Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 1/1 kur. 3-6
  • Njia ya Uzima Yafunguliwa kwa Wanadamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Njia ya Uzima Yafunguliwa kwa Wanadamu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • HEKALU AMBALO KUTOKA KWALO MAJI YA UZIMA YATIRIRIKA
  • UZIMA KWA WAOKOKAJI WA HAR-MAGEDONI
  • UZIMA KWA MAELFU YA MAMILIONI AMBAO SASA WAMEKUFA
  • Baraka ya Yehova Juu ya “Nchi” Yetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • “Asikiaye na Aseme, Njoo!”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • “Waeleze . . . Kuhusu Hekalu”
    Hatimaye Ibada Safi ya Yehova Yarudishwa!
  • ‘Weka Moyoni Mwako’ Hekalu la Mungu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 1/1 kur. 3-6

Njia ya Uzima Yafunguliwa kwa Wanadamu

Makala hii ni ya kutumia kwa Mafunzo ya Kitabu ya Kundi

1-3. Ni tumaini gani linalotolewa na maneno yaliyomo katika Ufunuo 22:17?

“ROHO na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”​—Ufu. 22:17.

2 Maneno haya yaliyo karibu na mwisho wa Biblia yanatoa tumaini lenye mambo mazuri. Yanatoa ahadi ya uzima ambao ni bora kuliko muda mfupi wa maisha unaotaabisha tulio nao leo. Je! kuna nafasi ya kuanza kushika namna hiyo ya uzima sasa?

3 Iko. Yesu Kristo alisema kwamba yeye alikuja ili watu waweze kuwa na uzima tele. Basi, nini haya maji ya uzima, nayo yawezaje kupatikana?​—Yohana 10:10.

4. Yesu alifanya ulinganifu gani kati ya “maji ya uzima” na dhabihu yake?

4 Ni dhabihu ya uhai wa Yesu mwenyewe iliyofungua njia ya uzima wa milele kwa wanadamu. Kwa hiyo, Yesu alionyesha kwamba maji yenye kutoa uzima yanakamatana na dhabihu yake alipomwambia mwanamke Msamaria: “Ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele.”​—Yohana 4:14.

5. Biblia inaonyeshaje kwamba “maji ya uzima,” katika Ufunuo 22:17, yanamaanisha kile ambacho kitaleta uzima duniani?

5 Je! huu uzima wa milele ambao Yesu anatoa unamaanisha kwamba wote watakaoishi kwa umilele lazima waende mbinguni? Hata kidogo. Kwa maana unabii katika Ufunuo unasema juu ya maji yenye kung’aa kama bilauri ya mto wa uzima: “Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo!” Sasa, bibi-arusi ndilo kundi la Kikristo ambalo Kristo ndiye Kichwa chake kama mume. (Kol. 1:18; Efe. 5:23; 2 Kor. 11:2) Hawa wanaoshiriki uzima wa kimbinguni pamoja na Yesu Kristo hesabu yao ni watu 144,000. (Ufu. 14:1, 3) ‘Maji ya uzima’ yanatolewa na roho na bibi-arusi kwa hata wengine. Kwa hiyo yanafananisha mpango wa Mungu wa uzima wa kidunia, uzima wa milele wa kibinadamu katika ukamilifu juu ya dunia iliyogeuzwa kuwa paradiso, inayofaa kwa wanadamu wakamilifu.

6. Haya “maji ya uzima” yanafananisha nini, na je! yote yanapatikana sasa?

6 ‘Maji ya uzima’ yanafananisha mipango yote ya uzima kupitia kwa Yesu Kristo. Je! haya yote yapatikana leo? Hapana, kwa maana lazima kwanza Mungu aiondoe taratibu mbovu iliyopo ya mambo pamoja na mtawala wake asiyeonekana Gogu, ambaye ndiye Shetani Ibilisi tangu alipotupwa nje ya mbingu (kama ilivyozungumzwa katika matoleo mawili yaliyotangulia ya gazeti hili). Lakini twaweza kutwaa yapatikanayo ya haya “maji” sasa kwa kuzisikia na kuzitii habari njema za Ufalme na kupatanisha maisha zetu nazo.​—Yohana 3:16; Rum. 12:2.

HEKALU AMBALO KUTOKA KWALO MAJI YA UZIMA YATIRIRIKA

7. Katika njozi ya Ezekieli, hekalu linafananisha nini?

7 Nabii wa Mungu Ezekieli alipewa njozi inayokamilisha njozi ya mtume Yohana katika kitabu cha Ufunuo. Humo Ezekieli aliona hekalu. Halikuwa hekalu la kujengwa na wanadamu, kama yale ya Sulemani ama Zerubabeli, kwa maana wakati huo hakukuwako hekalu lo lote katika Yerusalemu, kwa kuwa lilikuwa limeharibiwa na Mfalme Nebukadreza wa Babeli karibu miaka kumi na minne iliyotangulia, nao Yerusalemu wenyewe ulikaa ukiwa. Hekalu hili lilikuwa tofauti na hekalu la Sulemani katika namna. Njozi inalifananisha kama lililokwisha jengwa tayari, tayari kwa ukaguzi na kupimwa. Lakini, lilikuwa la unabii, kwa kweli la kitu fulani cha kusimamishwa nyumaye. Lilifananisha “ile hema ya kweli, ambayo [Yehova] aliiweka wala si mwanadamu.”​—Ebr. 8:2.

8. Hii “hema ya kweli” au hekalu ilitokea lini?

8 Mwandikaji wa Kikristo wa barua kwa Waebrania anazungumza hema hii au hekalu kwa kirefu, akionyesha kwamba ilikuja mahali pa mahekalu ya zamani, la mwisho ambalo lilikuwa hekalu la Zerubabeli, lililojengwa upya na Mfalme Herode. Hii “hema ya kweli” ilitokea katika mwaka wa 29 C.E., wakati ambapo Yesu alijifanya mwenyewe apatikane kusudi atolewe dhabihu juu ya “madhabahu” ya mapenzi ya Mungu kwake kama “Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu.” Nyuma ya ufufuo wa Yesu yeye aliingia katika chumba cha Patakatifu Zaidi Sana pa hekalu hilo, mbingu zenyewe, kumtolea Mungu ustahili wa dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu aliyokuwa ametoa duniani juu ya madhabahu ya kiroho ya Yehova, “mapenzi” ya Mungu.​—Ebr. 9:23, 24; Yohana 1:29.

9, 10. (a) Twajifunza nini kutokana na uhakika wa kwamba hekalu aliloona Ezekieli lilikuwa “juu ya mlima mrefu sana”? (b) Hali ya watu wa Yehova ni nini sasa, kwa kiroho?

9 Katika njozi ya Ezekieli aliona hekalu “juu ya mlima mrefu sana,” jambo ambalo lingeweka wakati wa utimizo wa njozi ya Ezekieli katika wakati wa mbali, ambapo, kama ilivyotabiriwa na Isaya, “mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima.” Ezekieli aliongozwa katika utalii wa hekalu na malaika, anayefananishwa katika njozi na mwanadamu. “Kuonekana kwake kulikuwa kama kuonekana kwa shaba, naye alikuwa na uzi wa kitani mkononi mwake, na mwanzi wa kupimia.”​—Eze. 40:2, 3; Isa. 2:2.

10 Kwa wakati uliopo Yehova amewarudishia watu wake duniani ‘paradiso ya kiroho.’ Wao wanafurahia ufahamu wa makusudi ya Mungu na wanasitawi katika kuyatangaza makusudi haya ulimwenguni pote. Ibada ya Yehova ‘imewekwa imara’ na ‘ikainuliwa’ leo. Mamia mengi ya maelfu wanaanza kunywa “maji ya uzima bure.” Wao, nao, wanawaambia wengine: ‘Njoni!’ nayo makundi ya mashahidi wa Yehova yanasitawi kwa amani na utaratibu mzuri, kila mara yakiongezeka katika idadi.

UZIMA KWA WAOKOKAJI WA HAR-MAGEDONI

11. Lakini aliyoyaona Ezekieli yaliipitaje paradiso ya kiroho ya leo ya watu wa Mungu?

11 Lakini Ezekieli aliona jambo fulani lipitalo hili. Alikuwa amekwisha onyeshwa kushindwa kwa majeshi ya kidunia ya Shetani na kufutiliwa mbali kwa “nchi ya Magogu,” makao yasiyoonekana ambayo kutoka kwayo Shetani sasa anaitaabisha dunia. (Eze. 39:6) Kisha Ezekieli alipewa mfano wa wazi wa yatakayotukia duniani mnamo utawala wa miaka 1,000 wa Yesu Kristo, wakati ambapo hakutakuwako “Gogu,” Shetani Ibilisi, wala ye yote wa mashetani zake, wa kujiingiliza. Malaika aliyemwongoza Ezekieli katika njozi alimchukua katika utalii wa kukagua hekalu. Kisha Ezekieli asema:

12, 13. (a) Eleza alichokiona Ezekieli kinachopatana na maneno ya Ufunuo 22:17. (b) Nini kinachoonyeshwa juu ya maji pale chanzoni na kinakoelekea kijito?

12 “Baadaye akanileta tena mpaka lango la nyumba; na tazama, maji yalitoka chini ya kizingiti cha nyumba, kwa njia ya mashariki, maana upande wa mbele wa nyumba ulielekea upande wa mashariki; nayo maji yakashuka toka chini ya upande wa kuume wa nyumba, upande wa kusini wa madhabahu.”​—Eze. 47:1.

13 Maji yalitoka mahali ambapo Yehova alikaa katika patakatifu nayo yakatiririka kuelekea mashariki kupita madhabahu katika ua, ikionyesha kwamba Mpaji wa Uzima, Yehova Mungu, anaikubali dhabihu ya ukombozi ya Mwanawe na Kuhani Mkuu Yesu Kristo. Maji yaliendelea kutiririka nje ya ua nayo yakaelekezwa kulikohitajiwa uzima.​—Linganisha 1 Yohana 1:7; 5:11, 12.

14, 15. (a) Nini lililo la maana juu ya miendo ya dhiraa (mikono) elfu ambazo malaika alipimia? (b) Ni kwa faida ya nani “maji yakafika mpaka viweko vya miguu”?

14 Sasa malaika wa Yehova aliutumia uzi wake uliotengenezwa kwa kitani wa kupimia. Asema Ezekieli: “Alipotoka mtu yule, mwenye uzi wa kupimia mkononi mwake, kwenda masharikini, akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale; maji yakafika mpaka viweko vya miguu.”​—Eze. 47:3.

15 Ni jambo la maana kuangalia ya kwamba malaika alipima kuelekea mashariki katika miendo ya dhiraa elfu, ikitukumbusha mara kwa mara kuwa mambo yote yaliyofananishwa kama yaliyotimilizwa na kijito yanatukia mnamo utawala wa Kristo wa miaka 1,000. Wakati wa kipimo cha kwanza, maji hayakuwa yenye kina kirefu sana, yakifikia viweko vya miguu tu. ‘Kina cha kufikia viweko vya miguu’ kitakuwa maji yatoayo uzima ya kutosha mara tu nyuma ya vita ya Har–​Magedoni, ambamo majeshi ya kidunia ya Gogu yanashindwa. Kwa sababu gani? Kwa sababu wale tu wanaosimama imara upande wa ufalme wa Mungu mbele ya “dhiki kubwa” inayofikia upeo katika vita hiyo ndio watakaookoka. Hawa, ijapokuwa wanatajwa kama “mkutano mkubwa,” watakuwa wachache wakilinganishwa na idadi ya sasa ya dunia, na bila shaka ndivyo ilivyo wakilinganishwa na maelfu ya mamilioni ambao wameishi duniani. (Ufu. 7:9) Wao watakuwa kama Nuhu na jamaa yake, ambao waliokoka gharika ya duniani pote. “Mkutano mkubwa” utaipa jamii ya kibinadamu mwanzo wenye haki. Watakuwa ndio msingi wa “nchi mpya,” yaani, wa jamii ya kibinadamu kama itakavyosimamiwa chini ya ufalme wa kimbinguni wa Kimasihi.​—2 Pet. 2:5; 3:5-13.

UZIMA KWA MAELFU YA MAMILIONI AMBAO SASA WAMEKUFA

16, 17. Waokokaji wa “dhiki kubwa” watakapokunywa kabisa katika mto wa maji ya uzima, je! hii itakomesha matumizi ya faida za ukombozi? Eleza.

16 Lakini, Mungu hayaachi makusudi yake bila ya kutimizwa, wala yeye hapendelei. (Isa. 46:9, 10; Matendo 10:34, 35) Faida zenye kutoa uzima za dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo ni za wanadamu kwa jumla. Juu ya matumizi yake kwa wengine wengi, twasoma: “Twamwona yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya kila mtu.” (Ebr. 2:9) Vile vile: “Ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” (1 Yohana 2:2) “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote.”​—1 Tim. 2:5, 6.

17 Juu ya msingi huu, Yesu Kristo alisema: “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.” (Yohana 5:28, 29) Ah, ndiyo, kama vile mtume Paulo alivyotangaza: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.”​—Matendo 24:15.

18. Nini kinachofananishwa na kina cha kijito na kuongezeka kwa wingi hivyo kwamba maji yakafika “mpaka magoti”?

18 Wafu wanapofufuliwa, kutakuwako maji ya uzima ya kutosha kuwaponya na kuwarudisha kwenye utimilifu wa uzima. Hii inahakikishwa tunapoona kijito kikiongezeka kina chake: “Kisha [malaika] akapima dhiraa elfu, akanivusha maji yale, maji yakafika mpaka magoti.”​—Eze. 47:4.

19, 20. Nini kinachofananishwa na kuzidi kwa kina cha kijito kuwa kirefu, hivyo kwamba kikafika “mpaka viuno”?

19 Lakini kijito hakikuacha kuongezeka kina hapa. Kutokana na hili twaweza kusadiki kwamba si maelfu yote ya mamilioni ya wafu yatakayofufuliwa mara moja, jambo ambalo lingewafanya waokokaji wa Har–​Magedoni kuwa na idadi kubwa kupita kadiri mikononi mwao. Namna gani, basi, yawezavyo mambo ya kimwili yaliyo ya lazima kufanywa kwa ajili ya waliofufuliwa, licha ya kufundishwa kwao na kuzoezwa katika njia ya Yehova ya uzima?

20 Kipimo kilichofuata kilikipata kijito chenye maji mengi zaidi sana: “Kisha akapima dhiraa elfu, akanivusha, maji yakafika mpaka viuno.” (Eze. 47:4) Kadiri miaka 1,000 itakavyoendelea mbele, ndivyo idadi za waliofufuliwa zitakavyoongezeka, kwa maana watakuwako raia zaidi za Ufalme za kuwaangalia. Lakini, wengine kati ya waliofufuliwa, hawatashukuru kwa fadhili zisizostahili za Yehova nao hawatakuwa watiifu, kama tutakavyoona katika ufunuo unaoendelea wa unabii, utakaozungumzwa katika toleo la nyumaye la Mnara wa Mlinzi. Lakini maelfu ya mamilioni walio watiifu watakuwa wafanya kazi pamoja katika kurudishwa kwa paradiso na katika kusaidia watakaofufuliwa nyumaye wamjue Yehova Mpaji wa Uzima na Mwanawe, Mfalme, wakipokea misaada yake yenye kurudisha uzima kama Kuhani Mkuu wa Mungu.

21, 22. Nini kinachofananishwa na kufikia kwa maji kadiri ya wingi na kina cha bubujiko?

21 Mwishowe, malaika “akaendelea kupima [dhiraa] elfu. Lilikuwa bubujiko nisiloweza kuvuka, kwa maana maji yalikuwa yamekwisha panda juu, maji ya kutosha kuogelea, bubujiko lisiloweza kuvukika.”​—Eze. 47:5, NW.

22 Mbele ya miaka 1,000 ya utawala wa Masihi kumalizika kaburi la kawaida la kidunia la wanadamu (Haʹdes) na bahari ya makaburi yenye maji ya wanadamu wengi lazima viondolewe wale waliofungwa navyo katika mauti na kuwa vitupu. (Ufu. 20:13, 14) ‘Maji ya uzima’ ya mfano lazima yaenezwe kwa wa mwisho yule wa wafu wa wanadamu waliokombolewa. Hakuna kiwezacho kulizuia bubujiko la ‘maji ya uzima’ kutowafikia wanadamu kuwaletea uzima tele.

23. Ujuzi huu wa mapema una matokeo gani juu ya watu wenye kushukuru?

23 Yehova anatoa ujuzi huu wa mapema wa mipango yake ya ajabu kwa wanadamu akiwa na kusudi akilini. Kwanza, unatoa tumaini katika ulimwengu usio na tumaini. (1 The. 4:13) Vile vile, unawachochea wenye mioyo yenye shukrani kumkaribisha kila mtu wawezaye kufikia aanze kunywa maji haya yatoayo uzima sasa, kwa maana watu wanayahitaji sana sana. Wote wasikiao, na kufahamu kweli kweli, kwa furaha wanaungana na roho na bibi-arusi katika kusema, ‘Njoni! Myatwae maji ya uzima bure.’

​—Kutoka Kitabu “The Nations Shall Know that I Am Jehovah”​—How?

[Picha katika ukurasa wa 4]

Njozi ya Ezekieli Juu ya PATAKATIFU PA YEHOVA

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki