Wale Watakaopata Faida za Ufufuo Kutoka “Hell”
1, 2. (a) Ni mzee gani wa ukoo wa Kiebrania aliyesema alitarajia kwenda hell? (b) Yesu alitoaje uhakika wa kufaidika kwa Yakobo kutoka huko, alipokuwa akilitetea fundisho la ufufuo?
KATI ya wale waliokufa katika hell na watakaofaidika kwa njia ya ufufuo kutoka kwa wafu watakuwamo akina nani? Twakumbuka kwamba mzee wa ukoo Yakobo alitarajia kwenda hell au “Sheol.” (Mwa. 37:35) Je! yeye atakuwamo kati ya watakaopata faida hizo? Ndiyo. Twayakumbuka maneno ya Yesu Kristo, ambaye, mbele ya kumfufua rafiki yake Lazaro kutoka katika hali yake ya kufa kwa siku nne, alimwambia hivi Martha dada yake: “Mimi ndimi ufufuo na uzima: yeye aniaminiye mimi, ajapokuwa amekufa, ataishi.” (Yohana 11:25, Douay) Majuma machache tu kufuata hapo, ilimlazimu Yesu kulitetea fundisho la ufufuo mbele ya wasioamini wa Kiyahudi, Masadukayo. Akifanya hivyo alimtaja Yakobo. Kwa kulijibu ulizo la kumtegea aliloulizwa na Masadukayo, Yesu alisema:
2 “Sasa kwamba wafu hufufuka tena, Musa vile vile alionyesha, penye kichaka, alipomwita Bwana, Mungu wa Ibrahimu, na Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo; kwa maana yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai: kwa maana kwake yeye wote wanaishi.”—Luka 20:37, 38, Douay.
3. (a) Ni kulingana na maoni ya nani Ibrahimu, Isaka na Yakobo sasa wanaishi, na kwa sababu gani? (b) Yehova ni Mungu wa watu wa namna gani?
3 Kwa hiyo, kulingana na maoni ya Mungu, Ibrahimu, Isaka na Yakobo walikuwa wakiishi wakati huo. Ufufuo wa wazee hawa wa ukoo ulikuwa hakika sana katika wakati wa Mungu uliowekwa, hata Mungu akazungumza juu ya wanaume hao watatu kana kwamba walikuwa hai, wajapokuwa walikuwa wamekufa, wasio na fahamu, katika hell, katika “Haʹdes au “Sheol.” Kama ingaliwapasa kubaki wamekufa milele na kutokutoka kamwe katika hell (“Haʹdes au “Sheol”), Yehova asingalisema na nabii Musa penye kichaka chenye kuwaka moto katika jangwa la Sinai kama akiwa ndiye Mungu wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Kwa hiyo Yesu alisema kwamba kufanya kwa Mungu tangazo hilo kulihakikisha kwamba kungekuwako ufufuo wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, na, bila shaka, wa wengine wote waliomo pamoja nao katika hell. Yehova si Mungu wa kale wa watu waliokufa kale, bali ndiye Mungu wa waabudu wake waaminifu watakaoishi wakati ujao kwa njia ya ufufuo wa wafu.
4. Waebrania 11:17-19 yahakikishaje kwamba Ibrahimu aliamini katika ufufuo wa mwanawe Isaka?
4 Mzee wa ukoo Ibrahimu aliamini katika ufufuo kwa ajili ya mwanawe Isaka. Kwa kuhakikisha hili tunayo maneno yaliyoongozwa na roho ya Mungu ya Waebrania 11:17-19, NW: “Kwa imani Ibrahimu, alipojaribiwa, alikuwa karibu kumtoa Isaka kama dhabihu, naye mwanamume huyu aliyekuwa amezipokea ahadi kwa furaha alijaribu kumtoa mwanawe mzaliwa wa pekee kama dhabihu, ajapokuwa alikuwa amekwisha kuambiwa: ‘Kitakachoitwa “uzao” wako kitakuwa kupitia kwa Isaka.’ Lakini yeye aliamini kwamba Mungu angeweza kumwinua hata kutoka kwa wafu; na kutoka hapo alimpokea vile vile katika njia ya mfano [kwa usemi wa mfano, The Jerusalem Bible; kama mfano, Catholic Confraternity Version]”
5. Waebrania, sura ya 11, yaonyeshaje kwamba wanaume hata mbele ya Ibrahimu, Isaka na Yakobo, na wanaume wenye imani tangu wakati huo, waliamini katika ufufuo kutoka hell?
5 Kwa wazi mbele ya wakati wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, wanaume wenye imani wanaoitwa Habili, Henoko na Nuhu waliamini katika ufufuo wa wafu kutoka hell, kwa maana wamepangwa kati ya “wingu kubwa la mashahidi” wanaotajwa katika Waebrania, sura ya 11. (Waebrania 11:1 mpaka 12:1) Wakati mwandikaji aliyeongozwa na roho ya Mungu anapotaja namna ambavyo nabii Eliya alimfufua mwana wa mjane wa Sarepta na namna ambavyo nabii Elisha alimfufua mwana wa mwanamke mwenye ukaribishaji mwema wa Shunami, anasema: “Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa. Lakini wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi, ili wapate ufufuo ulio bora. . . . Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi; kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi.” (Ebr. 11:35-40) Hivyo tunao uhakika ulioongozwa na roho ya Mungu kwamba, mbele ya kuja kwa Yesu Kristo, wanaume na wanawake wenye imani katika Mungu Mwenye Nguvu Zote Yehova waliutazamia ufufuo wa wafu kutoka hell au “Sheol.”
6. Martha wa Bethania na Hana mama yake Samweli walionyeshaje imani yao katika ufufuo kutoka hell?
6 Ndiyo sababu mwanamke Martha wa Bethania alimwambia Yesu hivi, mbele ya yeye kumfufua ndugu yake Lazaro kutoka kwa wafu: “Najua kwamba atainuka tena, katika ufufuo katika siku ya mwisho.” (Yohana 11:24, Douay) Vile vile, ndiyo sababu mwanamke Hana wa zaidi ya miaka 1,000 mapema alisema hivi, alipomtoa mwanawe Samweli kwa kuhani mkuu wa Israeli: “Bwana huua na kufufua, yeye hushusha katika hell [“inferi,” Kirumi; Sheol, Kiebrania ] na kurudisha tena.”—1 Wafalme (au, 1 Samweli) 2:6, Douay.
KANISA LA KWELI LARUDI KUTOKA “HELL”
7, 8. (a) Ni kwa njia gani “milango ya “hell” haitalishinda kundi la kweli la Kristo? (b) Ufunuo 2:10 unahitaji Yesu aishinde milango ya hell kwa njia gani?
7 Si kwamba tu Yesu Kristo mwenyewe alikwenda hell na kutokea tena, lakini yeye aliwahakikishia mitume wake kwamba Kanisa la kweli, kundi la kweli la Kikristo, lingemwiga yeye katika hili. Alipokuwa akizungumza na mtume Petro mitume wengine wakisikia, Yesu alisema: “Wewe ndiwe Petro [Petros, Kigiriki]; na juu ya mwamba huu [petra, Kigiriki] nitalijenga kanisa langu nayo milango ya hell [Haʹdes, Kigiriki; infernus, Kirumi] haitalishinda.” (Mt. 16:18, Douay) Kwa kufa washiriki wa kundi la kweli la Kikristo wangepita katika milango hiyo na kuingia hell. (Isa. 38:10, 18, Douay) Lakini hiyo “milango ya hell” isingelishinda kundi la Kikristo kwa kulifungia kundi milele. Kwa sababu gani sivyo? Kwa sababu Yesu Kristo aliyefufuliwa, aliye na “funguo za mauti na hell,” atautumia ufunguo na kuifungua milango hiyo na kulitoa kundi lake nje kwa ufufuo.
8 Hivyo “milango ya hell” haitalishinda kundi la Kristo, bali Kristo ataishinda “milango ya hell” kwa ajili ya kundi lake. Hii yaeleza sababu gani aliliambia kundi hivi: “Iweni waaminifu hata kufa: nami nitawapeni taji ya uzima.”—Ufu. 2:10; 1:17, 18, Douay.
9. Ni wangapi watakaolifanyiza hili kundi la Kikristo, nacho ni nini “kitu kilicho bora” ambacho ‘Mungu alitangulia kuwawekea’?
9 Kundi hili la kweli la washiriki waaminifu 144,000 tu linaitwa litoke katika hell (“Haʹdes,” au, “infernus”) kwenye ufufuo wa kimbinguni, wa kiroho. Hivyo wanakuwa “bibi-arusi, mkewe Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 21:9 mpaka 22:17, Douay) Kama vile mke mwaminifu, wao wameungana milele na Bwana-arusi wa kimbinguni Yesu Kristo katika kifungo cha arusi. Imeandikwa hivi juu ya ufufuo wao: “Hupandwa mwili wa asili, utafufuka mwili wa kiroho.” (1 Kor. 15:42-44, Douay) Makao haya ya kiroho ya kimbinguni ndicho “kitu kilicho bora” ambacho ‘Mungu alitangulia kuliwekea’ kundi la wafuasi waaminifu na waigaji wa Mwanawe Yesu Kristo.—Ebr. 11:39, 40.
WAFU WA WANADAMU WALIOKOMBOLEWA WATOKA “HELL”
10. (a) Ni kwa ajili ya nani wengine Yesu ataishinda milango ya hell, na namna gani? (b) Kwa hiyo n’nini ambacho mtume Yohana aliona kikitukia katika njozi ambacho wengine watakiona kikitukia kweli?
10 Yesu Kristo aliyefufuliwa atafanya mengi zaidi kuliko kuishinda “milango ya hell” kwa ajili ya kundi lake la bibi-arusi. Vile vile ataishinda “milango” hiyo kwa ajili ya wanadamu wote ambao kwa ajili yao aliutoa uhai wake kama ukombozi. (Mt. 20:28, Douay) Yeye atazitumia ‘funguo zake za mauti na za hell’ na kuifungua “milango” hii ya mfano na kuwatoa nje wanadamu hawa kwa ufufuo wa uzima duniani chini ya ufalme wake mwenyewe na bibi-arusi wake wa kiroho wa kimbinguni. Wale waliozikwa katika kaburi lenye maji baharini watafufuliwa katika nchi kavu. Wale waliozikwa katika nchi kavu katika kaburi moja moja, au katika maziara, nao vile vile watafufuliwa katika dunia chini ya serikali mpya, ufalme wa Mungu wa kimbinguni kwa njia ya Mwanawe Yesu Kristo. Mamia ya maelfu walio hai leo wataiokoka “dhiki kubwa” inayokuja wakalione kweli jambo ambalo mtume Yohana aliliona katika njozi ya ufunuo, anayoisimulia, akisema: “Nami nikawaona wafu, wakubwa na wadogo, wamesimama mbele za kiti cha enzi, . . . na bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake, nayo mauti na hell [“infernus,” Kirumi; Haʹdes, Kigiriki] vikawafungua wafu waliokuwamo ndani yavyo.”—Ufu. 20:12, 13; 7:14, Douay.
11. Hii yatia ndani akina nani waliokwenda hell mbele ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., na yatia nani waliokwenda humo tangu wakati huo, kulingana na 1 Yohana 2:2 na 1 Timotheo 2:5, 6?
11 Hii itatia ndani na Habili, Henoko, Nuhu, Ibrahimu, Isaka, Yakobo, Ayubu, Musa, ndiyo, wafu wote waliomo katika hell waliokwenda humo mbele ya kundi la Kikristo kuanzishwa katika siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., wakati ambapo mtume Petro alihutubia maelfu ya Wayahudi juu ya ufufuo wa Yesu Kristo kutoka hell (kaburi la kawaida la wanadamu waliokufa). Itatia ndani vile vile na wale wote wa wanadamu waliokwenda hell tangu siku ile ya Pentekoste na wasiokuwa washiriki wa kundi la bibi-arusi la Yesu Kristo. Hakuna wo wote kati ya hawa walio wenyeji wa “kanisa la mzaliwa wa kwanza, walioandikwa mbinguni.” (Ebr. 12:23, Douay) Kwa ajili ya hawa wote Yesu alikufa kama dhabihu ya ukombozi, sawa na alivyoandika mtume Yohana, akiliambia kundi: “Naye ndiye kipatanisho kwa ajili ya dhambi zetu: na siyo kwa ajili ya zetu tu, bali pia na kwa ajili ya zile za ulimwengu mzima.” (1 Yohana 2:2, Douay) Kupatana na hilo mtume wa Kikristo Paulo alimwandikia Timotheo: “Kwa maana kuna Mungu mmoja, na mpatanishi mmoja wa Mungu na wanadamu, mwanadamu Kristo Yesu: ambaye alijitoa mwenyewe kama ukombozi kwa ajili ya wote.”—1 Tim. 2:5, 6, Douay.
12. Kwa sababu gani wazo la kurudi kwa hawa wote kutoka hell laweza kushtua watu wengine?
12 Walakini, huenda watu wengine wakashtuka kwa kulifikiria hili. Huenda wakasema: ‘Je! hii haitaigharikisha dunia kwa maelfu ya mamilioni ya watenda maovu na kuijaza dunia na uovu zaidi na jeuri kuliko ambavyo imekuwa nayo hapo kwanza? Kwa maana je! mtume Paulo hakusema: “Kutakuwako ufufuo wa walio haki na wasio haki”?’ (Matendo 24:15, Douay) Bila shaka katika ufufuo wa kutoka hell wasio haki watawapita sana walio haki katika wingi. Na kwa watawala wa kawaida wa kibinadamu hiyo ingetokeza ugumu mzito.
13, 14. (a) Ni majeshi gani ambayo kufunguliwa kwa milango ya hell hakutawatolea wakaaji wa dunia, na kwa sababu gani sivyo? (b) Namna gani juu ya serikali za kibinadamu zisizokamilika wakati huo na wale wanaopatikana mwishowe wakizitegemeza?
13 Kufunguliwa kwa “milango ya hell hakutawafungulia wakaaji wa dunia majeshi ya mashetani na mkuu wao, Shetani Ibilisi. Wao hawajapata kuwamo katika hell wakimngoja Yesu Kristo autumie ufunguo na kuifungua milango ya hell.
14 Furaha kwa wanadamu ni kwamba, wakati wa hell kuachwa utupu Shetani na malaika zake wa kishetani watafungwa kana kwamba kwa minyororo na kutengwa wawe peke yao na kuzuiwa katika ambacho mtume Yohana anakiita “shimo lisilo na kikomo” au “Shimo Kubwa.” (Ufu. 20:1-3, Douay; The Jerusalem Bible) Kwa hiyo majeshi haya ya kiroho ambayo yamewachochea wanadamu katika uovu yatatoweka. Kutakuwako serikali yenye haki ya kimbinguni juu ya dunia yote na wafu wote waliofufuliwa. Zaidi ya hayo, serikali zisizokamilika za kibinadamu zilizoitawala dunia hazitakuwapo. Zitakuwa zimekwisha kupondwa-pondwa katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” penye Har–Magedoni, mara tu mbele ya kufungwa na kutiwa shimoni kwa watawala wazo wasioonekana, Shetani Ibilisi na majeshi yake ya mashetani. (Ufu. 16:13-16; 19:11-21; 20:1-3) Katika hiyo “vita ya siku ile kuu” ya ulimwengu wote watu wote watakaopatikana wakizitegemeza serikali hizo za kibinadamu mahali pa ufalme wa Mungu kwa njia ya Kristo wataangamizwa pamoja nazo. Hawataokoka.
15. (a) Ni mwanzo wa namna gani jamii ya kibinadamu itakaopewa kama ulivyotangulia kufananishwa na Nuhu na jamaa yake kufuata gharika? (b) Nini zitakazokuwa mbingu mpya ambazo Petro alitazamia, nazo zitafikiliza nini hapa?
15 Kama vile jamii ya kibinadamu ilivyokuwa na mwanzo mpya wenye haki katika Nuhu na jamaa yake ilipokwisha gharika ya dunia ya miaka ya 2370-2369 B.C.E., ndivyo wanadamu watakavyokuwa na mwanzo mpya tena katika waokokaji wenye kumcha Mungu wa vita ya ulimwengu wote penye Har–Magedoni, na wakati huu bila ya Shetani Ibilisi na mashetani zake kuwa wangali huru kuitawala dunia wakiwa katika hali yao isiyoonekana, yenye nguvu kupita zile za mwanadamu. (Mt. 24:37-39; Mwanzo 8:15 mpaka 9:17) Hata mtume Petro aliutazamia wakati huo mtukufu kwa wanadamu. Muda mfupi tu mbele ya mateso ya kikatili kutoka kwa Mfalme wa Kirumi Nero juu ya kundi la Kikristo, Petro aliandika: “Twatazamia mbingu mpya na dunia mpya kulingana na ahadi zake, ambamo haki hukaa.” (2 Pet. 3:13, Douay) “Mbingu mpya,” yaani, ufalme wa Mungu wa kimbinguni mikononi mwa Yesu Kristo, ambaye amepewa uwezo wote unaohitajiwa mbinguni na duniani, zitafikiliza haki kamili isiyozuiwa duniani. (Mt. 28:18) Kwa hiyo Wakristo wa kweli hawasali bure hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litukuzwe. Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatendeke duniani kama yanavyotendeka mbinguni.”—Mt. 6:9, 10, Douay.
16. Ufufuo kutoka hell utaendeleaje, nao uangalizi wa mambo ya kibinadamu utawekwa mikononi mwa nani duniani?
16 Kumbuka hili: Hell haitawamimina wafu wake wote katika wakati mmoja, katika siku moja ya saa 24, kwa njia hiyo ikitokeza idadi ya watu yenye kufadhaisha kwa waokokaji wenye kumcha Mungu wa vita ya ulimwengu wote ya Har–Magedoni walio wachache kwa kulinganisha. Kufunguliwa kwa wafu kutoka hell kutaongozwa kwa hekima kutoka mbinguni na ufalme wa Mungu chini ya Kristo. (1 Kor. 15:23) Hakuna ye yote kati ya wanasiasa wa wakati uliopita, wala serikali za kilimwengu zilizoharibiwa atakayerudishwa katika mamlaka. Uangalizi wa mambo ya kibinadamu utawekwa mikononi mwa wapenda Yehova Mungu, tangu Habili hata wamchao Yehova Mungu leo, ambao, mnamo maelfu ya miaka iliyopita, wameutazamia ufalme wa Mungu.
17. Kwa sababu gani majina ya wengine hayataandikwa katika “kitabu cha uzima,” nao hawa watatendewa nini?
17 Wote wale watakaofunguliwa kutoka hell na ambao, nyuma ya kipindi cha kutosha cha jaribu! watakataa kwa ugumu wa kichwa kujifunza haki na kuutii Ufalme watauawa. Majina yao hayataandikwa katika “kitabu cha uzima” kama wanaostahili uzima wa milele. Sivyo, hawatarudishwa hell na kukaa humo milele. Yohana anatuambia: “Nayo hell na mauti vikatupwa katika kiziwa cha moto. Hii ndiyo mauti ya pili. Na mtu awaye yote asiyeonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika kiziwa cha moto.”—Ufu. 20:14, 15, Douay.
18. (a) “Kiziwa cha moto” chafananisha nini, na ni jambo gani litakalowapata kwa sababu hiyo? (b) Ni watu wa namna gani ambao “mauti ya pili” ya hao wasioandikwa itaacha duniani, naye Mwamuzi Aliye Mkuu Zaidi atawahesabia kustahili nini?
18 Hicho “kiziwa cha moto,” kinachofananisha “mauti ya pili,” kinalingana na alichokiita Yesu Jehanum alipokuwa duniani. Kwa hiyo kinafananisha uharibifu wa milele, kifo ambacho hakina ufufuo. Kama vile kifo kilichorithiwa kutoka kwa Adamu na Hawa na hell vitakavyokoma, ndivyo na raia hawa wa kidunia walio wakaidi wa ufalme wa Mungu watakavyokoma nao watakuwa kana kwamba hawajapata kuwako wakati wo wote. Hii itawaacha duniani wale tu wapendao haki kwa moyo wao wote na wanaojihakikisha wenyewe kuwa waaminifu kwa serikali ya kitheokrasi ya Yehova Mungu Mwenye Nguvu Zote kwa kutokushindwa. Hawa ndio watakaopatikana wameandikwa katika “kitabu cha uzima,” ambao Mwamuzi Aliye Mkuu Zaidi Yehova anawahesabia kustahili uzima wa milele katika amani na furaha katika Paradiso ya Furaha itakayorudishwa wakati huo duniani.
19, 20. (a) Ni akina nani hao ambao hawatakwenda hell wakati wo wote, na kwa sababu gani sivyo? (b) Wawezaje kuwa kati yao?
19 Hata hivyo, ebu wazia wewe! Wako watu walio hai leo katika dunia hii iliyochafuliwa na kuogofishwa na vita ambao hawatakwenda hell hata kidogo. Haitawapasa kutolewa kutoka hell wakati wo wote. Je! hawa ni akina nani, na je! yawezekana kwa ye yote kati yetu kuwamo kati yao?
20 Hawa ni watu wenye mfano wa kondoo wamchao Mungu wanaotoa tegemezo lao kwa moyo wote na utumishi kwa ufalme wa kimbinguni wa Mwana mpendwa wa Mungu Yesu Kristo na hivyo kujiepusha na siasa za ulimwengu huu. (Mt. 25:31-46) Sasa, mbele ya vita ya ulimwengu wote ya Har–Magedoni, wao wanamshangilia Yehova Mungu kwa unyofu wa moyo akiwa katika kiti chake cha enzi cha kimbinguni na Mwana wake aliye mfano wa Mwana-Kondoo Yesu Kristo. Jamii hii ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova itahifadhiwa hai kupita mwisho mkali sana wa taratibu ya mambo ya dunia iliyopo na kuingizwa katika taratibu mpya ya mambo ya Mungu ambamo haki lazima ikae. (Ufu. 7:9-17) Humo kifo kilichorithiwa kutoka kwa Adamu na Hawa, ambacho tayari kimekwisha kuweka maelfu ya mamilioni katika hell, kitafutiliwa mbali, hivi kwamba waokokaji hawa hawatakuwa na haja tena ya kuiogopa hell wakati huo. Kwa kuendelea kuufuata mwendo wao wa haki na kujitoa kwa ufalme wa Mungu kwa njia ya Kristo, wataendelea kuishi kuiona bahari na hell vikiwatoa wafu waliomo ndani yavyo. Ndiyo, kwa kufanya jambo lipaswalo sasa, wewe waweza kuwa kati ya waokokaji hao waliobarikiwa.
—Kutoka The Watchtower, April 15, 1973.
[Picha katika ukurasa wa 182]
Wakati Yesu alipopaza sauti, “Lazaro, njoo huku nje” alifufuka nyuma ya kupita siku nne akiwa mfu. Hivyo Yesu aliyafananisha maneno yake ya kwanza: “Mimi ndimi ufufuo na uzima”
[Picha katika ukurasa wa 183]
Kati ya wale watakaofaidika kutokana na ufufuo atakuwamo Habili, Nuhu, Ibrahimu, Musa na wanaume wengine wa imani wanaotajwa katika Waebrania sura ya 11. “Walio haki” katika nyakati za kisasa waliokufa, wakiwa waaminifu kwa Mungu na ufalme wake, nao vile vile watafaidika
[Picha katika ukurasa wa 185]
Vita ya ulimwengu wote inayokuja itakapokwisha, waokokaji wenye kumcha Mungu watakuwa na mwanzo mpya wenye haki—bila ya Ibilisi na mashetani zake kuitawala dunia
[Picha katika ukurasa wa 186]
Utakuwa wakati mtukufu kuishi katika taratibu mpya ya Mungu yenye haki na ya kiparadiso na furaha yenye kusisimua kuzungumza na waliofufuliwa kama vile Habili na Ibrahimu. Je! wewe utalifurahia pendeleo hili kwa kufanya jambo lipaswalo sasa?