Je! Wewe Unauitikia Upendo wa Mungu?
KUSUDI la Mungu kuwafufua wafu ni wonyesho wa upendo wake. Yeye hayuko chini ya wajibu wo wote kwa wanadamu wenye dhambi, wenye kufa. Yeye hana deni ya ufufuo ya wanadamu waliokufa. Na hali upendo wake kwa ulimwengu wa wanadamu ni mkubwa sana kwamba hakukataa kumtoa Mwanawe aliye mpendwa zaidi akatoe msingi wa kushughulika na wanadamu na kufufua wanadamu waliokufa. (Rum. 8:32) Kama Yesu Kristo alivyosema: “Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
Alichofanya Yehova Mungu katika kumtoa Mwanawe kiliwezeshea mamilioni yaliyokufa bila ya ujuzi wa kweli juu yake kufufuliwa na kuja kumjua na kumpenda yeye. Kwa habari ya wale walioingia katika ujamaa na Mungu, tumaini la ufufuo liliwawezesha kuvumilia kwa uaminifu hata kifo chenyewe na kupata faraja juu ya kupoteza wapendwa.—1 The. 4:13, 14; Ufu. 2:10.
Je! wewe unauitikiaje upendo wa Mungu? Je! inakuvuta wewe upate kumjua yeye kwa njia bora zaidi, ujifunze mengi kama uwezavyo juu ya njia zake na matendo kwa wanadamu?
Kwa roho yake, Yehova Mungu aliongoza karibu watu 40 mbalimbali kwa zaidi ya kipindi cha karne kumi na sita waandike kumbukumbu lenye kutegemewa la makusudi yake, njia na matendo. Kumbukumbu hili limo katika vitabu 66 vya Biblia Takatifu. Linafunua mambo ambayo Yehova Mungu alifanya katika kushughulika na watu mmoja mmoja, makundi ya watu na mataifa kwa muda wa karne nyingi. Linatusaidia kulifahamu itikio la Mungu katika hali mbalimbali na sababu za matendo yake. Hivyo, kwa njia ya Biblia, twaweza kuja kumjua Mungu vema.
Ikiwa wavutwa kuisoma Biblia kwa sababu ya tamaa ya unyofu wa moyo ya kumjua Mungu kwa njia bora zaidi, wewe unauitikia upendo wa Mungu. Unaonyesha kwamba unashukuru kwamba Mungu ametoa, kumbukumbu la kutegemewa lililoandikwa kwa ajili ya wanadamu.
Bila shaka, funzo la Biblia lenyewe halitoshi. Lazima vile vile tutake kuyatumia mambo tuliyojifunza, tukizitii amri zake na kuziiga sifa za Mungu zinazompendekeza—upendo wake, haki, huruma na rehema. “Huku ndiko kumpenda Mungu,” aliandika mtume Yohana aliyeongozwa na roho ya Mungu, “kwamba tuzishike amri zake.”—1 Yohana 5:3.
Twaweza kukaa tukihakikisha kwamba jambo liwalo lote analotuamuru Mungu katika Neno lake litakuwa kwa faida yetu. Kwa kuwa ni Mungu wa upendo, haki na hekima isiyo na mpaka, yeye ameweka amri zile zinazoweza kuhakikisha furaha na hali njema ya wanadamu peke yake. Mtumishi mwaminifu wa Mungu aliyefahamu hivi sana alikuwa Mfalme Daudi. Yeye alikiri hivi: “Sheria ya [Yehova] ni kamilifu, huiburudisha nafsi. Ushuhuda wa [Yehova] ni amini, humtia mjinga hekima. Maagizo ya [Yehova] ni ya adili, huufurahisha moyo. Amri ya [Yehova] ni safi, huyatia macho nuru. Kicho cha [Yehova] ni kitakatifu, kinadumu milele. Hukumu za [Yehova] ni kweli, zina haki kabisa. Ni za kutamanika kuliko dhahabu, kuliko wingi wa dhahabu safi. Nazo ni tamu kuliko asali, kuliko sega la asali. Tena mtumishi wako huonywa kwazo, katika kuzishika kuna thawabu nyingi.”—Zab. 19:7-11.
Mojawapo ya amri zinazowakalia Wakristo ni kwamba imewapasa kukutana kwa kawaida na wale wanaotamani kuongeza ujuzi wa kweli wa Mungu. Wakati wengine walipokuwa wakikuachilia mbali kukutana huko kwa pamoja katika karne ya kwanza C.E., walitiwa moyo hivi: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane.”—Ebr. 10:24, 25.
Kukusanyika pamoja na wengine kwaweza kuwa wonyesho wa upendo kwao. Je! si kweli kwamba twafurahia kuwa pamoja na wale tuwapendao? Kwa hiyo, basi, kama tungekuachilia mbali kukutana na wale wanaotaka kufanya mapenzi ya Mungu, je! kwa sababu hiyo tusingekuwa tukisema kwamba hatuwapendi vya kutosha kuweza kutaka kuwa pamoja nao?
Mikutano ya Wakristo waliojitoa ina kusudi lenye kufaa. N’nini kusudi hilo? Ni kutoa faraja ya kuonyesha wazi upendo katika pande zote za maisha na kujazwa na matendo mema. Matendo mema hayo yanatia ndani kutoa msaada wa kimwili na mambo mengine ya fadhili kwa walio na shida, kusaidia watu wapate ujuzi wa kweli juu ya mapenzi ya Mungu na kuendelea kuwa na usemi ufaao na wenye kujenga, na mwenendo mwema.—Mt. 28:19, 20; Efe. 4:28; Flp. 4:14-19; Tito 2:6-10; Yak. 1:27.
Maneno mbalimbali ya unyofu yanayotoka moyoni ya wale wanaohudhuria mikutano ya Kikristo yanasaidia ‘kuhimiza wengine katika upendo na kazi nzuri.’ Wale wanaosikia maneno hayo wanatiwa nguvu kwa njia hiyo kuendelea katika utumishi wao mwaminifu kwa Mungu.
Ikiwa wewe sasa hushiriki na mashahidi wa Yehova wa Kikristo, twakualika uchunguze wao ni watu wanaouitikia upendo wa Mungu kweli kweli. Unapofanya uchunguzi wako, itumie kanuni iliyowekwa na Yesu Kristo: “Mtawatambua kwa matunda yao. Je! watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti? Vivyo hivyo kila mti mwema huzaa matunda mazuri; na mti mwovu huzaa matunda mabaya. Mti mwema hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti mwovu kuzaa matunda mazuri.”—Mt. 7:16-18.
Kwa kufaa yakupasa utazamie kupata watu wanaoiheshimu Biblia. Imewapasa wawe wakionyesha kwa neno na tendo kwamba wao wanaamini kwamba “andiko lote liliongozwa na roho ya Mungu na ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kutengeneza mambo, kwa kuadibisha katika haki, ili mtu wa Mungu apate kuwa na uwezo wa kutosha, aliye tayari kabisa kwa kila kazi njema.”—2 Tim. 3:16, 17, NW.
Hii maana yake ni kwamba imekupasa uweze kuchunguza katika maisha za mashahidi wa Yehova wa Kikristo kwamba kutumia kwao mafundisho ya Biblia kumetokeza waume bora na akina baba, wake bora na akina mama na wana bora na binti. Imekupasa uweze kuona watu wanaojitahidi kufanya ambavyo Mungu anahitaji kwa Wakristo:
“Uchungu wote na ghadhabu na hasira na kelele na matukano yaondoke kwenu, pamoja na kila namna ya ubaya; tena iweni wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo alivyowasamehe ninyi. Hivyo mfuateni Mungu, kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi; tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato. Lakini uasherati usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wala kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali kushukuru. . . . Enendeni kama watoto wa nuru; kwa kuwa tunda la nuru ni katika wema wote na haki na kweli.”—Efe. 4:31–5:9.
Ikiwa wewe wataka kuwa kati ya watu wanaotamani kuzipatanisha maisha zao na matakwa haya yaliyo bora, twakualika uende penye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova lililo karibu zaidi na nyumba yako. Sababu gani usifanye hivyo juma hii?