Je, Kulalamika kwa Namna Zote Ni Kubaya?
Ni udhia gani mbalimbali ulio wenye kuumiza zaidi kuliko ule ambao hatuwezi kulalamika juu yake?—Marquis De Custine, 1790-1857.
KWA miaka miwili alikuwa amevumilia kusumbuliwa kingono na mwajiriwa mwenzake. Kuteta kwake dhidi ya jambo hilo kulitokeza shambulio la maneno machafu na kupuuzwa kimakusudi. Mkazo aliofungia ulikuwa ukiathiri afya yake, lakini angeweza kufanya nini? Vivyo hivyo, mwanafunzi aliyekuwa akiongoza katika darasa lake alifukuzwa shuleni kwa sababu dhamiri yake haingemruhusu kushiriki katika mazoezi ya mbinu za kupigana yaliyotakwa na shule. Wote wawili walihisi kwamba walikuwa wamekosewa, lakini je, walalamike? Ikiwa wangelalamika, je, wangeweza kutumaini kupata kitulizo, au jambo hilo lingefanya mambo kuwa mabaya zaidi tu?
Kulalamika kwa aina hiyo na nyinginezo ni kwa kawaida leo, tunapoishi kama vile tuishivyo miongoni mwa watu wasio wakamilifu katika ulimwengu usiofaa. Kulalamika hutia ndani mambo yote kuanzia kuonyesha kutopendezwa kimyakimya, huzuni, maumivu, au uchungu wa moyo juu ya hali fulani hadi kufikia madai rasmi dhidi ya mtu fulani. Watu walio wengi hupendelea zaidi kuepuka kulalamika na makabiliano; lakini je, lazima mmoja anyamaze sikuzote? Maoni ya Biblia ni nini?
Matokeo Mabaya juu Yako Mwenyewe na juu ya Wengine
Hapana shaka kwamba roho ya kulalamika daima ni yenye madhara, na yalaumiwa katika Biblia. Mlalamikaji atajiletea madhara ya kimwili na ya kiroho na kuwaletea usumbufu wale alalamikao dhidi yao. Ikimrejezea mke mwenye kulalamika, mithali ya Biblia husema hivi: “Kutona-tona daima siku ya mvua nyingi, na mwanamke mgomvi ni sawasawa.” (Mithali 27:15) Kulalamika kuelekezwako dhidi ya Yehova au dhidi ya mojawapo ya maandalizi yake kwalaumika hasa. Taifa la Israeli lilipolalamika juu ya mana iliyoandaliwa kimuujiza wakati wa safari yao ya miaka 40 nyikani, wakiiita ‘chakula dhaifu,’ Yehova alituma nyoka wenye sumu ili kuadhibu hao walalamikaji wasiokuwa na staha, na wengi walikufa.—Hesabu 21:5, 6.
Zaidi, Yesu aliwashauri wafuasi wake wasilalamike juu ya “unyasi” wa makosa yaonwayo katika wanadamu wenzetu bali tujue vizuri juu ya “boriti” lililo kubwa zaidi la kasoro mbalimbali ambazo sisi wenyewe tuko nazo. (Mathayo 7:1-5) Vivyo hivyo, Paulo alilaumu kuhukumu (namna fulani ya kulalamika) mwingine kuwa ‘kusiko na sababu ya kujitetea kwa sababu wewe uhukumuye wazoea kufanya mambo hayohayo.’ Tahadhari hizo dhidi ya kulalamika zapaswa zitusukume tuepuke kuwa wenye kuchambua isivyo lazima na kuepuka kusitawisha roho ya kulalamika.—Waroma 2:1.
Je, Kulalamika kwa Namna Zote Kwalaumika?
Basi, je, tukate kauli kwamba kulalamika kwa aina zote kwapaswa kulaumiwa? La, hatupaswi kufanya hivyo. Biblia huonyesha kwamba katika ulimwengu wenye dosari ambamo twaishi kuna ukosefu mwingi wa haki ambao kwa haki wahitaji kurekebishwa. Katika kielezi fulani, Yesu alimtaja hakimu fulani asiye mwadilifu ambaye shingo upande alimpatiliza kulingana na haki mjane fulani aliyeonewa ili ‘asifulize kuja kumpigapiga ngumi hadi kummaliza.’ (Luka 18:1-8) Katika mambo fulani huenda sisi pia tukadumu katika kulalamika kwetu mpaka makosa yarekebishwapo.
Kwa kututia moyo tusali Ufalme wa Mungu uje, je, Yesu hakutuhimiza tutambue upungufu mbalimbali wa ulimwengu huu wa sasa na ‘kupaaza kilio’ kwa Mungu ili tupate suluhisho? (Mathayo 6:10) “Kilio [“cha kulalamika,” NW]” kuhusu uovu wa Sodoma na Gomora ya kale kilipoyafikia masikio ya Yehova, aliwatuma wajumbe wake ili ‘kuona kama waliyotenda ni kiasi cha kilio kilichomjia’ na kusuluhisha mambo. (Mwanzo 18:20, 21) Baadaye Yehova alirekebisha hali kwa kuyaharibu hayo majiji mawili na wakaaji wake wasio na adili, kwa kitulizo cha wale waliokuwa wamemlalamikia.
Kutaniko la Kikristo
Je, iwe tofauti miongoni mwa ndugu katika kutaniko la Kikristo? Ingawa wao ni wanaume na wanawake wasio wakamilifu, Wakristo wanajitahidi kwa bidii kumtumikia Mungu katika amani na muungano. Lakini, hali zitatokea miongoni mwao zitakazosababisha kulalamika kwa kiasi fulani ambako kwahitaji suluhisho. Karne ya kwanza, hali ilitokea katika kutaniko la watiwa-mafuta upesi baada ya Pentekoste. Wakristo wengi waliogeuzwa imani karibuni walibaki Yerusalemu ili kupata maagizo na kitia-moyo zaidi. Kulikuwa na kushiriki ugavi mbalimbali wa chakula kilichopatikana. Hata hivyo, “mnung’uniko ulitokea kwa upande wa Wayahudi wenye kusema Kigiriki dhidi ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa hawaangaliwi katika ugawanyaji wa kila siku.” Badala ya kuwalaumu walalamikaji hawa kuwa wachochezi, mitume walichukua hatua ya kurekebisha hiyo hali. Ndiyo, kulalamika kwa haki kufanywako kwa staha istahiliyo na katika roho ifaayo kutasikilizwa kwa unyenyekevu na kuchukuliwa hatua na wale wenye kusimamia kutanikoni.—Matendo 6:1-6; 1 Petro 5:3.
Lalamikia Mamlaka Ifaayo
Je, ulitambua kutokana na vielelezo vilivyo juu kwamba kulalamika kwapaswa kufanywa katika roho ifaayo na kwa mamlaka ifaayo? Kwa kielelezo, hakungekuwako sababu ya kulalamikia polisi juu ya kodi nzito yenye kulemea au kulalamikia hakimu juu ya kuugua mbalimbali kwa kimwili. Kwa hiyo, pia, haingefaa kumlalamikia mtu ambaye hana mamlaka wala uwezo wa kusaidia katika hali fulani ama ndani ama nje ya kutaniko.
Katika nchi zilizo nyingi leo, kuna mahakama na mamlaka nyinginezo zifaazo ambako waweza kukata rufani kwa matumaini ya kupata kipimo fulani cha kitulizo. Mwanafunzi aliyetajwa mwanzoni mwa hii makala alipopelekea mahakama lalamiko lake, mahakimu waliamua kwa kumpendelea, naye akarudishwa shuleni na kuombwa radhi na hiyo shule. Vivyo hivyo, huyo mfanyakazi wa kike aliyesumbuliwa kingono alipata kitulizo kupitia chama cha wafanyakazi wanawake. Alirudishwa kazini tena na kuombwa radhi na bodi ya shule. Waajiri wake walichukua hatua za kukomesha usumbufu wa kingono.
Hata hivyo, haipasi kutarajiwa kwamba, kulalamika kwa namna zote kutakuwa na matokeo hayohayo. Mfalme Solomoni mwenye hekima alionelea hivi kihalisi: “Yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa.” (Mhubiri 1:15) Twafanya vema kutambua kwamba itabidi mambo fulani yamngojee Mungu tu kuyarekebisha katika wakati wake mwenyewe upasao.
[Picha katika ukurasa wa 31]
Wazee husikiliza na kuchukua hatua juu ya malalamiko ya haki