Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 12/15 kur. 10-15
  • “Asikiaye na Aseme, Njoo!”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Asikiaye na Aseme, Njoo!”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uhitaji wa Maji ya Uhai Unatokea
  • Jamii ya Bibi-Arusi Inatoa Mwaliko, “Njoo!”
  • Roho na Bibi-Arusi Wanasema, “Njoo!”
  • Kondoo Wengine Wanajiunga Katika Kusema, “Njoo!”
  • Jiunge Sasa Katika Mbiu
  • “Roho na Bibi-arusi Huendelea Kusema: ‘Njoo!’”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Njia ya Uzima Yafunguliwa kwa Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Shangilieni kwa Sababu ya Ndoa ya Mwana-Kondoo!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Maji Yanayobubujika Ili Kutokeza Uzima wa Milele
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 12/15 kur. 10-15

“Asikiaye na Aseme, Njoo!”

“Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.”—UFUNUO 22:17.

Muda wote wa mwaka unaokuja, Mashahidi wa Yehova katika mabara zaidi ya 200 ulimwenguni pote watakuwa wakijitahidi kupatana na andiko lao la mwaka wa 1991: “ASIKIAYE NA ASEME, NJOO!”

1. Ni “maji” gani ambayo kwenye hayo tunaalikwa “njoo!”?

WEWE unaalikwa “njoo!” Njoo kwa ajili ya nini? Njoo uzime kiu yako kwa maji. Haya si maji ya kawaida bali ni maji yale yale ambayo Yesu aliyataja aliposema hivi kwa mwanamke Msamaria kwenye kisima: “Ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele.” (Yohana 4:14) Yesu alipata wapi “maji” haya?

2. Ni nini chanzo cha “maji” hayo, nayo yangeweza kutiririka baada tu ya tukio gani?

2 Mtume Yohana alipendelewa kuona katika njozi chanzo kilichotoa “maji” haya, kama alivyosema kwenye Ufunuo 22:1: “Akanionyesha mto wa maji ya uzima, wenye kung’aa kama bilauri, ukitoka katika kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo.” Ndiyo, chanzo cha maji haya yanayong’aa kwa usafi kabisa yakiwa na vitu vyenye kutia uhai si mwingine ila Mpaji-Uhai, Yehova mwenyewe, ambaye anafanya yapatikane kupitia Mwana-Kondoo, Yesu Kristo. (Linganisha Ufunuo 21:6.) Kwa kuwa “kiti cha enzi cha Mungu, na cha Mwana-Kondoo” kimetajwa, ni lazima iwe ni baada ya kuanzishwa kwa Ufalme wa Kimesiya katika 1914, yaani, baada ya kuanza kwa siku ya Bwana, kwamba maji ya uhai yanaanza kutiririka.—Ufunuo 1:10.

3, 4. “Maji” hayo yanafananisha nini, nayo yatapatikana kwa ajili ya nani?

3 Maji haya ya uhai yafananisha nini? Yanafananisha uandalizi wa Mungu wa kurudisha uhai mkamilifu wa kibinadamu, uhai wa milele katika ukamilifu katika dunia iliyogeuzwa kuwa paradiso. Maji ya uhai yanafananisha maandalizi yote ya uhai kupitia Yesu Kristo. Je! yote haya yanapatikana sasa? Sivyo, si yote, kwa maana ni lazima kwanza Mungu aondoe mfumo mbovu wa mambo uliopo pamoja na mtawala wao asiyeonekana, Shetani Ibilisi. Lakini tunaweza kutwaa kutokana na yale yaliyopo sasa ya “maji” haya kwa kusikia na kutii habari njema za Ufalme na kupatanisha maisha zetu nazo.—Yohana 3:16; Warumi 12:2.

4 Hivyo, baada ya kumwonyesha Yohana ‘mto wa uzima,’ Yesu alimwambia Yohana juu ya kusudi Lake la kumtuma malaika Wake akiwa na njozi hiyo. Ndipo Yohana alipoisikia mbiu hii: “Na Roho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” (Ufunuo 22:17) Kwa sababu hiyo, watumishi wa Mungu wanawatolea wenye kiu mwaliko wa kuanza kunywa sasa kutokana na maandalizi ya Mungu ya kupata uhai wa milele duniani kupitia Mwana-Kondoo wa Mungu.—Yohana 1:29.

Uhitaji wa Maji ya Uhai Unatokea

5. Ainabinadamu ilikujaje kuhitaji uandalizi huu wa kimungu?

5 Kwa kuhuzunisha, wazazi wa kwanza wa familia ya kibinadamu hawakushika mwendo wa maisha ambao ungaliweza kuwapa wazao wao nafasi ya kuona milele shangwe ya uhai mkamilifu wa kibinadamu katika makao ya paradiso. Uhai wa milele kwa ainabinadamu ulitaka Adamu afanye lile chaguo la akili la kutumikia Muumba wake kwa utii. Chini ya uvutano wa kiumbe roho mwasi, Hawa alianzisha harakati iliyotokeza kifo kwa ainabinadamu, naye Adamu, mume wake mkamilifu, akachagua kujiunga naye katika mwendo wake wenye kifo. Hivyo, akiwa mpaji uhai wa kiasili kwa vizazi vyenye kufuatana vya aina ya kibinadamu, kwa kweli ni Adamu aliyeingiza utendaji wa kifo ndani ya familia nzima ya kibinadamu. Hivyo basi Biblia inasema hivi: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Ni baada ya Adamu na Hawa kuanguka ndani ya dhambi kwamba walianza kuongeza washiriki wapya kwenye familia ya kibinadamu.—Zaburi 51:5.

6. Kwa nini Yehova alipanga “maji” haya yapatikane?

6 Je! Mungu angezuiliwa milele asitimize kusudi lake la kuwa na dunia paradiso yenye kujaa wanadamu wakamilifu? Bila shaka, jibu la Biblia ni hapana! Hata hivyo, ili atimize kusudi lake, Yehova alifanya uandalizi wenye upendo ambao ungekinza ukosefu wa Adamu wenye msiba na hata hivyo upa-tane kabisa na haki na uadilifu, mambo ambayo ni Yeye anayeyaonyesha kwa ukamili na kwa upeo. Anafanya hivyo kupitia “mto wa maji ya uzima.” Kwa njia ya huo, atarudisha uhai mkamilifu wa kibinadamu kwa ainabinadamu iliyo tiifu, iliyopotezewa ruhusa ya kumfikia aliye Chanzo cha uhai. Mto huu unatiririka kikamili wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo. Hivyo, muda wote wa Utawala wa Mileani wa Kristo, wanadamu, kutia na wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu, ni lazima wanywe kutokana na “mto wa maji ya uzima.”—Linganisha Ezekieli 47:1-10; Matendo 24:15.

7. Uandalizi wa “maji” unafanywa kwa msingi gani?

7 Yehova anaonea shangwe uhai wake mwenyewe, naye anaona shangwe kuwapa baadhi ya viumbe wake pia pendeleo la kuwa na uhai wenye uelewevu. Msingi wa maandalizi ya Yehova yenye kutoa uhai ni dhabihu ya ukombozi ya Yesu. (Marko 10:45; 1 Yohana 4:9, 10) Pia Neno la Mungu linahusika, ambalo nyakati fulani Biblia inaliita “maji.” (Waefeso 5:26) Yehova Mungu yuko huru kusema, “Njoo!” kwa viumbe wa kibinadamu, waliopoteza maandalizi ya kwanza ambayo Mungu aliwafanyia wanadamu wawili wakamilifu, Adamu na Hawa.

Jamii ya Bibi-Arusi Inatoa Mwaliko, “Njoo!”

8. “Maji” haya yaliandaliwa kwanza kwa nani na wakati gani?

8 Wa kwanza kutoa mwaliko wa “njoo!” ni wale wanaojumlika kuwa bibi-arusi wa mfano wa Mwana-Kondoo, Mwana wa kiroho aliye mzaliwa wa kwanza wa Yehova. (Ufunuo 14:1, 3, 4; 21:9) Bibi-arusi wa kiroho wa Kristo hasemi “Njoo!” kwa yeye mwenyewe, yaani, kwa wale ambao bado Yehova Mungu angewakusanya wakiwa sehemu ya jamii ya bibi-arusi ili kuwafanya wawe 144,000 barabara. Maneno hayo ya mwaliko yanatolewa kwa wanadamu wanaotumainia kupata uhai mkamilifu wa kibinadamu duniani baada ya Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Wakati wa huu umalizio wa mfumo wa mambo kuanzia 1914, tumesikia mwaliko ukitolewa na “Bibi-arusi,” kwa kushirikiana na roho takatifu ya Mungu.

9. Tunajuaje kwamba hayo si kwa ajili ya kikundi kidogo tu?

9 Kwa kusisimua, kitabu cha mwisho cha Biblia kinaonyesha kwamba ‘umati mkubwa, ambao hakuna binadamu aliyeweza kuhesabu,’ ungeitikia mbiu ya habari njema za Ufalme wa Mungu na kujiweka imara upande wa serikali hiyo ya kifalme. (Ufunuo 7:9, 10, 16, 17, NW) Je! wewe ni mmoja wa umati mkubwa huo? Basi, kila “asikiaye na aseme, Njoo!”

Roho na Bibi-Arusi Wanasema, “Njoo!”

10. Ni lazima maji ya ufananisho yawe yanatoka wapi, na kwa nini?

10 Lakini kwa nini Mungu na Bwana-arusi wa mfano hawatajwi kwenye Ufunuo 22:17? Kwanza, angalia kwamba mstari huu hausemi ni chini ya mwelekezo wa nani roho inatenda kazi. Hata hivyo, kutaja roho kunaelekeza uangalifu wetu kwa Yehova Mungu mwenyewe. Baba hasukumwi kando, kwa kuwa yeye ndiye Chanzo chenyewe cha roho takatifu. Pili, Mwana anashirikiana kikamili na Baba yake, kama anavyosema yeye mwenyewe: “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda.” (Yohana 5:19) Zaidi ya hilo, ingawa mwaliko huu ni tamko lililovuviwa ambalo kwa msingi hasa linatoka kwa Yehova Mungu, wanadamu wanaweza kupokea mwelekezo wa kimungu, au “semi zilizovuviwa,” kwa njia ya Yesu Kristo, yule “Neno.” (Ufunuo 22:6; pia 22:17, Reference Bible, elezo la chini; Yohana 1:1) Basi, kwa kufaa tunashirikisha Kristo, aliye Bwana-arusi, na mwaliko huu. Ndiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba wote wawili Yehova Mungu, aliye Baba ya Bwana-arusi, na Yesu Kristo, aliye Bwana-arusi, wanajiunga na “Bibi-arusi” kwa njia ya roho takatifu katika kusema, “Njoo!”

11, 12. (a) Kulikuwa na wonyesho gani wa mapema kwamba mwaliko wa kunywa ungepanuliwa? (b) Jambo hilo lilizidije kuwa wazi muda wa miaka iliyopita?

11 Kwa makumi kadhaa ya miaka mwaliko huu wa “njoo!” umekuwa ukiendea watu wenye kiu ya “maji ya uzima.” Hata kule nyuma katika 1918, jamii ya bibi-arusi ilianza kuhubiri ujumbe uliowahusisha hasa wale ambao wangeweza kuishi duniani. Ilikuwa ile hotuba ya watu wote yenye kichwa “Mamilioni Wanaoishi Sasa Huenda Wasife Kamwe.” Hiyo ilitoa tumaini kwamba wengi wangeokoka Har–Magedoni na baada ya hapo wapate uhai wa milele katika dunia Paradiso chini ya Ufalme wa Kimesiya wa Mungu. Lakini ujumbe huo haukuonyesha wazi kabisa njia ya kupata pendeleo hili la kuokoka, isipokuwa katika uadilifu kwa ujumla.

12 Ili kufikia watu wengi zaidi na ule mwaliko, “Njoo!” katika 1922 ujumbe huu uliwaendea wote wale waliopendezwa na kutumikia Mungu: “Tangazeni Mfalme na Ufalme.” Katika 1923 jamii ya bibi-arusi ilielewa kwamba “kondoo” na “mbuzi” wa mfano wa Yesu kwenye Mathayo 25:31-46 wanaonekana wazi kabla ya Har–Magedoni. Halafu, katika 1929, Mnara wa Mlinzi la Machi 15 (Kiingereza) likakazia makala “Mwaliko Wenye Neema.” Andiko lake la kichwa lilikuwa Ufunuo 22:17, nalo lilikazia daraka la jamii ya bibi-arusi kuutoa mwaliko, “Njoo!”—Kurasa 87-9.a

Kondoo Wengine Wanajiunga Katika Kusema, “Njoo!”

13, 14. Katika miaka ya 1930, ni uelewesho gani zaidi uliofanywa ya kwamba wangekunywa kutokana na maji ya ufananisho?

13 Zaidi ya hilo, mapema hata huko 1932, Mnara wa Mlinzi lilionyesha wazi daraka la “kondoo wengine,” kwamba wao nao, kwa zamu yao, waseme, “Njoo!” (Yohana 10:16) Katika toleo lake la Agosti 1 (Kiingereza), ukurasa wa 232, fungu la 29 lilisema hivi: “Sasa Mashahidi wa Yehova wana bidii kama ile ya Yehu nao wanapaswa kuitia moyo jamii ya Yehonadabu [kondoo wengine] wafuatane nao kushiriki sehemu fulani katika kupigia wengine mbiu ya kwamba ufalme wa Mungu u karibu.” Halafu, baada ya kunakili Ufunuo 22:17, fungu hilo likasema hivi: “Acheni mabaki wawatie moyo wote watakaoshiriki katika kusimulia habari njema za ufalme. Si lazima wawe wapakwa-mafuta wa Bwana ili wajulishe rasmi ujumbe wa Bwana. Ni faraja kubwa kwa Mashahidi wa Yehova kujua kwamba wao wanaruhusiwa kupeleka maji ya uhai kwa jamii ya watu ambao huenda wakachukuliwa kupita Har–Magedoni na kupewa uhai wa milele duniani kwa sababu ya wema tele wa Yehova.”b

14 Kuanzia 1934 na kuendelea, mabaki wapakwa-mafuta walionyesha wazi kwamba kondoo wengine hawa ni lazima wajiweke wakfu kwa Mungu na kufananisha wakfu huu kwa ubatizo katika maji halafu wajiunge na jamii ya bibi-arusi katika kusema, “Njoo!” kwa wenye kiu wengine zaidi. Hivyo, sasa kukawa na mwaliko wa wazi wenye kutolewa kwa jamii ya bibi-arusi ili kukusanya kondoo wengine hawa wenye kiu pamoja ndani ya “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja,” Yesu Kristo. (Yohana 10:16) Katika 1935 mabaki wapakwa-mafuta walichochewa kujua kwenye mkusanyiko wao mkuu mwaka huo kwamba jamii ya watu walio kama kondoo waliokuwa wakiwaambia, “Njoo!” kwa kweli ilikuwa ule “umati mkubwa” wa Ufunuo 7:9-17, NW. Hiyo iliipa kichocheo kikubwa ajabu ile kazi ya mwaliko.

15. “Roho” ilihusikaje katika ule mwaliko, “Njoo”?

15 Katika kusema, “Njoo!” jamii ya bibi-arusi ilipatana na roho ya Mungu. Kwa kutumia roho yake kufungua maana ya unabii mbalimbali wa Neno lake lililoandikwa, alisababisha mabaki ya jamii ya bibi-arusi watoe mwaliko. Huo unabii mbalimbali uliokuwa msingi wa mwaliko wao ulikuwa umevuviwa na roho ya Mungu. Hivyo basi, ilikuwa ni kama roho ya Mungu yenye kutiririka kupitia Kristo na bibi-arusi wake ndiyo iliyokuwa ikiambia umati mkubwa wa watu walio kama kondoo, “Njoo!”—Ufunuo 19:10.

16. Roho na bibi-arusi wanahusikaje pamoja na mwaliko leo?

16 Mpaka leo hii roho na bibi-arusi, wakiwakilishwa na mabaki, wanaendelea ‘kusema, Njoo!’ Mabaki wanaambia kondoo wengine hawa wawape wengine zaidi mwaliko wa “Njoo!” Hawapaswi kujiwekea wenyewe “maji ya uzima,” kama yanavyopatikana leo. Ni lazima watii amri kutoka kwa ‘roho na Bibi-arusi,’ yaani: “Naye asikiaye na aseme, Njoo!” Wote wale wanaozima kiu yao ni lazima wazunguke wakieneza mwaliko huo. Ni lazima watolee kila mmoja bila kujali rangi, utaifa, lugha, au dini ya sasa—kila mmoja kila mahali! Kiasi kile kilichopo sasa cha “maji ya uzima” ndicho Mashahidi wa Yehova kwa sasa wanaalika na kusaidia vikundi vyote vya watu vikitwae bure!

17. Ni “maji” ya namna gani yanayopatikana leo?

17 Duniani pote, Mwana-Kondoo, Yesu Kristo, kwa kweli anaongoza umati mkubwa “kwenye chemchemi za maji yenye uhai.” (Ufunuo 7:17) Haya si maji yaliyotiwa uchafuzi, bali ni maji safi, baridi, yenye mafaa kuanzia kwenye Chanzo chayo chenyewe. Maji haya ya ufananisho si maji katika maana ya kuelewa tu ukweli wa Biblia; yanamaanisha maandalizi yote ya Mungu kupitia Yesu Kristo ambayo hata sasa yanaanza kuweka umati mkubwa katika kijia cha kufikia uhai wa milele ulio mkamilifu katika furaha.

Jiunge Sasa Katika Mbiu

18. Mwaliko una mweneo wa kadiri gani katika wakati wetu?

18 Tayari, hesabu ya umati mkubwa huu imepanda juu kufikia milioni kadhaa. Wanaendelea kwa bidii kupiga mbiu ya habari njema za Ufalme katika dunia yote yenye kukaliwa. Wao wanaripoti kwa ukawaida utendaji wao mbalimbali wa shambani katika kuhubiri habari njema za Ufalme, ambazo sasa zimefikia mabara 212. Kwa kadiri ambavyo wakati katika huu umalizio wa mfumo wa mambo unaruhusu, mwaliko utaendelea kulingana na subira na ustahimilivu wa Yehova Mungu, yule Mtunza-Wakati Mkubwa. Yeye atajua muda ukimalizika na ufike wasaa ulio muhimu wa kujijulisha kwa wote kwamba yeye ni Yehova, kama vile ameahidi kufanya kulingana na semi zenye kurudiwa-rudiwa katika unabii wa Biblia.—Ezekieli 36:23; 38:21-23; 39:7.

19. Kwa nini tunaweza kusema kwamba “maji” haya yanatolewa bure?

19 Kwa hiyo, kukiwa bado na wakati, washiriki wa umati mkubwa wanashiriki kwa shangwe pamoja na andamano la bibi-arusi katika kusema: ‘Njoo utwae maji ya uhai bure!’ Wapiga mbiu wa habari njema hizi zenye kuokoa uhai wanapiga mbiu bila malipo, bila kutoza pesa kwa huduma wanazotoa wakati wanapoeneza ujumbe wa Ufalme katika sehemu zote za ulimwengu.

20. Ni nini kitakachotokea kwa sababu “maji” haya yanapatikana?

20 Maji ya uhai sasa yanapatikana kotekote kuizunguka dunia, hivi kwamba watu wanaotaka kuyatwaa wanaweza kufanya hivyo kwa utoshelevu kamili na kupata matokeo yenye kuokoa uhai. Ainabinadamu yenye kufidiwa itaona shangwe ya uhai usio na mwisho hapa hapa katika dunia hii, ambayo itageuzwa iwe paradiso, ikitetea kusudi la Yehova lenye thamani kubwa. Muumba wetu hakuifanya dunia bure bali iwe bustani ya Edeni yenye kuuzunguka ulimwengu, au Paradiso ya furaha, yenye kukaliwa na viumbe wakamilifu wa kibinadamu walio katika mfano na sura ya Mungu.

21. Kusudi la Mungu kwa dunia litatimizwaje?

21 Kwa uhakika, kuwamo katika ulimwengu mpya huo kutakuwa pendeleo na shangwe kubwa isiyo na kifani! Halafu utume ambao Mungu aliwapa wanadamu wawili wa kwanza kwenye Mwanzo 1:27, 28 utatimizwa kwa wingi. Shukrani kwa Yehova kwa kushughulikia kwa ustadi maafa yaliyopata familia ya kibinadamu, dunia itatiishwa kwa kadiri ya kuwa paradiso na kujazwa jamii kamilifu ya kibinadamu. Ndiyo, Mungu ataona kila kitu ambacho amefanya, na, tazama, kitakuwa chema sana. Je! wewe utakuwako? Ikiwa ndivyo, basi ni lazima uanze sasa kwa uthamini kutwaa maji ya uhai bure. “Njoo!” unywe ukatosheke na kuzima kiu yako kwa maji ya uhai ambayo yameanza kutiririka sasa na yataririka kwa ukamili wakati wa Mileani ijayo. Na acheni yeyote anayesikia mwaliko huu wa kupendeza aseme: “Njoo!”

[Maelezo ya Chini]

a Miongoni mwa mambo mengine, makala hii ilisema hivi: “Hakujapata kamwe kuwa na ushahidi mpana sana wa ukweli kama katika miaka michache iliyopita. . . . Mabaki wanawaletea ujumbe wenye kufurahisha, na wanawaambia hivi: ‘Na yeyote anayetaka, acheni atwae maji ya uhai bure.’ Wao wanaambiwa kwamba sasa wanaweza kuchukua msimamo wao upande wa Bwana, na dhidi ya Ibilisi, na kupokea baraka. Je! jamii ya watu wa jinsi hiyo siyo inayoweza sasa kutafuta usikivu na uadilifu, na kufichwa katika siku ya hasira kuu yake itakayoonyeshwa, na kupelekwa ng’ambo ya lile pigano kubwa la Har–Magedoni na kuishi milele isife? (Sef. 2:3) . . . Jamii yenye uaminifu ya mabaki inajiunga katika mwaliko huo wenye neema na kusema, ‘Njoo.’ Ujumbe huu unapasa kupigiwa mbiu kwa wale walio na tamaa ya uadilifu na ukweli. Ni lazima ifanyike hivyo sasa.”

b Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 1934 (Kiingereza), lilitaja pia daraka la kondoo wengine na kusema hivi katika ukurasa wa 249, fungu la 31: “Jamii ya Yonadabu ni wale ambao ‘wanasikia’ ujumbe wa ukweli na ambao ni lazima waseme hivi kwa wale wanaowasikia: ‘Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.’ (Ufu. 22:17) Wale wa jamii ya Yonadabu ni lazima waambatane na wale walio wa shirika la Yehu mfananishwa, yaani, wapakwa-mafuta, na watangaze ujumbe wa ufalme, hata ingawa wao si mashahidi wapakwa-mafuta wa Yehova.”

Jibu Lako Ni Nini?

◻ Ni “maji” gani yanayotajwa kwenye Ufunuo 22:17?

◻ Ni nini chanzo cha “maji” hayo?

◻ Kwa nini “maji” hayo yanahitajiwa, na ni wakati gani tu yangeweza kuanza kutiririka?

◻ Katika andiko letu, kutajwa kwa ‘roho’ kunaonyesha nini, na ‘bibi-arusi’ anahusikaje?◻ Ni nani anayeweza kuyatwaa “maji,” na kwa tokeo gani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki