi aliyewekwa, lakini ni nini kinachoweza kuharibu furaha hiyo?

13 Heshima kama hiyo na kutii kwa moyo wote pamoja na kushirikiana kwa wahubiri na mapainia katika kundi kunasaidia kazi ya watumishi waliowekwa iwe yenye furaha na ya kuthawabisha. Ndiyo sababu Paulo aliwaambia Wakristo Waebrania: “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya [nafsi] zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.” (Ebr. 13:17) Kunung’unika ko kote kunakofanyiwa ndugu hao walio na vyeo vya uangalizi kungeondolea kundi furaha nyingi. ‘Hakungelifaa’ kundi na kungeonyesha roho ya kutokuridhika na mpango wa mambo wa Yehova.

14. Ni jambo gani ambalo halipaswi kufanywa hata kama mwangalizi amekosa kujali kazi zake?

14 Namna gani basi, ikiwa mwangalizi katika kundi alikosa kujali juu ya kupanga mikutano na akose kuongoza katika utumishi? Labda bado kuna miezi miwili au mitatu kabla mwangalizi wa mzunguko kutembelea kundi. Je! isingefaa kwa habari hii ndugu fulani anung’unike juu ya jambo hili, hata afikie hatua ya kuwaomba wahubiri wote waweke sahihi ombi litumwe kwa Sosaiti likiuliza kwamba ndugu huyo aondolewe katika cheo chake cha uangalizi? La, bila shaka hii ingekuwa haifai! Kumbuka kwamba Daudi hakujaribu kuchukua kwa nguvu kiti cha enzi cha Sauli mwovu katika Israeli, ingawa alijua kwamba yeye ndiye angefuata kuwa mfalme. Yeye hakuona kwamba ilifaa achukue hatua ya kumwua Sauli, hata ingawa Sauli alikuwa mtu mwovu aliyekuwa amepoteza kibali ya Yehova. Yeye aliheshimu uhakika wa kwamba Sauli alikuwa “masihi wa [Yehova]” na yeye alikuwa na nia ya kutii mpango huu mpaka Yehova amwondoe katika cheo chake.​—1 Sam. 24:6.

15. (a) Onyesha namna gani mtu anayenung’unikia mtumishi aliyewekwa anakosa imani katika Yehova. (b) Ndugu aliyekomaa, angefanya nini ikiwa mwangalizi amekosa kujali kazi yake?

15 Daudi alionyesha imani kubwa katika Yehova nyakati zote. Yeye alijua kwamba Yehova alikuwa na uongozi kamili katika mambo na yeye aliridhika na kungojea wakati Wake wa kutenda. Ndugu ye yote anayetenda kinyume cha Daudi na kupanga ombi kwa njia ya kidemokrasi au anayenung’unikia waziwazi mtumishi ye yote aliyewekwa, anaonyesha kutokuwa na tumaini au imani katika uwezo wa Yehova wa kuliangalia tengenezo Lake. Ni kama kwamba ndugu huyo anasema kwamba, kwa kuwa Mungu hachukui hatua upesi iwezekanavyo, itamhitaji yeye achukue hatua. Hii ni njia ya kijinga na ya kutokukomaa namna gani ya kuona mambo! Wakati wote Yehova hafanyi mambo katika njia ambayo tunadhani yanapaswa kufanywa, lakini tunaweza kuwa na hakika kwamba yatafanywa ifaavyo na katika wakati unaofaa. Kwa hivyo jambo la kufanya ni kumngojea Yehova, kuwa na shughuli katika utumishi, kuwasaidia ndugu kwa njia ya upendo, na kuwatia moyo waheshimu mpango wa kitheokrasi wa mapango wa kitheokrasi wa mambo. Tendo lingine lo lote la haraka lingepunguza heshima katika mamlaka ya kitheokrasi na lingetokeza dhara kubwa la kiroho katika kundi.

16. Ni jambo gani tunaloweza kuwa na hakika nalo, na kwa hivyo tunapaswa kuwa na shughuli tukifanya nini?

16 Tunaweza kuwa na hakika kabisa kwamba Yehova anajua linaloendelea katika kila kundi la watu wake. “Wala hakuna kiumbe kisichokuwa wazi mbele zake, lakini vitu vyote vi utupu na kufunuliwa machoni pake yeye aliye na mambo yetu.” (Ebr. 4:13) Yeye halali na hakuna kitu kinachofanyika bila yeye kujua. Yeye hana haja ya kuarifiwa na ndugu mwenye kunung’unika ikiwa jambo linahitaji kusahihishwa. Maandiko hutuambia: “Macho ya [Yehova] yako kila mahali; yakimchunguza mbaya na mwema.” (Mit. 15:3) Tukikumbuka wazo hili lenye kufariji, tunaweza kuridhika na kufanya kazi zetu tulizogawiwa, tukifurahia kujua kwamba Mwenye Nguvu Zote, Mwenye Enzi Kuu yeye mwenyewe ana uongozi kamili katika tengenezo lake lionekanalo.

17. (a) Mtumishi aliyewekwa anawezaje kukuza roho ya manung’uniko? (b) Ndugu kama huyo amekosa kutambua nini, na hivyo yeye anahitaji kufanya nini?

17 Nyakati nyingine hata mtumishi aliyewekwa anapatwa na roho ya manung’uniko, akijiona kwamba ana kazi nyingi mno ya kufanya. Huenda akajiona analemewa na mzigo wa kuliangalia kundi la Mungu au huenda akakosa kuwasubiri ndugu, akinung’unika kwamba hawashirikiani naye au kwamba hawaelewi mambo upesi kama vile angependa. Ndugu huyu amekosa kwa muda kuelewa ukweli wa kwamba anafanya kazi na tengenezo la Yehova na kwamba anaangalia “kondoo” wa Yehova. Anaona kama kwamba mzigo wote wa kuangalia “kondoo” hawa umemwangukia yeye. Lakini, hii si kweli. Yehova ndiye anayejichukulia daraka la kuangalia “kondoo” zake na Yesu Kristo Mwanawe ndiye aliyetoa uhai wake kwa ajili yao. Hakuna mwangalizi ye yote anayepaswa kujichukulia daraka la kuangalia “kondoo” za Yehova peke yake. Anapaswa kumtegemea Yehova kabisa na kuwa na imani kamili katika yeye. Daudi, aliyekuwa na ujuzi wa mambo aliyeyaona katika muda wa miaka 33 akiwa mwangalizi wa taifa zima, alisihi: “Umtwike [Yehova] mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.”​—Zab. 55:22.

18, 19. (a) Musa alionyeshaje nia ya manung’uniko pindi moja, lakini je! tunaweza kusema kwamba yeye alikuwa mnung’unikaji? (b) Kwa nini waangalizi leo wana sababu nyingi za kuwa na uhakika?

18 Musa, mwangalizi aliyewekwa, wakati mmoja alijiachilia aingie katika hali ya kunung’unika alipokuwa akiwaongoza Waisraeli waasi jangwani. Hata aliyaelekeza manung’uniko yake kwa Mungu katika sala akisema: “Mbona umenitenda uovu mimi mtumishi wako? kwa nini sikupata neema machoni pako, hata ukanitwika mzigo wa watu hawa wote juu yangu? Je! ni mimi niliyewatungisha mimba watu hawa wote? je! ni mimi niliyewazaa, hata ikawa wewe kuniambia, Haya wachukue kifuani mwako, mfano wa baba mwenye kulea achukuavyo mtoto aamwaye, . . . ? Mimi siwezi kuwachukua watu hawa wote peke yangu, kwa kuwa ni mzigo sana wa kunishinda. Na kama ukinitenda hivi, nakuomba uniulie mbali.”​—Hes. 11:11, 12, 14, 15.

19 Kwa kawaida Musa alikuwa mtumishi wa Yehova mwenye furaha na mwenye kuridhika na bila shaka yeye hakuwa mnung’unikaji mzoevu. Hata hivyo, wakati huu manung’uniko ya Waisraeli yalimlemea sana, hata akapatwa na roho ya manung’uniko. Walakini, hakuna mwangalizi wa kibinadamu leo aliye na kundi kubwa kama hilo la kuangalia, na ni wachache wanaolazimika kushughulika na matatizo magumu kama yale Musa aliyoshughulika nayo. Pia, waangalizi leo wana uongozi wa upendo wa tengenezo unaowasaidia, pamoja na msaada wa Yehova na Mfalme wake aliyetawazwa. Kwa hiyo hakuna sababu ya kujiona kwamba umelemewa na mzigo au kunung’unika. Kwa kulitazama pendeleo la ajabu walilo nalo na kwa kuliona kwa furaha, wanaweza kumwiga “Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu.” Kwa kufanya hivyo, na kwa kushughulika na akina ndugu katika njia ya upendo, bila kutazamia mengi mno kutoka kwao, mwangalizi hatanung’unika, badala yake, yeye atakuwa na hakika na mwenye furaha, na hivyo aeneze hali ya furaha katika kundi lote.​—Ebr. 12:2.

KURIDHIKA NA KWELI ILIYOFUNULIWA

20. Wengine wananung’unikiaje maelezo ya Maandiko ya Sosaiti, na kwa nini hii ni hatari kwao wenyewe na kwa wengine?

20 Mara nyingine tunawasikia ndugu wakiongea kwa manung’uniko juu ya maelezo ya Maandiko na kweli zinazochapwa katika Mnara wa Mlinzi. Kwa kukosa kuelewa kabisa kwa nini jambo fulani limesemwa au kwa nini ufahamu wa wazi zaidi umetolewa kuhusu jambo fulani, wanaanza kuwaeleza wengine mashaka yao. Hii, bila shaka, inaleta mvurugo kati ya akina ndugu, na hasa wale wapya zaidi, na bila shaka haimsaidii mwenye kunung’unika kwa njia yo yote. Yeye anaonyesha roho ya kutoridhika na tengenezo la Yehova ambalo katika hilo Yeye anapashana habari, mara nyingi akifanya hivyo kwa haraka-haraka bila kujua kabisa mambo yote yanayohusika.

21. (a) Wengine wa wanafunzi wa Yesu waliacha kuandamana naye kwa sababu gani? (b) Tofauti na hii, ni nia gani yenye kusifiwa walioionyesha mitume kumi na wawili, kwa matokeo gani?

21 Roho ii hii ilikuwamo miongoni mwa wafuasi wa kwanza wa Yesu. Pindi moja, baada ya kumsikiliza Yesu akiwafundisha kweli mpya zenye nguvu, wengine wao walisema: “Neno hili ni gumu, ni nani awezaye kulisikia?” Maandishi yaliyoongozwa na Mungu yanatuambia matokeo ya hili, yakisema; “Kwa ajili ya hayo wengi miongoni mwa wanafunzi wake wakarejea nyuma, wasiandamane naye tena. Kwa sababu hii, Yesu akawauliza mitume wake kumi na wawili: “Je! ninyi nanyi mwataka kuondoka?” Upesi Petro akajibu: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:60, 66-68) Wale waliokwazika waliacha kuridhika haraka-haraka. Wao hawakujipatia wakati wala hawakutia bidii wachunguze kweli zilizoelezwa waone kama zilikuwa zinapatana na Neno la Mungu. Lakini, mitume, waliridhika kubaki pamoja na Yesu wafundishwe naye polepole. Hii haina maana kwamba walielewa kila kitu alichowaambia wakati huo, kwa kuwa kulikuwa na mambo mengi ambayo hawangeweza kuyaelewa. Hata hivyo, walikuwa na imani halisi. Walijua kwamba Yehova hangeweza kuwapa jiwe wakimwomba mkate, kwa hivyo walitosheka na kusikiliza na kujifunza, wakiuliza maswali wakati ambao hawakuelewa kabisa na jambo. (Mt. 7:9-11) Walibarikiwa sana kwa sababu hii wakapewa maono kamili ya mapenzi ya Yehova kwa wakati huo walipopokea roho takatifu wakati wa Pentekoste, 33 W.K.

22. Eleza jambo tunalopaswa kufanya tunapokuwa na shida ya kuelewa kweli fulani, na onyesha kwa nini huo ndio mwendo ulio wa akili peke yake.

22 Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mfano wa wanaume hawa waaminifu. Ni kweli kwamba mambo mengine ni vigumu kuyaelewa wakati wa kwanza, lakini, badala ya kunung’unika au kuyabishania, na kwa njia hiyo tuwe kana kwamba tunashindanisha maarifa yetu machache na hekima yasiyo na kipimo ya Yehova na ujuzi wa tengenezo lake linaloongozwa na roho, je! haingekuwa jambo la hekima kuchunguza jambo hilo zaidi? Baada ya kujifunza jambo hilo kwa uangalifu sana wewe mwenyewe, zungumza na ndugu waliokomaa kuhusu jambo hilo, si kwa njia ya manung’uniko, bali ili uelewe na maoni yao kuhusu jambo hilo. Ikiwa bado unaona ugumu wa kulielewa baada ya kufanya hivyo, ingekuwa vizuri kuliacha kwa kitambo kidogo, ukingojea maelezo zaidi kama mitume walivyofanya. Mwombe Yehova akusaidie uwe na hekima uelewe jambo la kweli. Utapata ufahamu kamili wakati ufikapo Yehova akiufunua kupitia kwa tengenezo lake, ikiwa utaendelea kushirikiana na tengenezo hilo kwa imani.

23. Tunawezaje kuepuka kuwa kama waasi-imani wanaotajwa katika 1 Timotheo 6:3-5?

23 Bila shaka hatutaki kuwa kama wale waliotajwa na Paulo katika 1 Timotheo 6:3-5: “Mtu awaye yote akifundisha elimu nyingine, wala hayakubali maneno yenye uzima ya Bwana wetu Yesu Kristo, wala mafundisho yapatanayo na utauwa, amejivuna; wala hafahamu neno lo lote; bali ana wazimu wa kuwazia habari za maswali, na mashindano na maneno, ambayo katika hayo hutoka husuda, na ugomvi, na matukano, na shuku mbaya; na majadiliano ya watu walioharibika akili zao, walioikosa kweli.” Wengi wamekuwa waasi-imani kwa kuachilia roho ya manung’uniko iwafanye wakasirikie tengenezo la Yehova. Kujiepusha usiwe mmoja wao, ni lazima ujiepushe na kunung’unikia hata mambo madogo, bali uridhike na kweli iliyofunuliwa kutoka kwa Yehova.

24. Ni ukosefu gani unaoonyeshwa na wale wanaonung’unikia tengenezo la Yehova, na unaweza kuondolewaje?

24 Kama vile mfano ambayo tumezungumza ionyeshavyo, kunung’unikia tengenezo mara nyingi kunatokezwa na kutoelewa njia za Yehova za kufanya mambo na kukosa imani kamili katika yeye na mipango yake. Kwa hivyo, ili tujiepushe na maelekeo ya kunung’unika, tunahitaji kukuza imani yetu katika Yehova na tengenezo lake, tupate ufahamu zaidi na uliokomaa kupitia kwa somo la pekee, sala na kushirikiana zaidi na watu wake.

25. Tunawezaje kuwa na uhakika wa kupata furaha nyingi sasa na pia katika “taratibu za mambo zijazo”?

25 Kwa hivyo sote na turidhike kufanya kazi katika sehemu tulizogawiwa katika tengenezo, tukitambua kwamba Yehova ndiye Mbuni na Mtayarishaji wa watu wake na tukijua kwamba Yesu Kristo ndiye Mfalme wake aliyewekwa ambaye sasa ametawazwa mbinguni. Kwa kufanya kazi zetu bila manung’uniko tutapata furaha nyingi sasa pamoja na udugu zetu kundini, na katika “taratibu zijazo za mambo,” tutajifurahisha baraka nyingi ambazo kwa sasa akili zetu haziwezi kufahamu Yehova atakapokuwa akifunua makusudi yake yenye utukufu katika karne zitakazokuja. Usikose kuupata wakati huu ujao wenye furaha kwa sababu ya kuwa mnung’unikaji asiye na furaha na asiyetazama mbele, bali jifurahishe kutosheka kwa kweli pamoja na amani ya akili ukiwa pamoja na watu wa Yehova waliojaribiwa na waliowaaminifu.​—⁠Efe. 2:7, NW.

​—Kutoka The Watchtower Aug. 1, 1967.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki