Thawabu Bora kwa Ajili ya Utumishi Mtakatifu
Kama Ilivyosimuliwa na Harry Bloor
Karibu miaka mia moja iliyopita, babu yangu alikuwa mshiriki thabiti wa Kanisa la Methodisti. Pia alikuwa mhubiri wa kawaida aliyestahiwa na watu, aliyetoa kwa ukarimu ili kutegemeza vikanisa vingi katika Stoke-on-Trent, mji wa ufinyanzi wa Uingereza. Kisha akapatwa na nyakati ngumu kifedha. Ili kumsaidia Babu, baba yangu alipanga Babu awe na duka dogo kijijini. Hilo duka lilikuwa na leseni ya kuuza pombe, na Wamethodisti walipopata kujua hilo, mara moja walimfukuza Babu kutoka kanisani.
BABA alighadhibika na kuapa kwamba hangejihusisha tena kamwe na dini hata kidogo—naye alitimiza maneno yake. Alikuwa amekuwa polisi, lakini baadaye akawa na kilabu ya pombe. Kwa hiyo nililelewa katikati ya harufu na moshi wa mahali hapo. Dini haikuwa na sehemu yoyote maishani mwangu, lakini nilipata kujifunza kucheza mingi ya michezo ya ubao kwa ustadi! Hata hivyo, kwa sababu ya uvutano wa mapema wa Babu, nilidumisha staha ifaayo kwa Biblia, ingawa nilijua machache kuihusu.
Nilijifunza Kweli ya Biblia
Mwaka wa 1923, nilipokuwa na umri wa miaka 24, nilihamia mashariki hadi Nottingham na kuanza kutafuta uchumba na Mary, aliyeishi umbali wa kilometa zipatazo 40 katika kijiji cha Whetstone, kusini-mashariki ya Leicester. Baba yake, Arthur Rest, alikuwa amekuwa mpiga-kinanda kwenye kikanisa cha mahali hapo, lakini kufikia wakati huo alikuwa Mwanafunzi wa Biblia aliye thabiti, kama vile Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Sikuzote Arthur alikuwa akizungumza nami juu ya imani yake mpya—pasipo mafanikio sana. Hata hivyo, upendezi wangu uliamshwa nilipoandamana naye kwenye kikanisa cha mahali hapo alasiri ya Jumapili, Julai 13, 1924, ili kusikiliza mhadhara ambao ungetolewa na mshiriki wa bunge, ambaye alikuwa Mbaptisti mashuhuri. Habari yake, “Mafundisho ya Pasta Russell Yachunguzwa kwa Kutumia Maandiko,” yaliamsha kupendezwa kwangu. Bado nina maandishi niliyoandika wakati huo.
Wabaptisti walikataa ombi la Wanafunzi wa Biblia ili kujibu shambulio juu ya itikadi zao. Niliwaka hasira kwa sababu ya hilo, nikaazimia kupata mahali badala pa kufanyia mkutano huo. Ghala lililokuwa karibu lilithibitika kuwa mahali pafaapo. Tulilifagia likawa safi, tukatoa tando za buibui, tukasongeza upande mmoja mashine za kupuria, kisha sisi sote tukawa tayari. Tulikusanya viti 70, nasi tukachapisha vikaratasi vya kukaribisha watu.
Frank Freer alipofika kutoka Leicester ili kutoa hiyo hotuba, viti vyote vilikuwa vimekaliwa, na watu wengine 70 walikuwa wamesimama! Kusababu kwa Frank kulikokuwa wazi kutoka katika Maandiko kulinivutia, kama vile kulivyovutia wengine wengi waliokuwapo. Tangu wakati huo na kuendelea, lile kutaniko dogo la Wanafunzi wa Biblia katika Blaby karibu na Leicester lilipanuka upesi. Ulikuwa pia wakati wa badiliko la maana maishani mwangu—na maishani mwa Mary vilevile. Mwaka wa 1925 sote wawili tulijiweka wakfu kwa Yehova, tukabatizwa, na kuoana.
Baraka za Kiroho
Mwaka uliofuata, niliwekwa rasmi kuwa mwelekezaji wa utumishi katika Kutaniko la Blaby. Mke wangu nami tulitaka kufuata hatua za makolpota, tukawe waeneza-evanjeli wa wakati wote, lakini upesi ikaonekana kwamba afya ya Mary haingemruhusu kuendeleza ratiba hiyo yenye shughuli nyingi. Ingawa alikuwa na afya mbaya hadi kifo chake mwaka wa 1987, alikuwa mwandamani mzuri na mhudumu bora ambaye alikuwa stadi wa kutoa ushahidi wa vivi hivi na kuanzisha mafunzo ya Biblia. Usiku kwa usiku tulikuwa ama tukihudhuria mikutano ama kushiriki kweli za Biblia pamoja na jirani zetu.
Nilikuwa mhandisi na nilifanya kazi katika kiwanda kilichotengeneza mashine za kiwanda cha kupasulia mbao. Kazi yangu ilihusisha kusafiri sana kuzunguka Uingereza, na pia Ufaransa, na mara nyingi Mary aliandamana nami. Safari hizo zilituwezesha kupata fursa za kutoa ushahidi sana.
Misingi ya Mpanuko
Mwaka wa 1925 tulijenga jengo zuri kwa ajili ya mikutano yetu katika Blaby, na kutoka hapo tulipanga programu ya kutoa ushahidi yenye matokeo. Kila asubuhi ya Jumapili, tulikodi basi lililotupeleka kwenye vijiji vilivyotawanyika na kwenye miji midogo-midogo. Wahubiri walishukia njiani ili kuhubiri, kisha wakachukuliwa na basi lilipokuwa likirudi. Wakati wa miezi ya kiangazi yenye joto, tulikuwa na funzo la Biblia Jumapili alasiri, tukitumia makala ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi. Baadaye, saa mbili kamili, tulikutana sokoni Leicester kwa ajili ya hotuba ya watu wote iliyofanyika nje. Usiku mmoja watu 200 walisikiliza. Utendaji huu uliweka misingi ya makutaniko mengi ambayo sasa yako Leicester na kandokando.
Mwaka wa 1926, mkusanyiko wenye kuanzisha kipindi kipya cha historia ulifanywa kwa muungano kwenye Alexandra Palace ya London na Royal Albert Hall. Kwenye pindi hiyo Joseph F. Rutherford, msimamizi wa awali wa Watch Tower Society, alitoa kitabu Deliverance. Azimio “Ushahidi kwa Watawala wa Ulimwengu” na hotuba ya watu wote yenye nguvu ya ndugu Rutherford “Sababu Serikali za Ulimwengu Zinatetereka—Kiponyi” zilichapwa zikiwa kamili katika gazeti kuu siku iliyofuata kutolewa kwake. Watu zaidi ya 10,000 walisikia mhadhara wa watu wote, na nakala 50,000,000 za hilo azimio ziligawanywa baadaye ulimwenguni pote. Kusanyiko hilo liliongeza mwendo wa kazi ya kuhubiri katika Uingereza.
Mkusanyiko Mkubwa Wakati wa Vita
Vita ya ulimwengu ya pili ilizuka Septemba 1939, na kufikia mwaka wa 1941 vita ilikuwa kali zaidi. Ndege za mabomu za Ujerumani zilishambulia mchana na usiku, na umeme ulizimwa kotekote katika taifa. Chakula kilikuwa haba, na kilichopatikana kiligawanywa sawasawa. Usafiri ulikuwa mchache sana, hata kwa garimoshi. Vijapokuwa vizuizi hivyo vilivyoonekana kuwa visivyoshindwa, Septemba 3-7, 1941 tulifanya mkusanyiko wa kitaifa wa siku tano.
Jumba la De Montfort Hall la Leicester lilichaguliwa kuwa mahali pa mkusanyiko kwa sababu jiji la Leicester liko katikati ya Uingereza. Kwa kuwa nilikuwa katika kiwanda cha mbao, niliweza kusaidia kutengeneza ishara za matangazo. Pia nilipanga usafiri wa wakusanyikaji wa mahali hapo. Kwa kununua tikiti mapema na kulipa zaidi ya bei ya kawaida, tramu za Leicester ziliendelea kusafiri hata Jumapili.
Kwa sababu kulikuwa na vizuizi vya usafiri, tumaini letu lilikuwa kwamba labda Mashahidi 3,000 wangeweza kuja. Wazia ule msisimko wajumbe 10,000 waliposema kwamba wangekuwako! Lakini wangekaa wapi? Kwa fadhili raia wa Leicester waliwaalika wengi wakae nyumbani kwao. Kwa kuongezea, watu wapatao elfu moja walikaa katika mahema yaliyosimamishwa katika uwanja ulio kilometa tatu kutoka mahali pa mkusanyiko. Camp Gideon, kama tulivyopaita, paliamsha upendezi mkubwa katika jumuiya.
Mahema makubwa meupe yalikodiwa ili yatumiwe kwa ajili ya idara mbalimbali za mkusanyiko na ili kuandaa mahali pa kukaa umati mkubwa uliomiminika. Ilipopambanuliwa kwamba katika mbalamwezi, mahema hayo yangelengwa na ndege za mabomu za Nazi, yalifunikwa haraka. Watu wote walihangaishwa na vita, na hasa kutoshiriki kwa Mashahidi katika vita. Mamia ya Mashahidi walikuwa gerezani wakati huo kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo wenye kutegemea Biblia.—Isaya 2:4; Yohana 17:16.
Gazeti la habari Sunday Pictorial, la Septemba 7, 1941, liliripoti hivi: “Ni jambo lenye kushangaza kukuta watu 10,000, wengi wao vijana, wakitumia juma zima kuzungumza juu ya dini bila kutaja vita, ila tu liwe jambo lisilo muhimu.
“Niliuliza ikiwa hao Mashahidi walikuwa na washiriki wowote Ujerumani. Ndiyo, niliambiwa, na karibu wote, wapatao 6,000, walikuwa katika kambi za mateso.”
Huyo mwandishi wa habari aliongeza kusema hivi: “Oh, ndiyo, ni kweli kwamba askari wa Nazi ndio maadui, lakini Mashahidi wanafanya machache sana kuwahusu, ila tu kuuza trakti na kusikiliza hotuba mbalimbali.”
Kwa ujumla maelezo ya gazeti la habari juu yetu yalikuwa hasi, na wapinzani hata waligeukia jeuri katika majaribio yasiyo na mafanikio ili kuvuruga mkusanyiko wetu. Hata hivyo, gazeti la habari Daily Mail la London lilikubali hivi, likiwa na wivu kwa kiasi fulani: “Hiyo mipango ilikuwa mitulivu, isiyojitanguliza, na yenye matokeo.”
Tulishtakiwa kwamba tulisababisha upungufu wa ugavi wa sigareti katika jiji hilo. Lakini gazeti la habari The Daily Mail lilieleza hivi: “Wala Leicester wala Tobacco Controller hawawezi kulalamika kwamba Mashahidi wanamaliza ugavi wa sigareti za Leicester. Wao hawavuti sigareti.” Pia, malalamiko ya kwamba wakaaji wenyeji walinyanganywa chakula na Mashahidi yaliondolewa ilipoelezwa kwamba walikuwa wameleta sehemu kubwa ya ugavi wao wa chakula walipokuja. Kwa hakika, mwishoni mwa mkusanyiko, mikate 150 yenye uzani wa kilogramu 1.8 ilichangwa kwa Leicester Royal Infirmary—mchango mkubwa nyakati hizo za upungufu wa chakula.
Huo mkusanyiko uliboresha hali ya kiroho ya Mashahidi wapatao 11,000 katika Uingereza. Walisisimka kwamba watu wapatao 12,000 walihudhuria! Wajumbe walishiriki kwa shangwe katika kutoa ushahidi katika barabara za Leicester kwa kiwango kisicho na kifani, nao walitembelea vijiji vya mbali wakiwa na utoaji mbalimbali kwa kutumia kinanda cha gramafoni.
Hotuba kuu za mkusanyiko zilikuwa mirekodi iliyofanywa mwezi uliotangulia ya hotuba zilizotolewa kwenye mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova wa siku tano katika St. Louis, Missouri, Marekani. Mrekodi wa hotuba ya Ndugu Rutherford “Watoto wa Mfalme” ulikuwa jambo kuu la mkusanyiko. Kwa kuwa haikuwezekana kuingiza kutoka nchi za nje nakala za kitabu Children kilichotolewa St. Louis, chapa ya pekee ya kitabu kilichojalidiwa kwa karatasi ilitokezwa baadaye Uingereza. Nakala yake ilipelekewa kila mtoto aliyekuwa amehudhuria huo mkusanyiko.
Mkutano wa Pekee wa Kila Mwaka wa Leicester
Baada ya vita ongezeko la wapiga-mbiu wa Ufalme katika Uingereza lilikuwa la kustaajabisha! Kufikia mapema miaka ya 1980, idadi ya makutaniko katika Leicester ilikuwa imekua kufikia kumi. Kisha tukafahamishwa kwamba Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilikuwa limeamua kuwa na mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society katika Leicester mwaka wa 1983. Nikiwa mwangalizi wa jiji la Leicester, upesi nilihusika katika matayarisho, kutia na kukodi De Montfort Hall tena.
Washiriki 13 wa Baraza Linaloongoza walikuja kutoka makao makuu ya Sosaiti ya Brooklyn kwa ajili ya tukio hilo. Jumla ya wajumbe 3,671—wakati huu kutoka ulimwenguni pote, na hasa wale wa zamani—walijaza huo ukumbi. Wengine 1,500 zaidi walisikiliza programu hiyo katika Jumba la Kusanyiko la karibu.
Albert D. Schroeder, aliyekuwa amekuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi ya Watch Tower Society huko London wakati wa mkusanyiko wetu wa Leicester uliofanywa wakati wa vita, alisimamia mkutano huo wa kila mwaka. Akikumbuka ya nyuma juu ya mkusanyiko wa mwaka wa 1941, Ndugu Schroeder aliuliza hivi: “Ni wangapi kati yenu mlio nasi leo waliokuwapo wakati huo?” Zaidi ya nusu ya wasikilizaji waliinua mikono yao. “Loo! Ni muungano ulioje kwa nyinyi nyote waaminifu, wenye uaminifu-mshikamanifu!” akasema kwa mkazo. Kwa kweli lilikuwa jambo lisiloweza kusahaulika.
Nikiwa na umri wa miaka 98, bado natumikia nikiwa mwandishi katika kutaniko letu na naendelea kutoa hotuba za watu wote, ingawa sasa nafanya hivyo nikiwa nimeketi. Baada ya kifo cha Mary mwaka wa 1987, nilimwoa Bettina, mjane ambaye Mary nami tulikuwa tumemjua kwa miaka mingi. Nashukuru kutunzwa vizuri sana, kimwili na kiroho pia. Vijapokuwa vizuizi vilivyotokezwa na afya mbaya ya Mary, na vitokezwavyo sasa na uzee wangu mwenyewe, nimepata kujua kwamba kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi mtakatifu kumekuwa kwenye thawabu bora sikuzote.—1 Wakorintho 15:58.
[Picha katika ukurasa wa 26]
Tayari kushiriki katika huduma miaka ya 1920
[Picha katika ukurasa wa 26]
Mandhari za mkusanyiko wa Leicester