Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w74 1/1 kur. 7-22
  • Kutengenezwa Ili Kumsifu Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutengenezwa Ili Kumsifu Mungu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘KUTOKA GIZANI KUINGIA KATIKA NURU YA MUNGU YA AJABU’
  • BARAKA YA YEHOVA INATAJIRISHA
  • KUMTANGAZA MFALME NA UFALME
  • WANATEGEMEZWA NA MUNGU WANAYEMSIFU
  • WANAELIMISHWA NA KUTIWA NGUVU ILI WAMSIFU MUNGU
  • Kupiga Mbiu ya Kurudi kwa Bwana
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Wakati wa Kutahini (1914-1918)
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
w74 1/1 kur. 7-22

Kutengenezwa Ili Kumsifu Mungu

“Nitamshukuru [Yehova] kwa moyo wangu wote; nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu; nitafurahi na kukushangilia Wewe; nitaliimbia jina lako, Wewe Uliye juu.”​—Zab. 9:1, 2.

1, 2. (a) Maana yake nini kuwa wenye tengenezo, kama inavyoonyeshwa na wapiga muziki wa kale wa hekaluni? (b) Kwa sababu gani tengenezo lenye utaratibu, lenye kupatana linamfaa Yehova?

NAMNA inavyofurahisha kuusikia muziki na wimbo mzuri! Zaidi iko hivyo wakati sifa za Yehova Mungu zinapoimbwa. Wakati Waisraeli wa kale walipoadhimisha sikukuu katika mahali patakatifu pa Yehova, waliwasikia waimbaji na wapiga muziki wa kabila la Lawi. (1 Nya. (Sik.) 6:16, 31, 32) Maneno ya nyingi za nyimbo hizo ambazo waliimba yametunzwa mpaka leo hii katika kitabu cha Biblia cha Zaburi. Lo! namna nyimbo hizo za kumsifu Aliye Juu Zaidi zilivyokuwa zenye kufurahisha!

2 Mafundi hao wa muziki na nyimbo walitengenezwa vizuri. (1 Nya. sura ya 25) Yaani, kila mmoja aligawiwa kazi kwa kusudi la kuunganisha jitihada zao, kuziweka tayari kwa kazi ya shirika. Tengenezo ni kikundi cha watu walioungana kwa kusudi fulani. Tengenezo lenye utaratibu na upatano​—kama lile la Walawi hao​—lamfaa Yehova, “kwa maana Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” (1 Kor. 14:33) Wale waliosikiliza walifanya hivyo kwa kushukuru wakati Walawi walipomsifu Yehova katika wimbo, kwa sababu walikuwa wakiusikia muziki kwa kusudi lake bora.

3. Tengenezo la malaika watakatifu linatumikia kusudi gani?

3 Kama vile Walawi hao walivyotengenezwa ili wamsifu Mungu, ndivyo na wengine wametengenezwa wamsifu vile vile. Ikiwa ungeweza kuchungulia katika makao ya kiroho, ungeona tengenezo la ajabu​—malaika watakatifu kwa mamilioni. (Dan. 7:9, 10; Ufu. 5:11, 12) Wanatumikia kusudi gani? Chini ya uongozi wa roho ya Mungu Daudi alipaza sauti hivi: “Mhimidini [Yehova], enyi malaika zake, ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, mkiisikiliza sauti ya neno lake. Mhimidini [Yehova], enyi majeshi yake yote, ninyi watumishi wake mfanyao mapenzi yake.” (Zab. 103:20, 21) Ili malaika watakatifu walitende neno lake Yehova na kufanya mapenzi yake, bila shaka ni lazima watengenezwe vizuri.​—Isa. 6:1-6; linganisha Waebrania 12:22.

‘KUTOKA GIZANI KUINGIA KATIKA NURU YA MUNGU YA AJABU’

4. Ijapokuwa ukafiri, twajuaje kwamba watu fulani walipata kibali kutoka kwa Mungu wakati wa karne zenye giza kwa kiroho?

4 Katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, Mungu aliwaita watu wenye mioyo minyofu ‘watoke gizani wakaingie katika nuru yake ya ajabu.’ Waligeuka kuwa sehemu ya kundi la Kikristo, ambalo vile vile lilitengenezwa ili limsifu Mungu na “kuzitangaza fadhili zake.” (1 Pet. 2:9) Walakini, wakati uliofuata kulitokea ukafiri na giza la kiroho likaenea katikati ya wanadamu. (Matendo 20:29, 30; 1 Tim. 4:1, 2) Hata hivyo, kulingana na mfano wa Yesu Kristo, wakati wa karne hizo zenye giza la kiroho watu fulani walijifurahisha nuru na kibali kutoka kwa Mungu. (Zab. 43:3) Wakristo fulani wa kweli, walifananishwa na Yesu na “ngano,” walikulia katikati ya “magugu” au Wakristo wa uongo. Kwa vile “mavuno” au “mwisho wa taratibu ya mambo” ulikaribia, Yehova alitenda ili aonyeshe walio mfano wa ngano walivyo. (Mt. 13:24-30, 36-43, NW) Kama Wakristo wa karne ya kwanza, walionekana kuwa watu walioitwa ‘watoke gizani wakaingie katika nuru yake ya ajabu.’ Wakristo hawa wa kisasa wanaweza kujulikana kwa vyepesi kwa sababu ya bidii yao katika ‘kuzitangaza fadhili za Yehova,’ wakimshukuru yeye kwa moyo wao wote na kuliimbia jina lake. (Zab. 9:1, 2) Kurudia kwa ufupi historia yao kunaonyesha kwamba nao vile vile wametengenezwa ili wamsifu Mungu.

5. Charles Taze Russell alikuwa nani, na mengine ya maono yake ya kwanza ya kidini yalikuwa nini?

5 Katika habari hii, matukio ya karne ya kumi na tisa C.E. yanatuvuta fikira. Wakati huo vikundi fulani vya kidini vilitazamia kwamba kuja kwa kimwili kwa Yesu Kristo kulikaribia sana. Lakini fikira zetu zinavutwa juu ya Allegheny, Pennsylvania. Aliyezaliwa huko katika mwaka wa 1852 alikuwa Charles Taze Russell, mwana wa Joseph L. na Eliza Bimey Russell. Hata katika utoto wake Charles alionyesha kupendezwa kwake sana na Mungu. Ijapokuwa alizaliwa katika dini ya Kipresbiteri, baadaye alijiunga na Kanisa la Congregational. Lakini kijana Russell aliudhiwa sana na mafundisho ya kwamba Mungu amewaandikia wengine uzima wa milele na wengine amewaandikia wapate hukumu na mateso katika moto wa milele. Alipopata umri wa miaka kumi na saba akawa mwenye mashaka. Halafu likatukia jambo la maana. Baadaye, Russell aliandika juu ya hili akisema:

Jioni moja, inaelekea kwa bahati nilizuru jumba moja lenye mavumbi na chafu-chafu katika Allegheny, Pa., ambamo nilikuwa nimesikia kwamba ibada zilifanyiwa humo, ili nione ikiwa watu wachache waliokutanika humo walikuwa na lo lote la maana zaidi la kutoa kuliko imani za makanisa makubwa. Kwa mara ya kwanza nilisikia huko jambo fulani juu ya maoni ya imani ya kuja mara ya pili kwa Kristo, likitolewa na Jonas Wendell . . .

Ijapokuwa maelezo yake ya Maandiko hayakufahamika sana, . . . yalitosha, chini ya Mungu, kuiimarisha tena imani yangu yenye kuyumbayumba katika kuongozwa kwa Biblia na roho ya Mungu, na kuonyesha kwamba maandishi ya Mitume na Manabii yanapatana sana.

6. Je! Russell pamoja na wale waliokutana naye kwa ajili ya funzo la Biblia walipokea nuru ya kiroho kutoka kwa Mungu?

6 Muda kidogo kufuata hapo Russell na wengine wachache walianza kukutana kila juma ili wapate kujifunza Biblia kwa sala na kwa utaratibu. Nuru ya kiroho waliyopokea kutoka kwa Mungu iliongezeka, kwa maana “njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.” (Mit. 4:18) Kwa mfano, walifahamu kwamba Yesu angerudi kama roho, na kwa njia hiyo awepo ijapokuwa bila kuonekana.​—1 Pet. 3:18.

7. (a) Ukamatano wa C. T. Russell na N. H. Barbour ulikuwa nini, na nini kilichotukia kwa huu? (b) The Watchtower lilichapwa wakati gani kwa mara ya kwanza, nao msimamo wake ni nini juu ya fundisho la ukombozi?

7 Karibu na Januari wa mwaka wa 1876, C. T. Russell alikutana na gazeti The Herald of the Morning, lililochapwa na N. H. Barbour wa Rochester, New York. Gazeti hili lilikubali imani ya kuwapo kwa Yesu Kristo bila kuonekana. Mwisho darasa la Biblia la Pittsburgh la Russell lilijishirikisha na kikundi cha Barbour na Russell akawa mwenzi wake wa kuandika gazeti Herald, akitoa vile vile msaada wa fedha. Lakini katika mwaka wa 1878, kulingana na Russell, Bw. Barbour aliandika makala katika Herald “akikana kwamba kufa kwa Kristo hakukuwa bei ya Ukombozi wa Adamu na jamii yake.” Akiandika katika gazeti, Russell aliunga mkono sana mafundisho ya Biblia juu ya ukombozi. (1 Tim. 2:5, 6) Lakini hii haikuwa na matokeo, basi Russell alijitenga na Barbour. Halafu, katika Julai 1879, C. T. Russell alichapa toleo la kwanza la Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, sasa linaitwa The Watchtower (Mnara wa Mlinzi). Sikuzote gazeti hili limetangaza waziwazi kweli ya Maandiko juu ya ukombozi.

8. Nini kinachotoa ushuhuda kwamba The Watchtower limekuwa na msaada wa kimungu?

8 Hiyo ilikuwa “siku ya mambo madogo,” lakini haikupaswa idharauliwe. (Zek. 4:10) Toleo la kwanza la Zion’s Watch Tower lilikuwa na makala zapata 6,000 tu. Lakini wanafunzi wa Biblia waliokuwa wakilichapa walitamani wamsifu Mungu nao walisadiki kwamba gazeti hili lilipata msaada wa Yehova. Leo mwenezo wake unazidi wastani ya nakala 7,800,000 kila toleo katika lugha zaidi ya 70. Tendo hilo ijapokuwa upinzani wa mataifa yote uliotokea ni ushuhuda wa msaada wa kimungu.​—Yohana 17:14-17; Zab. 127:1.

9. Taja mwanzo na kusudi la Watch Tower Society.

9 Kuanzishwa kwa shirika “Watch Tower Tract Society” lililofanywa chini ya sheria ya Pennsylvania katika mwaka wa 1884 kama “Zion’s Watch Tower Tract Society” (sasa linaitwa “Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania”), kuliufanya mwaka wa 1881 kuwa wa maana. Shirika hili halikuanzishwa kwa kusudi la kupata faidi za kichoyo za kibiashara. Katiba yake inasema hivi:

Kusudi la kuanzishwa kwa Shiriki ni, kuenezwa kwa kweli za Biblia katika lugha mbalimbali kwa njia za vitabu, magazeti na hati nyingine za kidini, na kwa kutumia njia nyingine zote za halali ambazo Halmashauri ya Wakuu wake, ambayo imefanywa, itaona kuwa zafaa kwa kuendeshwa kwa kusudi lililoelezwa.

Shirika hili na mashirika mengine yenye kusudi linalofanana ni vyombo vya halali tu vinavyotumiwa na watumishi wa Yehova wakati wanapomtumikia na kumsifu Mungu.

10. (a) Wanafunzi wa Biblia ‘walimheshimu Yehova kwa mali’ namna gani? (b) Nini iliyokuwa “Nyumba ya Biblia”?

10 Kwa moyo wa kupenda, wanafunzi wa Biblia walichanga fedha ili waendeshe kazi. ‘Walimheshimu Yehova kwa mali zao,’ naye aliwabariki sana. (Mit. 3:9, 10; 2 Kor. 9:7, 11) Mungu alitoa makao na vifaa vilivyokusudiwa visaidie kutimiza kutakiwa kukubwa kwa vitabu vya Biblia. Katika mwaka wa 1889 walihamia katika jengo lao jipya la matofali lenye orofa nne linaloitwa “Nyumba ya Biblia,” lililojengwa katika Allegheny kwa gharama ya shilingi 238,000/-. Miaka kidogo iliyofuata, wakati uenyeji wa jengo zima ulipotolewa kwa Sosaiti, halmashauri yake ya wakuu ilikadiri gharama ya jengo na vifaa vyake kuwa zaidi ya shilingi 1,000,000/-.

11-13. (a) Ni kwa njia gani chakula cha kiroho kilivyotolewa? (b) Watu fulani walikiitikiaje chakula cha kiroho katika Zion’s Watch Tower na vitabu vinavyofanana?

11 Kwa kadiri roho takatifu ya Yehova au nguvu ya utendaji ilivyoendelea kutoa uongozi na nuru, ndivyo chakula tele cha kiroho kilivyotolewa kupitia kwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili” na baraza yake inayoongoza. (Luka 12:42-44; linganisha Matendo 15:4-29.) Chakula bora cha kiroho kiliwafikia watafutaji wa kweli kupitia kwa Zion’s Watch Tower na vitabu vya namna hiyo. C. T. Russell mwenyewe aliandika vitabu sita vya Millennial Dawn (wakati uliofuata vikaitwa “Studies in the Scriptures”) kutoka mwaka wa 1886 kufika 1904. Wakati huo, kweli ya Mungu ilipelekwa moja kwa moja kwenye nyumba za watu na mapainia kwa kuhubiri nyumba kwa nyumba.​—Matendo 5:42; 20:20.

12 Lakini watu walikiitikiaje chakula hicho cha kiroho? Hakuwezi kuwako shaka kwamba roho ya Yehova iliongoza mambo. Kwa mfano, kutoka London, Uingereza, likaja ombi hili katika mwaka wa 1882: “Tafadhalini mnifundishe namna na jambo la kuhubiri ili niitimize kazi yenye baraka ambayo Mungu anataka ifanywe.” Barua ya mwaka wa 1887 kutoka Nebraska ilisema hivi: “Mimi sitauona kama wajibu tu bali vile vile pendeleo lenye baraka kusaidia, kwa kila njia niliyo nayo, katika kuitangaza injili hii.”

13 Vile vile roho ya Yehova ilikuwa ikitenda katika nchi zilizo mbali zaidi. Mnamo mwaka wa 1887 na 1888 kweli ilikuwa imeenea kufika Uchina. Kutoka Makedonia, Uturuki wa Ulaya, ikaja ripoti hii ya mwaka wa 1888: “Maturuki, Wayahudi, Wabulgaria na Wamakedonia wanapendezwa sana na kweli.” Punde kufuata hapo, iliripotiwa kwamba kweli ilikuwa ikiendelea vizuri upande wa pwani ya Afrika ijapokuwa mateso. Na, kutoka Deccan, India, ikaja barua ya mwaka wa 1890 kutoka kwa mmoja wa wamisionari wa Kristendomu “maili 30 misituni” aliyesoma Zion’s Watch Tower na vikaratasi vya Wanafunzi wa Biblia “kwa kupendezwa sana.” Yeye aliandikisha gazeti hilo kwa miaka miwili na akaagiza vitabu vingine.

14. (a) J. F. Rutherford alitoaje shukrani yake kwa vitabu vya Millenial Dawn? (b) Toa habari fulani kwa urefu juu ya utendaji mbalimbali wa nyumaye wa Ndugu Rutherford.

14 Katika mwaka wa 1894 vitabu vya Millennial Dawn vilinunuliwa na mwanamume aliyesema hivi katika barua yake iliyopokewa na Sosaiti:

Nilivipeleka vitabu nyumbani, na sikuviweka maanani sana, mpaka yakapita majuma machache, nilipopata nafasi kidogo, nikaanza kukisoma kitabu cha kwanza, nacho kilikuwa chenye kupendeza sana hata sikuweza kuacha kusoma. Matokeo yake, mke wangu na mimi mwenyewe tumefurahia sana kuvisoma vitabu hivi, na tunaiona kuwa baraka kuu ya Mungu kwa vile tumepata nafasi ya kuvipata. Ni msaada sana wa kujifunza Biblia. Kweli kubwa zinazofunuliwa katika kujifunza vitabu hivi zimegeuza tamaa zetu za kidunia; na kwa kujua nafasi kubwa ya kumtumikia Kristo, tunakusudia tuitumie nafasi hii vizuri katika kuvigawa vitabu hivi, kwanza, katikati ya jamaa na rafiki zetu, halafu katikati ya maskini wanaotamani kuvisoma lakini hawawezi kuvinunua.

Barua hii ilitiwa sahihi na J. F. Rutherford, aliyebatizwa katika mwaka wa 1906, katika kuonyesha wakf wake kwa Mungu, na ambaye mwisho akamfuata C. T. Russell kama msimamizi wa Watch Tower Society.

BARAKA YA YEHOVA INATAJIRISHA

15. Nani waliokuwa wahaji walioshirikiana na Sosaiti, nao walisaidiaje waamini wenzao?

15 “Baraka ya [Yehova] hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo.” (Mit. 10:22) Namna ilivyo kweli! Kwa baraka ya kimungu, makundi ya Wanafunzi wa Biblia yalikuwa yakiongezeka. Mwisho, “wahaji”​—wajumbe wenye kusafiri wa Watch Tower Society​—waliyatembelea kwa kawaida. Wahaji walipata furaha kutokana na utumishi wao nao ‘walitamani sana kuwaona waamini wenzao ili wawape karama ya rohoni’ kwa njia ya hotuba na njia nyinginezo. (Rum. 1:11, 12) “Lo! namna hawa walivyoongeza furaha nyingi kwetu na utajiri wa imani yetu!” anapaza sauti Hazelle M. Krull juu ya wahaji hawa. “Na namna walivyotusaidia tulifahamu tengenezo la Yehova!”

16. (a) Mikutano ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo inatoa nafasi gani? (b) Viingilio vinachukuliwa katika makusanyiko haya?

16 Mikutano iliyofanywa na Wanafunzi wa Biblia ilitoa maagizo bora ya Biblia. Vile vile ilitoa nafasi ya “kuhimizana katika upendo na kazi nzuri.” (Ebr. 10:24, 25) Mpaka leo hii, mikutano ya mashahidi wa Yehova wa Kikristo inatangazwa kwa maneno “Viti bure, hakuna kiingilio.” “Mmepata bure, toeni bure,” akasema Yesu Kristo.​—Mt. 10:8.

17. Ni wakati gani na wapi ilipoanzishwa afisi ya tawi ya kwanza ya Sosaiti nje ya United States, na ni afisi ngapi za tawi zilizokuwako mnamo mwaka wa 1972?

17 Katika mwaka wa 1891, C. T. Russell alikuwa amesafiri katika nchi nyingine. Kutoka hapo vitabu vya Watch Tower Society vilichapwa katika Kijeremani, Kifaransa, Kiswedi, Kidano-Norway, Kipolishi, Kigiriki na wakati uliofuata katika Kiitalia. Afisi ya tawi ya kwanza ya Sosaiti nje ya nchi ya United States ilianzishwa katika London, Uingereza, katika mwaka wa 1900. Habari inaonyesha kwamba tangu wakati huo kumekuwako ongezeko na baraka ya kimungu. Mnamo mwaka wa 1972, afisi za tawi za Sosaiti zilikuwa 95.

18. Nini kilichotukia kwa habari ya makao makuu ya Sosaiti katika mwaka wa 1909?

18 Miaka ya 1908 na 1909 ilileta mpanuko zaidi. Wajumbe wa Sosaiti walinunua nyumba ya zamani ya misheni inayoitwa “Plymouth Bethel” iliyo katika 13-17 Hicks Street, na Henry Ward Beecher iliyo katika 124 Columbia Heights, Brooklyn, New York. Ile nyumba “Plymouth Bethel” iliitwa upya “Brooklyn Tabernacle” na nyumba ya zamani ya Beecher iliitwa “Bethel,” makao ya washiriki wa jamii ya wafanya kazi wa Sosaiti katika makao makuu. Basi, mnamo mwaka wa 1909, Brooklyn ikawa mahali pa makao makuu ya ulimwengu ya Sosaiti. Leo Watchtower Bible and Tract Society of New York, Incorporated, ina nyumba kubwa yenye makao, afisi na viwanda katika Brooklyn. Vifaa vyote hivi vinatumiwa na mashahidi wa Yehova wakati wanapomsifu Mungu na kuzitangaza habari njema za Ufalme.​—Marko 13:10.

19, 20. (a) Wanafunzi wa Biblia walitumiaje shirika lenye kuchapa magazeti? (b) Simulia Photo-Drama of Creation.

19 Wanafunzi wa Biblia waliendelea kuwapatia watu kweli za Maandiko vile vile kwa kutumia shirika la mataifa yote lenye kuchapa magazeti ambalo walitengeneza. Wakati mmoja yapata magazeti 3,000 katika United States, Canada na Ulaya yalikuwa yakichapa mahubiri ya C. T. Russell. Walakini, kwa miaka mingi Wanafunzi wa Biblia walikuwa wametangaza kwamba Majira ya Mataifa au “nyakati zilizowekwa za mataifa” zenye muda wa miaka 2,520 zingemalizika katika mwaka wa 1914. (Luka 21:24, NW) Wakati mwaka huo ulipokaribia, Russell aliona njia mpya ya uhodari ya kutangazia habari njema.

20 Sinema zilikuwa bado ndipo zinaanza. Sinema za biashara ambazo ni bora na zenye kutoa sauti zilikuwa hazijafanywa bado; wala sinema zenye kuonyesha picha zenye rangi hazikuwa zimekamilishwa kwa matumizi ya kawaida. Lakini katika mwaka wa 1912 Russell aliazimia kutoa ushuhuda mkubwa kupitia kwa chombo hiki. Yeye aliandika na akafanyiza Photo-Drama of Creation, sinema yenye kuchukua muda wa saa nane, picha na ufanyizaji kamili ikieleza kusudi la kimungu kwa dunia na wanadamu tangu kuumba mpaka mwisho wa utawala wa Yesu Kristo wa miaka elfu. (Ufu. 20:6) Ikionyeshwa katika sehemu nne, Photo-Drama iliunganisha maneno yaliyotiwa katika rekodi pamoja na vipande vya picha. Ilionwa na mamilioni nao ulikuwa ushuhuda mkubwa juu ya makusudi ya Yehova.

21. Je! kazi ya Wanafunzi wa Biblia ilimtegemea mtu mmoja?

21 Akiwa katika safari ya kuhubiri, Charles Taze Russell mwenye kuugua alifia ndani ya gari la moshi katika Pampa, Texas, Oktoba 31, 1916. Lakini, ijapokuwa huzuni iliyotokea, wingi wa Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba kazi yao haikutegemea mtu mmoja. Ilikuwa kazi ya Yehova, ikiongozwa na roho takatifu yake. Mungu angeiendeleza na kuifanikisha.​—Matendo 5:38, 39.

KUMTANGAZA MFALME NA UFALME

22. Ni magumu gani yaliyowapata mashahidi wa Yehova wa Kikristo muda mfupi tu nyuma ya J. F. Rutherford kuwa msimamizi wa Watch Tower Society, lakini mambo yakawaje?

22 J. F. Rutherford alimfuata C. T. Russell kama msimamizi aliyechaguliwa wa Watch Tower Society. Lakini alikutana uso kwa uso na watu wenye kutaka makuu, wenye kupinga ndani ya tengenezo ambao walijaribu kulizuia, na wakati fulani ulipita mbele ya jitihada zao kushindwa kabisa. Wakati ule ule, mateso yaliyochochewa na viongozi wa dini yalipata kuwa makali sana juu ya mashahidi wa Kikristo wa Yehova. (Mt. 24:9) Zaidi ya hayo, ilielekea kuwa kazi yao ingeharibiwa sana wakati ambapo, tarehe ya Mei 7, 1918, J. F. Rutherford na wengine saba walioshirikiana sana na Sosaiti walipokamatwa, nyumaye wakajaribiwa, na mwishowe wakatiwa hatiani juu ya mashtaka ya uongo. Ilishtakiwa kwamba wao​—

Kwa haramu na kwa hatia walifanya shauri, wakaungana, wakashirikiana na kukubaliana pamoja, na watu wengineo wasiojulikana na Wasikilizaji Wakuu wa mashtaka, kusudi watende jambo fulani baya juu ya United States of America, yaani: kosa la kuleta maasi, kutokutii na kukataa kazi katika majeshi ya nchi kavu na ya baharini ya United States of America kwa haramu, kwa hatia na kwa kupenda wakati ambapo United States ilikuwa vitani . . . kwa njia ya vishawishi vya kipekee, barua, hotuba za watu wote, kugawa na kuzungusha waziwazi katika United States of America yote kitabu fulani kinachoitwa “Volume VII. Bible Studies. The Finished Mystery,” na kugawa na kuzungusha waziwazi katika United States yote makala fulani zilizochapwa katika vijitabu vinavyoitwa “Bible Student’s Monthly,” “Watch Tower,” “Kingdom News” na vijitabu vingine visivyotajwa.

Nyuma ya miezi mingi wakiwa katika gereza la serikali katika Atlanta, Georgia, waliachiliwa huru kwa dhamana. Kufikia Mei 14, 1919, mathibitisho yao ya hatia ya uongo yalishindwa, na tarehe ya Mei 5, 1920, wakatolewa katika lawama kabisa. Kwa usemi wa mfano, “mashahidi wawili” wa Mungu, wafuasi waliotiwa mafuta wa Kristo, walikuwa wamekufa. Nyuma ya kufunguliwa kwa wajumbe wa Sosaiti kutoka gerezani, “roho ya uhai kutoka kwa Mungu” iliwatia nguvu nao wakatokea mara nyingine, wakiwa wametengenezwa ili wamsifu Mungu.​—Ufu. 11:3-12, NW.

23, 24. (a) Kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia katika Cedar Point, Ohio, katika mwaka wa 1919 liliipasa kazi yao kwa njia gani? (b) Kusanyiko la mwaka wa 1922 lilikuwa na maana gani kwa habari ya utangazaji wa Ufalme?

23 Mwaka wa 1919 ulileta kusanyiko lenye kusisimua katika Cedar Point, Ohio​—ambalo lilitoa nguvu mpya kwa kazi ya Wanafunzi wa Biblia. Kati ya mambo mengine, huko walipokea chombo kipya cha matumizi katika kazi yao ya kuhubiri. Kilikuwa The Golden Age, gazeti lenye kufunua kosa la kidini na kukazia fikira kwenye tumaini na faraja ipatikanayo katika Maandiko Matakatifu. Sasa, nyuma ya karibu nusu karne, lingali linatimiza kusudi lile lile chini ya jina jipya​—Awake!

24 Mara nyingine Wanafunzi wa Biblia walikusanyikia Cedar Point, katika mwaka wa 1922. Wakati huu hotuba ya J. F. Rutherford ya Ijumaa, Septemba 8, juu ya kichwa “Ufalme” zaidi ilikuwa ya maana sana. Kwa uhodari aliimalizia kwa maneno: “Tazameni, Mfalme atawala! Ninyi ndio mawakili wake wa kueneza habari. Kwa hiyo mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni Mfalme na ufalme wake.” Kufuatia hili, kitambaa cha futi 36 kwa urefu kikakunjuliwa juu ya kibao cha msemaji. Kilisema “Mtangazeni Mfalme na Ufalme!” Watumishi wa Mungu wameutangaza Ufalme tangu wakati huo.

25. Chini ya hali gani Wanafunzi wa Biblia walilikubali kwa moyo jina “mashahidi wa Yehova”? Je! ni la Biblia?

25 Mwaka wa 1931 ukafika. Wanafunzi wa Biblia wakakusanyika katika Colombus, Ohio. Huko kwa azimio walilikubali kwa moyo jina la Biblia “mashahidi wa Yehova.” (Isa. 43:10-12, NW) Kwa furaha wamelichukua jina la Yehova, wakishuhudia juu ya Mungu na makusudi yake duniani mwote.

WANATEGEMEZWA NA MUNGU WANAYEMSIFU

26, 27. Taja mfano ukionyesha kwamba, kwa wale waliotengezwa wamsifu yeye, Yehova amekuwa ‘ngome salama kwa nyakati za shida.’

26 Miaka iliyofuata ilileta baraka nyingi, lakini mateso mengi vile vile. Kwa mfano, maono mengi yenye kujaribu yaliwapata watumishi wa Yehova mnamo Vita ya Pili ya Ulimwengu. Ndugu mmoja, aliyetiwa kifungoni na Wanazi, alisema:

Kwa sababu ya kunyimwa chakula mara nyingi sana na kufanya kazi nzito kila siku, nguvu zetu za kimwili zilionekana kupungua. Nilikuwamo katika hali ya kwamba nisingeweza kuusogeza mwili wangu wenye mifupa mitupu. Ndugu wawili walikuwa wakinitegemeza makwapani wakati wa kwenda kambini: Mara nyingi nilimeza mchanga kidogo ili tumbo langu lipate jambo la kufanya. Ndugu wengine walifanya hivi vile vile. Kwa hiyo tulifanya kila kitu kilichowezekana kuendelea kuwa hai na hivyo kumwaibisha Shetani na watu wake wa SS kama waongo, kwa maana mara nyingi walisema: “Yehova wenu yuko wapi? Na awasaidieni yeye!” Lazima niseme kwamba alitusaidia kwa njia nzuri sana.

27 Yehova anawasaidia watumishi wake kweli kweli. Roho yake inakaa juu ya watu wake kama tengenezo na kama watu mmoja mmoja. Mara nyingi, kwa wale waliotengenezwa kumsifu Mungu, Yehova amekuwa ‘ngome salama kwa nyakati za shida.’​—Zab. 9:9.

WANAELIMISHWA NA KUTIWA NGUVU ILI WAMSIFU MUNGU

28. Watchtower Bible School of Gilead ilianzishwa wakati gani, nayo imefanya kitu gani?

28 J. F. Rutherford alikufa tarehe ya Januari 8, 1942. Siku tano nyumaye N. H. Knorr alichaguliwa na wote kuwa msimamizi wa Watch Tower Society. Yeye na washiriki wake waliingia kwa haraka katika kazi ya kuelimisha. Tarehe ya Februari 1, 1943, ilikuwa ya wakf na mzinduo wa Watchtower Bible School of Gilead. Katika miaka iliyofuata shirika hili limetayarisha maelfu ya wahudumu kwa kazi ya umisionari ya nchi za kigeni na migawo mingine muhimu ya utumishi katika mpanuko wa tengenezo la watumishi wa Yehova.

29. Ni kwa njia gani Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inawafaidi watu mmoja mmoja?

29 Vile vile katika mwaka wa 1943 shule mpya ilianzishwa katika makundi moja moja ya mashahidi wa Yehova. Ilikuwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, iliyokuwa wazi kwa uandikishaji wa wanaume hapo kwanza. Leo inasaidia wanaume, wanawake na watoto walioandikishwa, na kuwafaidi sana wote wanaohudhuria vipindi vyake vya kila juma. Walioandikisha wanafundishwa kukusanya, kukuza na kutoa habari ya Biblia. Elimu inayopatikana katika mkutano huu na mingine ya mashahidi wa Yehova inazidisha maarifa ya Biblia na ufahamu nayo inaongezea uwezo wa kuhudumu.

30. Shule ya Huduma ya Ufalme ilianzishwa wakati gani, nalo kusudi lake ni nini?

30 Katika mwaka wa 1959 mpango mwingine wa kitengenezo ulianza. Huu ulikuwa Shule ya Huduma ya Ufalme. Zikiwa mahali panapofaa na kufanya kazi chini ya uongozi wa Watch Tower Society katika nchi mbalimbali, shule hizi zinazoeza waangalizi waliowekwa na roho kutimiza madaraka yao ndani ya kundi la Kikristo.​—Matendo 20:28; 1 Tim. 3:1-10, 12, 13; 1 Pet. 5:1-4.

31. Ni kusanyiko gani kuu la mashahidi wa Yehova lililofanywa katika mwaka wa 1958?

31 Tengenezo la kidunia la Yehova limepanuka kwa maana Mungu ameifanikisha kazi ya waabudu wake waliojitoa. Makusanyiko yao makubwa hayakuwa yenye maana ndogo. Kati ya haya lilikuwamo “Mapenzi ya Kimungu” Kusanyiko la Mataifa Yote la Mashahidi wa Yehova, tarehe ya Julai 28-Agosti 3, 1958, wakati ambapo watu 253,922 walijaza Yankee Stadium wa mji wa New York na Polo Grounds kwa ajili ya hotuba ya watu wote ikitolewa na N. H. Knorr juu ya kichwa “Ufalme wa Mungu Watawala​—Je! Mwisho wa Ulimwengu u Karibu?”

32. Kwa sababu gani tengenezo la Yehova la kidunia limepata kutiwa nguvu kwa kiroho na ongezeko?

32 Baraka ya kimungu imetia tengenezo la Yehova nguvu kwa kiroho na vile vile imetokeza mazao katika kazi ya kuuhubiri Ufalme. Leo inaendelezwa katika nchi 208 chini ya uongozi wa afisi za tawi za Watch Tower Society 95. Inapaswa sifa kwa ongezeko hili apewe Yehova peke yake. Mungu amewabariki watumishi wake waaminifu, nayo roho takatifu yake imewategemeza katika kazi yao ya kuyatangaza makusudi yake na kufanya wanafunzi.​—Mt. 28:19, 20.

33. Ni maulizo gani yanayofaa kwa wale ambao wamejifunza kweli katika miaka ya karibuni wajiulize wenyewe?

33 Maelfu mengi zaidi yameendelea kumiminikia tengenezo la Yehova hata kufikia wakati uliopo, na ni vizuri sana kuwaona wakija! Lakini watafanya nini na habari njema wanazojifunza? Je! wataonyesha namna ya bidii ambayo wale watumishi wa Mungu wenye bidii walionyesha katika miaka iliyopita? Je! wataonyesha uvumilivu ule ule? Kumbuka, wamo watu katika tengenezo la Yehova leo ambao wamekuwa wakienda nje katika utumishi wa shambani kwa zaidi ya miaka 50, wakiendelea bila ya kujali hali mbaya ya hewa, afya mbaya wala mateso. Ni upendo wa kweli kwa Yehova uliowachochea kusonga mbele.

34. (a) Kwa kupatana na mfano uliowekwa na Yehova, imetupasa tumwone mtu na mwenzake namna gani katika tengenezo la Yehova? (b) Ni katika kazi gani ya haraka mna mengi ya kufanya kwetu sote?

34 Labda wewe umekuja kushirikiana na tengenezo la Yehova miaka michache tu iliyopita. Huenda ukawa hukuwajua hawa wazee zaidi kwa muda mrefu sana; unawaona katika miaka yao ya nyumaye tu ya maisha. Je! wewe wawaonaje? Karibuni barua iliyopokewa na Watch Tower Society ilisema juu ya jambo hili: “Nataka kutoa shukrani yangu kwa 1973 Yearbook. . . . Pengine fungu moja lililonivuta mimi zaidi sana ni fungu la tatu katika ukurasa wa 32 chini ya ‘Matendo ya Mashahidi wa Yehova katika Nyakati za Kisasa.’ Fungu hili linakazia fikira kwenye hali fulani ambayo ipo kweli kweli. ‘Nyakati nyingine kizazi kilichopo kinafikiri tu juu ya kinayotimiza. Kwa kweli, kizazi kilichopo cha mashahidi wa Yehova kinakua juu ya ambayo watangazaji wa injili waaminifu walifanya miaka mingi iliyopita.’ Lo! ni kweli kama nini! Namna 1973 Yearbook kilivyotayarishwa, kitatusaidia sisi ‘tulio wachanga zaidi katika kweli’ kuwatazama ‘ndugu wazee zaidi katika kweli’ kupitia kwa macho mbalimbali, na si kuwaona kama ‘rafiki wa zamani’ tu ama ‘ndugu wazee na dada.’ “Kila mmoja wa watumishi wa Yehova ana nafasi katika tengenezo lake, na kila mmoja ni bora kwa Yehova. Kunayo kazi kwa wote kufanya, nayo Biblia yatusihi ‘tuzidi sana kutenda kazi ya Bwana,’ tukijua kwamba hiyo ndiyo kazi yenye kufaa kupita zote awezayo kuifanya ye yote. (Zek. 2:8; Hag. 2:7; 1 Kor. 15:58) Kama kikundi kilichoungana, mashahidi wa Yehova duniani pote wataendelea kumsifu Baba yao wa kimbinguni, wakiwa na shukrani kwamba wametengenezwa ili wamletee yeye sifa.

[Picha katika ukurasa wa 8]

C. T. RUSSELL

[Picha katika ukurasa wa 13]

Katika kusanyiko la Cedar Point katika mwaka wa 1922 msimamizi wa Sosaiti, J. F. Rutherford, alitilia mkazo mwingi kuuhubiri ufalme wa Mungu, akisihi kwa mkazo mwingi: “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni Mfalme na ufalme wake!”

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nyuma ya N. H. Knorr kuwa msimamizi wa Watch Tower Society, mkazo mwingi ulitiliwa juu ya elimu. Mojawapo ya shule zilizoanzishwa ilikuwa Watchtower Bible School of Gilead

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki